Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Walisadikishwa Katika Kathmandu
MSTADI mmoja wa sanaa mwanamke alianza utafutaji wake wa kweli katika Brittany, Ufaransa, katika 1980. Alikuwa na mazungumzo pamoja na Wapentekoste naye alijifunza dini za Mashariki—bila uradhi. Halafu akawa na mazungumzo pamoja na mmoja wa Mashahidi wa Yehova lakini upesi akaacha. Alikutana na mstadi mwingine wa sanaa mwanamume, akaenda kufanya kazi na kuishi pamoja naye.
Muda mfupi baada ya hilo wenzi hao wasiofunga ndoa wakaamua kutembelea Nepali. Walivutiwa sana na uzuri na amani ya nchi hiyo lakini wakahuzunishwa na mfumo wa vyeo vya kijamii, ulioonekana kutokuwa wenye haki katika macho yao ya Magharibi.
Waliporudi Ufaransa, mwanamke huyo akadokezea mwenzi wake kwamba wajifunze Biblia pamoja, na kwa mshangao wake akakubali. Walimwendea Shahidi ambaye mwanamke huyo alikuwa amekuwa na mazungumzo pamoja naye miaka miwili mbeleni. Mwanzoni, walitumia Biblia tu, lakini hatimaye walikubali kutumia kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele na baadaye kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Katika mwaka mmoja waliacha kutumia dawa za kulevya.
Baada ya kutembelea Nepali tena kwa miezi miwili, wenzi hao walirudi Ufaransa ambapo waliendelea kujifunza. Waliacha kuvuta sigareti na kwenda kwenye mabaa (mahali pa kunywa vileo) na vilabu vya usiku wakaanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, walipomaliza kitabu Kuishi, waliamua kuacha kujifunza.
Walienda Nepali tena ambapo waliishi katika nyumba ndogo chini ya Milima ya Himalaya. Siku moja mwanamume mzee mzee, aliyekuwa amevaa suti na tai, akapiga hodi mlango wao. Mwanamke huyo alikuwa peke yake nyumbani, naye alifikiria kwamba ni lazima mwanamume huyo alikuwa mchuuzi wa vitu vya sanaa aliyekuja kuona picha zao. Kwa mshangao wake alikuwa Shahidi aliyekuwa akiwatembelea kwa ajili ya yule mtu aliyekuwa akijifunza nao katika Ufaransa. Muda mfupi mwenzi wake akarudi nyumbani, na mazungumzo ya muda wa saa mbili yakafuata.
Siku chache baadaye, wenzi hao wakahudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova katika Kathmandu nao wakavutiwa sana na sura safi ya wale waliohudhuria. Waliona upendo wa kidugu na furaha ile ile waliyokuwa wameona kwenye mikutano katika Ufaransa. Waliona pia umoja wa watu wa Nepali waliokuwako, ingawa hao walikuwa wametoka vyeo vya kijamii tofauti-tofauti. Sasa wakasadikishwa kwamba hili lazima liwe ni tengenezo la Yehova.
Mwezi mmoja baadaye walirudi Ufaransa na mara moja wakaanza tena funzo la Biblia na kuhudhuria mikutano. Wakaoana, wakaanza kushiriki katika kazi ya kutoa ushahidi, na hatimaye wakabatizwa. Mume sasa ni mtumishi wa huduma, na mke wake hushiriki kwa ukawaida katika utumishi wa painia msaidizi. Kwa kweli, wale walio na hali njema ya moyo watasaidiwa na roho ya Yehova kufanya maendeleo na kuwa waabudu wake.—Ufunuo 7:15-17.
[Sanduku/Ramani katika ukurasa wa 9]
NEPALI
Idadi ya Watu -17,712,221
Kilele cha Wahubiri cha 1990 -63
Uwiano, Mhubiri 1 kwa Watu -281,146
Wastani wa Wahubiri Mapainia -10
Idadi ya Makundi -1
Wastani wa Mafunzo ya Biblia -107
Hudhurio la Ukumbusho220
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
NEPALI
INDIA
[Picha katika ukurasa wa 9]
Tamasha ya sokoni katika Kathmandu, Nepali