Je! Kisasi Ni Kibaya?
Kwenye barabara moja ya mwendo wa hiari huko United States, gari moja lilichukua muda mrefu kuondokea jingine ili lipite. Dereva wa gari hilo la pili alilipiza kisasi kwa kupiga risasi gari lililofanya kosa hilo, akimwua abiria asiyekuwa na hatia.
Msichana mmoja tineja alishindwa na mwingine katika kupata sehemu katika mchezo wa kuigiza wa shule. Alilipa kisasi kwa kumwambia rafiki-mvulana wa msichana huyo kwamba msichana huyo alikuwa akionana na mvulana mmoja katika shule nyingine. Hivyo akaharibu uhusiano wa msichana huyo na rafiki-mvulana huyo.
WATU wengi huona kwamba wana haki ya kulipa kisasi wanapofikiri wametendewa vibaya. Kwa njia moja au nyingine, wao hufuata maneno haya: “Usikasirike, bali lipa kisasi tu.” Leo, upendo wa jirani umepungua sana, na roho ya kisasi inazidi kuongezeka.—Mathayo 24:12.
Lakini, wewe huonaje kisasi? Ikiwa unaamini Biblia, labda wahisi kwamba kwa msingi kisasi ni kibaya. Lakini kuishi katika ulimwengu usiomhofu Mungu kama tuishivyo, huenda ukahisi kwamba msamaha, kinyume cha kulipa kisasi, mara nyingi si jambo lenye kutumika. Wewe ungetendaje ikiwa ungedanganywa au kushambuliwa kwa kuviziwa? Mtu akikupuuza au kukuharibia sifa kwa wengine, je, wewe hulipa kisasi? Je! wewe ni mwenye kutaka kulipa kisasi au ni mwenye kusamehe?
Mwelekeo wa Kutaka Kulipa Kisasi Huumiza
Bila shaka, kuna kadiri za kosa. Lakini watu wengi wanaotaka kulipiza kisasi hawajaviziwa au kushambuliwa kihalifu. “Makosa” yaliyonukuliwa mwanzoni mwa makala hii hayakuwa makubwa sana, ingawa yalionekana kuwa makubwa katika akili za wale walioamua kulipiza kisasi.
Biblia husema kwamba hatupaswi kusitawisha mwelekeo wa kulipa kisasi. Mithali 24:29 hushauri hivi: “Usiseme, Nitamtenda kama alivyonitenda mimi; nitamlipa mtu huyo sawasawa na tendo lake.” Kwa nini? Kwanza, mwelekeo kama huo ni wenye uharibifu kihisiamoyo na kimwili. Mawazo ya kutaka kulipa kisasi huondoa amani ya akili na huzuia kusababu kuzuri. Angalia ripoti hii ya habari: “Wakulima wawili waliokuwa wakifyatuliana risasi wakiwa katika pikapu zao waliuana kwenye maegesho, wakakomesha uadui wa miaka 40 ulioanza walipokuwa watoto.” Ebu wazia, katika maisha yao yote kufikiri kwa wanaume hao wawili kulikuwa kumepotoshwa na roho yenye uchungu, ya kutaka kulipa kisasi!—Mithali 14:29, 30.
Sababu nyingine ya kutositawisha roho ya kutaka kulipa kisasi ni kwamba wenye kufanya makosa—hata wenye kufanya makosa mazito—waweza kubadilika. Kwa mfano, wakati mmoja mtume Paulo ‘aliona vema kwa kuuawa’ kwa mwanafunzi Stefano naye ‘alitisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana.’ Lakini alibadilika. Miaka mingi baadaye mtume Petro—ambaye uhai wake ulihatarishwa na Paulo wakati ule wa mapema zaidi—alimwita “ndugu yetu mpenzi Paulo.” (Matendo 8:1; 9:1; 2 Petro 3:15) Wakristo wangalijaribu kulipa kisasi juu ya Paulo, hasa wakati alipokuwa akingojea, akiwa kipofu, huko Dameski. (Matendo 9:3-15) Hilo lingalikuwa kosa lenye kuhuzunisha kama nini!
Kwa hiyo, Paulo angeweza kwa kufaa kushauri hivi, katika Warumi 12:20: “Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe.” Kwa nini? Kwa sababu tukimlipa kisasi adui, tunaimarisha mwelekeo wake na kufanya uadui ulio kati yetu uwe wa daima. Lakini tukifanya mema kwa mtu anayetuudhi au kutuumiza, huenda tukalainisha mwelekeo wake na kumfanya aliyekuwa adui kuwa rafiki.
Kutambua udhaifu wetu wenyewe kwasaidia pia katika kushinda uchungu unaoongoza kwenye kutaka kulipa kisasi. Mtunga zaburi aliuliza hivi: “BWANA [Yehova, NW], kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Sisi sote tumeumiza au kuudhi wengine. Je! hatukufurahi ikiwa hawakujaribu kulipa kisasi? Basi sisi, hatupaswi kutenda kwa kujizuia vivyo hivyo? Yesu alishauri hivi: “Yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii.”—Mathayo 7:12.
Ni kweli, Biblia husema: “Uchukieni uovu.” (Zaburi 97:10; Amosi 5:15) Lakini haituambii tumchukie mtu anayefanya uovu huo. Kwa kweli, Yesu alituamuru hivi: “Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi.” (Mathayo 5:44) Tukilipa dhara kwa dhara, tunaiga roho ya mtenda mabaya. Mithali ya kale husema hivi: “Usiseme, Mimi nitalipa mabaya; mngojee BWANA [Yehova, NW], naye atakuokoa.” (Mithali 20:22) Ni mwelekeo wenye hekima kama nini! Ni jambo zuri zaidi kama nini kujionyesha wenyewe kuwa washindi kwa kupinga kishawishi cha kuwaiga watenda mabaya.—Yohana 16:33; Warumi 12:17, 21.
Kuadhibiwa—Na Nani?
Bila shaka, vitendo vingine ni vyenye uzito kuliko machukizo au maudhiko ya kibinafsi. Vipi ikiwa sisi ndio wenye kupatwa na uhalifu? Kwa asili, tunahisi kwamba jambo fulani lapasa lifanywe kwa kusudi la kutekeleza haki. Lakini jambo gani? Katika jamii nyingine si jambo lisilo la kawaida kushughulikia mambo kibinafsi na kulipa kisasi. Lakini jamii kama hizo zimekuja kuvunjwa-vunjwa na mapigano ya kiadui ya umwagaji damu. Leo, wala sheria za Mungu wala sheria za kibinadamu, katika hali zilizo nyingi, haziruhusu watu walipe kisasi cha kibinafsi kwa uhalifu mbalimbali, na ni kwa sababu nzuri. Jeuri ya kibinafsi kama hiyo huanzisha tu jeuri zaidi.
Basi, je! mwenye kupatwa na uhalifu apaswa kuvumilia kutendewa vibaya bila kufanya jambo lolote? Si kwa lazima. Kama mali yetu au sisi wenyewe tunatendewa vibaya, kuna mamlaka tunazoweza kugeukia. Huenda ukataka kuwaita polisi. Kazini, mwendee msimamizi. Shuleni, huenda ukataka kumwona mwalimu mkuu. Hiyo ni sababu moja ya kuwapo kwao—ili kutegemeza haki. Biblia hutuambia kwamba mamlaka za kiserikali ni “mtumishi wa Mungu, amlipizaye kisasi mtenda mabaya kwa ajili ya ghadhabu.” (Warumi 13:4) Haki hutaka kwamba serikali itumie mamlaka yayo, ikomeshe kutenda mabaya, na kuadhibu watenda mabaya.
Ni kweli, nyakati nyingine inachukua muda mrefu kabla ya haki kutekelezwa. Mwandikaji mmoja aliyechoshwa na maisha ya ulimwengu alisema hivi: “Haki ni kama gari-moshi ambalo huchelewa karibu sikuzote.” Kwa kweli, nyakati nyingine gari-moshi hilo haliji kamwe. Wadhalimu huenda wakawa wenye nguvu nyingi mno hivi kwamba mamlaka haziwezi kuwadhibiti. Hata hivyo, njia yenye hekima ni kujizuia mwenyewe. “Mpumbavu hudhihirisha hasira yake yote; bali mwenye hekima huizuia na kuituliza,” yasema Biblia.—Mithali 29:11.
Kisasi—Kilipwe na Nani?
Hivyo kujizuia tusilipe kisasi kutatuletea manufaa, nasi twaweza kungojea kwa utulivu, tukijua kwamba ikiwa haki yahitaji kutekelezwa, Mungu atafanya hivyo kwa wakati unaofaa. Yehova atambua kwamba kutenda mabaya kusikozuiwa huongoza kwenye uovu. (Mhubiri 8:11) Yeye hataruhusu waovu wenye mioyo migumu waidhulumu ainabinadamu milele. Ndiyo sababu mtume Paulo alitushauri hivi: “Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana.” (Warumi 12:19) Kwa kweli, Biblia husema juu ya siku ya kisasi kwa upande wa Muumba. Siku hiyo ya kisasi itakuwa nini? Nao ni nani watakaokuwa shabaha ya kisasi cha Mungu? Tutazungumzia hilo katika makala inayofuata.
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Ili kudhibiti maoni ya kutaka kulipa kisasi, kumbuka kwamba
□ Mungu huhangaikia haki
□ kuweka mwelekeo wa kutaka kulipa kisasi kunadhuru
□ kuwa mwenye fadhili mara nyingi hupunguza matatizo pamoja na wengine
□ tumesamehewa makosa yetu mengi
□ wenye kutenda makosa huenda wakabadilika
□ tunashinda ulimwengu kwa kupinga njia zao