Njooni Kwenye “Wachukuaji Nuru” Mkusanyiko wa Wilaya
“TAZAMA, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu.” (Isaya 60:2) Hayo maneno ni ya kweli kama nini leo! Pasipo shaka, dini bandia inakosa kuarifu watu kuhusu aina ya ibada inayompendeza Mungu. Kwa nini? Kwa sababu Shetani, mungu wa mfumo huu wa mambo, “amepofusha akili za wasioamini.”—2 Wakorintho 4:4, NW.
Mashahidi wa Yehova wako tofauti kabisa na wale waliopofushwa na Shetani. Maneno ya nabii Isaya yaweza kutumiwa kwao: “BWANA [Yehova, NW] atakuzukia wewe, na utukufu wake utaonekana juu yako.” (Isaya 60:2) Wao wanashukuru kama nini kuwa wametoka gizani kuingia katika nuru ya Mungu iliyo nzuri ajabu! Hiyo ni nuru ya kiroho, kweli ya Neno la Mungu inayoangazia akili, hivi kwamba hata wale walio vipofu halisi waweza kuiona kweli.
Pasipo shaka, msaada unahitajika. Haielekei kwamba mtu anayesoma Biblia tu bila kujinufaisha na misaada yenye kuandaliwa kimungu aweza kuitambua nuru. Hiyo ndiyo sababu Yehova Mungu ameandaa “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” aliyetabiriwa kwenye Mathayo 24:45-47. Leo “mtumwa” huyo huwakilishwa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Ni chini ya mwelekezo wa baraza hilo kwamba “Wachukuaji Nuru” Mkusanyiko wa Wilaya umepangwa.
Kusudi la mkusanyiko huo ni kusaidia watu wote wa Yehova wawe wachukuaji nuru walio bora zaidi, kwa kupatana na maneno ya Paulo kwenye Wafilipi 2:15, NW. Hapo, Wakristo wanahimizwa “kung’aa kama vimulikaji katika ulimwengu.”—Mathayo 5:14, 16.
Katika United States, mfululizo wa “Wachukuaji Nuru” Mikusanyiko ya Wilaya imeratibiwa kuanza Ijumaa, Juni 5. Saa 4:20 za asubuhi, programu ya muziki itasaidia wote wawe na hali ya moyo na akili inayofaa, ikiwatayarisha kwa ajili ya programu ya kiroho iliyo mbele. Kila siku ina kichwa chayo yenyewe, na kichwa cha Ijumaa ni “Peleka Nuru Yako na Kweli Yako.”—Zaburi 43:3.
Jambo kuu la programu ya Ijumaa asubuhi litakuwa hotuba ya msingi, “Wachukuaji Nuru—Kwa Kusudi Gani?” Kwa hakika, Wakristo si wachukuaji nuru wenye kusudi la kibinafsi, lenye ubinafsi. Badala ya hiyo, wao hutumikia kwa sababu zile zile ambazo Yesu Kristo, Mchukuaji Nuru Mkuu, alikuja duniani, ili kushuhudia kweli na kulitukuza jina la Muumba. Kwa kufaa, Yesu alisema hivi kuhusu yeye mwenyewe: “Muda nilipo ulimwenguni, mimi ni nuru ya ulimwengu.” (Yohana 9:5) Hivyo, alituachia kielelezo tufuate nyayo zake kwa ukaribu. (1 Petro 2:21) Alasiri ya siku hiyo ya kwanza itakazia hotuba na pia drama ya Biblia inayoshughulika na Mfalme Yosia, itakayokuwa yenye upendezi wa kipekee kwa vijana.
Kichwa cha Jumamosi ni “Ninyi Ni Nuru ya Ulimwengu . . . Acheni Nuru Yenu Iangaze.” (Mathayo 5:14, 16, NW) Jambo kuu la programu ya asubuhi litakuwa mfululizo wenye kichwa “Kuacha Nuru Yako Iangaze.” Nafasi itaandaliwa kwa wale ambao wamejifanya wakfu kwa Yehova wabatizwe. Programu ya alasiri itatokeza mfululizo wenye kuangazia ulio na kichwa “Kuangaza Nuru Kwenye Kuwapo na Kufunuliwa kwa Kristo.”
Kichwa kilichochaguliwa kwa Jumapili, siku ya tatu na ya mwisho ya mkusanyiko huo, ni “Endeleeni Kuenenda Kama Watoto wa Nuru.” (Waefeso 5:8) Programu ya asubuhi itakuwa na mfululizo wenye kichwa “Kutunzana Katika Nyumba ya Kikristo,” itakayoshughulika na wajibu mbalimbali wa familia. Kutakuwako pia na hotuba inayoeleza kinachomaanishwa na kuwa katika ujitiisho kwa Mungu na Kristo.
Mkusanyiko utafikia upeo wao Jumapili asubuhi kwa hotuba ya watu wote yenye kichwa “Fuata Nuru ya Ulimwengu.” Hotuba hiyo itakuwa na mazungumzo juu ya Yohana 1:1-16 na itaonyesha uhitaji wa maarifa ya Biblia, ikikazia kwamba Yesu Kristo ndiye nuru ya ulimwengu. Mkusanyiko huo utamalizika na himizo lenye bidii la “Kuendelea Kuenenda Katika Nuru.”
Onyesha uthamini wako kwa karamu hiyo ya kiroho ambayo Yehova anaandalia kupitia tengenezo lake linaloonekana. Uwepo kutoka wimbo wa kufungua Ijumaa asubuhi hadi sala ya kumalizia Jumapili alasiri. Toa uangalifu kwa yote yanayosemwa kutoka jukwaani. Andika habari ili ikusaidie ukazie fikira na kwa ajili ya marejezeo ya wakati ujao. Hatimaye, panga kushiriki katika namna fulani ya utumishi wa kujitolea. Hivyo, utaonea shangwe si ile baraka ya kupokea tu bali pia hata ile baraka kubwa zaidi ya kutoa.—Matendo 20:35.