Je! Sanamu Zaweza Kukuleta Karibu Zaidi na Mungu?
SANAMU nyingi sana za Kimisri, Kibabuloni, na Kigiriki hujaza majumba ya kuhifadhi leo. Sanamu-umbo zilizopewa heshima wakati mmoja huonyeshwa sasa kuwa tu kazi za sanaa ya kale. Nguvu zazo zilikuwa katika mawazo tu ya wale walioziabudu. Watu waliozipa heshima walipopitilia mbali hatimaye, zile nguvu ambazo sanamu hizo zilidhaniwa kuwa nazo zilitoweka pia. Sanamu hizo zilifunuliwa kuwa bila nguvu—ambavyo kwa kweli ndivyo zilikuwa sikuzote—vitu vya mbao, jiwe, au chuma visivyo na uhai.
Vipi juu ya sanamu zinazoheshimiwa na kuabudiwa na watu leo? Je! sanamu hizo zina nguvu nyingi kuliko zile sanamu za kale za Kimisri, Kibabuloni, na Kigiriki? Je! zimesaidia kweli kweli kuwaleta watu karibu zaidi na Mungu?
Kila kizazi kipitapo, ainabinadamu yaonekana kuwa yazidi kupeperuka kutoka kwa Mungu. Na sanamu zote zilizoko ulimwenguni zaweza kufanya nini juu ya hilo? Zisipotunzwa, hupatwa na vumbi na hatimaye kulika au kuoza. Haziwezi kujitunza zenyewe, licha ya kufanyia wanadamu jambo lolote. Hata hivyo, la maana zaidi ni, Biblia ina nini ya kusema juu ya jambo hilo?
Za Gharama Kubwa, Zenye Madoido, Bali Zisizofaa Kitu
Haishangazi kwamba, Biblia hufunua sanamu kuwa zisizofaa kitu na zisizoweza hata kidogo kusaidia wale wanaozitolea uchaji wamkaribie Mungu zaidi. Ingawa sanamu za kidini kwa kawaida huwa za gharama kubwa na zenye madoido, Biblia huonyesha thamani yao ya kweli inaposema hivi: “Sanamu zao ni fedha na dhahabu, kazi ya mikono ya wanadamu. Zina vinywa lakini hazisemi, zina macho lakini hazioni, zina masikio lakini hazisikii, zina pua lakini hazisikii harufu, mikono lakini hazishiki, miguu lakini haziendi, wala hazitoi sauti kwa koo zake. Wazifanyao watafanana nazo, kila mmoja anyezitumainia.”—Zaburi 115:4-8.
Biblia haifunui tu kwamba sanamu hazina thamani bali pia hutoa lawama kuhusu sanamu na waabudu wazo: “Mfano wao ni mfano wa mtende, kazi ya cherahani, hawasemi; hawana budi kuchukuliwa, kwa sababu hawawezi kwenda. Usiwaogope; kwa maana hawawezi kutenda uovu, wala hawana uwezo wa kutenda mema. Kila mtu amekuwa kama mnyama, hana maarifa; kila mfua dhahabu amefedheheshwa na sanamu yake ya kuchonga; maana sanamu yake ya kuyeyuka ni uongo, wala hamna pumzi ndani yake, ni ubatili tu, ni kazi za udanganyifu.”—Yeremia 10:5, 14, 15.
Maoni ya Katoliki
Ni kweli kwamba, wengi wanaozisujudia, wanaosali na kuziwashia mishuma, na kuzibusu sanamu za kidini hawajioni wenyewe kuwa waabudu wa sanamu. Kwa mfano, Wakatoliki hudai kwamba wao huzipa sanamu za Kristo na Mariamu heshima, si kwa sababu sanamu hizo zenyewe huwa na uungu wowote, bali kwa sababu ya wale wanaowakilishwa na sanamu hizo. The World Book Encyclopedia hutaarifu kwamba “katika Kanisa la Katoliki ya Kiroma, sanamu huheshimiwa kuwa ufananisho wa watu wanaowakilishwa nazo.” Makasisi Wakatoliki wamehubiri kwamba inafaa kuzipa sanamu heshima maadamu heshima hiyo ni ya hali ya chini kwa ile inayowiwa na Mungu mwenyewe.
Ukweli ni kwamba sanamu hizo zinapewa heshima. Hata New Catholic Encyclopedia hukiri kwamba heshima kama hiyo ni “kitendo cha ibada.” Hata hivyo, Yesu Kristo alifutilia mbali matumizi ya sanamu kuwa misaada katika kumkaribia Mungu aliposema hivi: “Mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” (Yohana 14:6) Haishangazi basi, kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walikataa kata kata matumizi ya sanamu katika ibada.
Hata hivyo, leo dini za Jumuiya ya Wakristo hupita nyingine zote katika wingi wa sanamu. Naam, ujapokuwa ushuhuda wote wa kihistoria na wa Kimaandiko unaofunua upumbavu wa kuzipa sanamu heshima, wale wanaodai kuwa Wakristo ulimwenguni pote huendelea kusujudu na kusali mbele ya sanamu katika kutafuta-tafuta kwao Mungu kwa moyo mweupe. Kwa nini?
Wavutwa na Adui
Nabii Isaya alitaarifu kwamba waabudu wa sanamu wa siku yake walishindwa kuona upumbavu wa vitendo vyao kwa sababu macho yao yalikuwa ‘yamefumbwa, wasione, na mioyo yao, wasiweze kufahamu.’ (Isaya 44:18) Ni nani angeweza kuwa na uvutano huo juu ya wanadamu? Baraza la kiikonoklasti (uvunjaji sanamu) la 754 W.K., lilitangaza rasmi kwamba kuzipa sanamu heshima kuliletwa na Shetani kwa kusudi la kumvuta mwanadamu mbali na Mungu wa kweli. Je! mkataa huo ulikuwa sahihi?
Ndiyo, kwa kuwa unapatana na Biblia iliyopuliziwa roho, iliyotaarifu karne kadhaa mapema zaidi kwamba adui mkuu wa Mungu, Shetani Ibilisi, “amepofusha fikira” za watu ili kweli “isiwazukie.” (2 Wakorintho 4:4) Kwa hiyo mtu anapoipa sanamu heshma, badala ya kumkaribia Mungu zaidi, kwa kweli anatumikia masilahi ya roho waovu.—1 Wakorintho 10:19, 20.
Kumkaribia Mungu Zaidi
Sanamu haziwezi kutusaidia kumkaribia Mungu zaidi. Muumba Mtukufu, Yehova Mungu, huchukia heshima inayopewa sanamu. (Kumbukumbu la Torati 7:25) “BWANA [Yehova, NW] ni Mungu mwenye wivu.” (Nahumu 1:2) Asema hivi: “Mimi ni BWANA [Yehova, NW]; ndilo jina langu; na utukufu wangu sitampa mwingine, wala sitawapa sanamu sifa zangu.” (Isaya 42:8) Kulingana na hilo, Biblia huonya kwamba wale wanaozipa sanamu heshima “hawataurithi ufalme wa Mungu.”—Wagalatia 5:19-21.
Hata hivyo, Yehova ni Mungu mwenye rehema na mwenye kusamehe pia. Biblia husema juu ya wale waliomgeukia Mungu kutoka kwa sanamu zao na wakatangazwa rasmi kuwa waadilifu baada ya kuacha mazoea yao ya ibada ya sanamu. (1 Wakorintho 6:9-11; 1 Wathesalonike 1:9) Walitii maneno ya Yesu: “Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa wamwabudu katika roho na kweli.”—Yohana 4:24.
Funzo la bidii la Biblia litafunua kwamba si vigumu kumkaribia Mungu zaidi. (Matendo 17:26-28) Yeye ana utu mchangamfu, wenye upendo, na wenye kukaribika, na hutukaribisha na kututazamia sisi tusitawishe uhusiano wa ukaribu sana pamoja naye.—Isaya 1:18.
Mashahidi wa Yehova wanakukaribisha upate kumjua Baba yetu wa kimbingu akiwa Mtu, kujifunza kuhusu jina lake, Yehova, na kuhusu sifa zake na utendaji wake pamoja na ainabinadamu. Kupitia kurasa za Neno lake, Biblia, utapata kufahamu ni kwa nini huhitaji kwa kweli misaada yenye kuonekana, kama vile sanamu-umbo na picha, ili kumkaribia Mungu. Naam, “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Wanahistoria Wanaonelea Kwamba: . . .
◻“Ni jambo linalojulikana sana kwamba Ubuddha, ulioanzishwa katika karne ya sita KWK, haukuona sanamu ya kwanza ya mwanzilishi wao mpaka karibu karne ya kwanza WK.”
“Kwa karne kadha, mapokeo ya Kihindu kwa msingi yalikuwa bila matumizi ya sanamu.”
“Uhindu na Ubuddha zote mbili zilianza bila matumizi ya sanamu na zilikubali sanamu katika ibada yazo pole kwa pole tu. Ukristo ulifanya vivyo hivyo.”—The Encyclopedia of Religion, ya Mircea Eliade.
◻“Kutokana na masimulizi mbalimbali ya Biblia ni wazi kwamba ibada ya kweli ya Mungu haikuwa na sanamu. . . . katika AJ [Agano Jipya], pia, ibada ya miungu na sanamu za kigeni hukatazwa.”—New Catholic Encyclopedia.
◻ “Sanamu hazikujulikana katika ibada ya Wakristo wa mapema.”—Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature, ya McClintock and Strong.
◻ “Wala katika Agano Jipya, wala katika maandiko yoyote ya kweli ya enzi ya kwanza ya Ukristo, hamwezi kupatikana ishara yoyote ya utumizi wa sanamu-umbo au picha katika ibada ya Wakristo, iwe ya wazi au ya faraghani.”—A Concise Cyclopedia of Religious Knowledge, ya Elias Benjamin Sanford.
◻ “Wakristo wa mapema wangalitazama kwa hofu dokezo tu la kuweka sanamu katika makanisa, na wangaliona kusujudu au kusali mbele yazo kuwa sawa na ibada ya sanamu.”—History of the Christian Church, ya John Fletcher Hurst.
◻ “Katika kanisa la mapema, kufanyiza na kuzipa picha za Kristo na watakatifu heshima kulipingwa muda wote.”—The New Encyclopædia Britannica.
◻ “Ingawa Kanisa la mapema halikuchukia sanaa, hata hivyo halikuwa na sanamu za Kristo.”—Schaff-Herzog Encyclopedia of Religious Knowledge.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Yesu alikazia kwamba Mungu anatafuta wale ‘wanaomwabudu Baba katika roho na kweli’