Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 3/15 kur. 18-23
  • Uhuru wa Kupewa na Mungu Waleta Shangwe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uhuru wa Kupewa na Mungu Waleta Shangwe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Shangwe ya Yehova Ndiyo Nguvu Yetu
  • Thamini Uhuru wa Kupewa na Mungu
  • Tumikianeni Katika Upendo
  • Kutofautisha Matunda
  • Sababu Nyingine za Kuwa na Shangwe
  • Kubarikiwa na Msaada Uliopo Kila Wakati
  • Thamini Uhuru Wako wa Kupewa na Mungu
  • Shangwe ya Yehova ni Ngome Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Usikose Kusudi la Uhuru wa Kupewa na Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Tumikia Yehova kwa Shangwe ya Moyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Mtumikie Yehova kwa Moyo Wenye Kujaa Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 3/15 kur. 18-23

Uhuru wa Kupewa na Mungu Waleta Shangwe

“Furaha [shangwe, “NW”] ya BWANA [Yehova, “NW”] ni nguvu zenu.”—NEHEMIA 8:10.

1. Shangwe ni nini, na ni kwa nini wale waliojiweka wakfu kwa Mungu waweza kuiona?

YEHOVA huijaza shangwe mioyo ya watu wake. Hali hiyo ya shangwe au furaha nyingi hutokana na kutwaa au kutazamia mema. Wanadamu waliojiweka wakfu kwa Mungu waweza kupata hisia kama hiyo kwa sababu shangwe ni tunda la roho takatifu au kani ya utendaji yake. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa hiyo hata ikiwa majaribu yenye kutaabisha yanatukumba, twaweza kuwa wenye shange tukiwa watumishi wa Yehova, wanaoongozwa na roho yake.

2. Ni kwa nini Wayahudi walishangilia kwenye pindi maalum katika siku ya Ezra?

2 Katika pindi maalum katika karne ya tano K.W.K., Wayahudi waliutumia uhuru wao wa kupewa na Mungu kufanya Sikukuu ya Vibanda yenye shangwe katika Yerusalemu. Baada ya Ezra na Walawi wengine kusoma na kuwaelezea Sheria ya Mungu, “watu wote wakaenda zao kula na kunywa, na kuwapelekea watu sehemu, na kufanya furaha [kushangilia kukubwa, NW] nyingi, kwa sababu walikuwa wameyafahamu maneno yale waliyohubiriwa.”—Nehemia 8:5-12.

Shangwe ya Yehova Ndiyo Nguvu Yetu

3. “Shangwe ya Yehova” yaweza kuwa nguvu zetu chini ya hali zipi?

3 Katika sikukuu hiyo, Wayahudi walitambua ule ukweli wa yale maneno: “Furaha [shangwe, NW] ya BWANA [Yehova, NW] ni nguvu zenu.” (Nehemia 8:10) Shangwe hiyo ndiyo nguvu zetu pia ikiwa tunasimama imara kwa ajili ya uhuru wa kupewa na Mungu tukiwa Mashahidi wa Yehova waliojiweka wakfu, na kubatizwa. Wachache wetu wamepakwa mafuta kwa roho takatifu na kupata kufanywa wana katika familia ya Mungu kuwa warithi wenzi wa kimbingu pamoja na Kristo. (Warumi 8:15-23) Walio wengi wetu leo wana lile taraja la uhai katika paradiso ya kidunia. (Luka 23:43) Twapaswa kuwa wenye shangwe kama nini!

4. Ni kwa nini Wakristo waweza kuvumilia mateso na minyanyaso?

4 Ingawa tuna matarajio mazuri ajabu, si jambo rahisi kuvumilia mateso na minyanyaso. Hata hivyo, twaweza kufanya hivyo kwa sababu Mungu hutupa sisi roho takatifu yake. Tukiwa nayo tuna shangwe na usadikisho kwamba hakuna lolote liwezalo kutunyang’anya tumaini letu au upendo wa Mungu. Isitoshe, twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakuwa nguvu zetu maadamu twampenda kwa moyo, nafsi, nguvu, na akili zetu zote.—Luka 10:27.

5. Twaweza kupata wapi sababu za kushangilia?

5 Watu wa Yehova hufurahia mibaraka mingi na wana sababu nyingi za kushangilia. Baadhi ya sababu za shangwe zinadokezwa katika barua ya Paulo kwa Wagalatia. Nyinginezo zinaonyesha mahali pengine katika Maandiko. Itatuchangamsha kuchunguza mibaraka hiyo yenye shangwe.

Thamini Uhuru wa Kupewa na Mungu

6. Ni kwa nini Paulo aliwasihi Wakristo Wagalatia wasimame imara?

6 Tukiwa Wakristo, tuna ile baraka yenye shangwe ya kuwa na msimamo wenye kukubalika pamoja na Mungu. Kwa kuwa Kristo aliwaweka wafuasi wake huru na Sheria ya Musa, Wagalatia walisihiwa wasimame imara na kutojiruhusu kufungwa katika ile “nira ya utumwa.” Vipi na sisi? Ikiwa tulijaribu kutangazwa rasmi kuwa waadilifu kwa kufuata Sheria, tungetenganishwa na Kristo. Hata hivyo, tukiwa tumesaidiwa na roho ya Mungu, twangojea ule uadilifu uliotumainiwa unaotokana na imani inayotenda kupitia upendo, si kutokana na tohara ya kimwili au matendo mengine ya Sheria.—Wagalatia 5:1-6.

7. Twapaswa kuonaje utumishi mtakatifu wa Yehova?

7 Ni baraka kutumia uhuru wetu wa kupewa na Mungu ‘kumtumikia Yehova kwa kushangilia.” (Zaburi 100:2) Kwa kweli, ni pendeleo lisilokadirika kutoa utumishi mtakatifu kwa “Yehova Mungu, Mweza Yote,” aliye hasa “Mfalme wa umilele”! (Ufunuo 15:3, NW) Ukipatwa na hisia za kutojistahi sana, huenda ikasaidia kung’amua kwamba Mungu amekuvuta kwake mwenyewe kupitia Yesu Kristo na kukupa sehemu katika “ile kazi takatifu ya habari njema ya Mungu.” (Warumi 15:16, NW; Yohana 6:44; 14:6) Hizo ni sababu zilizoje za shangwe na shukrani kwa Mungu!

8. Watu wa Mungu wana sababu gani ya shangwe, kwa habari ya Babuloni Mkubwa?

8 Sababu nyingine ya shangwe ni uhuru wetu wa kupewa na Mungu kutoka Babuloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini bandia. (Ufunuo 18:2, 4, 5) Ingawa kahaba huyo wa kidini kwa ufananisho ‘huketi juu ya maji mengi,” ikimaanisha kwamba “jamaa na makutano na mataifa na lugha,” yeye haketi juu ya, au kuvuta na kudhibiti kidini, watumishi wa Yehova. (Wagalatia 17:1, 15) Tunashangilia katika nuru ya Mungu iliyo nzuri ajabu, huku waungaji mkono wa Babuloni Mkubwa wakiwa katika giza la kiroho. (1 Petro 2:9) Naam, huenda ikawa vigumu kuyaelewa baadhi ya “mafumbo ya Mungu.” (1 Wakorintho 2:10) Lakini sala zitolewazo ili kupata hekima na msaada kwa roho takatifu hutusaidia kufahamu kweli ya Kimaaniko inayoweka huru kiroho wenye kuwa nayo.—Yohana 8:31, 32; Yakobo 1:5-8.

9. Ikiwa tutaonea shangwe baraka za uhuru wenye kuendelea kutoka katika makosa ya kidini, ni lazima tufanye nini?

9 Tunaonea shangwe uhuru wenye kuendelea kutoka katika makosa ya kidini, lakini ili kudumisha uhuru huo, ni lazima tukatalie mbali uasi-imani. Wagalatia walikuwa wamepiga vema mbio ya Kikristo, lakini wengine walikuwa wakiwazuia wasiitii kweli. Uvutano huo mbovu wenye kusadikisha haukutoka kwa Mungu na ulipaswa ukinzwe. Kama vile chachu kidogo huchachua donge zima, walimu bandia au mwelekeo upande wa uasi-imani waweza kufisidi kundi zima. Paulo alitaka kwamba watetezi wa tohara waliojaribu kukengeusha imani ya Wagalatia wasitahiriwe tu bali wakatwe viungo vya uzazi. Maneno makali kweli kweli! Lakini twapaswa kuwa imara vivyo hivyo katika kukataa uasi-imani ikiwa tutadumisha uhuru wetu wa kupewa na Mungu kutoka katika makosa ya kidini.—Wagalatia 5:7-12.

Tumikianeni Katika Upendo

10. Daraka letu ni jipi tukiwa sehemu ya udugu wa Kikristo?

10 Uhuru wa kupewa na Mungu umetuleta katika ushirika pamoja na udugu wenye upendo, lakini ni lazima tufanye sehemu yetu tuonyeshe upendo. Wagalatia hawakupaswa watumie uhuru wao kuwa “sababu ya kuufuata mwili” au udhuru wa ubinafsi usio wenye upendo. Walitakiwa watumikiane wakisukumwa na upendo. (Mambo ya Walawi 19:18; Yohana 13:35) Ni lazima sisi pia tuepuke yale masengenyo na chuki inayoweza kutokeza katika kuangamizana kwetu. Pasipo shaka, hilo halitatukia ikiwa tunaonyesha upendo wa kidugu.—Wagalatia 5:13-15.

11. Twaweza kuwa baraka kwa wengine jinsi gani, na wao waweza kutubarikije?

11 Kwa kuonyesha uhuru wetu wa kupewa na Mungu kupatana na miongozo ya roho ya Mungu, tutaonyesha upendo na kuwa baraka kwa wengine. Lapasa kuwa zoea kwetu kujiruhusu kudhibitiwa na kuongozwa na roho takatifu. Kisha hatutaelekea kutaka kutosheleza mnofu wetu wenye dhambi ambao “hutamani ukishindana na Roho.” Ikiwa tunaongozwa na roho ya Mungu, tutafanya mambo ya upendo lakini si kwa sababu kanuni huhitaji kufuatwa na huwapa watenda mabaya adhabu. Kwa mfano, upendo—siyo sheria tu—itatuzuia tusiwe wenye kuwachongea wengine. (Mambo ya Walawi 19:16)Upendo utatusukuma tuseme na kutenda katika njia za fadhili. Kwa sababu tunaonyesha tunda la roho la upendo, wengine watatubariki, au kusema mema juu yetu. (Mithali 10:6) Isitoshe, ushirika pamoja nasi utakuwa baraka kwao.—Wagalatia 5:16-18.

Kutofautisha Matunda

12. Ni baadhi gani ya mibaraka inayoshirikishwa na kuepuka “matendo ya mwili” ya dhambi?

12 Mibaraka mingi inayoshirikiswa na uhuru wetu wa kupewa na Mungu hutokana na kuepuka “matendo ya mwili.” Tukiwa watu wa Mungu, sisi, kwa ujumla, huepuka uchungu mwingi kwa sababu hatuzoei uasherati, uchafu, na mwenendo mbaya. Kwa kuepuka ibada ya sanamu, tuna ile shangwe inayotokana na kumpendeza Yehova katika jambo hilo. (1 Yohana 5:21) Kwa kuwa hatuzoei uwasiliani-roho, tuko huru na utawala wa roho waovu. Udugu wetu wa Kikristo hauharibiwi na uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, migawanyiko, mafarakano, na husuda. Na shangwe yetu haipotei katika ulevi na karamu za ulevi na ulafi. Paulo alionya kwamba wale waliokuwa wakiyazoea matendo hayo ya mwili hawataurithi Ufalme wa Mungu. Hata hivyo kwa sababu sisi hutii maneno yake, tutashikamana na tumaini la Ufalme lenye shangwe.—Wagalatia 5:19-21.

13. Roho takatifu ya Yehova hutokeza matunda gani?

13 Uhuru wa kupewa na Mungu hutuletea shangwe kwa sababu Wakristo huonyesha matunda ya roho ya Yehova. Kutokana na maneno ya Paulo kwa Wagalatia, ni rahisi kuona kwamba matendo ya mwili wenye dhambi yako kama miiba yanapotofautishwa na matunda ya roho yaliyo mazuri sana ya upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujidhibiti yanayokazwa imara katika mioyo ya wenye kumtii Mungu. Tukiwa na azimio la kuishi kinyume cha tamaa za mwili wenye dhambi, twataka kuongozwa na roho ya Mungu na kuishi kulingana nayo. Roho hutufanya tuwe wanyenyekevu na wenye amani, si ‘wenye kujisifu bure, tukichokozana na kuhusudiana.’ Haishangazi kwamba ni shangwe kushiriki pamoja na wale wanaoonyesha matunda ya roho!—Wagalatia 5:22, 23.

Sababu Nyingine za Kuwa na Shangwe

14. Ni silaha gani tunazohitaji katika pigano letu dhidi ya majeshi ya roho waovu?

14 Inayoshirikiana pamoja na uhuru wetu wa kiroho wa kupewa na Mungu ni ile baraka ya ulinzi dhidi ya Shetani na roho wake waovu. Ili tufanikiwe katika kushindana kwetu mweleka dhidi ya majeshi ya roho waovu, ni lazima tuvae “suti ya silaha kamili kutoka kwa Mungu.” Tunahitaji mshipi wa kweli na bamba la chuma la kifuani la uadilifu. Ni lazima nyayo zetu zivishwe kama viatu vifaa vya habari njema za amani. Inayohitajika pia ni ile ngao kubwa ya imani, ambayo kwayo twaweza kuyazima makombora yenye moto ya yule mwovu. Ni lazima tuvae kofia ya chuma ya kukinga kichwa ya wokovu na kutumia “upanga wa roho,” Neno la Mungu. Acheni pia ‘tuendelee kusali kila pindi katika roho.’ (Waefeso 6:11-18, NW) Tukivaa silaha hizo za kiroho na kukataa ushetani, twaweza kuwa bila woga na kuwa wenye shangwe.—Linganisha Matendo 19:18-20.

15. Ni baraka gani yenye shangwe iliyo yetu kwa sababu tunajiendesha wenyewe kulingana na Neno la Mungu?

15 Shangwe ni yetu kwa sababu mwenendo wetu hupatana na Neno la Mungu, na sisi tuko huru na hatia inayowasumbua watenda mabaya wengi. ‘Tunajizoeza katika neno hili tuwe na dhamiri isiyo na hatia mbele za Mungu na mbele za watu sikuzote.’ (Matendo 24:16) Kwa hiyo, hatuhitaji kuhofu kile kisasi cha kimungu kitakachowajia hivi karibuni watenda dhambi wa makusudi wasiotubu. (Mathayo 12:22-32; Waebrania 10:26-31) Kwa kutumia lile shauri la Mithali 3:21-26, twapata kutambua utimilizo wa maneno hayo: “Shika hekima kamili na busara. Basi yatakuwa uzima kwa nafsi yako, na neema shingoni mwako. Ndipo utakapokwenda katika njia yako salama, wala mguu wako hautakwaa. Ulalapo hutaona hofu; naam utalala na usingizi wako utakuwa mtamu. Usiogope hofu ya ghafula, wala uharibifu wa waovu utakapofika. Kwa kuwa BWANA [Yehova, NW] atakuwa tumaini lako, naye atakulinda mguu wako usinaswe.”

16. Sala ni sababu ya kuwa na shangwe jinsi gani, na roho ya Yehova ina sehemu gani katika jambo hilo?

16 Sababu nyingine ya shangwe ni uhuru wetu wa kupewa na Mungu wa kumkaribia Yehova katika sala tukiwa na uhakikisho kwamba tutasikiwa. Ndiyo, sala zetu hujibiwa kwa sababu tuna ile “hofu ya Yehova” yenye kicho. (Mithali 1:7, NW) Isitoshe, tunasaidiwa kuendelea kuwa katika upendo wa Mungu kwa “kuomba katika Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].” (Yuda 20, 21) Twafanya hivyo kwa kudhihirisha hali ya moyo inayokubalika na Yehova na kwa kuomba chini ya uvutano wa roho mambo yanayopatana na mapenzi yake na Neno lake, linalotuonyesha jinsi ya kusali na mambo ya kuomba katika sala. (1 Yohana 5:13-15) Ikiwa tunajaribiwa sana na hatujui mambo ya kuomba, ‘roho naye hutusaidia udhaifu wetu, hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa.’ Mungu hujibu sala za jinsi hiyo. (Warumi 8:26, 27) Acheni tusali ili kupata roho takatifu na kuiruhusu itokeze ndani yetu matunda yayo yanayohitajika hasa ili kukabili jaribu fulani. (Luka 11:13) Tutaongeza shangwe yetu pia tukijifunza kwa sala na kwa bidii-nyendelevu Neno la Mungu lenye kupuliziwa roho na vichapo vya Kikristo vilivyotayarishwa chini ya mwongozo wa roho.

Kubarikiwa na Msaada Uliopo Kila Wakati

17. Yaliyompata Musa na pia maneno ya Daudi huonyeshaje kwamba Yehova yuko pamoja na watu wake?

17 Kwa kuutumia uhuru wetu wa kupewa na Mungu inavyofaa, tuna shangwe ya kujua kwamba Yehova yu pamoja nasi. Hali mbaya sana zilipomfanya Musa aondoke Misri, kwa imani “alistahimili kama amwonaye yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:27) Musa hakutembea peke yake; alijua kwamba Yehova alikuwa pamoja naye. Vivyo hivyo, wana wa Kora waliimba hivi: “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, ijapopepesuka milima kwa kiburi chake.” (Zaburi 46:1-3) Ikiwa una imani kama hiyo katika Mungu, yeye hatakuacha kamwe. Daudi alisema hivi: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA [Yehova, NW] atanikaribisha kwake.” (Zaburi 27:10) Ni shangwe iliyoje kujua kwamba Mungu hujali watumishi wake sana sana!—1 Petro 6:6, 7.

18. Ni kwa nini wale walio na shangwe ya Yehova huwa na uhuru wa kupewa na Mungu kutoka katika mahangaiko mengi mno?

18 Tukiwa na shangwe ya Yehova, tuna uhuru wa kupewa na Mungu kutoka katika mahangaiko mengi mno. “Msijisumbue kwa neno lo lote,” akasema Paulo, “bali katika kila neno kwa kusali na kuomba pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Amani ya Mungu ni utulivu usio na kifani hata katika hali zenye kujaribu zaidi. Tukiwa nayo mioyo yetu hubaki mitulivu—jambo linalotufaa kiroho, kihisia-moyo, na kimwili. (Mithali 14:30) Hiyo hutusaidia pia kudumisha usawaziko wa kiakili, kwani twajua kwamba hakuna lolote ambalo Mungu huruhusu liwezalo kutudhuru daima. (Mathayo 10:28) Amani hiyo inayotokana na uhusiano wa ukaribu pamoja na Mungu kupitia Kristo ni yetu kwa sababu tumejiweka wakfu kwa Yehova na kujitiisha kwa mwongozo wa roho yake, inayotokeza matunda kama vile shangwe na amani.

19. Ni kukazia mioyo yetu nini kutatusaidia kuwa wenye shangwe?

19 Kukazia mioyo yetu uhuru wetu wa kupewa na Mungu na tumaini la Ufalme kutatusaidia tuwe wenye shangwe. Kwa mfano, nyakati nyingine twaweza kufanya kidogo kuhusu afya mbaya, lakini twaweza kusali ili kupata hekima na imara ya kukabiliana nayo na huenda tukapata faraja katika kufikiria afya ya kiroho tunayoonea shangwe na maponyo ya kimwili yatakayotukia chini ya utawala wa Ufalme. (Zaburi 41:1-3; Isaya 33:24) Ingawa huenda tukalazimika kuvumilia upungufu wa mahitaji leo, hakutakuwako ukosefu wa mahitaji ya maisha katika ile dunia-Paradiso iliyo karibu sana. (Zaburi 72:14, 16; Isaya 65:21-23) Naam, Baba yetu wa kimbingu atatutegemeza sasa na kukamilisha shangwe yetu hatimaye.—Zaburi 145:14-21.

Thamini Uhuru Wako wa Kupewa na Mungu

20. Kulingana na Zaburi 100:1-5, twapaswa kujitokezaje mbele za Yehova?

20 Tukiwa watu wa Yehova, kwa hakika twapaswa kuthamini ule uhuru wa kupewa na Mungu ambao umetuletea shangwe na mibaraka mingi. Si ajabu kwamba Zaburi 100:1-5, HNWW, hutusihi tuje mbele za Mungu ‘tukiimba kwa shangwe.’ Sisi ni mali ya Yehova na yeye atujali akiwa Mchungaji mwenye upendo. Naam, “sisi ni watu wake, na kondoo wa malisho yake.” Uumbaji na sifa zake tukufu hutuandalia kichocheo cha kuingia nyua za patakatifu pake tukiwa na sifa na shukrani. Tunasukumwa “kulisifu jina lake,” kusema mema juu ya Yehova Mungu. Zaidi ya hayo, twaweza sikuzote kutegemea fadhili zake za upendo, au huruma yake, kwetu. “Vizazi vyote” Yehova ni mwaminifu, thabiti katika kuwaonyesha upendo wale wafanyao mapenzi yake.

21. Ni kitia-moyo gani kilichotolewa katika toleo la kwanza la gazeti hili, na twapaswa kufanya nini kuhusu uhuru wa kupewa na Mungu?

21 Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, hatuwezi sasa kuponyoka majaribu yote. Hata hivyo, kwa msaada wa kimungu, twaweza kuwa Mashahidi wa Yehova wenye moyo mkuu na wenye shangwe. Yenye kutokeza katika habari hiyo ni haya maneno yanayopatikana katika toleo la kwanza la jarida hili (Julai 1879, Kiingereza): “Uwe na moyo mkuu . . . ndugu au dada yangu Mkristo, unayejaribu kwa bidii kupiga mbio katika ile njia nyembamba. Usiione njia hiyo kuwa ngumu; imetakaswa na kutukuzwa na miguu ya Bwana yenye kubarikiwa. Ona kila jambo lililo kama mwiba kuwa ua; kila jambo lililo kama mwamba wenye ncha kali kuwa jiwe la kuonyesha maendeleo, likikuharakisha kuelekea mradi wako. . . . Kazia zawadi jicho lako.” Mamilioni wanaomtumikia Yehova sasa hukazia zawadi macho yao na wana sababu nyingi za kuwa na moyo mkuu na kuwa wenye shangwe. Pamoja nao, simama imara kwa ajili ya uhuru wa kupewa na Mungu. Usikose kusudi lao, na ile shangwe (furaha) ya Yehova na iwe nguvu zako sikuzote.

Ungejibuje?

◻ “Furaha [shangwe, NW] ya Yehova” yaweza kuwa nguvu zetu jinsi gani?

◻ Kusema kidini, uhuru wa kupewa na Mungu umewaletea watu wa Yehova mibaraka gani?

◻ Kwa nini tutumikiane kwa upendo?

◻ Ni mibaraka gani iliyoshirikishwa na uhuru wa kupewa na Mungu?

◻ Watu wa Mungu waweza kubakije wakiwa wenye shangwe?

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Ona kila jambo lililo kama mwiba kuwa ua; kila jambo lililo kama mwamba wenye ncha kali kuwa jiwe la kuonyesha maendeleo, likikuharakisha kuelekea mradi wako”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki