Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 9/1 kur. 10-14
  • ‘Kupanda kwa Machozi na Kuvuna kwa Kilio cha Shangwe’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Kupanda kwa Machozi na Kuvuna kwa Kilio cha Shangwe’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujifunza Kweli
  • Kuwatunza Ndugu
  • Kufungwa Gerezani Tena
  • Kuhojiwa
  • Kushirikiana Upya
  • Kuanza Mazoezi ya Mtoto
  • Kurudi Japani
  • Kumtolea Yehova Binti Yangu
  • Kumtumikia Mungu Nyakati za Magumu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Je, kwa Kweli Wewe Wathamini Baraka za Yehova?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Hatimaye Familia Yetu Yaungana!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Yehova Huwavuta Wanyenyekevu Kuijua Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 9/1 kur. 10-14

‘Kupanda kwa Machozi na Kuvuna kwa Kilio cha Shangwe’

Kama ilivyosimuliwa na Miyo Idei

“Ninakufa! Ninakufa! Nisaidie!” Baba yangu alikuwa akijikaza kupaza sauti. Sauti yake ilisikika kila mahali nilipokuwa nikikimbia kwenda nje ya nyumba. Ilikuwa usiku wa manane, na baba yangu alikuwa ameshikwa na ugonjwa wa ghafula wa moyo. Nilikimbia mbio kwa mjomba wangu, aliyeishi karibu, lakini tuliporudi, mpigo wa moyo wa Baba haukuweza kusikika tena.

HILO lilitukia siku ya Desemba 14, 1918. Nikiwa mwenye umri wa miaka 13, niliachwa bila wazazi. Mama yangu alikuwa amekufa nikiwa na umri wa miaka 7. Kwa kupoteza wazazi wote wawili mapema sana maishani mwangu, nilianza kuuliza, ‘Kwa nini watu hufa? Ni nini kinachotukia baada ya kifo?’

Baada ya kuhitimu kwenye shule ya walimu, nikawa mwalimu katika Tokyo nikafundisha kwenye Shule ya Msingi ya Shinagawa. Baadaye, mtu niliyemjua akanijulisha kwa mwanamume kijana, Motohiro, ambaye alinioa nilipokuwa mwenye umri wa miaka 22. Kwa miaka 64 iliyopita, tumeshiriki pamoja maono ya maisha mazuri na machungu pia. Upesi tukahamia Taiwani, iliyokuwa chini ya utawala wa Japani wakati huo. Wakati huo sikufikiria kwamba ningekuwa na sababu ya kilio cha shangwe katika nchi hiyo.

Kujifunza Kweli

Katika masika ya 1932, tulipokuwa tukiishi kandokando ya Chiai katika Taiwani ya kati, mwanamume aitwaye Saburo Ochiai alitutembelea. Alionyesha kwamba unabii mbalimbali wa Biblia ulitia ndani ahadi ya ufufuo wa wafu. (Yohana 5:28, 29) Taraja zuri ajabu kama nini! Nilitaka sana sana kuwaona mama na baba yangu tena. Maneno yake yakiwa na hoja za kufuata akili, maelezo yenye maana na ushuhuda thabiti wa Kibiblia, yalionekana kuwa ya kweli. Wakati ulipita haraka tulipopisha siku nzima tukizungumza juu ya Biblia. Kwa ghafula nikaona Biblia kuwa kitabu chenye kuvutia.

Muda mfupi Bw. Ochiai akaondoka kwenda mahali pengine, akituachia vitabu kama vile Creation, Harp of God, Government, Prophecy, Light, na Reconciliation, vyote vikiwa vyatangazwa na Watch Tower Bible and Tract Society. Nikajishughulisha sana katika kuvisoma, na nilipofanya hivyo, nilihisi msukumo wa kuambia wengine yale niliyokuwa nikiyasoma. Ikiwa Yesu alianza huduma yake katika Nazareti mji alimokulia, kwa nini nisianze nilipokuwa nimeishi? Nilimtembelea jirani wangu wa karibu zaidi. Hakuna yeyote aliyenifunza jinsi ya kuhubiri, kwa hiyo nilienda nyumba kwa nyumba na Biblia yangu na vitabu amba-vyo nilikuwa nimesoma, nikihubiri kwa njia bora niwezavyo. Watu waliitikia vizuri na kukubali magazeti. Niliomba Todaisha, kama vile Watch Tower Society ilivyokuwa ikiitwa Japani wakati huo, inipelekee nakala 150 za kijitabu chenye kichwa The Kingdom, the Hope of the World, nikazigawanya.

Siku moja mtu aliyekuwa amekubali vichapo aliniambia kwamba polisi walikuja mara tu nilipoondoka wakamnyang’anya vile vitabu. Muda mfupi tu baada ya hilo, makachero (polisi wapepelezi) wanne wakaja nyumbani kwangu na kuninyang’anya vitabu na magazeti yangu yote. Waliacha Biblia tu. Kwa miaka mitano, sikukutana na yeyote wa watu wa Yehova, lakini bidii na tamaa yangu ya kweli haikupunguka.

Halafu Desemba 1937 ikaja! Makolpota wawili kutoka Japani wakatutembelea. Kwa kustaajabu, niliuliza hivi: “Mlipataje kujua juu yetu?” Wakasema hivi: “Tunalo jina lako hapa hapa.” Yehova alikuwa ametukumbuka! Mashahidi hao wawili Yoriichi Oe na Yoshiuchi Kosaka, walikuwa wameendesha baiskeli kuukuu kwa mwendo wa karibu kilometa 240 kutoka Taipei hadi Chiai, mizigo yao nyuma ikiwa imerundamana mpaka juu. Walipokuwa wakiongea nasi, nilihisi kama towashi Mwethiopia aliyesema hivi: “Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” (Matendo 8:36) Usiku waliofika, mume wangu na mimi tukabatizwa.

Kuwatunza Ndugu

Waliofungwa Gerezani

Katika 1939 kukamatwa kwa Mashahidi wa Yehova kukaanza bila kutazamiwa na kwa ghafula kotekote Japani. Muda mfupi wimbi la mnyanyaso likafika Taiwani. Katika Aprili Ndugu Oe na Kosaka pia wakakamatwa. Miezi miwili baadaye sisi pia tukakamatwa. Kwa kuwa nilikuwa mwalimu, niliachiliwa siku iliyofuata, lakini mume wangu alibaki kizuizini kwa miezi minne. Baada ya mume wangu kuachiliwa, tulihamia Taipei. Kwa kuwa sasa tulikuwa karibu zaidi na gereza ambapo ndugu wale wawili walikuwa wamewekwa, hilo lilithibitika kuwa mpango mzuri.

Gereza la Taipei lilikuwa gereza lenye ulinzi mkali. Nikiwa na mavazi na chakula, nilienda kuona akina ndugu. Kwanza, Ndugu Kosaka alitokea akiwa na mlinzi na kachero nyuma ya dirisha la sentimeta 30 za mraba lenye wavu wa chuma. Alikuwa mwenye kufifia na midomo yake ilikuwa myekundu kama nyanya zilizoiva. Alikuwa amepatwa na ugonjwa wa kifua kikuu.

Halafu Ndugu Oe akaja nje akitabasamu, akirudia-rudia kwa furaha: “Ni vema kwamba uliweza kuja.” Kwa kuwa uso wake ulikuwa wa kimanjano na ulikuwa umefura, nilimuuliza juu ya afya yake. “Mimi ni mzima kabisa!” akajibu. “Mahali hapa ni pazuri. Hamna kunguni wala chawa. Hata naweza kula tambi za ngano. Mahali hapa ni kama tu nyumba yenye bustani,” akasema. Polisi na mlinzi hawakuweza kuzuia kicheko na kusema: “Loo, hatuwezi kumshinda huyu Oe.”

Kufungwa Gerezani Tena

Karibu na usiku-kati wa Novemba 30, 1941, siku chache baada ya kurudi kutoka kuwatembelea hao ndugu, mlango uligongwa-gongwa. Niliona maumbo ya kofia zilizo kama mlima kupitia mlango wa kioo wenye kusukumika upande. Nilizihesabu zikawa nane. Walikuwa mapolisi. Waliingia nyumba yetu kwa nguvu na kupindua kila kitu katika nyumba—lakini bila kupata chochote. Baada ya muda wa saa moja ya kuchokora-chokora kila mahali, walininyang’anya vitabu vyangu vya kuwekea picha wakatuambia tuende nao. Nikakumbuka kwamba Yesu alikamatwa katikati ya usiku. (Mathayo 26:31, 55-57; Yohana 18:3-12) Kuona wanaume wanane wakipoteza wakati juu ya sisi wawili tu kulinichekesha.

Tulipelekwa kwenye jengo tusilolifahamu lililokuwa kubwa na lenye giza. Baadaye tuligundua kwamba lilikuwa Gereza la Taipei Hichisei. Tuliketishwa mbele ya dawati kubwa, na mahoji yakaanza. Tena na tena waliuliza: “Mnajua nani?” na kila mmoja wetu akajibu: “Sijui yeyote.” Tungeweza kujuaje ndugu waliokuwa katika Japani bara? Tuliwajua tu Ndugu Oe na Ndugu Kosaka, nasi hatukuongea juu ya majina yoyote mengine ambayo huenda tukawa tuliyasikia kwa njia isiyo ya moja kwa moja.

Muda mfupi ikawa saa kumi na moja asubuhi, na makachero wawili wakanipeleka kwenye seli yangu. Ilichukua muda kabla ya kuzoea mazingira hayo mapya. Nilikabili kunguni kwa mara ya kwanza maishani mwangu. Wadudu hao wadogo, wakiwa na nia ya kujifurahisha na wageni, walinisumbua pasipo huruma, wakiwaacha kabisa wale wanawake wengine wawili waliokuwa katika seli hiyo—ijapokuwa nilikuwa nimeponda wale walionijia. Mwishowe nikaacha na kuwakubali wafyonze damu yangu.

Chakula chetu kilikuwa nusu kikombe cha uji wa mashendea yasiyopikwa vizuri, lakini mdomo wangu ulisisitiza kuufikiria kuwa mchele mbichi. Pamoja na mashendea hayo kulikuwako kiasi kidogo cha majani ya daikoni (mboga ya Kijapani kama figili) yenye chumvi yakiwa bado na uchafu wa vichangarawe. Mwanzoni, kwa sababu chakula kilinuka na kilikuwa kichafu, sikuweza kukila, na wale wafungwa wengine walikuwa wakija kukila. Bila shaka, polepole nikajirekebisha ili kuokoka.

Maisha gerezani yalikuwa yenye kuhuzunisha. Pindi moja nilisikia mwanamume mmoja aliyedhaniwa kuwa mpelelezi, akilia kwa nguvu siku baada ya siku kwa ajili ya kuteswa. Niliona pia mtu katika seli iliyofuata akifa kwa maumivu makali. Nikiona hayo yote yakitukia mbele yangu, nilitaka sana mfumo huu uishe, na tumaini langu katika ahadi za Mungu likawa lenye nguvu zaidi ya wakati mwingine wowote.

Kuhojiwa

Nilifungiwa gerezani kwa karibu mwaka mmoja nikahojiwa mara tano. Siku moja wakili wa mashtaka alikuja kwa mara ya kwanza, nami nikapelekwa ndani ya chumba kidogo sana cha kuhojia. Jambo la kwanza alilosema ni: “Ni nani aliye mkuu zaidi, Amaterasu Omikami [mungu-mke-jua] au Yehova? Niambie!” Nilifikiria kidogo jinsi ya kujibu.

“Niambie ni nani aliye mkuu zaidi, au nitakupiga!” Akanitazama kwa hasira.

Nikajibu kwa utulivu: “Kwenye mwanzo kabisa wa Biblia, imeandikwa hivi, ‘Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.’” Sikuona uhitaji wa kuongeza jambo lolote. Alinikodolea macho tu usoni bila kusema lolote halafu akabadili habari.

Hata hivyo, sababu ya kufungwa kwangu ilikuwa nini? Rekodi ya uchunguzi ilisema hivi: “Inahofiwa kwamba huenda akapotosha watu kwa maneno na vitendo vyake.” Hiyo ndiyo sababu nilifungiwa bila kuhukumiwa.

Yehova alikuwa karibu nami sikuzote nilipokuwa nikivumilia yote hayo. Kwa fadhili ya Yehova, niliandaliwa kitabu cha ukubwa wa kuchukulia mfukoni cha Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kachero mmoja alikitupa ndani ya seli yangu siku moja, akisema hivi: “Nitakuruhusu uwe na hiki.” Nilikisoma kila siku kufikia hatua ya kujifunza kwa moyo yale niliyokuwa nikiyasoma. Mifano ya ujasiri wa Wakristo wa karne ya kwanza katika kitabu cha Matendo ikawa chanzo kikubwa cha kitia moyo. Barua 14 za Paulo ziliniimarisha pia. Paulo alipatwa na mnyanyaso wa kupita kiasi, lakini roho takatifu ilimtegemeza sikuzote. Maandishi kama hayo yaliniimarisha.

Nikawa mwembamba na dhaifu sana, lakini Yehova alinitegemeza, mara nyingi katika njia zisizotazamiwa. Jumapili moja kachero mmoja ambaye sikuwahi kukutana naye kamwe alikuja na kifurushi kilichofungiliwa kitambaa kidogo. Alifungua mlango wa seli na kunipeleka nje kwenye ua. Tulipofika kwenye mti mkubwa wa kafuri, alifungua kifurushi hicho. Tahamaki! Ndizi na mikate midogo-dogo zilikuwa ndani. Aliniambia nizile hapo. Kachero huyo alisema hivi: “Ninyi nyote ni watu wazuri sana. Hata hivyo twalazimika kuwatendea vibaya hivi. Ningependa kutoka kwenye kazi hii upesi.” Hivyo walinzi na makachero wakaanza kunitendea kwa fadhili. Waliniamini na kuniruhusu kusafisha vyumba vyao na kunipa aina nyingine mbalimbali za kazi zenye mapendeleo.

Karibu na mwisho wa 1942, niliitwa na mmoja wa makachero waliotukamata. “Ingawa unastahili hukumu ya kifo, utaachiliwa leo,” akatangaza rasmi. Mume wangu alikuwa amerudi nyumbani mwezi mmoja hivi kabla ya kuachiliwa kwangu.

Kushirikiana Upya

Pamoja na Mashahidi

Tulipokuwa tungali gerezani, Japani iliingia Vita ya Ulimwengu 2. Halafu, katika 1945, tulisikia kwamba Japani ilikuwa imeshindwa vitani, tukasoma katika magazeti ya habari kwamba wafungwa wa kisiasa wangeachiliwa. Tulijua kwamba Ndugu Kosaka alikuwa amekufa gerezani kwa ajili ya ugonjwa, lakini nilipeleka barua mara moja kwenye gereza katika Taipei, Hsinchu, na miji mingine na kuuliza juu ya mahali alikokuwa Ndugu Oe. Hata hivyo, sikupata jibu lolote. Baadaye nilipata kujua kwamba Ndugu Oe alikuwa ameuawa kwa risasi na kikundi cha askari wenye kutekeleza hukumu ya kifo.

Katika 1948 tulipokea barua isiyotazamiwa kutoka Shanghai. Ilitoka kwa Ndugu Stanley Jones, aliyekuwa ametumwa China kutoka Gileadi, shule ya misionari iliyoanzishwa karibuni na Mashahidi wa Yehova. Yehova alikuwa ametukumbuka tena! Nilifurahi sana kuwa na ukaribu huo pamoja na tengenezo la Yehova. Miaka saba ilikuwa imepita tangu tulipokuwa tumeona Ndugu Oe. Ingawa tulitenganishwa kabisa na Mashahidi wengine wakati huo wote, nilikuwa nimekuwa nikiambia wengine juu ya habari njema.

Ndugu Jones alipotuzuru kwa mara ya kwanza, ulikuwa wakati wa kushangilia. Alikuwa mwenye urafiki sana. Ingawa hatukuwahi kukutana naye kamwe mbeleni, tulihisi kana kwamba tulikuwa tunakaribisha nyumbani mwetu mtu wa ukoo wa karibu sana. Wakati mfupi tu baada ya hapo, Ndugu Jones aliondoka kwenda T’ai-tung, ng’ambo ile nyingine ya milima, mume wangu akiwa mkalimani wake. Walirudi baada ya juma moja, wakati ambao walikuwa na kusanyiko la siku moja na watu 300 wa kutoka kabila ya Amis ya mashariki mwa pwani wakabatizwa.

Ziara ya Ndugu Jones ilikuwa yenye maana kwangu katika njia nyingine. Nilikuwa nimekuwa nikihubiri mwenyewe mpaka wakati huo. Na sasa wenzi wa ndoa, mume akiwa ndiye mwenye nyumba yetu, walibatizwa wakati wa ziara ya Ndugu Jones. Tangu wakati huo, nimekuwa nikionea shangwe ya kufanya wanafunzi pamoja na shangwe ya kutangaza rasmi Ufalme. Baadaye tukahamia Hsinchu, ambapo Ndugu Jones alitutembelea mara tatu, kila wakati kwa majuma mawili. Nilionea shangwe sana ushirika huo wenye manufaa. Kwa pindi ya mwisho alisema hivi: “Wakati ujao nitaleta mwenzangu, Harold King.” Lakini “wakati ujao” huo haukufika, kwa maana upesi baada ya hapo wote wawili walifungwa gerezani huko China.

Katika 1949, Joseph McGrath na Cyril Charles, wamisionari kutoka darasa la 11 la Gileadi, walifika Taiwani. Walipanua kazi katika Taiwani, wakitumia nyumba yetu kuwa kitovu cha utendaji. Mifano yao ilinitia moyo sana. Hata hivyo, hali ya kisiasa iliwalazimu waondoke kwenda Hong Kong. Sikuweza kuzuia machozi yangu yasitoke walipoondoka wakiwa na polisi. “Usilie, Miyo,” akasema Joe. Akaongeza hivi: “Asante,” akanipa kalamu yake ya wino iliyokuwa imetumiwa sana kuwa ukumbusho.

Kuanza Mazoezi ya Mtoto

Mume wangu nami hatukuwa na watoto wowote, kwa hiyo tulimchukua mpwa wa kike wa mume wangu kuwa mtoto wetu akiwa na umri wa miezi minne. Uhai wa mama yake ulihatarishwa na ugonjwa wa pumu.

Katika 1952, Ndugu Lloyd Barry, aliyekuwa akitumikia akiwa misionari katika Japani, alitembelea Taiwani kutafuta utambuzi wa kisheria kwa ajili ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Alikaa nasi na kututia moyo sana. Wakati huo binti yetu alikuwa mwenye umri wa miezi 18. Alimwinua na kumuuliza: “Jina la Mungu ni nani?” Kwa mshangao, nikamuuliza: “Wamaanisha tunapaswa kumfundisha akiwa mchanga hivi?” “Ndiyo,” akajibu kwa uthabiti. Kisha akaniambia juu ya umaana wa kuzoeza mtoto kutoka miaka ya uchanga sana. Maneno yake: “Yeye ni zawadi kutoka kwa Yehova kuwa kitulizo chako,” yalibaki akilini mwangu.

Mara moja nikaanza kumzoeza binti yangu, Akemi, kumjua na kumpenda Yehova na kuwa mtumishi wake. Nilimfundisha herufi za matamshi, nikianza na herufi tatu e, ho, na ba zinazofanyiza neno “Ehoba,” au Yehova katika Kijapani. Alipofika miaka miwili, aliweza kuelewa yale niliyokuwa nikimwambia. Kwa hiyo kila usiku kabla ya kulala, nilimwambia hadithi za Biblia. Alisikiliza kwa upendezi na kuzikumbuka.

Alipokuwa mwenye umri wa miaka tatu na nusu, Ndugu Barry alitembelea tena na kumpa Akemi Biblia ya Kijapani cha kimaongezi. Alitembea kuzunguka chumba akiwa na Biblia, akisema: “Biblia ya Akemi! Biblia ya Akemi!” Halafu dakika chache baadaye, akasema ghafula: “Biblia ya Akemi haina Yehova! Mimi sitaki hii!” Akaitupa chini. Kwa mshtuko, nikachungulia yaliyomo. Kwanza nilifungua Isaya sura 42, mstari 8. Hapo neno “Bwana” lilikuwa limewekwa mahali pa jina Yehova. Nilifungua maandiko mengine, lakini sikuweza kupata jina la kimungu, Yehova. Akemi alitulizwa nilipomwonyesha tena jina la Yehova katika Biblia yangu ya zamani, iliyokuwa katika Kijapani cha kale.

Kurudi Japani

Tulirudi Japani katika 1958 na kushiriki pamoja na kundi la Sannomiya katika Kobe. Nikiwa na sababu nyingi sana za kumshukuru Yehova, nilitaka kuonyesha shukrani hiyo kwa kuwa painia—mtumishi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Nilijitahidi mwenyewe katika utumishi wa upainia. Tokeo likawa kwamba niliweza kuongoza mafunzo mengi ya Biblia nyumbani nikaona shangwe ya kusaidia watu kama 70 hadi 80 waingie katika kweli. Kwa muda fulani nilipendelewa hata kutumikia nikiwa painia wa pekee, nikifanya saa zaidi ya 150 kila mwezi shambani, hali pia nikiwatunza mume na binti yangu.

Kwa kuwa tulikuwa tumeishi katika Taiwani kwa miaka zaidi ya 30, maisha ya utamaduni katika Japani yalikuwa ya kushtusha, nami nilipatwa na mambo mengi yenye kujaribu. Katika nyakati hizo Akemi akawa kitulizo na utegemezo wangu, kama vile tu Ndugu Barry alikuwa ameniambia miaka mingi mbeleni. Niliposhuka moyo, yeye alikuwa akiniambia: “Mama, jipe moyo. Yehova atatokeza njia.” “Ndiyo, atafanya hiyo, sivyo?” niliweza kujibu na kumkumbatia kwa nguvu. Chanzo kilichoje cha kitia moyo! Ningekosaje kumshukuru Yehova!

Kumtolea Yehova Binti Yangu

Akemi alikuwa mhubiri alipokuwa mwenye umri wa miaka 7 akabatizwa alipokuwa na miaka 12, katika kiangazi cha 1963. Nilijaribu kupisha wakati mwingi iwezekanavyo pamoja naye. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Kulikuwako nyakati ngumu wakati alipokuwa katika ubalehe, lakini kukiwa na mifano mizuri na kitia moyo kutoka mapainia wa pekee waliotumwa kundi letu, Akemi alifanya kupainia katika maeneo mapya kuwa mradi wake.

Kwenye mkusanyiko wa wilaya katika 1968, aliigiza binti ya Yeftha katika drama (mchezo wa kuigiza) ya Biblia. Nilipokuwa nikitazama drama hiyo, niliamua, kama Yeftha alivyokuwa amefanya, kumtolea Yehova binti yangu wa pekee, ambaye nilikuwa nimempenda sana mpaka wakati huo, kwa ajili ya utumishi wa wakati wote. Maisha yangekuwaje bila kuwa na binti yangu karibu? Huo ulikuwa mwito wa ushindani, kwa kuwa nilikuwa tayari mwenye umri wa miaka zaidi ya 60.

Katika 1970 wakati wa binti yangu kutuacha ukafika. Alipata ruhusa kutoka kwa mume wangu akaenda Kyoto kutumikia akiwa painia. Akiwa anaelewa hisia zetu, ilionekana kama kwamba alikuwa akituonea huruma alipokuwa akituacha. Nilinukuu Zaburi 126:5, 6 kuwa andiko la kumwaga: “Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha [kilio cha shangwe, NW]. Ingawa mtu anakwenda zake akilia, azichukuapo mbegu za kupanda. Hakika atarudi kwa kelele za furaha, aichukuapo miganda yake.” Maneno hayo yalithibitika kuwa yenye kitia moyo kwangu pia.

Baadaye Akemi aliolewa akaendelea kufanya upainia wa pekee pamoja na mume wake. Tangu 1977, mume wake alipopewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko, wamekuwa wakitumikia katika kazi ya kusafiri. Kwa kawaida huwa ninafungua wazi ramani na “kusafiri” kwenye ramani pamoja na binti yangu. Ni furaha yangu kusikia mambo waliyoona na kufahamiana na dada wengi kupitia binti yangu.

Tayari nina umri wa miaka 86. Siku ambazo zimepita zaonekana kuwa kama zamu moja tu ya kulinda wakati wa usiku. Siwezi kufanya kazi nyingi kadiri nilivyokuwa nikifanya mbeleni, lakini utumishi wa shambani ungali waniletea shangwe. Ninapotafakari juu ya miaka 60 ambayo imepita tangu nilipojifunza kweli, Ahadi ya Mungu yenye kutumainisha hububujika moyoni mwangu. Naam, Yehova atakayetenda kwa ushikamanifu na walio washikamanifu anatuacha tuvune shangwe kwa wingi.—Zaburi 18:25.

[Picha of Miyo Idei katika ukurasa wa 10]

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki