Je, kwa Kweli Wewe Wathamini Baraka za Yehova?
KENICHI, mwanamume wa makamo, alizuru duka fulani la dawa ili kupata dawa ya mafua kidogo. Alipomeza hiyo dawa, mwili wake wote ulipatwa na mizio isababishayo vipele vyenye kuwasha na malengelenge yenye majimaji. Haishangazi kwamba, Kenichi alianza kushuku ikiwa mwenye duka hilo la dawa alikuwa ametolea uangalifu wa kutosha mahitaji yake.
Huenda watu fulani wakamfikiria Yehova Mungu kama vile Kenichi alivyomwona mwenye hilo duka la dawa. Wanashuku kwamba Mungu mweza-yote, Yehova, kwa kweli apendezwa na sisi binafsi. Ingawa wanatambua kwamba Mungu ni mwema, hawasadikishwi kwamba yeye hutujali sisi tukiwa watu mmoja-mmoja. Hilo ni kweli hasa wakati ambapo mambo si shwari au kushikamana kwao na kanuni za Biblia kufuatwapo na matatizo magumu. Kwa sababu ya kukosa ufahamu, wanaona matatizo yao kama vipele vyenye kuwasha na malengelenge ambayo Kenichi alipata bila kutarajia, kana kwamba kwa njia fulani ni kosa la Mungu.—Mithali 19:3.
Yehova hapaswi kulinganishwa na wanadamu wasiokamilika. Wanadamu wamepungukiwa katika ujuzi na uwezo. Wanashindwa kufahamu kikamili mahitaji halisi ya wengine, kama alivyofanya mwenye duka la dawa alikokwenda Kenichi. Kinyume cha hivyo, hakuna kitu kisichoonekana kwa macho ya Yehova. Mara nyingi Yehova hutusaidia bila sisi kufahamu wala kuthamini jambo hilo kwa sababu tuna mwelekeo wa kukazia fikiria vitu ambavyo hatuna na kupuuza baraka nyingi tulizo nazo. Badala ya kuwa wenye haraka kumlaumu Yehova kwa sababu ya matatizo yoyote tukabiliyo, twapaswa kujaribu kufahamu baraka tuoneazo shangwe kutoka kwa Yehova.
Kulingana na Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary, “baraka” yaweza kufasiliwa kuwa “kitu kiletacho furaha au hali njema.” Je, wathamini kwamba ni kweli hasa kwa habari ya baraka kutoka kwa Yehova?
Mwandalizi Asiye na Kifani
Mke asemapo kwamba mume wake ni mwandalizi mwema, kwa kawaida yeye humaanisha kwamba mume wake huhangaikia vya kutosha mahitaji ya familia, akiandaa chakula cha kutosha, makao, na mavazi ili familia iwe na furaha na hali njema. Yehova ni mwema kadiri gani akiwa Mwandalizi wetu? Tazama kwa ukaribu sayari yetu Dunia, makao ya mwanadamu. Iko kilometa 150,000,000 kutoka lilipo jua, umbali ufaao kwa ajili ya halijoto za kiasi zifanyazo uhai uwezekane duniani. Ule mwinamo wa digrii 23.5 wa tufe letu umebuniwa kikamilifu, ukitokeza majira yenye kutofautiana yachangiayo mavuno mengi. Tokeo ni kwamba, dunia hulisha watu zaidi ya bilioni tano. Kwa kweli, Yehova ni Mwandalizi wa ajabu!
Isitoshe, Biblia hutuhakikishia kwamba Yehova anapendezwa sana nasi tukiwa watu mmoja-mmoja na pia anapendezwa na hali njema yetu. Ebu fikiria, Yehova ajua kila moja ya mabilioni ya nyota kwa jina, na hakuna mbayuwayu hata mmoja aangukaye kwenye ardhi bila yeye kujua. (Isaya 40:26; Mathayo 10:29-31) Yeye huwajali kwa kadiri kubwa zaidi kama nini wanadamu wampendao na walionunuliwa kwa damu yenye thamani ya Mwana wake mpendwa, Yesu Kristo! (Matendo 20:28) Yule mtu mwenye hekima alitangaza vema: “Baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.”—Mithali 10:22.
Baraka Zitutajirishazo
Twapaswa kuwa wenye shukrani kwa sababu tuna kitu fulani chenye thamani kubwa. Hicho ni nini? Biblia hukitambulisha isemapo hivi: “Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu, kuliko maelfu ya dhahabu na fedha.” (Zaburi 119:72; Mithali 8:10) Sheria ya Yehova yapaswa kutamaniwa zaidi sana, hata kuliko dhahabu yenye thamani kubwa. Ujuzi sahihi wa sheria yake pamoja na ufahamu wenye kina na ufahamu ambao Yehova hutolea watafutaji wa kweli wenye moyo mweupe ni vitu vipaswavyo kuthaminiwa. Hivyo hutuandalia vifaa vya kujilinda wenyewe, vya kukabiliana na hali zilizo ngumu, na vya kushughulika na matatizo kwa mafanikio, na hivyo kuridhika na kuwa wenye furaha.
Hilo ni kweli kuhusu hata wale wachanga kabisa. Fikiria jinsi msichana mdogo alivyotatua matatizo yake kwa kufuata sheria ya Yehova. Huyo msichana, Akemi, huishi karibu na Tokyo. Baba na mama yake walitumia kanuni za Biblia katika kumzoeza na kwa neno na kielelezo walimsaidia binti yao asitawishe upendo kwa Yehova na kwa jirani. Wakiona kimbele matatizo ambayo angekabili shuleni, walijaribu kumtayarisha katika njia bora walivyoweza. Hata hivyo, Akemi alipoingia shule ya msingi alionwa na baadhi ya wanafunzi wenzake kuwa “tofauti” kwa sababu alisali kabla ya milo na aliepuka utendaji mbalimbali usio wa Kimaandiko kwa kudhamiria. Upesi akaanza kusumbuliwa na kikundi cha wakandamizaji ambao wangemzingira baada ya shule na kumzaba makofi usoni, kuipopotoa mikono yake, na kumdhihaki.
Akemi mchanga hakulipiza kisasi, wala hakujikunyata mbele ya watesi wake. Badala ya hivyo, alijaribu kutumia aliyokuwa amejifunza. Tokeo la mwenendo wake mzuri na moyo mkuu wake ni kwamba, alistahiwa na wengi wa wanafunzi wenzake. Walimjulisha mwalimu jambo hilo, na tangu siku hiyo, Akemi hajatendewa vibaya shuleni.
Ni nini kilichomsaidia Akemi kushughulika kwa mafanikio na hali ngumu? Ujuzi sahihi, ufahamu wenye kina, na hekima kutoka kwa Yehova ambayo wazazi wake walikuwa wamekaza kikiki ndani yake. Alifahamu vizuri uvumilivu wa Yesu, nao ulimsukuma aige kielelezo chake. Biblia ilimsaidia afahamu kwamba watu fulani hufanya makosa kwa sababu ya kutokuwa na ujuzi, na hilo lilimtia moyo kuchukia makosa ambayo wakandamizaji hao walifanya wakati uleule kutowachukia watu wenyewe.—Luka 23:34; Waroma 12:9, 17-21.
Bila shaka, hakuna wazazi ambao wangetaka kumwona mtoto wao akidhihakiwa na kutendewa vibaya. Hata hivyo, waweza kuwazia jinsi wazazi wa Akemi walivyohisi waliposikia mambo yote yaliyotokea. Watoto kama hao kwa kweli ni baraka kutoka kwa Yehova.—Zaburi 127:3; 1 Petro 1:6, 7.
Kumngojea Yehova kwa Subira
Ingawa hivyo, nyakati nyingine lazima ungoje wakati wa Yehova kabla ya kupokea baraka zake. Yehova ajua hali yako na huandalia kila uhitaji wakati ambapo utakufaa zaidi. (Zaburi 145:16; Mhubiri 3:1; Yakobo 1:17) Huenda ikawa wewe hupenda kula tunda, lakini ungefikirije juu ya mkaribishaji ambaye angekupa tunda kabla halijawa tayari kuliwa? Liwe tofaa, chungwa, au tunda jinginelo, ungependelea tunda bivu, lenye maji mengi, na lililo tamu. Vivyo hivyo, Yehova huandaa unachohitaji katika wakati ufaao—si mapema sana wala kuchelewa mno.
Kumbuka kisa cha Yosefu. Kwa kosa lisilo lake, alijikuta katika gereza la Misri. Mfungwa mwenzake, mnyweshaji wa Farao, alitumainia kuachiliwa na aliahidi kumjulisha Farao juu ya kisa cha Yosefu. Lakini baada ya kuachiliwa kwake alisahau mambo yote juu ya Yosefu. Ilionekana kana kwamba Yosefu alikuwa ameachwa. Hata hivyo, miaka miwili kamili baadaye, hatimaye aliachiliwa kutoka gerezani na mwishowe kufanywa kuwa mtawala wa pili katika Misri. Badala ya kutokuwa na subira, Yosefu alimngojea Yehova. Kwa sababu ya hilo, alibarikiwa katika njia iliyomaanisha kuokoa uhai wa Waisraeli na wa Wamisri.—Mwanzo 39:1–41:57.
Masashi alikuwa mzee katika kutaniko fulani la kaskazini mwa Japani. Hakuwa gerezani, lakini ilimbidi kumngojea Yehova. Kwa nini? Tangu Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, shule ya kuwazoeza wahudumu Wakristo wenye sifa za kustahili, ilipoanzishwa Japani, alifanya mradi wake mkubwa uwe kuihudhuria. Alisali kwa juhudi nyingi juu ya pendeleo hilo. Painia mwenzake alialikwa, lakini ijapokuwa tamaa yake yenye hamu, Masashi hakualikwa. Alitamaushwa sana.
Hata hivyo, alichukua hatua za kukabiliana na hisia zake. Alijifunza Biblia na vichapo vilivyochapishwa na Watch Tower Society, akikazia fikira mambo kama vile kuwa mnyenyekevu na kudhibiti hisia zake. Alirekebisha kufikiri kwake na hivyo akaona uradhi zaidi katika mgawo wake. Kisha, bila kutarajia hata kidogo, alipokea mwaliko wa kuhudhuria hiyo shule.
Akiwa amesitawisha sifa kama vile subira na unyenyekevu, alinufaika zaidi kutokana na hiyo shule. Baadaye, Masashi alipewa pendeleo la kutumikia ndugu zake akiwa mwangalizi asafiriye. Ndiyo, Yehova alijua alichohitaji Masashi na akakiandaa wakati tu ambao kingetimiza mema zaidi.
Tafuta Baraka Zake
Kwa sababu hiyo, Yehova si kama yule mwenye duka la dawa. Ingawa huenda tukakosa kufahamu utunzaji na hangaiko la Yehova, fadhili zake huja katika njia tofauti-tofauti—katika nyakati na katika njia ambazo zatufanyia mema zaidi. Kwa hiyo endelea kutafuta baraka zake. Kumbuka kwamba tayari una sababu nyingi za kuwa mwenye shukrani. Umebarikiwa na maandalizi ya msingi ili uendelee kuishi duniani. Umepewa ujuzi juu ya Yehova na njia zake kamilifu. Umepewa ufahamu wenye kina. Na umejipatia ufahamu. Yote hayo huchangia hali njema na furaha yako.
Ili kujionea kikamili hata zaidi baraka za Yehova, endelea kujifunza Biblia kwa ukawaida. Mwombe Yehova kwa bidii ili akusaidie uelewe na kutumia mafundisho yaliyo kama vito kutoka katika Neno lake lililopuliziwa. Yatakutajirisha kwelikweli, hivi kwamba hutakosa kitu. Ndiyo, yatamaanisha furaha na uradhi wako sasa na uhai kwa wingi katika ulimwengu mpya ujao.—Yohana 10:10; 1 Timotheo 4:8, 9.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Baraka ya Yehova ni yenye thamani zaidi ya dhahabu