Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 8/15 kur. 382-384
  • Tulitanguliza Utumishi wa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tulitanguliza Utumishi wa Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MATOKEO YA KUSHIRIKIANA MWANZONI
  • UTENDAJI WAKATI WA VITA YA ULIMWENGU YA PILI
  • MIKUTANO WAKATI WA VITA
  • NDOA NA JAMAA
  • KUHAMIA ENEO JIPYA
  • KUPATA BARAKA NYINGI ZA YEHOVA
  • Njia ya Yehova Ndiyo Njia Bora Zaidi ya Kuishi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Tuliazimia Kumtumikia Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 8/15 kur. 382-384

Tulitanguliza Utumishi wa Mungu

BABA alikuwa mkulima wa kutoka magharibi ya Finland. Karibu na mwaka 1911 alipewa vitabu fulani na Wanafunzi wa Biblia, waliodai kwamba mwaka 1914 ungekuwa wenye badiliko kubwa la ulimwengu. Mwaka 1912 alitoa jina lake awe akipokea Mnara iva Mlinzi wa Kifinland, akapokea toleo la Desemba 1, 1912, ambalo ndilo lililokuwa la kwanza kuchapwa katika Kifinland.

Hata sasa nina magazeti ya baba yangu ya Mnara wa Mlinzi kuanzia na toleo la kwanza la chapa ya Kifinland. Kwa sababu ya mambo yaliyotukia tangu mwaka 1914, baba aliona wazi kwamba unabii mbalimbali ulikuwa ukitimizwa. Hivyo akawa Mwanafunzi wa Biblia mwenye juhudi, kama Mashahidi wa Yehova walivyokuwa wakiitwa siku hizo.

Mimi nilizaliwa Septemba 7, 1914, nami nakumbuka sana jinsi baba alivyokuwa mwenye bidii ya kuhubiri nilipokuwa mtoto. Alikuwa mwenye shughuli katika mambo ya baraza ya mji, naye alitumia umashuhuri wake katika mtaa kuzitangaza habari njema juu ya ufalme wa Mungu kati ya watu. Hata farasi wake wa kijivujivu, aliyempeleka siku za Jumapili akatoe hotuba za watu wote, alijulikana mahali pengi sana.

MATOKEO YA KUSHIRIKIANA MWANZONI

Nilipokuwa na umri wa miaka kumi na mitatu niliondoka nyumbani nikahudhurie shule katika wilaya nyingine. Kwa hiyo, baba hakuwa karibu kunipa maagizo, kwa hiyo mafundisho ya kilimwengu yakaanza kuongoza kabisa mawazo yangu. Ingawa moyoni mwangu nilimheshimu sana baba, nilikuwa nikitumia mambo niliyojifunza shuleni kujaribu kuhakikisha kwamba imani zake za Biblia zilikuwa na makosa.

Mwaka 1935 niliingia chuo kikuu kiitwacho Helsinki Technical University niendelee na masomo yangu. Makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Finland yako Helsinki, na wakati huo chumba kimoja hakikuwa na mtu. Kwa kuwa baba alikuwa Shahidi, niliruhusiwa kuishi humo kwa muda huku nikienda chuo kikuu.

Ingawa masomo yangu na maisha katika chuo kikuu yalinimalizia wakati mwingi, nilifanya maendeleo mengi kwa sababu ya kuonana daima na washiriki wa jamaa ya Betheli (kama vile iitwavyo jamaa ya wafanya kazi wa makao makuu). Hapo nilijionea mwenyewe jinsi kweli za Biblia zinavyoweza kubadili sana maisha za watu. Roho ya Kikristo iliyoonyeshwa wazi katika Betheli ilianza kugeuza nia yangu kidogo kidogo, na mwishowe Septemba 1939, nikabatizwa nionyeshe kwamba nilikuwa nimejiweka wakf nimtumikie Yehova Mungu. Tangu wakati huo maisha yangu yamejawa na baraka za Yehova na fadhili zake zisizostahilika.

UTENDAJI WAKATI WA VITA YA ULIMWENGU YA PILI

Baadaye katika vuli ya mwaka huo, vita ilitokea kati ya Finland na Urusi. Imani yangu ilijaribiwa mara nyingi nilipokuwa nikieleza sababu gani mimi Mkristo nisingeweza kushiriki katika siasa au vita. Mwishowe nikawa nikifanya kazi katika idara ya ufundi ya Reli ya Taifa huko Helsinki, nami nilistahili kuwa na cheo hicho kwa sababu nilikuwa na sifa za fundi wa mitambo ya mji.

Wakati huo wa vita kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kuhubiri hadharani ilikaribia kukomeshwa kabisa. Tengenezo letu la Kikristo lilivunjwa kwa agizo la mahakma, magazeti yetu yakapigwa marufuku, tukanyang’anywa vitabu vyetu, mwangalizi wa tawi akawekwa kizuizini, na Mashahidi wengi wakatupwa gerezani. Mashahidi wa Yehova walitendwa yote hayo kwa sababu waliendelea kutokuwamo katika vita.

Lakini, Mashahidi waliokuwa huru bado waliendelea kujitahidi walivyoweza. Kwa mfano, kikundi kimoja chetu kilishiriki katika kazi ya pekee kusaidia waliofungwa. Kikundi hicho kiliitwa “Wadhamini wa Mashahidi wa Yehova,” na nyakati nyingine kilikuwa na majina mengine. Kikundi hicho kilifanya kazi gani ya pekee?

Wakati wote wa vita tulipelekea kila mtu maombi, tangu Rais wa Jamhuri mpaka washiriki mmoja mmoja wa Bunge. Tuliomba marufuku juu ya Mashahidi wa Yehova iondolewe au Mashahidi wenye kuteswa wasaidiwe. Wakati wote vita ilipoendelea, hatukufaulu sana, lakini inaelekea tulifaulu sana kutoa ushuhuda. Wakuu wa serikali tuliowatembelea wanatuheshimu na kutustaajabia hata sasa.

Kwa mfano: Mwishoni mwa vita Mashahidi watatu walihukumiwa kufa katika Yugoslavia. Halmashauri ya Mashahidi ilimwendea Waziri wa Mambo ya Nje wa Finland kumweleza kisa hicho, lakini akasema asingeweza kuingilia mambo ya nchi nyingine. Halafu tukamwendea Waziri wa Ulinzi, ambaye tulikuwa tumefahamiana sana naye kwa sababu kabla ya hapo tulihojiana naye mara nyingi. Tulishangaa alipokubali kutusaidia, akamwandikia Rais Tito barua asaidie ndugu zetu Wakristo. Hukumu ya kuwaua iliondolewa.

Miaka michache iliyopita mtu huyo aliyekuwa Waziri wa Ulinzi, ambaye sasa ni mashuhuri akiwa mwandika vitabu na mwalimu wa kuhutubia vyuo katika Finland, alinikaribisha nimtembelee. Hata wakati huo alikumbuka sana kwamba alimwandikia Rais Tito barua asaidie ndugu zetu Wakristo. Alinieleza kwamba hata ikiwa hajafanya tendo lo lote jema maishani mwake, anajua kwamba angalau katika kisa hicho aliokoa maisha za watu watatu, naye hajaacha kufurahia tendo hilo alilolifanya.

MIKUTANO WAKATI WA VITA

Wakati wa vita mikutano yetu yote ya Kikristo ilipigwa marufuku pia, lakini ikawa ikifanywa kwa kawaida. Hata tulikuwa na makusanyiko makubwa. Huenda ukataka kujua jinsi tulivyoweza kufanya hivyo.

Mikutano hiyo ilifanywa katika makusanyiko ya faragha. Kwa mfano, mtu alipewa kadi ya ukaribishaji yenye sahihi yangu kisha ikathibitishwa na Mashahidi wawili wenye kutumainika. Kwa njia hiyo, Mashahidi wote wa Helsinki walipokea ukaribishaji huo baada ya muda mfupi sana, wahudhurie “kusanyiko la faragha.” Mikutano hiyo ilifanywa kwa kawaida katika vyumba vya shirika fulani la wanafunzi. Makusanyiko makubwa yalipangwa kwa njia iyo hiyo. Tuliona kwamba Yehova alitulinda katika mipango hiyo, kwa sababu hata mkutano mmoja haukuzuiwa.

Nyakati nyingine hata tulipelekea wakuu wa serikali barua tukiwa katika mkutano wa namna hiyo. Siku kadha baada ya barua moja kupelekwa na Mashahidi 580, niliagizwa na polisi niende nikahojiwe. Mwenye kunihoji aliishika barua yetu mkononi akadai nimweleze jinsi tulivyofanya mikutano yetu. Alisema kwamba wao walijua karibu mambo yote, hata yaliyosemwa na watu barabarani, kisha akazidi kuuliza: “Imewezekanaje kwamba mwafanya mikutano ya namna hii katikati ya Helsinki na hali sisi hatujui?” Mkutano huo tuliufanya majumba machache tu kutoka makao makuu ya polisi!

NDOA NA JAMAA

Mwaka 1941, vita ilipokuwa ikiendelea kuvuma, nilimwoa Kaisa Alastalo. Alikuwa amekuwa Shahidi muda mrefu kama mimi, akawa ametumikia akiwa mhubiri “painia” (anayetumia saa zisizopungua 90 kwa mwezi akihubiri). Baadaye jamaa yetu ikawa na binti mmoja na wana wanne. Sasa kukawa na kazi ngumu ya kukaza ndani ya watoto wetu kumpenda Yehova Mungu na kutaka kumtumikia.

Jambo la kwanza nililojaribu kukaza katika akili zao ni kumthamini sana Yehova na kundi la watu wake. Kila siku tulianza mambo yetu kwa kuzungumza andiko la Biblia na kusali. Hatukukosa kuhudhuria hata mmoja wa mikutano ya kundi iliyofanywa kila juma, isipokuwa tulipokuwa wagonjwa. Wakati wo wote tulipoelekea kuruhusu watoto wetu waache mambo yaliyokuwa ya kuwafaidi sana kwa sababu ya kuwahurumia, mke wangu alikuwa akisema “Huruma hupotezea watu uhai.” Tulibarikiwa sana’

Mtoto wetu mkubwa, aliye msichana, alituomba ruhusa awe painia alipokuwa na umri wa miaka kumi na mitatu. Tulikubali kwa kumpa sharti la kwamba hakupaswa kuendelea vibaya masomoni wala kuharibu afya yake. Aliendelea vizuri miaka miwili aliyopainia huku akienda shuleni. Mwaka 1957 alitoka shuleni akawa painia wa pekee mbali na nyumbani, katikati ya Finland. Baadaye aliolewa, na sasa anatumikia pamoja na mumewe akiwa mshiriki wa jamaa ya Betheli ya Finland.

KUHAMIA ENEO JIPYA

Miaka ya 1950 Mashahidi wa Yehova walikaribishwa wahamie mahali penye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Jamaa yetu ilikuwa ikilizungumza jambo hilo mara kwa mara. Lakini, kazi yangu ilikuwa nzuri, na tulikuwa na nyumba nzuri kando kando ya Helsinki, mahali palipofaa sana kulelea watoto. Lakini siku moja niliona gazeti likitangazia mafundi wa mitambo kazi katika Reli ya Taifa. Nilikuwa na ujuzi wa kazi katika Reli, nazo nafasi za kazi zilipatikana katika miji ambako Mashahidi walikuwa wachache. Kama kweli tulitaka kuhama tukatumikie kulikokuwa na uhitaji mkubwa zaidi, hiyo ndiyo iliyokuwa nafasi yetu.

Siku moja wakati wa majira ya baridi mwaka 1960 gari kubwa lilikuja nyumbani kwetu tulikokuwa tumekaa miaka kumi, likapakia mali zetu. Tulihamia Seinajoki, karibu maili 250 (kilomita 400) kaskazini ya magharibi ya Helsinki, kulikokuwa na kiungo cha reli. Wakati huo kulikuwa na kundi la Mashahidi kumi na wawili katika mji huo wenye watu 20,000. Mshahara niliopata katika kazi yangu mpya ulipita ule wa zamani kwa theluthi moja tu, lakini jamaa haikupunguziwa furaha na jambo hilo. Mwaka uliofuata tulijenga nyumba, tena tukasaidia kundi lijenge Jumba la Ufalme dogo katika mstari uo huo.

Tulifaulu kuhamisha wavulana kwenye shule nyingine, mazingira ya mashambani yakatuletea afya bora kuliko Helsinki. Sikuzote tulionyesha wavulana wetu walipaswa kujitahidi kufikia mradi unaofaa wa kupainia. Nilifurahi sana wakati mwana wetu mkubwa alipoingia katika kigari kidogo tulichokuwa tumemnunulia akasafiri kwenda kwenye mgawo wake wa upainia kaskazini ya Finland, baada ya kuondoka shuleni mwaka 1961. Baadaye, ndugu yake mdogo alimfuata. Zamu ilipofika ya mwana wetu wa tatu, wengine walijiunga pamoja wakasema naye. Walimwambia, “Hatutatembea nawe upande mmoja wa bara-bara usipokwenda kupainia.”

Mtoto wetu aliye mdogo zaidi alipatwa na ugonjwa mbaya sana alipokuwa na umri wa mwaka mmoja, na miaka ilipozidi kupita ugonjwa ukamzidia. Sasa, akiwa mwenye umri wa miaka 21, amelazwa kitandani. Vilevile hana akili nzuri na hawezi kuongea. Tulimtunza nyumbani alipotimia umri wa miaka tisa, lakini kazi ya kumtunza ikatuzidia mno tukampeleka hospitali ya kisasa mahali ambapo twaweza kumtembelea kwa kawaida. Hivyo, wavulana wale wengine wetu walipoondoka nyumbani wakapainie, mke wangu alipata nafasi mwaka 1970 kuanza kupainia. Alikuwa amekuwa na mradi huo muda fulani, nayo jamaa nzima inathamini juhudi yake katika utumishi wa Yehova.

KUPATA BARAKA NYINGI ZA YEHOVA

Sikuzote nimetaka kusaidia jamaa yangu ifurahie kazi ya kuhubiri wakati wote, nami nimefanya mabadiliko katika kazi yangu ya kimwili kwa kusudi hilo. Mwaka 1967 Msimamizi Mkuu wa Reli alinikaribisha nije Helsinki kusimamia idara fulani na kujiunga na Baraza ya Wasimamizi wa Reli. Nilikubali kwa kumpa masharti mawili.

Kwanza, kwamba ningeweza kuondoka kazini mapema kutosha mwishoni mwa juma nikahudhurie mikutano ya kundi nyumbani. Pili, kwamba nikiisha kumaliza kurekebisha mambo ya usimamizi ambayo niliona ni ya lazima, ningeweza kurudia kazi yangu ya zamani katika Seinajoki. Lakini, miezi sita baadaye nilipokea ukaribishaji niwe Naibu Msimamizi Mkuu. Nilikubali kupandishwa ngazi hivyo kwa kutoa masharti yale yale.

Cheo kipya hicho kilinipa nafasi nyingi za kutolea watu ushuhuda, ambao nisingaliweza kufikia na ujumbe wa Ufalme. Vilevile, watoto wangu mapainia wakawa wakija kututembelea katika nyumba niliyokodi Helsinki au kuhudhuria makusanyiko, wakiwa wametoka sehemu mbalimbali za nchi. Hata wakati huo pia niliweza kuangalia madaraka yangu ya kundi katika Seinajoki (ingawa nilikuwa nikisafiri mbali na kurudi) naye mke wangu alikuwa na wakati mwingi wa kupainia.

Lakini, baada ya miaka michache niliona ilifaa nirudi tena Seinajoki nikakae huko daima. Kwa hiyo nikamkumbusha Msimamizi Mkuu mapatano tuliyofanya, akayakumbuka sana. Lakini alishangaa sana kwamba nilitaka kuacha cheo hicho cha umashuhuri nirudie kazi yangu ya zamani. Nilipoirudia mwaka 1973, watu walishangaa sana hata makala zikaandikwa katika magazeti makuu ya Kifinland zikitoa sifa nzuri juu ya Mashahidi wa Yehova.

Kundi hapa katika Seinäjoki lilikua sana hata Jumba la Ufalme tulilojenga karibu na nyumbani kwetu mwaka 1961 likawa dogo mno. Kwa hiyo masika yaliyopita wahubiri wetu 60 wa Ufalme walianza kujenga Jumba la Ufalme jipya katika uwanja mpana tuliokodishwa na mji. Sote tulishangaa kumaliza jumba kubwa hilo, lililo zuri, mwanzoni mwa Septemba, kwa muda unaopungua miezi sita!

Nilichangamka sana wakati jumba lilipokuwa likiwekwa wakf. Hiyo ni kwa sababu nilizungusha macho katika Jumba la Ufalme lililokuwa limejaa pomoni nikaona washiriki wanane wa jamaa yangu wakiwa wamehudhuria, kutia na mimi na mke wangu, na watoto wetu watatu na wake zao. Katika jamaa yetu, sita wanatumikia kama mapainia na wawili wako Betheli!

Sasa ninapotazama siku zilizopita, naweza kusema kwamba mke wangu nami tumekuwa na maisha yenye furaha na kusudi halisi katika utumishi wa Mungu, kama yale ambayo baba yangu alikuwa nayo na ambayo watoto wangu wanayo sasa. Tena twatazamia kupata baraka nyingi siku zijazo katika utumishi wa Mungu. Tunapokubali ukaribishaji wa Yehova tumtumikie, hakika yeye anatutimizia ahadi yake, iliyoandikwa na nabii wake wa kale: “Mkanijaribu kwa njia hiyo . . . mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha.”​—Mal. 3:10.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki