Je! Ni Lazima Wewe Usherehekee Krismasi?
ILI KUONYESHA ulinganifu na tofauti kati ya njia ya Mashariki na Magharibi ya kusherehekea Krismasi, habari inayoonyeshwa hapa ni katika njia ya barua mbili ambazo zilibadilishanwa kati ya mwandikaji wa Kijapani na rafiki yake katika Uingereza. Habari hii inakusaidia kujibu ulizo hili: Je! ni lazima mimi nisherehekee Krismasi?
Kwa David,
Wanasherehekea tena. Wafanya biashara wanaongoza watu kama makuhani wakuu. Baba-Krismasi ndiye bwana mkubwa wa sherehe. Miti ya Krismasi inatumika kuwa kifananisho cha sherehe. Na matoleo ya keki na vitu vya kuchezea vya Krismasi vinatolewa. Wafanya biashara wanatangaza dini ya Krismasi katika Japani. Kazi yao ya misheni imefanikiwa sana kwa miongo mitatu au minne iliyopita. Hesabu kubwa ya Wajapani imegeuzwa kwenye “dini” hii—angalau kwa siku chache katika mwaka!
Jambo hili limenivutia mimi. Mara nyingi nimetaka kujua kwa nini Wajapani wengi, hasa wale ambao si Wakristo, wangekuwa wakisherehekea sikukuu ya “Kikristo.” Tangu lini Wajapani wengi walipoanza kusherehekea Krismasi kwa kadiri hii? Sababu ni nini?
Nilipochunguza chanzo cha Krismasi ya Kijapani, nilipata hadithi hii yenye kupendeza. Sōseki Natsume, mwandikaji mkuu wa kipindi cha Kimeiji (1868-1912), alimpelekea Shiki Masaoka, mtunga mashairi mwenye kujulikana sana, kadi ya Krismasi kutoka Uingereza, ikieleza tamasha yenye kuvutia ya Krismasi katika Uingereza mwishoni mwa mwaka 1900. Shiki hata alitunga haiku, shairi fupi la Kijapani, kuhusu kanisa dogo Siku ya Krismasi. Yaonekana, Krismasi ilikuwa jambo jipya mwanzoni mwa karne [ya 20] katika Japani. Basi, ni wakati gani halisi Wajapani waliposherehekea Krismasi yao ya kwanza?
Utapendezwa kujua kwamba mamlaka fulani zinadai kwamba Krismasi ilisherehekewa katika shule ya wasichana katika Ginza mapema mwaka wa nane wa Meiji (1875). Hata hivyo “desturi ya kusherehekea Krismasi ilikuwa haijaanza kuimarika katika Japani mpaka 1945,” ndivyo lilivyosema jarida The Christian Century. Huo ndio wakati Wajapani walipoona jamii za askari Waamerika na wamisionari wakisherehekea Krismasi. Baada ya kushindwa katika Vita ya Ulimwengu ya Pili na kuachwa katika hali tupu ya kiroho, kwa ujumla Wajapani walihitaji kitu cha kuwachangamsha.
Krismasi ilitosheleza uhitaji huo. Kama unavyoweza kuwazia, wafanya bishara hawakupoteza wakati wo wote katika kutumia mapambo-mapambo ya Krismasi ili kuendeleza mauzo yao ya mwishoni mwa mwaka. Kimpei Shiba, mhariri wa gazeti alisema kwamba mapambo-mapambo hayo ya Krismasi “yalifanya kazi kama kiinimacho ili kuwavuta wanunuzi.” Aliongezea kwamba “hii ilikuwa kwa sababu mapambo hayo yalivutia na kutokeza shangwe.”
Lakini, David, kwa kuwa unaishi Uingereza huenda usijue kwamba Wajapani wamekuwa na desturi ya kubadilishana zawadi za mwisho wa mwaka muda mrefu kabla ya zawadi za Krismasi zitokee. Sikuzote Desemba imeleta faida kwa wachuuzi. Watu wakiwa na vipochi vyao vilivyojaa pesa kutokana na bakshishi za mwishoni mwa mwaka wanazitumia kama mchezo. Walakini “hali hii [ya Krismasi], inawatia watu katika moyo wenye furaha ya kutumia pesa na kuwashawishi wanunue osei-bo [zawadi za mwishoni mwa mwaka] zaidi ya walivyofanya kwa kawaida, hivyo desturi ya kutumia mapambo ya Krismasi imeendelea,” anaeleza Bw. Shiba.
Leo, maduka makubwa-makubwa na wachuuzi wanafuata mtindo huo ili kuitumia kwa faida nyingi “roho ya Krismasi” ambayo inaonekana inaleta matokeo mazuri zaidi. Watengenezaji wa vitu vya kuchezea watoto na sehemu za kuokea mikate wanakazia fikira hali hii ili kupata faida ya kipindi hicho. Wakati wa Desemba, mauzo katika Kiddy, duka mojapo lililo kubwa la kuuza vitu vya kuchezea watoto katika Japani, yamekuwa mengi mara nne zaidi ya miezi mingine. Inakadiriwa kwamba asilimia 5 mpaka 10 ya keki zinafanyizwa katika Japani kila mwaka zinaweza kuitwa “keki za Krismasi.”
Nilipata kujua ya kwamba watu wengine wanakasirika kwa sababu biashara inatawala tamasha ya Krismasi katika Japani. Kwa mfano, The Daily Yomiuri linataja Mwamerika mmoja ambaye ameishi katika Japani kwa muda mrefu kuwa akisema: “Wajapani wamekubali karibu mbinu zote za Krismasi lakini kwa njia fulani roho ya kipindi hicho haipo.” Alikuwa akizungumzia sehemu ya kidini ya Krismasi.
Jambo hili lilinichochea mimi nichunguze upande wa kidini kuhusu Krismasi. Watu wenye kwenda kanisani wanadai kwamba Krismasi (Desemba 25) ni siku ya kuzaliwa kwa Kristo. Nilishangazwa sana kupata katika Encyclopedia of Japanese Religions kwamba haiwezi kuthibitishwa kwamba Yesu alizaliwa Desemba 25! Ensaiklopidia hiyo inasema: “Ijapokuwa siku halisi ya kuzaliwa kwa Yesu haijulikani, Krismasi imesherehekewa Desemba 25 kuanzia karne ya tatu . . . Tarehe hii inafika karibu sana na siku ya kikomo cha jua katika majira ya baridi, na ilichukua mahali pa sikukuu iliyotangulia Ukristo ya kuzaliwa tena kwa Jua.” Kuzaliwa tena kwa Jua? Nilifikiri ilipasa kuwa siku ya kuzaliwa kwa Yesu. Basi, Wakristo wanyofu wangewezaje kusherehekea karamu ambayo mwanzoni ilikuwa sikukuu ya kipagani ya kikomo cha jua katika majira ya baridi? Haikuwa siku ya kuzaliwa kwa Yesu bali sikukuu ya kuzaliwa tena kwa jua. Basi, watu wenye kwenda kanisani wa nchi za Magharibi wangewadhihakije Wajapani kwamba wao hawana kanuni katika kusherehekea sikukuu ya “Kikiristo” hali kiasili wao wenyewe wana desturi ya aina hiyo?
Basi, David, ningethamini sana ikiwa ungeweza kuyajibu maulizo haya kwa ajili yangu, kwa kuwa yananisumbua sana.
Rafiki yako,
Ichiro
Kwa lchiro
Asante sana kwa barua yako ikieleza sherehe ya Krismasi katika nchi yenu. Ni jambo lenye kutupendeza sana sisi watu wa Magharibi kujua jinsi watu wa Mashariki wanavyosherehekea sikukuu ya watu wa Magharibi.
Nikiweza kusema wazi, una sababu nzuri kabisa kwa kusema kwamba Krismasi ni sikukuu ya kipagani. Karibu kitabu cho chote cha marejezo kitakuambia kwamba sikukuu ya Krismasi ilianzia katika sherehe ya kipagani ya Saturnalia, sikukuu ya Kiroma kwa ajili ya mungu wao wa kilimo Saturn.
Ndiyo, kama vile ninyi watu wa Japani mmeitia Krismasi katika utamaduni wenu wa Kibudha na Kishinto, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yametia sikukuu za kipagani katika desturi zao za “Kikristo.” Katika maana hiyo huenda ikawa dhambi hata zaidi kwa kuwa huku Wajapani wakisherehekea Krismasi kuwa karamu ya kigeni, watu wenye kwenda kanisani wanaiadhimisha sherehe ya kipagani ya Saturnalia kuwa Krismasi ya “Kikristo.”
Hasa, kuna wakati ambapo hapa Uingereza sherehe ya kilimwengu na ya kidini ya Krismasi ilitangazwa kuwa haramu kwa vile ni zoea la kipagani. Huo ulikuwa wakati Wapurita walipotawala Uingereza. Katika Koloni ya Guba ya Masachuseti katika Amerika Kaskazini, Wapurita waliohama Uingereza kwa sababu ya imani zao walipiga marufuku pia Krismasi na kutoza faini kwa kufanya shangwe wakati wa kipindi hicho.
Lakini nafikiri ni lazima ujue maoni ya Biblia kuhusu kuchanganya Ukristo na dini za kipagani. “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini.” Ndivyo alivyosihi mtume Paulo kwenye 2 Wakorintho 6:14-17. Kisha kwenye 2Ko 6 mstari wa 17 aliendelea kutumia maneno ya kitabu cha Isaya (52:11, kwa ajili ya rejezo lako): “Tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema [Yehova], msiguse kitu kilicho kichafu.”
Tunawezaje kujitenga na wasioamini na huku tungali tukiendelea kusherehekea karamu iliyoanzishwa na dini za kipagani? Ulizo hilo limewasukuma Wakristo wengi wanyofu kuacha desturi yao ya kusherehekea Krismasi. (Lazima ikupendeze kufungua Biblia yako kwenye Mathayo 15:3-6 na kuyasoma maneno ya Yesu yaliyoandikwa humo.) Hata hivyo kuna sababu nyingi za kuepuka sherehe kama hizo.
Ikiwa Desemba 25 si siku ya kuzaliwa kwa Yesu, kusherehekea tarehe hiyo kuwa siku ya kuzaliwa kwake kunakuwa ni kusema uwongo. Kama vile umesema katika barua yako, Mkristo ambaye anapenda ukweli na ameamriwa kuwa mnyofu angeendelezaje uwongo? (Waefeso 4:25) Kuanzia tarehe yenyewe mpaka kwa hadithi ya Baba-Krismasi, Krismasi imejawa kemkemu na uwongo mwingi. Walakini, Wakristo wanaambiwa kwenye Ufunuo 22:15 kwamba “kila mtu apendaye uongo na kuufanya” atakosa baraka ya kimungu ya uzima wa milele.
Basi, kwa nini wanaojiita Wakristo katika nchi za Magharibi wanasherehekea Krismasi? Sababu moja ni biashara, kama ilivyo katika nchi yako. Nilisoma habari ya kasisi wa Kibaptisti huko United States aliyeomboleza hivi: “Ikiwa sehemu ya kibiashara ingeondolewa kabisa, watu wengi wangehisi kwamba hawajaijua Krismasi. Lakini fikira za kidini zingeweza kuondolewa kabisa na idadi kubwa ya watu isitambue tofauti.” Maneno hayo yanahusu katika Uingereza pia.
Jambo la kupendeza ni kwamba, Biblia inafunua uhusiano wa karibu sana uliopo kati ya biashara na inachoita “Babeli Mkuu.” Baada ya kuonyesha kwa taswira kuanguka kwa “Babeli Mkuu,” Biblia inasema hivi (kwenye Ufunuo 18:2, 11-19): “Nao wafanya biashara wa nchi walia na kumwombolezea, kwa sababu hapana mtu anunuaye bidhaa yao tena; . . . Na wafanya biashara wa vitu hivyo, waliopata mali kwake, watasimama mbali, kwa hofu ya maumivu yake; wakilia na kuomboleza.”
Je! unaweza kumtambua “Babeli Mkuu”? Basi, ni nani ambaye amewapa “wafanya biashara wa nchi” hapa Uingereza na Japani faida kubwa sana kwa kueneza mafundisho ya uwongo kuhusu Krismasi? Je! si dini za Jumuiya ya Wakristo? Ndiyo, nimejifunza kutokana na funzo langu la Biblia kwamba “Babeli Mkuu” anamaanisha milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, kutia na Jumuiya ya Wakristo?
Unafikiri tunaweza kufanya nini? Maelezo ya Biblia kuhusu “Babeli Mkuu” yalinisaidia mimi kuamua jambo ambalo ni lazima nilifanye. Ufunuo 18:4 husihi hivi: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.”
‘Kutoka kati yake,’ yaani, kuacha dini inayoeneza uwongo, kulimaanisha tendo la kukata maneno upande wangu. Halikuwa jambo rahisi kuvunja desturi zote zilizochanganywa na Krismasi. Krismasi ni sikukuu ya kijamii na kidini pia hapa. Ilinilazimu kujipa moyo ili niwe tofauti na wengine. Maneno niliyopata kwenye Mithali 29:25 yalithibitika kuwa yenye msaada: “Kuwaogopa wanadamu huleta mtego; bali amtumainiye [Yehova] atakuwa salama,”
Nilipata kuona habari hizo kutokana na Mashahidi wa Yehova. Maelfu ya watu katika Uingereza wamechukua mwendo huo na ‘kutoka katika Babeli Mkuu’ pamoja na mazoea yake yote ya kidini ya uwongo, kutia na kusherehekea Krismasi. Lakini haimaanishi kwamba sisi hatumheshimu Yesu Kristo. Tunamheshimu, si kwa kuonyesha “roho ya Krismasi” mara moja kwa mwaka, bali kwa kuonyesha roho kama ya Kristo mwaka mzima.
Rafiki yako wa moyo mnyofu,
David
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Wafanya biashara ni kama makuhani wakuu. Baba-Krismasi ndiye bwana mkubwa wa sherehe
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Wafanya biashara walitumia Krismasi ili kuendeleza mauzo ya mwishoni mwa mwaka
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Jambo hili lilinichochea mimi nichunguze upande wa kidini kuhusu Krismasi
[Blabu katika ukurasa wa 6]
“Tokeni kati yao . . . msiguse kitu kilicho kichafu”
[Blabu katika ukurasa wa 6]
“Nao wafanya biashara wa nchi walia na kumwombolezea”
[Blabu katika ukurasa wa 7]
“Kuwaogopa wanadamu huleta mtego; bali amtumainiye [Yehova] atakuwa salama”