Sababu kwa Nini Biblia Ni Zawadi Yenye Pumzi Kutoka kwa Mungu
BIBLIA husema kwamba “Mungu ni upendo” na humhesabia hekima na uwezo. (1 Yohana 4:8; Ayubu 12:13; Isaya 40:26) Inatuambia kwamba “njia zake zote ni haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Kulingana na Biblia, Mungu huonyesha pia sifa ya rehema na ya huruma.—Kutoka 34:6; Warumi 9:15.
Kwa sababu Biblia humhesabia Yehova Mungu sifa kama hizo, inawavuta kwake wanadamu wenye kupapasa. Kitabu hicho husema juu ya uumbaji, chanzo cha dhambi na kifo, na njia ya kupatanishwa na Mungu. Inatoa tumaini lenye kusisimua la Paradiso iliyorudishwa duniani. Lakini hayo yote yana thamani ikiwa tu inaweza kuthibitishwa kwamba Biblia ni zawadi yenye pumzi kutoka kwa Mungu.
Biblia na Sayansi
Biblia imeshinda uchambuzi daima. Kwa mfano, inaposomwa kwa maoni yenye kukubali mambo, inapatikana kuwa inapatana na sayansi ya kweli. Bila shaka, Biblia ilitayarishwa kuwa mwongozo wa kiroho, si kuwa kitabu cha mafundisho ya sayansi. Lakini ebu tuone kama Biblia hukubaliana na mambo ya sayansi.
Anatomia (Elimu ya Miili ya Viumbe): Biblia husema kwa usahihi kwamba sehemu “zote” za kiinitete cha kibinadamu ‘zimeandikwa.’(Zaburi 139:13-16) Ubongo, moyo, mapafu, macho—hizo pamoja na sehemu nyinginezo zote za mwili “ziliandikwa” katika msimbo jeni (utaratibu wa urithi wa tabia) wa yai lililotungishwa katika tumbo la uzazi la mama. Katika msimbo huo mna orodha zinazoratibu wakati ambao kila ya sehemu hizo itatokea kwa utaratibu unaofaa. Na ebu fikiria! Jambo hilo juu ya ukuzi wa mwili wa kibinadamu lilirekodiwa katika Biblia karibu miaka 3,000 kabla ya wanasayanisi kuvumbua msimbo jeni.
Wanyama: Kulingana na Biblia, “sungura [sungura-mwitu, New World Translation of the Holy Scriptures] . . . hucheua.” (Mambo ya Walawi 11:6) François Bourlière (The Natural History of Mammals, 1964, ukurasa 41) asema hivi: “Tabia ya ‘ucheuaji,’ au kupitisha chakula mara mbili katika matumbo badala ya mara moja tu, yaonekana kuwa tukio la kawaida katika sungura na sungura-mwitu [vitungule]. Kwa kawaida sungura waliofugwa hula na kumeza bila kutafuna mavi yao ya usiku, ambayo asubuhi hufanyiza nusu ya yale yaliyomo tumboni. Kwa sungura wa mwitu ucheuaji hutukia mara mbili kila siku, na tabia iyo hiyo huonekana kwa sungura-mwitu wa Ulaya.” Kwa habari hiyo, kitabu Mammals of the World (cha E. P. Walker, 1964, Buku 2, ukurasa 647) hutaarifu hivi: “Huo huenda ukawa sawa na ‘ucheuaji’ katika mamalia wacheuzi.”
Akiolojia: Wafalme, majiji, na mataifa ya Kibiblia yamehuishwa kwa sababu ya uvumbuzi wa mabamba ya udongo, vyombo vya udongo, maandishi, na vitu kama hivyo. Kwa mfano, watu kama vile Wahiti wanaotajwa katika Maandiko walikuwako kikweli. (Kutoka 3:8) Katika kitabu chake The Bible Comes Alive, Sir Charles Marston alisema hivi: “Wale ambao wamedhoofisha imani ya watu kwa ujumla katika Biblia, na kidogokidogo wakaharibu mamlaka yayo, nao wamedhoofika pia kwa sababu ya ushuhuda ambao umevumbuliwa, na mamlaka yao imeharibiwa. Mambo yanayovumbuliwa na waakiolojia yanaondolea mbali uchambuzi wenye kuharibu kutoka uwanja wa mambo yaliyoshukiwa hadi uwanja wa mambo yanayotambuliwa.”
Akiolojia imeunga mkono Biblia katika njia nyingi. Kwa mfano, uvumbuzi mbalimbali umethibitisha mahali-mahali na majina yanayopatikana katika Mwanzo sura 10. Waakiolojia wamefukua mji wa Ukaldayo, Uru, kitovu cha kibiashara na cha kidini ambako Abrahamu alizaliwa. (Mwanzo 11:27-31) Sehemu ya juu ya chemchemi ya Gihoni katika kusini-mashariki mwa Yerusalemu, waakiolojia walipata mji wa Kiyebusi uliotwaliwa na Mfalme Daudi. (2 Samweli 5:4-10) Mwandiko wa Siloami uliochongwa kwenye sehemu moja ya mwisho wa mfereji wa maji wa Mfalme Hezekia, ulivumbuliwa katika 1880. (2 Wafalme 20:20) Kushindwa kwa Babuloni na Sairasi (Koreshi) Mkuu katika 539 K.W.K., kunasimuliwa katika Masimulizi ya Matukio ya Nabonido, yaliyofukuliwa katika karne ya 19 W.K. Maelezo madogo madogo katika kitabu cha Esta yamethibitishwa na maandishi kutoka Persepolis na uvumbuzi wa jumba la mfalme la Mfalme Zaksi (Ahasuero) katika Shushani, au Susa, kati ya 1880 na 1890 W.K. Sarafu zilizotumiwa katika karne ya kwanza W.K. huthibitisha kuwako kwa gavana Mroma Pontio Pilato, aliyemkabidhi Yesu ili atundikwe.—Mathayo 27:11-26.
Astronomia (Elimu ya anga na nyota): Miaka 2,200 hivi iliyopita—muda mrefu kabla ya watu kwa ujumla kujua kwamba dunia ni duara—nabii Isaya aliandika hivi: “Yeye ndiye anayeketi juu ya duara ya dunia.” (Isaya 40:22) Neno la Kiebrania chug, linalotafsiriwa hapa kuwa “duara,” laweza pia kufasiriwa kuwa “tufe.” (A Concordance of the Hebrew and Chaldee Scriptures, cha B. Davidson) Halafu pia, “duara” ya upeo wa macho wa dunia huonekana kwa wazi kutoka angani na nyakati nyingine wakati wa kusafiri kwa ndege katika kimo cha juu. Kwa tukio zuri, Ayubu 26:7 husema kwamba Mungu “hutandaza kaskazi [dunia, NW] juu ya nafasi isiyo na kitu.” Hilo ni kweli, kwani waastronomia wanajua kwamba dunia haina tegemeo lolote lenye kuonekana.
Botania (Elimu ya Mimea): Wengine hukata maneno isivyofaa kwamba Biblia si sahihi kwa sababu Yesu Kristo alisema juu ya “punje [mbegu, NW] ya haradali” kuwa “ndogo kuliko mbegu zote.” (Marko 4:30-32) Yaelekea, Yesu alimaanisha mbegu ya mmea wa haradali nyeusi (Brassica nigra au Sinapis nigra), iliyo na kipenyo cha karibu milimeta 1 hadi 1.6 tu. Ingawa kuna mbegu zilizo ndogo zaidi, kama vile mbegu za okidi (mrembo) zilizo laini kama unga, Yesu hakuwa akiongea na watu waliopanda okidi. Wayahudi hao Wagalilaya walijua kwamba miongoni mwa mbegu za aina mbalimbali zilizopandwa na wakulima wa huko, mbegu ya haradali ndiyo iliyokuwa ndogo zaidi. Yesu alikuwa akiongea juu ya Ufalme, hakuwa akifundisha somo la botania.
Jiolojia: Kuhusu usimulizi wa Biblia wa uumbaji, mwanajiolojia mashuhuri Wallace Pratt alisema hivi: “Ikiwa mimi nikiwa mwanajiolojia ningeombwa nieleze kwa ufupi mawazo yetu ya ki-siku-hizi juu ya mwanzo wa dunia na kusitawi kwa uhai juu yayo kwa watu sahili, walio wachungaji, sawa na yale makabila ambayo kwayo Kitabu cha Mwanzo kilielekezwa, singeweza kutoa usimulizi bora zaidi ila kufuata kwa ukaribu sana maneno ya sura ya kwanza ya Mwanzo.” Pratt alionyesha kwamba utaratibu wa matukio katika Mwanzo—mwanzo wa bahari, kutokea kwa bara, na kisha kutokea kwa uhai wa baharini, ndege, na mamalia—ndio mfuatano hasa wa migawanyiko mikuu ya wakati wa kijiolojia.
Tiba: Katika kitabu chake The Physician Examines the Bible, C. Raimer Smith aliandika hivi: “Inanishangaza sana kwamba Biblia ni sahihi sana kuhusu maoni ya kitiba. . . . Mahali utibabu unapotajwa, kama vile kwa habari ya majipu, majeruhi, na kadhalika, ni sahihi hata kulingana na viwango vya ki-siku-hizi. . . . Ushirikina mwingi ungali unaaminiwa na idadi kubwa ya watu kama vile, kwamba kuweka mbegu ya mti bakiai mfukoni kutazuia baridi yabisi (ugonjwa wa viungo); kwamba kushika vyura kutasababisha chunjua; kwamba kuvaa kitambaa chekundu shingoni kutaponya vidonda vya kooni; kwamba kubeba mfuko wenye sehemu ya mmea mvuje kutazuia magonjwa; kwamba kila wakati mtoto anapokuwa mgonjwa yeye ana minyoo; na kadhalika, lakini hakuna taarifu zozote kama hizo katika Biblia. Hilo lenyewe ni lenye kutokeza na kwangu ni uthibitisho mwingine wa chanzo chayo cha kimungu.”
Yenye Kutegemeka Katika Maelezo ya Kihistoria
Katika kitabu chake A Lawyer Examines the Bible, wakili Irwin H. Linton alionelea hivi: “Ingawa vitabu vya hadithi za kimahaba, hekaya na ushuhuda bandia huwa zenye uangalifu kuweka matukio yaliyosimuliwa katika mahali palipo mbali sana na katika wakati usio dhahiri, hivyo kuvunja kanuni za kwanza ambazo sisi mawakili hujifunza juu ya kutetea vizuri kesi mahakamani, kwamba ‘ni lazima usimulizi utaje wakati na mahali,’ masimulizi ya Biblia hutupa sisi tarehe na mahali pa mambo yaliyosimuliwa kwa usahihi kabisa.”
Ili kuthibitisha jambo hilo, Linton alitaja Luka 3:1, 2. Hapo mwandishi wa Gospeli alitaja maofisa saba ili athibitishe wakati ambao Yesu Kristo alianza huduma Yake. Ona yale maelezo madogo madogo ambayo Luka aliandaa katika maneno haya: “Mwaka wa kumi na tano wa kutawala kwake Kaisari Tiberio, Pontio Pilato alipokuwa liwali wa Uyahudi, na Herode mfalme wa Galilaya, na Filipo, ndugu yake, mfalme wa Iturea na nchi ya Trakoniti, na Lisania mfalme wa Abilene, wakati wa ukuhani mkuu wa Anasi na Kayafa, neno la Mungu lilimfikia Yohana, mwana wa Zekaria, jangwani.”
Biblia imejaa maelezo madogo madogo kama hayo. Isitoshe, sehemu zayo kama vile Gospeli ziliandikwa katika kipindi ambacho tamaduni za Kiyahudi, Kigiriki, na Kiroma zilikuwa zimesitawi sana. Ulikuwa wakati wa mawakili, waandishi, watawala, na watu kama hao. Kwa hakika, basi, ikiwa maelezo madogo madogo yanayopatikana katika Gospeli na sehemu nyingine za Biblia yasingalikuwa ya kweli, yangalifunuliwa kuwa ya uwongo. Lakini wanahistoria walimwengu walithibitisha mambo kama vile kuwapo kwa Yesu Kristo. Kwa mfano, kwa habari ya Yesu na wanafunzi wake mwanahistoria Mroma Tacitus aliandika hivi: “Kristo, ambaye kutoka kwake jina hilo [Wakristo] lilipata asili, alipata adhabu ya kupita kiasi kabisa wakati wa utawala wa Tiberio mikononi mwa mmoja wa maprokureta wetu, Pontio Pilato.” (Annals, Kitabu 15, 44) Usahihi wa Biblia katika mambo ya kihistoria husaidia kuthibitisha kwamba hiyo ni zawadi kwa ainabinadamu kutoka kwa Mungu.
Ushuhuda Mkubwa Zaidi
Ingawa akiolojia, astronomia, historia, na nyanja nyinginezo za maarifa huiunga mkono Biblia, imani katika Biblia haitegemei uhakikisho huo. Miongoni mwa uthibitisho mwingi wa kwamba Biblia ni zawadi yenye pumzi kwetu kutoka kwa Mungu, hakuna ushuhuda mkubwa zaidi uwezao kutolewa kuliko utimizo wa unabii wayo.
Yehova Mungu ndiye Chanzo cha unabii wa kweli. Kupitia nabii wake Isaya, alisema hivi: “Tazama, mambo ya kwanza yamekuwa, nami nayahubiri mambo mapya; kabla hayajatokea nawapasheni habari zake.” (Isaya 42:9) Isitoshe, Biblia husema kwamba waandishi wayo walipuliziwa na Mungu kwa njia ya roho takatifu au kani ya utendaji yake. Kwa mfano, mtume Mkristo Paulo aliandika hivi: “Kila andiko, [ni] lenye pumzi ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16) Mtume Petro aliandika hivi: “Hakuna unabii katika maandiko upatao kufasiriwa kama apendavyo mtu fulani tu. Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].” (2 Petro 1:20, 21) Kwa hiyo acheni tuuchunguze unabii wa Biblia.
Miongoni mwa mamia ya unabii katika Biblia ni ule unaohusu mji mkuu wa Ashuru, Ninawi, “mji wa damu” uliosababisha hofu kuu kotekote katika Mashariki ya Kati ya kale kwa muda wa zaidi ya karne 15. (Nahumu 3:1) Hata hivyo, wakati wa upeo wa nguvu za Ninawi, Biblia ilitabiri hivi: “[Mungu] ataufanya Ninawi kuwa ukiwa, kuwa mahali pakavu kama jangwa. Na makundi ya wanyama watalala kati yake, wanyama wote wa mataifa; mwari-nyuni na nungu watakaa juu ya vichwa vya nguzo zake; sauti yao itasikiwa madirishani; vizingitini mwake mtakuwa ukiwa; kwa maana ameifunua kazi ya mierezi.” (Sefania 2:13, 14) Leo, wageni huona kwamba ni kilima tu kinachoonyesha mahali pa ukiwa pa Ninawi wa kale. Zaidi ya hayo, makundi ya kondoo hulisha hapo, kama ilivyotabiriwa.
Katika njozi, Danieli nabii wa Mungu aliona kondoo-dume na mbuzi wa kiume mwenye pembe kubwa kati ya macho yake. Mbuzi huyo alimwangusha chini kondoo-dume huyo, akizivunja pembe zake mbili. Baadaye, pembe kubwa ya mbuzi huyo ilivunjwa, na pembe nne zikatokea mahali payo. (Danieli 8:1-8) Malaika Gabrieli akaeleza hivi: “Yule kondoo mume [kondoo-dume, NW] uliyemwona, mwenye pembe mbili, hizo ndizo wafalme wa Umedi na Uajemi. Na yule beberu [mbuzi-dume, NW], mwenye manyoya mengi, ni mfalme wa Uyunani [Ugiriki, NW]; na ile pembe iliyo kati ya macho yake ni mfalme wa kwanza. Tena katika habari ya pembe ile iliyovunjika, ambayo badala yake zilisimama pembe nne, falme nne zitasimama kutoka katika taifa lile, lakini si kwa nguvu kama zake.” (Danieli 8:20-22) Kama vile historia imethibitisha yule kondoo-dume mwenye pembe mbili—Milki ya Umedi na Uajemi—iliangushwa na “mfalme wa Ugiriki.” Mbuzi-dume huyo wa ufananisho alikuwa na “pembe kubwa” ikiwa ni yule mtu Aleksanda Mkuu. Baada ya kifo chake, majemadari wake wanne walichukua mahali pa hiyo “pembe kubwa” kwa kujipatia wenyewe mamlaka katika “falme nne.”
Unabii mwingi katika Maandiko ya Kiebrania (“Agano la Kale”) umetimizwa kwa habari ya Yesu Kristo. Baadhi yao ulitumiwa kwake na waandishi wenye kupuliziwa roho kimungu wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (“Agano Jipya”). Kwa mfano, Mathayo, mwandishi wa Gospeli alionyesha utimizo wa unabii wa Kimaandiko katika kuzaliwa kwa Yesu na bikira, katika kuwa Kwake na mtangulizi, na katika kuingia Kwake Yerusalemu akiwa amepanda mwana wa punda. (Linganisha Mathayo 1:18-23; 3:1-3; 21:1-9 na Isaya 7:14; 40:3; Zekaria 9:9.) Unabii huo uliotimizwa husaidia kuthibitisha kwamba Biblia kwa kweli ni zawadi yenye pumzi kutoka kwa Mungu.
Utimizo wa sasa wa unabii wa Biblia unathibitisha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Vita, upungufu wa chakula, magonjwa ya kipuku, na matetemeko ya dunia ya kadiri isiyo na kifani ni sehemu ya “ishara” ya “kuwapo” kwa Yesu katika mamlaka ya Ufalme. Ishara hiyo hutia ndani pia ule utendaji wa ulimwenguni pote wa Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni nne, wanaohubiri habari njema za Ufalme uliosimamishwa. (Mathayo 24:3-14, NW; Luka 21:10, 11) Unabii wa Biblia unaotimizwa sasa hututhibitishia pia kwamba hivi karibuni serikali ya Mungu ya kimbingu chini ya Yesu Kristo italetea ainabinadamu tiifu ulimwengu mpya wenye furaha ya milele.—2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1-5.
Chati inayoandama yenye kichwa “Unabii wa Biblia Uliotimizwa” huonyesha unabii mchache tu kati ya mamia ya unabii wa Biblia ambao ungeweza kuorodheshwa. Utimizo wa baadhi yao ulionyeshwa katika Maandiko yenyewe, lakini wenye kutokeza hasa ni ule unabii mbalimbali unaotimizwa leo.
Yaelekea kwamba, wewe waweza kuona matukio fulani ulimwenguni pote yaliyotabiriwa katika Biblia. Lakini kwa nini usichunguze zaidi? Mashahidi wa Yehova watafurahi kuandaa maelezo zaidi unapowaomba. Na utafutaji wako wenye unyoofu wa maarifa juu ya yule Aliye Juu Zaidi na juu ya makusudi yake na ukusadikishe kwamba Biblia kwa kweli ni zawadi yenye pumzi kutoka kwa Mungu.
[Chati katika ukurasa wa 7]
UNABII WA BIBLIA ULIOTIMIZWA
UNABII UTIMIZO
Mwanzo 49:10 Yuda ndilo lililofanyiza kabila la kifalme la Israeli
Sefania 2:13, 14 Ninawi ulifanywa ukiwa katika yapata 632 K.W.K.
Yeremia 25:1-11; Kushindwa kwa Yerusalemu kwaanza ukiwa wao
Isaya 39:6 wa miaka 70 (2 Mambo ya Nyakati 36:17-21; Yeremia 39:1-9)
Isaya 13:1, 17-22; Sairasi ashinda Babuloni;
44:24-28; 45:1, 2 Wayahudi warudi nyumbani (2 Mambo ya Nyakati 36:20-23;
Danieli 8:3-8, 20-22 Umedi na Uajemi wapinduliwa na Aleksanda Mkuu
na Milki ya Ugiriki yagawanyika
Isaya 7:14; Mika 5:2 Yesu azaliwa na bikira katika Bethlehemu
Danieli 9:24-26 Kupakwa mafuta kwa Yesu kuwa Mesiya (29 W.K.)
Isaya 9:1, 2 Huduma ya Yesu yenye kutoa nuru yaanza katika
Galilaya (Mathayo 4:12-23)
Isaya 53:4, 5, 12 Kifo cha Yesu akiwa dhabihu ya fidia
Zaburi 22:18 Kupigia kura mavazi ya Yesu (Yohana 19:23, 24)
Zaburi 16:10; Ufufuo wa Kristo siku ya tatu
Luka 19:41-44; Uharibifu wa Yerusalemu na Waroma
21:20-24 (70 W.K.)
Luka 21:10, 11; Vita, njaa kuu, matetemeko ya dunia,
Mathayo 24: 3-13; magonjwa ya kipuku, uhalifu, na kadhalika,
2 Timotheo 3:1-5 yasiyo na kifani, yakiwa ishara za “siku za mwisho”
Mathayo 24:14; Kupiga mbiu ulimwenguni pote kwa Mashahidi
Isaya 43:10; wa Yehova kwamba Ufalme wa Mungu
Zaburi 2:1-9 umesimamishwa na hivi karibuni utashinda wapinzani wote
Mathayo 24:21-34; Familia ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova
Ufunuo 7:9-17 inayomwabudu Mungu na kujitayarisha ili kuokoka
“dhiki iliyo kuu”
[Picha katika ukurasa wa 8]
Vita, njaa kuu, magonjwa ya kipuku, na matetemeko ya dunia husababisha madhara mengi leo, lakini ulimwengu mpya wenye amani na furaha u karibu