Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 4/1 kur. 20-23
  • Njia ya Yehova Ndiyo Njia Bora Zaidi ya Kuishi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Njia ya Yehova Ndiyo Njia Bora Zaidi ya Kuishi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Urithi wa Kikristo
  • Kumbukumbu za Mapema
  • Shule na Uamuzi wa Maana
  • Kupainia na Utumishi wa Betheli
  • Kudumisha Kutokuwamo
  • Mapendeleo Mbalimbali ya Utumishi
  • Maisha Bora, Yenye Kuthawabisha
  • Tulitanguliza Utumishi wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Tuliazimia Kumtumikia Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Maisha Yenye Baraka Tele na Yenye Kuthawabisha Katika Utumishi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Nguvu za Mungu Zimeonekana Wazi Kupitia Udhaifu Wangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 4/1 kur. 20-23

Njia ya Yehova Ndiyo Njia Bora Zaidi ya Kuishi

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ERKKI KANKAANPÄÄ

TOKEA wakati nilikuwa mtoto, mradi wangu ulikuwa kutumika katika tawi la Finlandi la Mashahidi wa Yehova, au Betheli kama inavyoitwa. Hivyo wakati mwangalizi asafiriye aliponiuliza katika kiangazi cha 1941, “Una mipango gani kwa wakati ujao?“ Mimi nilijibu: “Sikuzote mimi nimetaka kwenda Betheli.”

“Afadhali usahau ndoto hizo; hutaalikwa kamwe,” akasema. Mwanzoni nilikatishwa tamaa sana, lakini ndipo nikaamua kuacha mambo mikononi mwa Yehova. Miezi michache baadaye, nilipokea mwaliko wa kutumika katika Betheli.

Nilikuwa mvulana mwenye haya wa mashambani mwenye miaka 17 nilipopiga kengele kwenye ofisi ya tawi katika Helsinki katika siku nyangavu, yenye baridi sana ya Novemba katika 1941. Upesi nikawa napokewa kwa furaha na Kaarlo Harteva, mwangalizi wa tawi. Wakati huo tawi lilikuwa na uangalizi juu ya Mashahidi 1,135 katika Finlandi.

Urithi wa Kikristo

Katika 1914 baba yangu alikuwa amepata nakala ya kichapo cha Watch Tower The Divine Plan of the Ages. Hata hivyo, vita ya kwanza ya ulimwengu ilifyatuka upesi baada ya hapo, naye hakupata wakati wa kukisoma.

Kupigania uhuru kwa Finlandi kulitokeza magumu. Vikundi viwili vyenye nguvu—Weupe na Wekundu—vikaundwa. Weupe waliwakilisha wabepari na jamii ya kati, hali Wekundu waliwakilisha wafanyakazi. baba yangu alijaribu kutokuwamo, asijiunge na chochote cha vikundi vyote viwili. Hata hivyo, vyote viwili vilimworodhesha kuwa mshukiwa.

Kama ilivyothibitika kuwa hatimaye, mara mbili baba alikuwa amehukumiwa kunyongwa, kwanza na Weupe kisha na Wekundu. Wakati mmoja, mtu fulani alipouawa, naye mwuaji hakuweza kushikwa, vijana kumi, kutia baba yangu walihukumiwa kifo. Mmoja wa waalimu wa baba yangu, aliyekuwa mshiriki wa kamati ya hukumu, akapendekeza msamaha kwa ajili yake, nao ukatolewa. Wale vijana wengine tisa wakanyongwa.

Katika pindi nyingine baba alisamehewa tena hukumu ya kifo. Baada ya hapo akaamua kujificha, kihalisi! Yeye na ndugu yake walichimba shimo, ambamo walikaa mpaka vita ilipokwisha. Ili kuendelea kuwa hai, ndugu yao mdogo aliwaandalia chakula na kinywaji.

Vita ilipokwisha katika 1918, baba alioa na kujenga makao karibu na shimo hilo. Baadaye nilipata kufahamiana sana nalo, kwa kuwa lilipata kuwa uwanja wangu wa michezo. baba aliniambia kwamba alisali sana alipokuwa amejificha humo chini ya ardhi. Aliahidi Mungu kwamba akipata kujifunza wakati wowote jinsi ya kumtumikia Yeye, atafanya hivyo.

Upesi baada ya kuoa, baba aliamua kuchukua kitu fulani cha kusoma aende nacho katika safari yake ya kikazi. Katika orofa ya juu kabisa, alipata The Divine Plan of the Ages alichokuwa amenunua miaka mingi iliyopita. Akakifungua kwenye sura “Siku ya Yehova” na kukisoma. Aliendelea kujiambia: ‘Hii ndiyo kweli, hii ndiyo kweli.’ Akishuka kutoka orofani, alimwambia mamangu: “Nimepata dini ya kweli.”

Karibu mara hiyo baba akaanza kuwahubiria wengine mambo aliyokuwa akijifunza, kwanza akanena na watu wa familia na jirani zake. Kisha akaanza kutoa hotuba za watu wote. Upesi wengine katika eneo hilo waka-jiunga naye. Baada ya kuwasiliana na Wanafunzi wa Biblia kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati ule, baba akabatizwa katika 1923. Wakati sisi watoto tulipozaliwa—hatimaye tulikuwa wanne—baba hakupuuza kutufundisha. Kwa kweli, baada ya kundi kufanyizwa, tulitakwa tuhudhurie kila mkutano.

Kumbukumbu za Mapema

Kumbukumbu langu la mapema ni kusanyiko lililopangwa katika kundi la nyumbani kwetu katika 1929, nilipokuwa wa miaka mitano. Watu wengi wakakusanyika kutoka makundi ya karibu, naye mwakilishi kutoka ofisi ya tawi alikuwapo pia. Katika siku hizo ilikuwa desturi, angalau katika Finlandi, kubariki watoto kwenye mikusanyiko. Kwa hiyo ndugu huyo wa kutoka Betheli alibariki watoto, kama alivyofanya Yesu wakati wa huduma yake. Sijasahau hilo kamwe.—Marko 10:16.

Kumbukumbu jingine la mapema ni kukubaliwa kwa jina Mashahidi wa Yehova katika 1931. baba yangu, akijua sana umaana wa pindi hiyo, alisomea kundi kwa uzito tangazo hilo kuhusu jina letu jipya.

Tangu huko nyuma kwa kadiri niwezavyo kukumbuka, nilikuwa nikijiunga na baba katika kazi ya kuhubiri. Mwanzoni, nilikuwa nikimsikiliza tu, lakini hatimaye nikawa nikifanya kazi hiyo mimi mwenyewe. Katika 1935, wakati mwangalizi asafiriye alipotutembelea, nilienda kwa jirani zetu wote nikawaalika wahudhurie mkutano. Pia niliwatolea vijitabu na baadhi yao walivikubali.

Shule na Uamuzi wa Maana

Sisi watoto wanne ni sisi pekee shuleni tuliokuwa na wazazi Mashahidi, nasi mara nyingi tulifanyiwa mzaha kwa sababu ya kutojiunga na vijana wengine katika mwenendo usio wa Kikristo. Ijapokuwa wanashule wenzangu walinishawishi nivute sigareti, sikufanya hivyo kamwe. Pia tuliitwa kwa mzaha Waruseli (Russell alikuwa msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society) au Waharteva (wakati huo Harteva akiwa ndiye mwangalizi wa tawi la Finlandi). Nafurahi kusema kwamba baadhi ya vijana waliotufanyia mzaha wakati mmoja, hatimaye walipata kuwa Mashahidi.

Mwalimu wangu alinitia moyo niendeleze elimu yangu, na katika wakati mmoja nilifikiria kuwa mhandisi. Kisha kukawa na mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova katika Pori katika masika ya 1939, ambao ulileta badiliko kubwa katika maisha yangu. Sote wawili ndugu yangu mdogo, Tuomo, nami tuliweka maisha yetu wakfu kwa Yehova na kuonyesha hivyo kwa ubatizo wa maji kwenye mkusanyiko huo, katika Mei 28, 1939. Kisha, mapema mwa Septemba, Vita ya Ulimwengu ya 2 ikafyatuka.

Hali katika Ulaya zilibadilika haraka sana. Hali kati ya Finlandi na Urusi ikawa yenye hatari. baba yangu alikazia kwamba Har–Magedoni ilikuwa inazidi kukaribia na hivyo akatutia moyo tupainie. Kwa hiyo, katika Desemba 1940, ndugu yangu nami tukaanza kupainia kaskazini mwa Finlandi.

Kupainia na Utumishi wa Betheli

Tulipokuwa tukipainia, tuliishi wakati ulio mwingi na Yrjö Kallio. Alikuwa ndugu ambaye, yapata miaka 30 iliyotangulia, alikuwa amekuwa Mwanafunzi wa Biblia katika Pennsylvania huko United States. Yrjö alikuwa mwenye moyo mchangamfu sana sana, naye alifanya yote awezayo kutuandalia mazingira yenye kupendeza. Ndugu yake wa kimwili, Kyösti Kallio, alitumika akiwa rais wa Finlandi kuanzia 1937 hadi 1940. Yrjö alitwambia kwamba alikuwa amempa ndugu yake ushahidi kamili, akimweleza kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee kwa serikali bora na amani ya ulimwenguni pote, yenye kudumu.

Kadiri wakati ulivyopita, ndivyo tamaa yangu ya kuwa mshiriki wa familia ya Betheli ilikua. Kwa furaha, lijapokuwa onyo la mwangalizi asafiriye dhidi ya kuchochea matumaini yangu, ombi langu la kutumika Betheli lilikubaliwa. Kazi yangu ya kwanza huko ilikuwa ya kutumwa-tumwa. Hata hivyo, upesi nikawa na pendeleo la kutumika katika kiwanda. Humo nilifanya kazi katika idara nyingi, kutia ndani chumba chetu kidogo cha mashine ya kupigia chapa na Idara ya Usafirishaji.

Kudumisha Kutokuwamo

Katika 1942, nikiwa na miaka 18, niliitwa kwa utumishi wa kijeshi. Kwa kuwa nilikataa kushawishwa, nilikuwa na vipindi virefu vya mahoji, katika pindi mbili nikiwa ninalengwa kwa bunduki. Nyakati nyingine jeuri ya kimwili ilitumiwa. Pia, wakati wa pindi ya kuhojiwa, nilifungiwa katika seli ya gereza isiyopashwa joto ambayo ilikuwa baridi sana.

Hatimaye, katika Januari ya 1943, wakati ukafika wangu mimi na Mashahidi wengine kuhukumiwa. Ofisa wa jeshi aliyekuwa ametuhoji akadai kwamba kifungo chetu kisiwe china ya miaka kumi. Kasisi wa kijeshi alitaka hukumu kali hata zaidi, akidai katika barua ‘hukumu ya kifo au wasaliti hao wapelekwe Urusi wakiwa wapelelezi wa jeshi la miavuli [kifo hakika], adhabu ambayo wangestahili.’

Jaribio bandia likapangwa. Nikaitwa mbele ya mahakama na kupewa hukumu ya kifo. Hata hivyo, hiyo ilithibitika kuwa jitihada nyingine ya kunitisha, kwa kuwa baadaye siku hiyo niliitwa mbele ya mahakama tena na kuhukumiwa miaka mitatu na nusu katika gereza. Nilikata rufani, nayo ikapunguzwa kuwa miaka miwili.

Humo gerezani, chakula kilikuwa haba sana, na yalikuwako matisho yenye kuumiza kutoka kwa wanagereza wengine. Mara mbili nilishambuliwa na wagoni-jinsia-moja, lakini kwa tukio zuri niliweza kuponyoka. Mmoja wao alitisha kuniua ikiwa singekubali madai yake. Lakini kama nilivyofanya katika majaribu yangu yote, nilimwita Yehova, naye akanisaidia. Kwa kweli, matisho ya mwanagereza huyo hayakuwa jambo dogo, kwani alikuwa ameua hapo mbeleni. Baada ya kuachiliwa kwake, mtu huyo alifanya uuaji mwingine naye akarudishwa gerezani.

Bila shaka ni kwa sababu Mashahidi wa Yehova wanajulikana kuwa wenye kutumainika kwamba upesi nikapewa mapendeleo fulani. Kazi yangu ilikuwa kuwapa wafungwa wengine chakula, na niliruhusiwa kutembea kotekote katika majengo ya gereza bila kizuizi. Kwa hiyo, si kwamba tu nilikuwa na chakula cha kunitosha mimi mwenyewe bali niliweza pia kuhakikisha kwamba ndugu zangu Wakristo walitunzwa vizuri. Ndugu mmoja hata aliongeza kilo kadhaa alipokuwa gerezani, jambo lililotukia mara chache sana kwa kufikiria upungufu wa chakula!

Niliachiliwa kutoka gerezani katika Septemba 1944, siku ile ile aliyoachiliwa Ndugu Harteva. Kuachiliwa kwangu kulimaanisha kurudia utumishi wangu wa Betheli. Nilifikiri hivi, ‘Kufanya kazi kwa bidii saa 16 katika Betheli ni afadhali zaidi kuliko maisha katika gereza.’ Tangu hapo sijaepa kazi!

Mapendeleo Mbalimbali ya Utumishi

Baadaye katika 1944, nilikutana na Märgit, painia kijana mwenye sura nzuri, ambaye aliitikia kupendezwa kwangu naye, nasi tukaoana katika Februari 9, 1946. Wakati wa mwaka wetu wa kwanza tukiwa tumeoana, mimi nilitumika Betheli huku Margit akiwa anafanya kazi katika Helsinki akiwa painia. Kisha katika Januari 1947 tukapewa mgawo kwenda katika kazi ya mzunguko.

Katika kazi ya kusafiri, mara nyingi tulikaa na familia mbalimbali na kushiriki nao chumba kimoja. Tulijua kwamba walituandalia kilicho bora zaidi walichokuwa nacho cha kutoa, nasi hatukulalamika kamwe. Siku hizo mizunguko ilikuwa midogo, na baadhi ya makundi hayakuwa na Mashahidi wowote waliobatizwa!

Katika 1948 tulialikwa turudie utumishi wa Betheli. Miaka miwili baadaye Wallace Endres akaja Finlandi kutoka United States, na upesi akawekwa rasmi kuwa mwangalizi wa tawi. Alitutia moyo kwa uchangamfu tuendelee kujifunza Kiingereza, jambo ambalo tulifanya. Hivyo, tulialikwa tuhudhurie darasa la kimishonari la 19 la Watchtower Bible School of Gilead, lililoanza huko South Lansing, New York, katika Februari 1952.

Baada ya kuhitimu tulipewa mgawo turudi Finlandi. Hata hivyo, kabla ya kuondoka United States, nilizoezwa kufanya kazi na mashine za kupiga chapa kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York.

Tuliporudi Finlandi, tulipewa mgawo kwenda kwenye kazi ya kusafiri, kisha katika 1955 tukaalikwa turudi kwenye tawi la Finlandi. Mwaka huo nikapata kuwa mwangalizi wa kiwanda, na miaka miwili baadaye, katika 1957, niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa tawi. Tangu 1976, nimetumika nikiwa msawazishi wa Halmashauri ya Tawi la Finlandi.

Kwa furaha, wote wawili baba na mama yangu pia waliendelea kuwa waaminifu kwa Yehova mpaka kifo chao. Baada ya wakati, watu zaidi ya mia moja wa jamaa ya baba walipata kuwa Mashahidi. Na hadi leo hii, ndugu yangu na dada zangu pamoja na familia zao wote wanatumikia Yehova, mmoja wa dada zangu akiwa painia.

Maisha Bora, Yenye Kuthawabisha

Miaka imekuwa ya kazi na kazi zaidi, lakini kazi hiyo, kwa sababu ni kazi ya Mungu, imekuwa bora na yenye kuthawabisha kweli kweli. (1 Wakorintho 3:6-9) Maisha yangu hayakuwa bila matatizo, yenye kupendeza tu. Kumekuwako matata na magumu pia. Mapema sana katika maisha yangu, nilitambua kwamba yakupasa kujifunza kujitia nidhamu. Huwezi sikuzote kufanya utakalo kabisa. Mara nyingi nilisahihishwa, na polepole nikajifunza njia ifaayo ya kuishi.

Kwa mfano, majaribu na kupungukiwa riziki kulikonipata wakati wa vita kulinifunza kuishi bila vitu vya anasa. Nilijifunza kutambua kama kitu fulani ni cha lazima kweli kweli au sivyo. Ningali nina zoea la kujiuliza kama ninahitaji hiki au kile. Kisha nikitambua kwamba si cha lazima kwa vyovyote, sikinunui.

Mwongozo uliotolewa na Yehova kupitia tengenezo lake umekuwa wazi. Nimekuwa na shangwe ya kuona hesabu ya Mashahidi wa Yehova ikikua wakati wa miaka yangu katika tawi la Finlandi kutoka 1,135 kufika zaidi ya 18,000! Kweli kweli, mimi naweza kuona kwamba kazi yangu imebarikiwa, lakini najua kwamba imebarikiwa kwa sababu kazi ni ya Yehova, si yetu. (1 Wakorintho 3:6, 7) Mapema maishani nilichagua njia ya Yehova, nayo imethibitika kweli kweli kuwa ndiyo njia bora zaidi ya kuishi.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Erkki Kankaanpää leo, pamoja na mke wake Margit

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki