Jifunze Utii kwa Kukubali Nidhamu
EBU wazia kwamba umesimama juu ya mwamba uliochongoka wa mlima mrefu sana ukihisi ukiwa juu ya ulimwengu kihalisi. Hiyo ni hisia ya uhuru yenye kufurahisha kama nini!
Hata hivyo kwa kweli uhuru wako ni wenye mipaka. Sheria ya nguvu za uvutano huzuia sana kila hatua unayochukua; hatua moja isiyofaa yaweza kutokeza msiba. Kwa upande ule mwingine, inaridhisha kama nini kujua kwamba sheria hiyohiyo ya nguvu za uvutano inakuzuia usipeperuke kuingia anga la nje bila kuweza kujizuia. Kwa hiyo kwa wazi sheria hiyo ni kwa faida yako mwenyewe. Kukubali mipaka ambayo inawekea hatua zako ukiwa juu kwenye kilele hicho cha mlima kunanufaisha, hata kuokoa.
Naam, nyakati nyingine sheria na kuzitii hizo huenda kukawekea mipaka uhuru wetu, lakini je, hilo lafanya utii uwe jambo lisilotamanika?
Jinsi Ambavyo Mungu Huona Utii
Akiwa “Muumba Mtukufu,” Yehova ndiye “chanzo cha uhai.” Kwa sababu hiyo viumbe vyake vyote vyawiwa naye utii kwa haki. Akionyesha mtazamo ufaao, mtunga zaburi aliandika hivi: “Njoni, tuabudu, tusujudu, tupige magoti mbele za BWANA [Yehova, NW] aliyetuumba. Kwa maana ndiye Mungu wetu, na sisi tu watu wa malisho yake, na kondoo za mkono wake.”—Mhubiri 12:1, NW; Zaburi 36:9, NW; 95:6, 7.
Tangu mwanzoni Yehova ametaka utii kutoka kwa viumbe vyake. Kuendelea kuwako kwa Adamu na Hawa katika Paradiso kulitegemea utii. (Mwanzo 2:16, 17) Utii ulitazamiwa vilevile kutoka kwa malaika, hata ingawa wana namna ya uhai ya juu zaidi kuliko wanadamu. Kwa sababu baadhi ya viumbe-roho hao ‘hawakutii hapo zamani, uvumilivu wa Mungu ulipokuwa ukingoja, siku za Noa,’ waliadhibiwa kwa kutiwa ndani ya “mashimo yenye giza zito mno wawekwe akiba kwa ajili ya hukumu.”—1 Petro 3:19, 20; 2 Petro 2:4, NW.
Kwa kusema waziwazi, Mungu huona utii kuwa takwa la kupata kibali chake. Twasoma hivi: “Je! BWANA [Yehova, NW] huzipenda sadaka za kuteketezwa na dhabihu sawasawa na kuitii sauti ya BWANA [Yehova, NW]? Angalia, kutii ni bora kuliko dhabihu, na kusikia kuliko mafuta ya beberu.”—1 Samweli 15:22.
Lazima Kujifunza Utii —Kwa Nini na Kwa Jinsi Gani
Utii huongoza kwenye msimamo mwadilifu pamoja na Mungu, kwa hiyo ni lazima kama nini tujifunze huo! Kama vile kujifunza lugha ya kigeni, twaweza kujifunza zoea la kutii tunapokuwa wachanga. Ndiyo sababu Biblia hukazia kuzoeza watoto tangu utoto wao.—Yoshua 8:35.
Baadhi ya watu wa ki-siku-hizi hupinga maoni ya Biblia, wakisema kwamba kutaka utii kutoka kwa watoto ni sawa na kudhibiti akili kinguvu. Wanatoa hoja kwamba watoto wanapaswa waruhusiwe wakuze mawazo na viwango vyao vya kibinafsi ambavyo watafuata maishani bila mwingilio wa mtu mzima.
Lakini katika miaka ya 1960 wakati wazazi wengi walipokuwa na maoni hayo, Wilhelm Hansen, mhadhiri, mhariri, na profesa wa saikolojia, hakukubaliana na hilo. Aliandika hivi: “Kwa mtoto aliye katika hatua zake za ukuzi za mapema, wakati uhusiano wake na wazazi wake ungali haujaimarika, wazazi hukataa lililo ‘baya’ nao hupendekeza au hupongeza lililo ‘zuri.’ Kwa hiyo, utii peke yake humwongoza mtoto katika njia ya kiadili na ya sifa nzuri za msingi ambazo kwazo uhusiano wake na utaratibu wa kiadili hutegemea.”—Linganisha Mithali 22:15.
Neno la Mungu hukazia uhitaji wa kujifunza utii. Twasoma hivi: “Najua, Ee BWANA [Yehova, NW], kwamba mwanadamu hawezi kujichagulia mwenyewe njia zake; wala mwanadamu hawezi kuamulia mwendo wake maishani.” (Yeremia 10:23, The New English Bible) Historia imejaa mifano inayoonyesha jinsi ambavyo wanadamu wamejipangia mwendo wao wenyewe wa maisha kulingana na viwango vya kibinafsi na wamepatwa na magumu mazito kwa sababu ya kufanya hivyo. Kwa nini hilo hutukia mara nyingi sana? Kwa sababu wanadamu hawana maarifa, hekima, na uelewevu wa kujipangia mwendo wao wa maisha bila msaada. Kwa ubaya zaidi, wana mwelekeo uliorithiwa wa kufanya maamuzi yasiyofaa. Mara baada ya Furiko, Yehova alisema hivi juu ya mwanadamu: “Mbetuko wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea.”—Mwanzo 8:21, NW.
Kwa hiyo, hakuna yeyote anayerithi mwelekeo wa kumtii Yehova. Ni lazima tuukazie kikiki katika watoto wetu na kuendelea kujifunza juu yao muda wote wa maisha yetu. Kila mmoja wetu anahitaji kusitawisha ile hali ya moyo ya Mfalme Daudi, aliyeandika hivi: “Ee BWANA [Yehova, NW], unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako, uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha. Maana Wewe ndiwe Mungu wa wokovu wangu, nakungoja Wewe mchana kutwa.”—Zaburi 25:4, 5.
Fundisha Utii kwa Kuwa Mtiifu
Mama ya Yesu na Baba mlezi wake walijua vema hali zilizozunguka kuzaliwa kwa Yesu. Kwa hiyo walitambua kwamba angekuwa na sehemu yenye maana katika utimizo wa makusudi ya Yehova. (Linganisha Luka 1:35, 46, 47.) Kwa habari yao yale maneno “Tazama, wana ndio urithi wa BWANA [Yehova, NW]” yalikuwa na maana ya pekee. (Zaburi 127:3) Walitambua kikamili daraka lao kubwa na hivyo walikuwa wepesi kutii mielekezo ya kimungu, kama vile wakati walipoambiwa wakimbilie Misri au baadaye kwenda Galilaya.—Mathayo 2:1-23.
Wazazi wa Yesu walitambua pia daraka lao kuhusu nidhamu. Ni kweli, wakati wa kuwapo kwake kabla ya kuwa mwanadamu, Yesu alikuwa amekuwa mtiifu sikuzote. Lakini alipokuwa duniani, alijifunza kuwa mtiifu chini ya hali mpya kabisa. Kwanza, alihitaji kuwatii wazazi wasio wakamilifu kwa sababu hata mtoto mkamilifu anahitaji nidhamu kwa namna ya maagizo na elimu. Wazazi wake walimwandalia hayo. Kwa upande ule mwingine, nidhamu kwa namna ya adhabu haikuhitajiwa. Yesu alitii sikuzote; hakuhitaji kuambiwa mambo mara mbili. Twasoma hivi: “Alienda nyumbani Nazareti pamoja nao [wazazi wake] na alikuwa mtiifu kwao.”—Luka 2:51, Phillips.
Yusufu na Mariamu pia walijua jinsi ya kumfundisha Yesu kwa njia ya mfano. Kwa mfano, twasoma kwamba “wazazi wake walikuwa na desturi ya kwenda Yerusalemu kila mwaka wakati wa sikukuu ya Pasaka.” (Luka 2:41, HNWW) Kwa kupanga kuichukua familia yake pamoja naye, Yusufu alionyesha kwamba alipendezwa na hali njema yao ya kiroho na kwamba alichukua ibada ya Yehova kwa uzito. Katika njia izo hizo, wazazi kwa utii wao wenyewe katika mambo ya ibada wanaweza kuwafunza watoto wao utii leo.
Kwa sababu ya kule kutia vizuri nidhamu katika uadilifu kwa upande wa Yusufu na Mariamu, “Yesu alizidi kuendelea katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu.” Huo ni mfano mzuri kama nini kwa wazazi Wakristo kufuata leo!—Luka 2:52.
“Watiini . . . Katika Mambo Yote”
“Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana.” (Wakolosai 3:20) Yesu aliweza kuwa mtiifu kwa wazazi wake katika mambo yote kwa sababu utii wao kwa Yehova ulifanya wasimdai Yesu—au ndugu na dada zake nusu—jambo lolote lililokuwa kinyume cha mapenzi ya Yehova.
Wazazi wengi leo wanafanikiwa pia kuwafundisha watoto wao kuwa watiifu katika mambo yote. Sikiliza akina baba watatu, waliokwisha kulea watoto na sasa hutumikia katika tawi moja la Watch Tower Society.
Theo husema juu ya jinsi yeye na mke wake walivyolea wana watano. Yeye asema hivi: “Ni jambo la maana kuwajulisha watoto tangu mwanzoni kwamba sisi watu wazima hufanya makosa pia. Kwa kusikitisha, sisi hata huyarudia na huhitaji daima kumwomba Baba yetu wa kimbingu msamaha na msaada. Tuliwaruhusu kimakusudi watoto wetu waone kwamba sawa na vile walivyokuwa wakipambana na mahangaiko ya ujana, sisi tulikuwa tukipambana na mahangaiko ya watu wazima.”
Ikiwa mtoto atajifunza utii, uhusiano wenye upendo kati yake na wazazi wake ni wa muhimu. Hermann asema hivi juu ya mke wake: “Hakuwa tu mama ya wana bali alikuwa rafiki yao pia. Walithamini hilo, kwa hiyo haikuwa vigumu kwao kuwa watiifu.” Halafu akiongeza shauri lenye kutumika kuhusu jinsi ya kuwa na uhusiano bora zaidi kati ya mzazi na mtoto, yeye asema hivi: “Tuliamua kimakusudi kutokuwa na mashine ya kuoshea vyombo kwa muda wa miaka kadhaa, ili vyombo vioshwe na kukaushwa kwa mkono. Wana wetu walipewa mgawo wa kuvikausha, kwa zamu. Hakukuwa wakati bora zaidi kwa ajili ya mawasiliano ya vivi hivi.”
Uhusiano wenye upendo kati ya mzazi na mtoto hutumika kuwa kielelezo cha ule uhusiano ambao ni lazima Mkristo awe nao pamoja na Yehova. Rudolf aeleza jinsi yeye na mke wake walivyowasaidia wavulana wao wawili waanzishe uhusiano wa jinsi hiyo: “Msingi wetu ulikuwa funzo la familia la kawaida. Tuliwapa watoto hesabu fulani ya vichwa vifaavyo vya kufanyia utafiti. Pia tulifanya usomaji wa Biblia pamoja kisha kuzungumzia habari hiyo. Wana wetu waliweza kuona kwamba Yehova hutazamia utii kutoka kwa wazazi, si kutoka kwa watoto tu.”
Wazazi Wakristo hutambua kwamba maandishi yenye kupuliziwa roho “Makaripio ya nidhamu ndiyo njia ya uhai” hutumika kwao pamoja na kwa watoto wao. Kwa hiyo ingawa watoto wana wajibu wa kuwa watiifu kwa wazazi wao katika mambo yote, ni lazima wazazi pia wawe watiifu katika mambo yote ambayo Yehova hutaka kwao. Licha ya kuimarisha ule uhusiano kati ya mzazi na mtoto, wazazi na watoto watataka kuimarisha uhusiano wao na Mungu.—Mithali 6:23, NW.
Kuwa na Maoni Yafaayo Juu ya Utii
Twaweza kushukuru kama nini kwamba Neno la Mungu linaandaa shauri lenye kutumika jinsi hiyo kuhusu kuwalea watoto! (Ona sanduku.) Watoto wanaojifunza utii kutoka kwa wazazi wanaowatia nidhamu katika uadilifu ni chanzo cha shangwe ya kweli kwa udugu wote wa Kikristo.
Kwa kuwa utii kwa Mungu unamaanisha uhai, ni lazima tuepuke hata kufikiria lile wazo la kuondosha vile vizuizi ambavyo amri za Mungu huwekea uhuru wetu wa kibinafsi—hata kwa muda tu. Kwa mfano, ebu wazia kwamba tungeweza kwa muda mfupi kuondosha ile sheria ya nguvu za uvutano. Tungesisimuka kama nini kuruka kutoka kilele cha mlima hadi angani bila jambo lolote la kuuzuia uhuru wetu! Lakini ni nini lingetukia mara mambo yangerudia hali ya kawaida? Ebu fikiria lile anguko ambalo lingetungojea!
Kujifunza utii kwa kukubali nidhamu huchangia ukuzi wa utu wenye usawaziko na hutusaidia tujue mipaka yetu. Kunatusaidia tuepuke kuwa wenye kudai mno na wenye kutojali haki na mahitaji ya wengine. Kunatusaidia tuepuke vipindi vya kukosa uhakika. Kwa ufupi, kunatokeza furaha.
Kwa hiyo uwe mtu mzima au mtoto, jifunze utii kwa kukubali nidhamu ili kwamba “upate fanaka” na ili kwamba ‘uishi miaka mingi duniani.’ (Waefeso 6:1-3, HNWW) Ni nani anayetaka kulihatarisha taraja lake la kuishi milele kwa kushindwa kujifunza utii kwa kutokubali nidhamu?—Yohana 11:26.
[Sanduku katika ukurasa wa 29]
WAZAZI, FUNDISHENI UTII KWA KUTIA NIDHAMU KATIKA UADILIFU
1. Tia nidhamu kwa msingi wa sheria na kanuni za Kimaandiko.
2. Tia nidhamu si tu kwa kudai utii bali kwa kueleza kwa nini utii ndio mwendo wenye hekima.—Mathayo 11:19b.
3. Usitie nidhamu ukiwa na hasira wala kwa kupiga kelele.—Waefeso 4:31, 32.
4. Tia nidhamu ndani ya uchangamfu wa uhusiano wenye upendo na wenye kujali.—Wakolosai 3:21; 1 Wathesalonike 2:7, 8; Waebrania 12:5-8.
5. Tia watoto nidhamu tangu utoto.—2 Timotheo 3:14, 15.
6. Tia nidhamu tena na tena na bila ugeugeu.—Kumbukumbu la Torati 6:6-9; 1 Wathesalonike 2:11, 12.
7. Jitie nidhamu wewe mwenyewe kwanza na hivyo ufundishe kwa mfano.—Yohana 13:15; linganisha Mathayo 23:2, 3.
8. Tia nidhamu ukimtegemea Yehova kikamili, ukimwomba msaada wake katika sala.—Waamuzi 13:8-10.
[Picha katika ukurasa wa 28]
‘Makaripio ya nidhamu ndiyo njia ya uhai”