Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 9/15 kur. 28-30
  • Vielezi Ufunguo wa kufikia mioyo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vielezi Ufunguo wa kufikia mioyo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Vielezi Vifundishavyo
  • Kupata Vielezi
  • Kuifanya Biblia Iwe Hai
  • “Hakuwa Akisema Nao Bila Mfano”
    ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
  • “Bila Kielezi Hakuwa Akisema Nao”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Mifano Inayofundisha
    Boresha Uwezo Wako wa Kusoma na Kufundisha
  • Mwige Mwalimu Mkuu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 9/15 kur. 28-30

Vielezi Ufunguo wa kufikia mioyo

DAUDI amekuwa akikimbia aponye uhai wake. Adui yake ni Sauli, Mfalme wa Israeli aliyepakwa mafuta. Hata hivyo, Sauli ni mwanamume mwenye kujaa chuki kwa Daudi, mwenye kuliwa kabisa na wivu. Katika jitihada yake ya uuaji, sasa mfalme ameambatana na askari 3,000. Wakiwa wamezidiwa sana idadi, Daudi na wanaume wake wamejificha ndani sana ya pango jangwani.

Daudi na wanaume wake wasongamanapo pamoja gizani, hali yageuka kuwa ya kushangaza. Mfalme Sauli aingia ndani ya pango lilo hilo ajipumzishe. Daudi amjia kwa utulivu adui yake aliye hoi, ameshika silaha mkononi. Lakini kwa mshangao wa wanaume wa Daudi, yeye hamwui mfalme. Akata tu rinda la vazi la Sauli. Akijuta hata kwa kufanya hivyo, Daudi asema: “Hasha! nisimtendee bwana wangu, masihi wa BWANA [Yehova, NW], neno hili, kuunyosha mkono wangu juu yake, kwa maana yeye ni masihi wa BWANA [Yehova, NW].”—1 Samweli 24:1-6.

Usimulizi huo wa Biblia wafundisha somo lenye maana kubwa juu ya kustahi mamlaka iliyopewa na Mungu. Pia laufikia moyo, labda hata kwa matokeo zaidi ya shauri lenye kutolewa moja kwa moja. Hivyo ndivyo yalivyo na nguvu masimulizi yaliyoandikwa katika Neno la Mungu kwa agizo letu.—Warumi 15:4.

Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufanya mengi kuliko kutaja mambo ya uhakika tu wahubiripo habari njema, kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani, kutoa hotuba za Kimaandiko, au kutoa ushahidi wa vivi hivi. Wao hujaribu kufikia mioyo kwa kusimulia mambo yaliyoonwa na kutumia vielezi. Kitabu chao Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi hueleza hivi: “Mifano inaamsha kupendezwa na kukazia mawazo ya maana. Inaamsha fikira za mtu na kufanya iwe vyepesi kufahamu mawazo mapya. Mifano iliyochaguliwa vizuri inaunganisha mvuto wa akili pamoja na mkazo wa moyoni. . . . Pindi nyingine, mfano waweza kutumiwa ili kuepuka chuki isiyo na sababu nzuri.”a—Ukurasa 168.

Katika kitabu chake Essentials of Public Speaking, Warren DuBois aandika hivi: “Mwandikaji au msemaji akieleza mawazo yake kama yatendwavyo au kusemwa na wanadamu, hapo hata habari isiyochangamsha sana huingiwa na uhai na uvutio.” Hivyo, kuongeza uhai na uvutio kwenye ujumbe ambao tayari ni wa kuchangamsha na wenye kutolea uhai hakika kutasaidia wahudumu Wakristo waufikie moyo.

Vielezi Vifundishavyo

Ni kielezi cha jinsi gani kiwacho na matokeo zaidi? Kwa kawaida, ni kile chenye msingi wa jambo fulani ambalo wasikilizaji waweza kuelewa kwa urahisi. Yesu Kristo aliweka kielelezo kizuri kwa habari hiyo. Katika Mahubiri yake Mlimani, Yesu alisema juu ya vitu vya kawaida kama chumvi, taa, na ndege. (Mathayo 5:1–7:29) Mathalani, kila mtu alifahamu taa zilizotumia mafuta ya mzeituni ambazo nyakati fulani ziliwekwa juu ya kinara cha taa. Kwa hiyo, ni lazima wanafunzi wa Yesu wawe waling’amua kwamba walipaswa kuwa wachukuaji wa nuru ya kiroho alipowaambia hivi: “Watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:15, 16) Vielezi visivyotatanika ambavyo vyafaa habari vitasaidia wa-hudumu Wakristo waeleweshe mawazo na mafundisho ya Biblia waziwazi.

Labda vielezi vya Yesu vilivyo na nguvu nyingi zaidi ni vile vilivyokaza fikira juu ya watu. Fikiria vile vilivyoandikwa katika Luka sura 15 na 16. Waandishi na Mafarisayo walikuwa wamechambua Yesu kwa kupokea watenda dhambi na watoza kodi. Kwa kujibu, yeye alisimulia hadithi za kugusa moyo zilizohusu watu. Alisema juu ya mchungaji aliyempata kondoo wake aliyepotea, mwanamke aliyepata sarafu iliyopotea, mwana mpotevu aliyerudi nyumbani, na wakili asiye mwadilifu.

Vielezi vinavyolingana na hali halisi na mambo yaliyoonwa kikweli maishani vyaweza kuwa vyenye mafaa sana kwa mhudumu Mkristo. Kwa kielelezo, angalia jinsi Alexander H. Macmillan, aliyesafiri sana akiwa mhutubu wa watu wote kwa miaka 60, alivyoeleza kweli ya Biblia juu ya wafu. Muda mfupi kabla ya kifo cha baba yake, aliyeamini kwamba nafsi haifi kamwe, Macmillan alifanya maongezi haya na yeye:

“Baba yangu aliniuliza swali hili la moja kwa moja: ‘Mwanangu, je! mimi nitakuwa mpweke kaburini nikingojea ufalme uanze kazi yao ya kujaza dunia ukamilifu?’

“Hilo lilikuwa swali ambalo mwanamume kijana hangeweza kujibu kwa utayari mpaka atosheleze mtu mzee-mzee asiyepata kamwe kufikiria mambo kwa njia hiyo.

“Kwa kujibu mimi nikamwuliza: ‘Baba, ulilala vema usiku?’

“Yeye akajibu, ‘Ndiyo, mwanangu, nililala baada ya daktari kunipa vibonge vya kulala.’

“‘Je! ulikuwa mpweke ulipokuwa umelala?’

“‘Sivyo. Laiti ningeweza kulala wakati wote, maana hapo sihisi maumivu yoyote.’”

Ndipo A. H. Macmillan akamsomea baba yake Ayubu 14:13-15 na 3:17-19 na kusema: “Hivyo basi waona, baba, wafu wamo katika usingizi wa kina kirefu na hawajui lolote wakiwa katika hali hiyo, hivyo basi wangewezaje kuwa wapweke?”

Lo, ufundishaji wenye matokeo kama nini! Ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, wewe pia waweza kutumia maandiko na vielezi kuvuta akili na moyo.

Kupata Vielezi

Lakini ni wapi uwezapo kupata vielezi vyenye matokeo au mambo yaliyoonwa kikweli maishani? Mengi yaweza kutolewa katika akiba yako ya hazina za mambo yaliyokupata kibinafsi. Mathalani, je! wahitaji kuonyesha baraka za imani, nguvu ya sala, au shangwe ya huduma? Ikiwa wewe ni Mkristo aliyejiweka wakfu, yaelekea ungeweza kusimulia matukio mbalimbali katika maisha yako mwenyewe. Huenda ukasikia kwenye mkutano fulani wa kundi mambo mazuri yaliyoonwa au wakati unapoongea na Wakristo wenzako. Au huenda ukasoma jambo lililoonwa lenye kutia moyo katika Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova. Kwa kweli, Watch Tower Publications Index (Faharisi) huandaa mpato wa mambo yaliyoonwa yakiwa yamepigwa chapa kutoka sehemu zote kuzunguka ulimwengu.

Waweza kusimuliaje kwa matokeo mazuri juu ya jambo lililoonwa? Kwanza, kuandalia hamu ya kutazamia yanayofuata hukusaidia ushike uangalifu wa wasikilizaji wako. Ungeweza kutoa dibaji ya jambo lililoonwa kwa kusema: “Painia mmoja alijifunza yeye mwenyewe jinsi Yehova abarikivyo wale wamtumainio.” Mara hiyo, wasikilizaji wako hujiuliza mhubiri huyo wa wakati wote wa Ufalme alionea shangwe mibaraka gani. Hakikisha kuwaambia.

Jaribu kusimulia jambo lililoonwa kwa maneno yako mwenyewe. Andaa maelezo madogo-madogo, kwa maana kufanya hivyo huiongezea hadithi uthabiti. Kwa kudhihirisha maelezo wazi juu ya hali zihusikazo, waweza kuchochea wasikilizaji wako kwa urahisi zaidi. Lakini hakikisha kwamba huhusiki katika kusimulia sana hadithi hivi kwamba wao washindwa kuelewa kwa nini unasimulia jambo hilo lililoonwa. Pia, epuka kutia chumvi, kwa maana ingawa kufanya hivyo huenda kukafanya hadithi ipendeze zaidi, kwaweza kupunguza kuaminika kwako. Kwa sababu iyo hiyo, epuka kusimulia uvumi au kusimulia mambo yaliyoonwa usiyoweza kuhakikisha.

Kuifanya Biblia Iwe Hai

Mambo yaliyoonwa yaliyo yenye kuagiza zaidi hupatikana katika Biblia yenyewe. Kwa kielelezo, tuseme wataka kuonyesha mwanafunzi wa Biblia au wasikilizaji fulani kwamba watoto waweza kuchukua msimamo upande wa Yehova Mungu. Ungeweza kuamua kutumia usimulizi wa yule msichana asiyetajwa jina aliyemwambia mke wa Naamani juu ya Elisha nabii wa Yehova. Kwanza, soma usimulizi kwenye 2 Wafalme 5:1-5. Halafu ungeweza kuuliza: “Wewe wafikiri ilikuwa vigumu kadiri gani kwa msichana huyo kudumisha uaminifu wa kimaadili katika bara la ibada bandia? Je! moyo mkuu haukuhitajiwa ili yeye aongee kwa usadikisho juu ya Yehova na nabii wake?”

Kutangulia kufanya utafiti huenda kukawa kulikusaidia kutia uhai katika usimulizi huo. Huenda ukawa ulipata habari zenye msaada “katika faharisi zilizo katika vichapo fulani vya Watch Tower.” Marejezo-mlingano katika Biblia fulani-fulani huenda yakawa yalikuongoza kuanzia usimulizi ulio katika 2 Wafalme hadi Zaburi 148:12, 13, ambapo twasoma hivi: “Vijana waume, na wanawali, wazee, na watoto; na walisifu jina la BWANA [Yehova, NW], maana jina lake peke yake limetukuka; adhama yake i juu ya nchi na mbingu.” Lo, ni kitia-moyo kilichoje kwa vijana kunena neno la Mungu kwa ujasiri!—Matendo 4:29-31.

Ikiwa wewe ni mhudumu Mkristo, ‘jitunze nafsi yako, na mafundisho yako’ kwa habari hiyo. (1 Timotheo 4:16) Usisimulie lililo kweli tu—litolee kielezi. Fanya masimulizi ya Biblia yadhihirike wazi na yawe yenye maana. Tumia mambo yaliyoonwa na vielezi vinavyofaa. Hizo ni njia za kufikia moyo.

[Maelezo ya Chini]

a Kimetangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kama Yesu wahudumu Wakristo wa kisasa waweza kutumia vielezi dhahiri ili kueleza ujumbe wao na kufikia mioyo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki