Maisha Yenye Baraka Tele na Yenye Kuthawabisha Katika Utumishi wa Yehova
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA LEO KALLIO
Ulikuwa mwaka wa 1914, na siku nzuri ya mwisho-mwisho wa kiangazi ilikuwa ikiisha katika kiunga chetu cha Turku, jiji katika Finlandi. Kwa ghafula, utulivu ulikomeshwa na habari za vita kuu iliyokuwa imetokea. Upesi barabara zilijaa watu waliokuwa wakitafakari maana ya matukio hayo. Nyuso zenye uzito za watu wazima zilifanya sisi watoto tutake kujua ni nini kingetokea. Nilikuwa na umri wa miaka tisa, nami nakumbuka kwamba michezo ya watoto yenye amani iligeuka kuwa michezo ya vita.
INGAWA Finlandi haikuhusika katika Vita ya Ulimwengu 1 (1914-18), nchi hiyo ilikuwa imekumbwa na vita ya wenyewe kwa wenyewe katika 1918. Watu wa ukoo na wale waliokuwa marafiki awali walipigana kwa sababu ya maoni tofauti ya kisiasa. Familia yetu ya watu saba ilipatwa na chuki hiyo. Baba yangu, aliyekuwa mtu mwenye kueleza maoni yake waziwazi, alikamatwa na kuhukumiwa miaka saba gerezani. Baadaye aliachiliwa, lakini kufikia wakati huo afya yake ilikuwa mbaya sana.
Familia yetu ilipatwa na njaa na ugonjwa katika kipindi hicho kibaya sana. Watatu kati ya dada zangu wachanga walikufa. Kaka wa baba yangu, aliyeishi jiji la Tampere, alisikia juu ya taabu yetu akaalika baba na mama yangu na sisi watoto wawili tuliokuwa tumebaki tuishi naye.
Miaka kadhaa baadaye, tulipokuwa tungali twaishi Tampere bado, nilikutana na msichana mwenye kuvutia sana aitwaye Sylvi. Alikuwa na malezi kama yangu. Babake aliuawa katika vita ya wenyewe kwa wenyewe, na baadaye rafiki wa karibu wa familia yake, Kaarlo (Kalle) Vesanto kutoka mji wa Pori, aliwaalika Sylvi, dadake, na mamake waishi nyumbani mwake. Alifanya mipango ili mamake Sylvi apate kazi na wasichana hao waende shuleni. Baadaye Sylvi alihamia Tampere kutafuta kazi, na huko ndiko tulikutana.
Jioni Iliyobadili Maisha Yangu
Katika 1928, Sylvi alikuwa mchumba wangu, na siku moja tulisafiri kwenda Pori kutembelea Kalle Vesanto na familia yake. Hakuna tukio jingine ambalo limeathiri maisha yangu kwa uthabiti hivyo. Kalle alikuwa amekuwa mfugaji na mpanda farasi wa mashindano ya mwendo wa matiti lakini alikuwa ameacha biashara hiyo. Yeye na mke wake walikuja kuwa wahubiri wenye bidii wa habari njema za Ufalme wa Mungu. Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1990 chaeleza jinsi alivyoajiri watu wapige rangi maneno “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe” kwenye ukuta wa nje wa nyumba yake yenye orofa mbili. Maandishi hayo yalikuwa makubwa vya kutosha kuweza kusomwa kutoka katika magari-moshi yaliyokuwa yakipita kwa kasi.
Usiku huo Kalle nami tuliongea hadi che. “Kwa nini? Kwa nini? Kwa nini?” nikauliza, naye Kalle akaeleza. Kihalisi, nilijifunza kweli za msingi za Biblia kwa usiku mmoja. Niliandika maandiko yaliyoeleza mafundisho mbalimbali. Baadaye, niliporudi nyumbani, nilipata kitabu cha kuandikia nikaandika maandiko hayo yote neno kwa neno. Kwa sababu sikuwa nimeifahamu Biblia bado, nilitumia kitabu hicho cha kuandikia ili kutolea ushahidi wale watu kwenye mahali pa ujenzi nilipofanyia kazi. Nilipofunua mafundisho ya dini bandia, mara nyingi nilijikuta mwenyewe nikirudia maneno ya Kalle: “Mmedanganywa kwelikweli, enyi jamaa!”
Kalle alinipa anwani ya nyumba fulani ndogo katika Tampere ambamo Wanafunzi wa Biblia 30 hivi walikuwa wakifanya mikutano yao. Nikiwa humo nilikuwa nikichuchumaa katika kona moja karibu na mlango kando ya Ndugu Andersson, mwenye nyumba hiyo ndogo. Sikuhudhuria kwa ukawaida, lakini sala ilisaidia sana. Nilipokuwa na matatizo mazito kazini, nilisali hivi wakati mmoja: “Tafadhali Mungu, ukinisaidia kushinda magumu haya, naahidi nitahudhuria kila mkutano.” Lakini hali ilizidi kuwa mbaya. Ndipo nikang’amua kwamba nilikuwa nikimwekea Yehova masharti, kwa hiyo nilibadili sala yangu hivi: “Lolote litukialo, naahidi kuhudhuria kila mkutano.” Ndipo taabu zangu zikapungua, nikawa mhudhuriaji wa mikutano wa kawaida.—1 Yohana 5:14.
Huduma Yetu Katika Miaka ya Mapema
Katika 1929, Sylvi na mimi tulioana, na katika 1934 sote wawili tulifananisha wakfu wetu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Katika siku hizo huduma yetu ilihusisha kubeba kinanda na rekodi hadi makao ya watu na kuwaomba kwa fadhili ikiwa tungeweza kutoa bila malipo, hotuba ya Biblia iliyorekodiwa. Mara nyingi watu walitualika nyumbani mwao, na baada ya wao kusikiliza hotuba iliyorekodiwa, walishiriki katika mazungumzo na kukubali baadhi ya fasihi yetu.
Kwa ruhusa ya wenye mamlaka, katika bustani za umma tulitumia vikuza-sauti kutoa hotuba zizo hizo za Biblia zilizorekodiwa. Na viungani tulikuwa tukiweka kikuza-sauti kwenye paa au juu ya dohani. Nyakati nyingine tulikuwa tukitoa hotuba hizo zilizorekodiwa tukiwa karibu na ziwa ambako watu wa mjini walikuwa wamekusanyika katika vikundi vikubwa. Tulikuwa tu tukivichukua vikuza-sauti katika mashua moja na kupiga makasia polepole karibu na ukingo wa ziwa. Jumapili tulikuwa tukienda zetu kwa basi kwenye kampeni ya kuhubiri mashambani, tukiwa na vikuza-sauti vyetu vyenye thamani na fasihi nyingi sana.
Badiliko Lililotahini Imani Yetu
Katika 1938, niliingia huduma ya wakati wote nikiwa painia, lakini niliendelea pia kufanya kazi nikiwa mwashi. Masika iliyofuata nilipokea mwaliko kutoka kwa ofisi ya tawi ya Sosaiti wa kuwa mhudumu asafiriye, ambaye sasa huitwa mwangalizi wa mzunguko. Haikuwa rahisi kukubali kwa sababu nilifurahia kufanya kazi pamoja na kutaniko letu katika Tampere. Isitoshe, tulikuwa na nyumba yetu wenyewe; tulikuwa na mwana mwenye umri wa miaka sita, aitwaye Arto, ambaye angeanza shule karibuni; na Sylvi alifurahia kazi yake akiwa msaidizi dukani. Lakini, baada ya kushauriana, nilikubali pendeleo hilo la ziada katika utumishi wa Ufalme.—Mathayo 6:33.
Kisha kipindi kingine kigumu kikaanza. Vita ilianza katika Novemba 30, 1939, wakati majeshi ya Sovieti yalipoingia Finlandi. Vita hiyo, iliyoitwa Vita ya Majira ya Baridi Kali, iliendelea hadi Machi 1940, Finlandi ilipolazimika kukubali yale makubaliano ya amani. Ilionekana kana kwamba hata mambo ya asili yalikuwa yakipigana, kwani hayo yalikuwa majira ya baridi kali zaidi niwezayo kukumbuka. Nilisafiri kwa baiskeli kutoka kutaniko moja hadi jingine huku kipima-joto kikishuka zaidi ya digrii sentigredi 30 chini ya sufuri!
Katika 1940 kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku Finlandi. Baadaye Mashahidi wengi wachanga Wafinlandi walitiwa gerezani wanyongony’ee humo chini ya hali zisizowafaa wanadamu. Kwa furaha, niliweza kuyatumikia makutaniko kwa muda wote wa vita ya ulimwengu ya pili, kutoka 1939 hadi 1945. Mara nyingi hilo lilitaka kwamba niwe mbali na Sylvi na Arto kwa vipindi vya miezi kadhaa. Zaidi ya hayo, kulikuwa na tisho la daima la kukamatwa kwa sababu ya kushiriki katika kazi isiyo halali.
Ni lazima iwe nilionekana kuwa mtu wa ajabu, nikiendesha baiskeli iliyochukua sanduku zito, mkoba wenye fasihi, na kinanda pamoja na rekodi. Sababu moja iliyonifanya nibebe rekodi za kinanda ilikuwa ili kuthibitisha kwamba sikuwa mpelelezi wa Warusi aliyeruka kutoka kwenye ndege, iwapo ningekamatwa. Yaani, ningeweza kutoa hoja kwamba kama ningalikuwa mtu aliyeruka kutoka kwenye ndege, rekodi zingalivunjika wakati wa kuruka.
Hata hivyo, wakati mmoja nilipokuwa nikizuru ujirani mmoja uliokuwa umeonywa juu ya mpelelezi, familia moja ya Mashahidi ilinidhania kuwa mpelelezi. Nilibisha mlangoni pao usiku mmoja wa majira ya baridi kali yenye giza, nao waliogopa sana kufungua. Kwa hiyo nililala usiku huo katika ghala ya nafaka, nikiwa ndani ya nyasi kavu ili kupata ujoto. Asubuhi iliyofuata waliweza kunifahamu vizuri, na ni lazima niseme, katika sehemu iliyobaki ya ziara yangu, washiriki wa familia hiyo walinionyesha ukaribishaji-wageni wa kipekee sana!
Katika ile miaka ya vita, ni Ndugu Johannes Koskinen na mimi tu tuliotumikia makutaniko ya katikati na kaskazini mwa Finlandi. Kila mmoja wetu alikuwa na maeneo makubwa ya kutunza, mengine yakiwa na umbali wa kilometa 600. Tulikuwa na makutaniko mengi sana ya kuzuru hivi kwamba tuliweza kubaki kwa muda wa siku mbili au tatu tu tukiwa na kila kutaniko. Mara nyingi magari-moshi yalichelewa, na mabasi yalikuwa machache na yenye watu wengi sana hivi kwamba ilikuwa ajabu kwamba tulifika mahali tulipotaka kwenda.
Kuponea Chupuchupu
Wakati mmoja, mapema katika Vita ya Majira ya Baridi Kali, nilikwenda kwenye ofisi ya tawi katika Helsinki nikachukua katoni nzito nne za fasihi iliyopigwa marufuku niende nazo kwa gari-moshi ili kuzipeleka kwenye makutaniko. Nilipokuwa katika kituo cha gari-moshi cha Riihimäki, king’ora cha kuonya juu ya shambulio la makombora ya kutupwa kutoka katika ndege kililia. Askari-jeshi waliokuwa katika gari-moshi hilo walijivika suti zao za majira ya baridi kali, na abiria wakaambiwa watoke kwenye gari-moshi mara iyo hiyo na kuelekea uwanja mtupu ulio ng’ambo ya kituo cha gari-moshi.
Niliwaomba askari-jeshi wanibebee katoni zangu, nikiwaeleza umaana wazo. Wanne kati yao walichukua katoni moja-moja, nasi tulikimbia karibu meta 200 hadi kwenye uwanja uliofunikwa kwa theluji. Tulijitupa ardhini, na mtu fulani akanipaazia sauti hivi: “Aisee, wewe raia, usisogee hata kidogo! Walipuaji makombora wakiona kusogea kokote watatulipua kwa makombora.” Nilikuwa na udadisi wa kutosha kuweza kugeuza uso wangu kwa uangalifu ili kutazama angani, nilikohesabu ndege 28!
Kwa ghafula ardhi ilianza kutetemeka kutokana na milipuko ya makombora. Ingawa kituo cha gari-moshi hakikulipuliwa kwa makombora, gari-moshi tulimokuwa tumesafiria hadi hapo lililipuliwa kwa makombora. Ono la gari-moshi lililoharibika kabisa na reli zilizopindapinda lilikuwa la ajabu kama nini! Asubuhi iliyofuata niliweza kuendelea na safari yangu pamoja na zile katoni, na askari-jeshi wakaendelea na safari yao katika gari-moshi jingine. Mmoja wao alikuwa Shahidi baada ya vita hiyo, naye aliniambia kwamba askari-jeshi hao walikuwa wameongea baadaye juu ya yule raia wa ajabu pamoja na katoni zake.
Wakati fulani baadaye Ndugu Koskinen, alipokuwa akisafiri kutumikia kutaniko dogo huko Rovaniemi katika Finlandi kaskazini, alikamatwa kabla ya kushuka kutoka gari-moshi. Alipelekwa gerezani, alikotendwa vibaya. Wakati ulipofika wa mimi kutumikia kutaniko lilo hilo, nilifanya mipango ya kushuka gari-moshi kwenye kituo kidogo cha gari-moshi cha Koivu. Huko Dada Helmi Pallari alifanya mipango niendelee na sehemu iliyobaki ya safari yangu katika kigari cha kubebea maziwa. Ziara yangu kwenye Kutaniko la Rovaniemi ilifanikiwa. Hata hivyo, nilipokuwa nikiondoka nilipatwa na magumu.
Tukiwa njiani kwenda kwenye kituo cha gari-moshi, mwenzangu nami tulikutana na wanajeshi wawili waliokuwa wakichunguza hati za wapita-njia wote. “Usiwaangalie. Kaza macho yako mbele,” nikasema. Tulitembea kati yao kana kwamba hawakuwako. Kisha wakaanza kutufuata. Mwishowe, kwenye kituo cha gari-moshi, niliweza kuwaepa katikati ya umati na kuruka ndani ya gari-moshi lililokuwa likienda. Katika siku hizo msisimuko haukukosekana katika kazi ya kusafiri!
Wakati mmoja nilikamatwa na kupelekwa kwa baraza la kuwaandikisha wanajeshi wapya. Kusudi lilikuwa kunipeleka kwenye eneo la mapigano. Lakini simu ikalia, na afisa wa jeshi aliyekuwa karibu kunihoji akainyanyua. Niliweza kusikia sauti kwenye simu ikipaaza sauti hivi: “Mbona waendelea kutuma watu hawa wagonjwa ambao hawafai kitu? Sisi tutawarudisha nyumbani tu. Twahitaji watu wawezao kufanya kazi!” Kwa furaha, nilikuwa na hati ya kitiba iliyoeleza juu ya tatizo la afya nililokuwa nalo. Nilipotoa hati hiyo, niliruhusiwa kwenda na hivyo nikaendelea na kazi yangu miongoni mwa makutaniko bila kukatizwa!
Kusaidia Katika Kesi Fulani
Msisimuko wa vita uliendelea kwa mshindo mkubwa, na rafiki yangu Ahti Laeste alikamatwa. Mke wake alinipigia simu. Nilipokwenda nyumbani kwao, nilipata miongoni mwa hati zake hati moja kutoka kwa polisi wa mahali hapo iliyompa Ahti ruhusa ya kutoa katika bustani za umma za jijini, hotuba zilizorekodiwa. Tuliwasili mahakamani tukiwa na hati hiyo. Walipomaliza kusoma shtaka, nilimpa Ndugu Laeste hati hiyo. Hakimu alimtuma askari-jeshi mmoja alete kinanda na utoaji mbalimbali wa Biblia uliorekodiwa ili mahakama isikilize. Baada ya kusikiliza kila utoaji, hakimu alisema kwamba hakuweza kuona jambo lolote lisilofaa katika yale yaliyosemwa.
Kisha Ahti, mke wake, na mimi tukaambiwa tuondoke hadi ukumbini ili tungojee uamuzi wa mahakama. Tulisimama huko tukiwa na wasiwasi. Hatimaye tukasikia sauti ikisema hivi: “Mshtakiwa, tafadhali ingia mahakamani.” Ndugu Laeste aliachiliwa! Kwa kweli mioyo yetu ilijaa shukrani kwa Yehova tulipoendelea na kazi yetu, Ndugu na Dada Laeste wakiwa na kazi yao katika kutaniko la hapo, nami nikiwa na yangu katika kazi ya kusafiri.
Vita Yaisha —Utumishi Wetu Waendelea
Marufuku juu ya kazi yetu ya kuhubiri iliondolewa vita ilipoisha, na ndugu wakaachiliwa kutoka gerezani. Katika miaka yangu mingi ya utumishi, nimevutiwa sana na fungu ambalo dada Wakristo wamekuwa nalo katika kazi ya Ufalme na katika kuwaunga mkono waume zao. Hasa nimeshukuru kwa ajili ya dhabihu na utegemezo ambao Sylvi ametoa. Kwa sababu hiyo, niliweza kuendelea na kazi ya kusafiri kwa muda wa miaka 33 bila kukatiza na baadaye kutumikia nikiwa painia wa pekee.
Sylvi nami pia tulimtia moyo Arto aanze kupainia alipomaliza shule, ajifunze Kiingereza, na kuhudhuria Watchtower Bible School of Gilead katika United States. Alihitimu Gileadi katika 1953. Baadaye alimwoa Eeva, na wakiwa pamoja wametumikia katika namna mbalimbali za utumishi wa wakati wote, kutia na kazi ya mzunguko, utumishi wa Betheli, na upainia wa pekee. Katika 1988 walihamia Tampere, jiji tunamokaa ili kutunza Sylvi na mimi huku wakiendelea wakiwa mapainia wa pekee.
Ingawa nguvu zetu zimepungua sana, Sylvi na mimi tumefurahia maisha yenye baraka tele na tuna kumbukumbu nyingi za kututia moyo. Inathawabisha sana kufikiria ule ukuzi ambao tumeona. Nilipoanza kuzuru makutaniko katika 1939, kulikuwa na wahubiri wa Ufalme 865 katika Finlandi, lakini sasa kuna zaidi ya 18,000!
Sikuwa nimeng’amua hata kidogo nilipoanza huduma ya wakati wote huko nyuma katika 1938 kwamba miaka 55 baadaye ningekuwa bado nashiriki sehemu katika huduma. Ijapokuwa tumezeeka, katika nguvu za Yehova twaendelea kutazamia zawadi yetu iliyoahidiwa. Twatumainia maneno haya ya mtunga-zaburi: “BWANA, [Yehova, NW] ndiye mwema; rehema zake ni za milele; na uaminifu wake vizazi na vizazi.”—Zaburi 100:5.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Leo na Sylvi Kallio walifananisha wakfu wao kwa Yehova katika 1934
[Picha katika ukurasa wa 23]
Picha ya karibuni ya Leo na Sylvi wakaribiapo miaka 60 ya utumishi wa kujitoa