“Nirudieni Mimi, Nami Nitawarudia Ninyi”
FAMILIA ilikuwa ikionea shangwe matembezi msituni. Halafu, Peter, mchanga zaidi, akapotea njia, akimfukuza kindi kuelekea chini ya kilima. Kwa ghafula, mawingu yakajaa angani, na mvua ikaanza kunyesha. Mwanzoni yalikuwa manyunyu yenye uanana, lakini kidato kwa kidato ikawa mvua nyingi. Familia ilikusanya vyombo vya kwa haraka na kukimbilia gari layo. Na kila mtu alitaka kujua aliko Peter.
Wakati huo huo, Peter alikuwa akijaribu kurudia familia. Ilikuwa vigumu kuona mbele, na kijia cha kupandia kilima kilikuwa chenye utelezi katika mvua hiyo. Bila kutazamia, ilionekana kana kwamba ardhi ilikuwa imetoweka chini ya miguu yake alipotumbukia katika shimo lenye kina kirefu, lililofichwa. Alijaribu kupanda ili atoke, lakini pande zalo zilikuwa zenye utelezi.
Maji ya mvua yalimwagika chini ya kilima hicho na yalikuwa yakilijaza shimo hilo na matope. Petro kwa kweli alikuwa katika hatari ya kuzama. Lakini baba yake alimpata akamvuta nje kwa kamba. Baadaye, Petro alikaripiwa vikali kwa ajili ya kupotea. Hata hivyo akiwa amefungiliwa blanketi mikononi mwa mama yake, karipio lilikuwa rahisi sana kukubali.
Ono hilo laonyesha vizuri lile linalowapata baadhi ya waliokuwa miongoni mwa watu wa Mungu. Wametumbukia katika lile shimo lenye kina kirefu la mfumo huu wa mambo nao wana jaribu sana kujikokota nje na kurudia ule usalama wa tengenezo la Yehova. Inapendeza kama nini kujua kwamba Yehova ni mwenye rehema na yuko tayari ‘kushusha kamba’ na kuwasaidia warudie usalama!
Shughuli za Mungu Zenye Rehema
Nyuma katika siku za Israeli, ujenzi wa hekalu ulipokamilishwa, Sulemani alitoa sala ya wakfu ambamo alimsihi Yehova asikilize dua zilizoelekezwa kwenye hekalu hilo. Kisha akasema hivi: “Ikiwa wamekutenda dhambi, (maana hakuna mtu asiyetenda dhambi), hata ukawaghadhibikia, ukawatia katia mikono ya adui zao, . . . wakijirudia nafsi zao katika nchi ile watakayochukuliwa mateka, wakitubu, na kukusihi katika nchi ya hao waliowachukua mateka, . . . uyasikie maombi yao na dua yao, huko mbinguni, makao yako, ukaitetee haki yao.”—1 Wafalme 8:46-49.
Ombi la Sulemani lilitimizwa katika pindi nyingi wakati wa historia ya Israeli. Mara kwa mara, watu wa Mungu waligeuka upande na kumwacha. Kisha wakatambua kosa lao wakarudi, wakimtafuta. Na Yehova aliwasamehe. (Kumbukumbu la Torati 4:31; Isaya 44:21, 22; 2 Wakorintho 1:3; Yakobo 5:11) Kupitia Malaki, Yehova alitoa muhtasari wa miaka elfu moja ya kushughulikia na watu Wake wakati Yeye aliposema hivi: “Tokea siku za baba zenu mmegeuka upande, mkayaacha maagizo yangu, wala hamkuyashika. Nirudieni mimi, nami nitawarudia ninyi.”—Malaki 3:7.
Visababishi vya Kukwazwa
Kama vile Waisraeli, baadhi ya watu wa Mungu leo hugeuka upande wakajitenga wenyewe na tengenezo la Yehova. Kwa nini? Wengine hufuata jambo lionekanalo kutokuwa lenye hatia mwanzoni, kama vile Peter alivyofuata yule kindi. Ndilo jambo lililompata Ada. Yeye aripoti hivi: “Ilikuwa desturi kwa sisi wafanyakazi wote kwenda kula mlo wa mchana pamoja kwenye mkahawa ulio karibu wakati wa adhuhuri. Kwa hiyo waliponialika kunywa kikombe cha kahawa mwisho wa siku moja, haikuwa vigumu kukubali. Nilitoa hoja kwamba sikuwa nikitumia wakati upaswao kutumiwa mikutanoni au kwa mahubiri. Sikutambua kwamba hilo huenda likawa ukosefu wa kuifuata ile kanuni kwenye 1 Wakorintho 15:33.
“Upesi, nilikuwa nikienda kupanda farasi pamoja nao siku za Jumamosi. Halafu nilikuwa nikienda kwenye sinema na kwenye jumba la michezo ya kuigiza pamoja nao. Hilo liliongoza kwenye kukosa kwangu mikutano. Hatimaye, sikuwa nikienda kwenye mikutano yoyote wala kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Nilipotambua kilichokuwa kikitukia, sikuwa tena nikishirikiana na tengenezo.”
Katika visa vinginevyo sababu huenda ikawa dhambi nzito iliyofichwa ambayo humfanya mtu ahisi kwamba hastahili kumtumikia Mungu. (Zaburi 32:3-5) Au huenda mtu akakwazwa juu ya jambo fulani lililosemwa au kufanywa na marafiki Wakristo, akikosa kuelewa, kama Sulemani alivyosema, kwamba “hakuna mtu asiyetenda dhambi.”—1 Wafalme 8:46; Yakobo 3:2.
Wengine bado huvunjika moyo wanapopokea nidhamu. (Waebrania 12:7, 11) Uvutano wa mitindo-maisha ya kufuatia mali umeongoza wengi waache kumtumikia Mungu. Mara nyingi, katika kutafuta ufanisi wa kilimwengu, wamejiingiza wenyewe kikamili katika kazi ya kilimwengu hivi kwamba hawajawa na nafasi yoyote maishani mwao kwa ajili ya utumishi wa Mungu. (Mathayo 13:4-9; 1 Timotheo 6:9, 10) Je! hali ya watu hao ni yenye kukosa tumaini?
Je! Utauitikia Mwaliko wa Yehova?
Pindi moja Yesu alisema jambo fulani liilokuwa gumu kuelewa, na wengine wakakwazwa. Rekodi husema hivi: “Wengi miongoni mwa wanafunzi wake wakarejea nyuma, wasiandamane naye tena.” Lakini si wote waliokwazwa. Usimulizi wa Biblia huendelea hivi: “Yesu akawaamibia wale Thenashara, Je! ninyi nanyi mwataka kuondoka? Basi Simoni Petro akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.” (Yohana 6:66-68) Mitume wa Yesu walitambua kwa hekima kwamba lingekuwa jambo la hasara kumwacha Yesu.
Wengine ambao huanguka huwa hatimaye na mkatao uo huo. Wao hutambua kwamba kuliacha tengenezo la Mungu kulikuwa hatua ya hasara kuchukua na kwamba kwa kuwa pamoja na Yehova na Yesu Kristo tu ndiko watapata yale maneno yanayoongoza kwenye uhai. Wanapopata utambuzi huo, wanapaswa watambue pia kwamba hakuwi kuchelewa mno kugeuka, kumwomba Yehova msamaha, na kumrudia. Ni Yehova mwenyewe aliyetoa ule mwaliko: “Nirudieni mimi, nami nitawarudia ninyi.”—Malaki 3:7.
Kwa kweli, Mristo mnyofu aweza kupata wapi furaha ikiwa si katika kumtumikia Yehova? Mtu akipeperuka baada ya kuwa amekuwa sehemu ya tengenezo la Mungu kwa muda fulani, ni nini kinachomngojea katika ulimwengu wa nje? Atatambua upesi kwamba yeye sasa ni sehemu ya ulimwengu unaozidi kuwa jeuri. Atajipata mwenyewe akihusika katika mfumo wa mambo uliojawa na unafiki, uwongo, ulaghai, na ukosefu wa maadili, ulimwengu wenye hatari na hali zisizopendeza sawa na lile shimo lenye matope lililohatarisha uhai wa yule Peter mchanga. Anapopata ufahamu na kutambua kwamba uhai wake wa milele umo hatarini, apaswa atafute kwa haraka msaada wa kujitoa katika hali hiyo. Hata hivyo, kurudi huenda kusiwe rahisi.
Je! wewe ni mmoja kati ya wale ambao wamejaribu kumrudia Yehova lakini wakakupata kuwa kugumu? Basi ujue kwamba unahitaji msaada. Na uamini kwamba ndugu na dada zako katika tengenezo la Mungu wana nia ya kukusaidia. Lakini ni lazima ujitahidi kumwonyesha Yehova tamaa yako. Ni wakati wa ‘kupata ufahamu’ na ‘kumrudia Yehova kwa kweli.’—1 Wafalme 8:47, NW.
Asaidiwa Kurudi
Ada aeleza lile lililomsaidia amrudie Yehova: “Kwa wakati ufaao tu, dada aliyekuwa ameongoza funzo pamoja na mimi alinialika nihudhurie kusanyiko la mzunguko pamoja na yeye. Alikuwa mzuri sana! Na yeye hakunishutumu hata kidogo! Alionyesha upendo mwingi sana. Mwaka mmoja ulikuwa umepita tangu nilipohudhuria mkutano wangu wa mwisho, lakini nilikuwa nikitafakari juu ya ile hali ya ulimwengu yenye utupu na juu ya jambo la kwamba, nyuma ya ule uvutano wa juujuu tu, kulikuwako huzuni, fadhaiko, na ukosefu wa maadili. Kwa hiyo niliamua kuhudhuria kusanyiko. Nilipofika lile jumba lilimofanywa, nilienda kwenye safu ya mwisho ya viti nikajificha mwenyewe katika kona yenye giza. Sikutaka akina ndugu wanione na kuniuliza maswali.
“Hata hivyo, programu hiyo ilinipa mimi shauri nililohitaji sana. Ilipoisha, niliazimia si kurudia tu watu wa Yehova bali pia kujitoa mwenyewe kwake kwa moyo wangu wote. Akina ndugu walinipokea kwa uchangamfu na ‘mwana mpotevu’ akarudi.” (Luka 15:11-24) Yote hayo yalitukia wakati fulani uliopita, na Ada amekuwa sasa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka zaidi ya 25.
Kisa cha mtu mwingine aliyepotea kilikuwa na tokeo la furaha vivyo hivyo. Wazee fulani walimpa José shauri lililoonyesha zaidi fikira zao wenyewe kuliko kanuni za Biblia. José, akiwa amevunjika moyo na mwenye uchungu, hatimaye akatumbikia katika kutotenda. Kwa miaka minane alikuwa amejitenga mwenyewe na watu wa Mungu, na katika wakati huo alimwoa mtu asiyeamini akawa baba ya watoto ambao mmoja kati yao aliruhusu abatizwe katika Kanisa la Katoliki.
Hatimaye, alisaidiwa wakati mwangalizi wa mzunguko alipomfanyia ziara za uchungaji na kuwatia wazee wafanye vivyo hivyo. Alirudishwa na akafurahi kumwona mke wake akipendezwa na kweli. Wakati huu José hutumikia akiwa mzee kundini. Kama maono hayo mawili yanavyoonyesha, Yehova hazuii baraka kutoka kwa wale wanaoitikia ule mwaliko wake wenye upendo wa kurudi.
Lakini, ili kuonea shangwe baraka hizo, ni lazima kwanza mtu athamini msaada unaotolewa na kuuitikia. Katika makundi mengi ndugu hukumbuka wale ambao wameacha kutenda na huwatembelea mara kwa mara, wakijaribu kuwasaidia. Kuitikia msaada wa jinsi hiyo huonyesha uthamini kwa ajili ya rehema ya Yehova.—Yakobo 5:19, 20.
Kwa kweli, huu ndio wakati wa kuuitikia mwaliko wa Yehova: “Nirudieni mimi.” (Malaki 3:7; Isaya 1:18) Usingojee muda mrefu zaidi. Matukio ya ulimwengu yanasonga kwa uharaka wenye kutokeza. Mahali palipofaa zaidi kuwapo katika zile nyakati za dhoruba zilizo mbele ni katika tengenezo la Yehova, salama chini ya ulinzi wake. Ni wale tu wanaomkimbilia Yehova ndio walio na tumaini thabiti la kufichwa kutoka kwa ghadhabu yake kwenye siku ya hasira yake.—Sefania 2:2, 3.
[Picha katika ukurasa wa 30]
Je! utauitikia mwaliko wa Yehova, “Nirudieni mimi”?