Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Watafutaji Kweli Wauitikia Ushahidi wa Vivi Hivi
Biblia hutuarifu kwamba watu wenye mfano wa kondoo wataiitikia sauti ya Mchungaji Mwema. (Yohana 10:27) Hali imekuwa hivyo katika nchi nyingi, kutia na Uingereza.
◻ Kwa mfano, katika 1988, kabla tu ya Krismasi, Pamela, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alijibu simu ofisini ambapo alikuwa akifanya kazi akasema na mchuuzi mmoja afanyaye kazi katika kampuni hiyo hiyo katika sehemu nyingine ya Uingereza. Mwisho wa mazungumzo hayo, mwanamume huyo aliuliza hivi: “Je! wewe u tayari kwa ajili ya Krismasi?” Pamela akasema: “La!” “Je! hujachelewa sana?” akauliza mwenye kupiga simu. “Mimi siadhimishi Krismasi,” akajibu Pamela. Mwanamume huyo akasema kwamba hilo si jambo la kawaida akauliza ni kwa nini. Pamela akamwambia kwamba yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova na akaendelea kueleza kwamba hakuna amri yoyote katika Biblia kuhusu kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa Yesu, na tena, Yesu hakuzaliwa Desemba 25. Isitoshe, Krismasi ilikuwa mwadhimisho wa kipagani mwanzoni. Mwenye kupiga simu alisema habari hiyo yote ilisikika kuwa yenye kupendeza.
Miezi mitatu baadaye Pamela alijibu simu, na mwenye kupiga simu akasema hivi: “Je! unakumbuka kuwa ulisema nami kabla ya Krismasi ukaniambia kwamba wewe huadhimishi Krismasi? Basi, nimepata kweli!” Ilikuwa mwanamume yule yule, naye akaeleza kwamba majuma mawili baada ya Krismasi, Mashahidi wawili walimtembelea nyumbani kwake. Aliwakaribisha ndani, na funzo la Biblia likaanzwa. Alisimulia kwamba alikuwa amefanya maendeleo ya haraka katika mafunzo yake. Alimwambia rafiki-msichana wake aliyekuwa akiishi naye kwamba mtindo wao wa maisha haukuwa ukimpendeza Yehova, kwa hiyo wakaachana, na sasa wote wawili walikuwa wakihudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme.
Mwisho wa mwaka huo, walikubaliwa kuwa wahubiri wasiobatizwa, nao wakaoana mwanzoni mwa 1990. Kisha wakabatizwa pamoja. Ni tokeo zuri sana kama nini la ushahidi mfupi wa vivi hivi kupitia simu!
◻ Yehova alimbariki dada mwingine aliyetoa ushahidi wa vivi hivi katika Uingereza. Mwanamume mwuzaji bima alipomtembelea, dada huyo alimwuliza ikiwa angependa kuhakikishiwa afya njema, furaha, na uhai wa milele. Alisema ndiyo na kumwuliza dada huyo ni mpango gani wa bima alikuwa akizungumzia. Alipoonyeshwa katika Biblia ahadi ya Mungu ya uhai wa milele katika Paradiso duniani, alikubali nakala ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani akasoma kichapo hicho chote kwa jioni moja. Alipomtembelea dada huyo tena, alimwambia kwamba habari hiyo ilikuwa nzuri ajabu—laiti tu angekuwa na imani ya kuiamini. Dada huyo alimweleza kwamba alihitaji kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Funzo la Biblia lilipangwa, naye akaanza kuhudhuria mikutano. Alibatizwa katika vuli ya mwaka huo huo. Mwaka mmoja tu baadaye, alimwoa binti wa dada ambaye alikuwa amemtolea ushahidi mara ya kwanza. “Kwa hiyo,” asema dada huyo, “Nilipata ndugu na mkwe pia kupitia ushahidi wangu wa vivi hivi!”
Ni jambo la hakika kwamba watafutaji kweli huitikia wakati kweli ya Biblia inapotolewa kupitia ushahidi wa vivi hivi. Kama Yesu alivyosema, kondoo wake huisikia sauti yake.y