Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 11/1 kur. 25-29
  • ‘Yehova Ni Mungu Wangu Nitakayemtumaini’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Yehova Ni Mungu Wangu Nitakayemtumaini’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Bidii Iliyo Mfano Mzuri ya Wazazi Wangu
  • Himizo la Baba Lenye Hekima
  • Ujumbe Kutoka Mbinguni!
  • Kushukuru kwa Ajili ya Kila Pendeleo la Utumishi
  • Kuendelea Kutenda Wakati wa Vita
  • Ziara Yenye Matokeo Yasiyotarajiwa
  • Kuvumilia Yajapokuwa Matatizo
  • Ndugu Knorr Arudi
  • Mishangao Mingine Mipya
  • Kukumbuka Yaliyopita
  • Maisha Ambayo Sikuyajutia Kamwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Mambo Niliyotimiza Katika Utumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Maisha Yangu Katika Tengenezo la Yehova Lenye Kuelekezwa kwa Roho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Je, Waweza Kujitolea?
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 11/1 kur. 25-29

‘Yehova Ni Mungu Wangu Nitakayemtumaini’

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA WILLI DIEHL

“KWA nini unataka kwenda Betheli?” Hilo ndilo lilikuwa swali la baba yangu katika masika ya 1931 nilipomwambia tamaa yangu ya kuanza utumishi wa Betheli. Wazazi wangu walioishi katika Saarlandi, walikuwa wamekuwa katika kweli kwa muda wa miaka kumi hivi, nao walikuwa wametuwekea sisi wavulana watatu mfano mzuri. Ile kweli ilikuwa maisha yao yote, nami nilitaka kuifanya iwe maisha yangu yote pia.

LAKINI wazazi wangu walipataje kujifunza juu ya Yehova na penzi lake takatifu? Kwa kutoridhika na dini iliyo madhubuti, walikuwa wameitafuta kweli kwa muda mrefu. Walijaribu makanisa na madhehebu mbalimbali, wakigundua kila mojawapo, moja baada ya jingine, halikufaa.

Siku moja kikaratasi cha mwaliko kilichokuwa kinatangaza hotuba yenye picha na sinema kuhusu kusudi la Mungu iitwayo “Photo-Drama of Creation” kiliachwa mlangoni petu. Baba alipaswa awe kazini ya wakati “Photo-Drama” hiyo ingeonyeshwa, lakini alimtia Mama moyo aende. “Labda,” yeye akasema “kuiona kwaweza kuwa na manufaa.” Baada ya kuiona jioni hiyo, Mama alikuwa na shauku. “Nimeipata kweli hatimaye!” akasema. “Njoo ujionee mwenyewe kesho jioni. Hiyo ni kweli ambayo tumekuwa tukiitafuta.” Hiyo ilikuwa katika 1921.

Wakiwa Wakristo wapakwa-mafuta, wazazi wangu waliendelea kuwa waaminifu mpaka walipokufa, Baba katika 1944, baada ya kutiwa-tiwa kifungoni mara kadhaa na Wanazi, na Mama katika 1970. Yeye pia alitumia wakati mrefu akiwa amefungwa gerezani chini ya utawala wa Nazi.

Bidii Iliyo Mfano Mzuri ya Wazazi Wangu

Kabla ya wao kufa, wazazi wangu walikuwa wenye bidii sana katika utumishi wa shambani. Mama yangu alikuwa mwenye bidii sana hasa katika kugawanya maazimio ya mikusanyiko yaliyotolewa tokea 1922 hadi 1928. Ecclesiastics Indicted (Viongozi wa Kidini Washtakiwa), iliyotia ndani azimio lililokubaliwa katika 1924, ilikuwa na shutuma kali kwa makasisi. Kuieneza kulihitaji ushujaa. Saa kumi za asubuhi wahubiri walikuwa wameamka, wakizipitisha trakti hizo chini ya milango. Ingawa nilikuwa mwenye umri wa miaka 12 tu, wazazi wangu waliniruhusu nishiriki. Mara nyingi tulianza saa kumi na moja asubuhi, tukiendesha baiskeli kwa muda wa saa tatu hadi nne ili kufikia eneo la mbali. Tulizificha baiskeli vichakani, nami nilizilinda wakati wengine walipokuwa wakifanya kazi kijijini. Alasiri tuliendesha baiskeli kurudi nyumbani, na jioni tulitembea muda wa saa moja kwenda mkutanoni.

Baadaye, mtu mchanga zaidi aliachwa akizilinda baiskeli, nami nikaenda pamoja na wahubiri. Lakini hakuna yeyote aliyefikiria kunizoeza. Waliniambia tu barabara ambayo nilipaswa kufanya kazi! Moyo wangu ukinidunda-dunda nilinyemelea nyumba ya kwanza, nikitumaini kwamba hakungekuwako mtu yeyote nyumbani. Masikini mimi, mwanamume mmoja alifungua mlango. Niliduwaa. Nikisitasita, nilionyesha kwa kidole ndani ya mfuko wangu. “Je! ni cha Jaji Rutherford?” akauliza. Nikatoa jibu la kigugumizi. “Je! ni kipya, nisichokuwa nacho?” “Naam, ni kipya,” nikathibitisha. “Basi ni lazima nijipatie. Kinauzwaje?” Hiyo ilinipa moyo niendelee.

Katika 1924 watu wazima waliongea sana kuhusu 1925. Wakati mmoja tulitembelea familia ya Wanafunzi wa Biblia, nami nilimsikia ndugu mmoja akiuliza hivi: “Bwana akituchukua mbinguni, itakuwaje kwa watoto wetu?” Mama, akiwa mwenye mwelekeo chanya (mzuri) kama kawaida, akajibu hivi: “Bwana atajua jinsi ya kuwatunza.” Habari hiyo ilinisisimua sana. Ilimaanisha nini? Mwaka 1925 ulikuja na kupita, na hakuna jambo lililotukia. Hata hivyo, wazazi wangu hawakuiacha bidii yao.

Himizo la Baba Lenye Hekima

Mwishowe, katika 1931, nilimwambia baba yangu kile nilichotaka kufanya na maisha yangu. “Kwa nini unataka kwenda Betheli?” baba yangu akauliza kwa kujibu. “Kwa sababu nataka kumtumikia Yehova,” nikajibu. “Tuseme umekubaliwa Betheli,” akaendelea. “Je! unatambua kwamba ndugu walioko huko si malaika? Wao si wakamilifu nao hufanya makosa. Nina hofu kwamba hilo huenda likakufanya utoroke na hata kuiacha imani. Hakikisha kwamba unalifikiria hilo kwa uangalifu.”

Nilishtuka kusikia jambo kama hilo, lakini baada ya kufikiria mambo kwa siku kadhaa, nilirudia tamaa yangu ya kupeleka maombi ya kwenda Betheli. “Niambie tena kwa nini wataka kwenda,” akasema. “Kwa sababu nataka kumtumikia Yehova,” nikajibu. “Mwanangu, usisahau hilo kamwe. Ukikaribishwa, kumbuka kwa nini unaenda. Ukiona jambo baya, usihangaike mno. Hata ikiwa unatendewa vibaya, usitoroke. Usisahau kamwe kwa nini umo Betheli—sababu unataka kumtumikia Yehova! Fanya kazi yako tu na kumtumaini.”

Kwa hiyo niliwasili Betheli katika Bern, Uswisi, mapema alasiri ya Novemba 17, 1931. Nilikaa chumba kimoja na wengine watatu na kufanya kazi katika kiwanda cha matbaa, nikijifunza kuendesha matbaa ndogo ya kutiwa karatasi kwa mkono. Mojawapo ya vitu vya kwanza nilivyopewa mgawo kupiga chapa kilikuwa ni Mnara wa Mlinzi katika Kiromania

Ujumbe Kutoka Mbinguni!

Katika 1933 Sosaiti ilitangaza The Crisis, kijitabu chenye hotuba tatu za redio ambazo Ndugu Rutherford alikuwa ametoa katika United States. Ndugu Harbeck, mtumishi wa tawi, aliarifu familia ya Betheli kwenye kiamsha-kinywa asubuhi moja kwamba kijitabu hicho kingeenezwa kwa njia ya kipekee. Vikaratasi vya kutangazia vingeangushwa chini kutoka kwa ndege ndogo ya kukodi ikiwa inaruka juu ya Bern, huku nao wahubiri wangesimama barabarani wakiwatolea watu kijitabu hicho. “Ni nani kati ya nyinyi ndugu vijana aliye tayari kwenda katika ndege hiyo?” akauliza. “Toeni majina yenu mara moja.” Nilitoa jina langu, na baadaye Ndugu Harbeck akatangaza kwamba nilikuwa nimechaguliwa.

Katika siku hiyo ya maana, tulienda na gari kwenye uwanja wa ndege tukiwa na vibweta vingi vya vikaratasi. Niliketi nyuma ya rubani na kuvirundika vikaratasi hivyo kwenye kiti kilichokuwa karibu nami. Maagizo ya waziwa-zi niliyopewa yalikuwa: kunja vikaratasi vya kukaribisha katika vifurushi vya mia-mia kila kimoja, na utupe kila kifurushi nje ya dirisha kutoka upande mmoja kwa nguvu nyingi iwezekanavyo. Kukosa uangalifu kungesababisha vikaratasi hivyo vikwame kwenye mkia wa ndege, na kusababisha matatizo. Lakini mambo yalienda vizuri. Baadaye Ndugu walisema jinsi walivyosisimuka kuuona huo ‘ujumbe kutoka mbinguni.’ Ilikuwa na tokeo lililotakiwa, na vijitabu vingi viliangushwa, hata ingawa watu wengine walipiga simu kulalamika kwamba bustani zao za maua zilikuwa zimejaa vikaratasi.

Kushukuru kwa Ajili ya Kila Pendeleo la Utumishi

Kila siku nilimshukuru Yehova kwa ajili ya shangwe na uradhi wa utumishi wa Betheli. Kundini, nilipewa mgawo wa kufungua Jumba la Ufalme, kupanga viti kwa utaratibu, na kuweka bilauri ya maji safi kwenye kinara cha msemaji. Niliona hilo kuwa heshima kubwa.

Katika Betheli, hatimaye nilifanya kazi na matbaa itumiayo mabamba ya kupigia chapa yaliyotandazwa, iliyotumiwa kuchapa The Golden Age (sasa Amkeni!) katika Kipolandi. Katika 1934 tulianza kutumia vinanda vya santuri, nami nilisaidia katika kuviunda. Nilipata shangwe nyingi katika kwenda nyumba kwa nyumba nikiwa na hotuba za Biblia zilizorekodiwa. Wenye nyumba wengi walikuwa na udadisi kuhusu kidude hiki kidogo, na mara nyingi familia nzima ilikuwa ikikusanyika isikilize, lakini hatimaye walikuwa wakiondoka mmoja mmoja. Familia yote ilipokwisha kuondoka, nilienda kwenye mlango uliofuata tu.

Kuendelea Kutenda Wakati wa Vita

Baada ya Vita ya Ulimwengu 1, nchi niliyozaliwa Saarlandi ilitengwa na Ujerumani na kutawalwa chini ya himaya ya Ushirika wa Mataifa. Hivyo, Saarlandi ilitokeza hati za utambulisho zayo yenyewe. Katika 1935 kura ya kupata maoni ya raia ilifanywa ili kuamua kama raia wayo walitaka kuunganishwa tena na Ujerumani. Nilichukua nafasi hiyo kuitembelea familia yangu, nikijua kwamba nisingeweza kufanya hivyo iwapo Saarlandi ingepata kuwa chini ya utawala wa Nazi. Na kwa kweli, kwa miaka mingi baadaye, sikupata habari yoyote kutoka kwa wazazi wangu au ndugu zangu.

Ingawa haikuhusika moja kwa moja katika Vita ya Ulimwengu 2, Uswisi ilitenganishwa kabisa wakati Ujerumani ilipoanza kuzikalia nchi jirani moja baada ya nyingine. Tulikuwa tumechapa vichapo kwa ajili ya Ulaya nzima isipokuwa Ujerumani, lakini sasa vichapo havikuweza kusafirishwa. Ndugu Zürcher, aliyekuwa mtumishi wa tawi wakati huo, alituambia kwamba kwa kweli hatukuwa na pesa. Naye akatuomba tufanye kazi nje ya Betheli mpaka mambo yarudi kawaida tena. Hata hivyo, nilikubaliwa nibaki, kwa kuwa kulikuwako vitu vichache vya kuchapa kwa ajili ya wahubiri wa kwetu elfu moja hivi.

Familia ya Betheli haitasahau kamwe Julai 5, 1940. Mara tu baada ya chakula cha mchana lori la kijeshi lilikuja. Askari waliruka nje na kuingia Betheli kwa kishindo. Tuliamriwa tusimame kimya, na kila mmoja wetu akalindwa na askari mwenye silaha. Tulikusanywa na kupelekwa kwenye chumba cha mezani wakati sehemu nyinginezo za jengo zilipokuwa zinapekuliwa-pekuliwa. Wenye mamlaka walidhani kwamba tulikuwa tumewaambia wengine wakatae utumishi wa kijeshi, lakini walishindwa kupata ushuhuda wowote.

Muda wa miaka hiyo ya vita, nilikuwa mtumishi wa kundi katika Thun na Frutigen pia. Hiyo ilimaanisha kwamba ratiba yangu ya mwisho-juma ilikuwa imejaa mambo mengi. Kila Jumamosi, mara tu baada ya chakula cha mchana, niliendesha baiskeli yangu kilometa 50 kwenda Frutigen, ambako niliongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi jioni. Jumapili asubuhi niliandamana na wahubiri katika utumishi wa shambani. Kisha, mapema alasiri, nilienda zangu Interlaken kuongoza Funzo la Kitabu na nikaongoza baadaye alasiri funzo la Biblia na Familia moja huko Spiez. Kuikamilisha siku, niliongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi katika Thun.

Usiku sana, utendaji wangu ukiwa umekamilishwa, niliimba na kupiga mbinja nilipokuwa ninarudi Bern, nikiwa nimeridhika sana. Sikukutana na magari mengi. Mandhari ya nchi yenye vilima-vilima iliyokuwa kana kwamba imefunikwa kitambaa cheusi kwani taa zilikuwa zimezimwa kwa sababu ya vita, ilikuwa tulivu na bila matata, ikimetameta mara kwa mara katika nuru ya mbalamwezi. Jinsi miisho-juma hiyo ilivyoyatajirisha maisha yangu na kunirudishia nguvu!

Ziara Yenye Matokeo Yasiyotarajiwa

Katika vuli ya 1945, Ndugu Knorr alitutembelea. Siku moja aliingia kiwandani nilipokuwa ninasimama kwenye matbaa ya kuzunguka. “Njoo chini!” akaita. “Ungependa kuhudhuria Shule ya Gileadi?” Nilipigwa butaa. “Ikiwa unafikiri naweza, ningefurahi kuhudhuria,” nikajibu. Mialiko ya Ndugu Fred Borys, Dada Alice Berner, na mimi iliwasili katika masika ya 1946. Lakini kwa sababu ya kuwa nilikuwa nimezaliwa Saarlandi, sikuwa na nchi ya kujitambulisha nayo na kwa hiyo nilipaswa nipeleke ombi Washington D.C., U.S.A., ili nipate viza ya kipekee.

Ijapokuwa wengine waliondoka kwa wakati uliofaa, mimi nilipaswa ningojee jibu la ombi langu. Shule ilipoanza Septemba 4, bado nilikuwa Uswisi, tumaini langu likiwa linadidimia. Kisha Balozi wa U.S. akapiga simu, akiniarifu kwamba viza yangu ilikuwa imewasili. Mara moja nilijaribu kufanya mipango ya kusafiri na mwishowe nikapata kijumba katika meli ya wanajeshi iliyokuwa ikisafiri kutoka Marseilles hadi New York. Hilo lilikuwa ono lililoje! Meli hiyo Athos II ilikuwa imejaa watu kupita kiasi. Nilipewa malazi katika chumba cha wazi. Siku ya pili baharini, mlipuko katika chumba cha mtambo ulifanya meli ikwame. Abiria na mabaharia pia walikuwa na wasiwasi, wakihofu kwamba huenda tukazama. Hilo lilinipa nafasi nzuri ajabu ya kutoa ushahidi kuhusu tumaini la ufufuo.

Ilichukua muda wa siku mbili kuitengeneza meli, kisha tukaendelea kwa mwendo wa pole. Tulifika New York siku 18 baadaye, lakini tulilazimika kubaki melini kwa sababu ya mgomo wa makuli. Baada ya mapatano, hatimaye tuliweza kuondoka melini. Nilikuwa nimepigia Sosaiti simu kuhusu hali hiyo, na nilipokuwa nikiondoka idara ya forodha na uhamiaji, mwanamume mmoja aliniuliza hivi: “Je! wewe ni Bw. Diehl?” Yeye alikuwa mmoja wa wasaidizi wa Ndugu Knorr, naye alinipeleka kwenye gari-moshi ya usiku kwenda Ithaca, karibu na Shule ya Gileadi, ambako niliwasili muda mfupi baada ya saa mbili asubuhi keshoye. Nilisisimuka kama nini kufika huko hatimaye, kuweza kuhudhuria darasa la kwanza la kimataifa la Gileadi!

Kuvumilia Yajapokuwa Matatizo

Kuhitumu kwa darasa la nane la Gileadi kulikuwa Februari 9, 1947, na kila mtu alikuwa na msisimuko mwingi. Tungetumwa wapi? “Kamba zangu” zilianguka juu ya kiwanda cha matbaa kilichokuwa kimefunguliwa karibuni kule Wiesbaden Ujerumani. (Zaburi 16:6) Nilirudi Bern ili kupeleka maombi yangu ya kupata vyeti vya idhini vilivyohitajiwa, lakini majeshi ya U.S. yaliyokuwa yametwaa Ujerumani yalikuwa yakikubali nchini tu watu ambao walikuwa wameishi huko kabla ya vita. Kwa kuwa sikuwa nimeishi huko, nilihitaji mgawo mpya kutoka kwa makao makuu ya Brooklyn. Niligawiwa kazi ya mzunguko kati-ka Uswisi, ambayo niliikubali nikimtumaini Yehova kikamili. Lakini nilipokuwa ninangojea mgawo huo, niliulizwa siku moja niwaonyeshe dada watatu Betheli na ua wayo. Mmoja wao alikuwa painia aitwaye Marthe Mehl.

Katika Mei 1949, nilitaarifu makao makuu huko Bern kwamba nilipanga kumwoa Marthe na kwamba tulitaka kubaki katika utumishi wa wakati wote. Itikio lilikuwa nini? Kukosa mapendeleo yote isipokuwa upainia wa kawaida. Tuliuanza Biel, baada ya arusi yetu katika Juni 1949. Sikukubaliwa kutoa hotuba, wala hatukuweza kutafuta makao kwa ajili ya wahudhuriaji wa kusanyiko ambalo lingeanza karibuni, hata ingawa tulikuwa tumependekezwa na mwangalizi wa mzunguko wetu kwa pendeleo hilo. Wengi waliacha kutusalimu, wakitutendea kama watu waliotengwa na ushirika, hata ingawa tulikuwa mapainia.

Hata hivyo, tulijua kwamba kufunga ndoa hakukuwa jambo lisilokuwa la kimaandiko, kwa hiyo tulifanya sala kuwa ngome yetu na tukamtumaini Yehova. Kwa kweli, hali hiyo ya kutendwa haikuonyesha maoni ya Sosaiti. Ilikuwa tokeo tu la utumizi mbaya wa miongozo ya kitengenezo.

Ndugu Knorr Arudi

Katika 1951, Ndugu Knorr alizuru Uswisi tena. Baada ya kutoa hotuba, nilitaarifiwa kwamba alitaka kuongea nami. Ingawa nilikuwa ninahofu kidogo, nilifurahi kwamba alipendezwa kuniona. Aliuliza kama tungekuwa na nia ya kukubali mgawo katika nyumba ya misionari iliyokuwa inakusudiwa iwe Geneva. Kwa hakika tulifurahi, ingawa kuondoka Biel kungeleta masikitiko. Siku iliyofuata ombi jingine kutoka kwa Ndugu Knorr lilitufikia. Je! tungependa kuanza kazi ya mzunguko tena, kwa kuwa kazi hiyo ilihitaji kuhudumiwa zaidi katika Uswisi? Tulikubali mara moja. Mwelekeo wangu sikuzote umekuwa kukubali mgawo wowote unaotolewa.

Utendaji wetu katika kazi ya mzunguko mashariki mwa Uswisi mashariki ulibarikiwa sana. Tulisafiri kutoka kundi moja hadi jingine kwa gari-moshi, tukiwa tumebeba mali zetu zote katika masanduku mawili. Mara nyingi ndugu walitulaki kwenye kituo wakiwa na baiskeli, kwa kuwa ni wachache tu waliokuwa na magari siku hizo. Miaka mingi baadaye ndugu mmoja alitupa gari, lililofanya utumishi wetu uwe rahisi zaidi.

Mishangao Mingine Mipya

Ilisisimua kama nini katika 1964 wakati mke wangu nami tulipoalikwa kwenye darasa la 40 la Gileadi, darasa la mwisho la mtalaa wa miezi kumi wenye masomo mengi, ambao sasa ulikuwa umefupishwa kuwa wa miezi minane. Marthe alilazimika kujifunza Kiingereza haraka, lakini alifaulu. Makisio ya ni wapi tungetumwa yalikuwa mengi. Mwelekeo wangu ulikuwa: ‘Sijali mahali ninapopewa mgawo, mradi tu isiwe ni kazi ya ofisini!’

Lakini hilo ndilo lililotukia hasa! Siku ya kuhitimu, Septemba 13, 1965, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa tawi la Uswisi. Betheli ingekuwa ono jipya kwa Marthe. Kwangu, ilimaanisha kurudi kwenye “Nyumba ya Mungu,” si kwenye kiwanda cha matbaa, ambapo nilikuwa nimetumikia kutoka 1931 hadi 1946, bali ofisini. Nilikuwa na mambo mengi mapya ya kujifunza, lakini kwa msaada wa Yehova niliweza kufanya hivyo.

Kukumbuka Yaliyopita

Muda wote wa miaka 60 ya utumishi wa wakati wote, nimemtumaini Yehova kikamili, kama baba yangu alivyoniambia nifanye. Na Yehova amemimina mibaraka mingi sana. Marthe amekuwa chanzo kikubwa sana cha kitia moyo katika nyakati za kukatisha tamaa au wakati migawo imekaribia kunilemea, kwa kweli amekuwa mwandamani mwaminifu-mshikamanifu mwenye kumtumaini Yehova kabisa.

Yehova na asifiwe kwa ajili ya mapendeleo mengi ya utumishi ambayo nimeonea shangwe! Ningali ninatumika nikiwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi katika Thun, na mara nyingi nimesafiri nikiwa mwangalizi wa eneo la dunia. Haidhuru ni nini ambalo nimeombwa nifanye, sikuzote nimemtegemea Yehova kwa mwongozo. Yajapokuwa makosa na upungufu wangu mwingi, ninaamini kwa moyo kwamba Yehova amenisamehe kupitia Kristo. Na niendelee kuwa mwenye kumpendeza. Na aendelee kuelekeza hatua zangu, ninapomtegemea daima akiwa “Mungu wangu nitakayemtumaini.”—Zaburi 91:2.

[Picha of Willi and Marthe Diehl katika ukurasa wa 25]

[Picha katika ukurasa wa 27]

Ndugu Diel mapema katika kazi-maisha yake ya Betheli

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki