Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 11/15 kur. 4-6
  • Sababu Kwa Nini Wengine Wanazaliwa Mara ya Pili

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sababu Kwa Nini Wengine Wanazaliwa Mara ya Pili
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kusudi la Mungu kwa Ainabinadamu
  • Ni Nini Linaloipata Nafsi Wakati wa Kifo?
  • Kuzaliwa Mara ya Pili Ili Kutawala Wakiwa Wafalme
  • Namna Gani Dunia?
  • Ni Nani Watakaonufaika?
  • Unaweza Kuamini Kutakuwa na Dunia Paradiso
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Kusudi la Mungu kwa Kufanya Wengine ‘Wazaliwe Mara ya Pili’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Yesu Kristo, Yeye Ambaye Kupitia Kwake Mungu Hubariki Wanadamu
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Je! Umepata Kujiuliza?
    Amkeni!—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 11/15 kur. 4-6

Sababu Kwa Nini Wengine Wanazaliwa Mara ya Pili

“MTU asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:3) Maneno hayo yamesisimua na kutatanisha watu wengi tangu Yesu Kristo alipoyasema zaidi ya miaka 1,900 iliyopita.

Ili kupata uelewevu ufaao wa taarifa za Yesu kuhusu kuzaliwa mara ya pili, ni lazima kwanza tujibu maswali haya: Kusudi la Mungu kwa ainakibinadamu ni nini? Ni nini linaloipata nafsi wakati wa kifo? Ufalme wa Mungu unapaswa kufanya nini?

Kusudi la Mungu kwa Ainabinadamu

Mtu wa kwanza, Adamu, aliumbwa akiwa mwana wa Mungu wa kibinadamu aliye mkamilifu. (Luka 3:38) Yehova Mungu hakunuia Adamu afe. Adamu na mke wake, Hawa, walikuwa na taraja la kutokeza familia ya kibinadamu isiyo na dhambi ambayo ingeishi milele na kuijaza dunia-paradiso. (Mwanzo 1:28) Kifo hakikuwa sehemu ya kusudi la Mungu la awali kwa mwanamume na mwanamke. Kiliingia mandhari ya kibinadamu kwa ghafula kikiwa tokeo tu la uasi dhidi ya sheria ya kimungu.—Mwanzo 2:15-17; 3:17-19.

Uasi huo ulitokeza masuala makubwa ya kiadili, kama vile haki ya enzi kuu ya Mungu na uwezo wa wanadamu wa kubaki waaminifu kwa sheria zake. Wakati ungehitajiwa ili kusuluhisha masuala hayo. Lakini kusudi la Yehova Mungu kwa ainabinadamu halikubadilika, na hawezi kushindwa katika lile ambalo amenuia kufanya. Anakusudia kikamili kuijaza dunia na familia ya kibinadamu kamilifu itakayofurahia maisha katika Paradiso. (Zaburi 37:29; 104:5; Isaya 45:18; Luka 23:43) Ni lazima tukumbuke kweli hiyo ya msingi tunapoyachunguza maneno ya Yesu kuhusu kuzaliwa mara ya pili.

Ni Nini Linaloipata Nafsi Wakati wa Kifo?

Wakiwa hawajui lile ambao roho takatifu ya Mungu ilikuwa imewafunulia waandishi wa Biblia, wanafalsafa Wagiriki waling’ang’ana kupata maana katika maisha. Hawakuweza kuamini kwamba mwanadamu alipaswa aishi kwa miaka michache tu, mara nyingi katika hali zenye kuhuzunisha, na kisha kukoma kuishi tu. Kwa habari hiyo walikuwa sahihi. Lakini katika mikataa yao kuhusu matarajio ya mwanadamu baada ya kifo, hawakuwa sahihi. Walikata maneno kwamba kuwako kwa kibinadamu kuliendelea katika umbo jingine baada ya kifo, kwamba ndani ya kila mtu mlikuwamo nafsi isiyoweza kufa.

Wayahudi na watu waliodai kuwa Wakristo walivutiwa na maoni kama hayo. Chasema kitabu Heaven—A History: “Wakati Wayahudi walioishi nje ya Palestina walipokutana na Wagiriki wenye weledi, wazo la nafsi isiyoweza kufa lilitokea.” Kitabu hicho chaongeza hivi: “Mafundisho ya Kigiriki kuhusu nafsi yalivutia sana imani za Kiyahudi na hatimaye za Kikristo. . . . Kwa kubuni mchanganyiko wa kipekee wa falsafa ya Kiplato na mapokeo ya kibiblia, Filo [mwanafalsafa Myahudi wa karne ya kwanza wa Aleksandria] aliwafungulia njia Wakristo wa baadaye wenye kufikiria.”

Filo aliamini nini? Kitabu icho hicho chaendelea hivi: “Kwake, kifo huirudisha nafsi kwenye hali yayo ya awali, ya kabla ya kuzaliwa. Kwa kuwa nafsi ni mali ya ulimwengu wa kiroho, maisha katika mwili si kitu bali ni kipindi kifupi, ambacho mara nyingi ni chenye kusikitisha.” Hata hivyo, hali ya Adamu “kabla ya kuzaliwa” ilikuwa ya kutokuwako. Kulingana na usimulizi wa Biblia, Mungu hakukusudia kamwe kuwe na uhamisho wa mara moja hadi makao mengine wakati wa kifo, kana kwamba dunia ilikuwa mahali pa kutayarishwa tu kwa ajili ya kuwako kwa juu zaidi au kwa chini zaidi.

Imani kwamba nafsi ya kibinadamu haiwezi kufa haifundishwi katika Neno la Mungu lililopuliziwa roho, Biblia. Haitumii hata mara moja maneno “nafsi isiyoweza kufa.” Inataarifu kwamba Adamu aliumbwa akiwa nafsi, si akiwa na nafsi. Mwanzo 2:7 husema hivi: “BWANA [Yehova, NW] Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” Ainabinadamu haikukabiliwa kamwe na taraja la ama uhai wa milele mbinguni ama kuteseka milele katika moto wa mateso. Biblia huonyesha kwamba nafsi, au mtu, anayekufa hayuko katika hali ya ufahamu. (Zaburi 146:3, 4; Mhubiri 9:5, 10; Ezekeli 18:4) Kwa hiyo, wanafalsafa wamekuwa na maoni yasiyo ya kimaandiko kuhusu nafsi. Tunahitaji kujilinda wenyewe dhidi ya mawazo yenye kuongoza vibaya ambayo yangeweza kutia kivuli uelewevu wetu wa maneno ya Yesu kuhusu kuzaliwa mara ya pili.

Kuzaliwa Mara ya Pili Ili Kutawala Wakiwa Wafalme

Yesu alimwambia Nikodemo kwamba wale ‘wanaozaliwa mara ya pili wanaingia ufalme wa Mungu.’ (Yohana 3:3-5) Ufalme huo ni nini? Katika lugha ya ufananisho mapema katika historia ya kibinadamu, Yehova Mungu alionyesha kusudi lake la kutumia “mbegu” ya pekee—mtawala anayekuja—kuponda kichwa cha Nyoka wa awali, Shetani Ibilisi. (Mwanzo 3:15, NW; Ufunuo 12:9) Kama ilivyofunuliwa kidato kwa kidato katika Maandiko, “mbegu” hiyo inatambulishwa kuwa Yesu Kristo, anayetawala pamoja na watawala washiriki katika dhihirisho la kipekee la enzi kuu ya Mungu, Ufalme wa Kimesiya. (Zaburi 2:8, 9; Isaya 9:6, 7; Danieli 2:44; 7:13, 14) Huo ni Ufalme wa mbingu, serikali mbinguni itakayotetea enzi kuu ya Yehova na kuiokoa ainabinadamu kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo.—Mathayo 6:9, 10.

Wenye kushirikiana na Yesu wakiwa watawala wenzi ni 144,000 wanaonunuliwa kutoka ainakibinadamu. (Ufunuo 5:9, 10; 14:1-4) Mungu amechagua watu fulani kutoka kwa familia ya Adamu ya kibinadamu isiyo kamilifu kuwa “watakatifu [hao] wake Aliye juu,” wanaotawala pamoja na Kristo katika Ufalme wa Kimesiya. (Danieli 7:27; 1 Wakorintho 6:2; Ufunuo 3:21; 20:6) Wanaume na wanawake hao wanaweka imani katika Yesu Kristo, aliyesema kwamba ‘wangezaliwa mara ya pili.’ (Yohana 3:5-7) Kuzaliwa huko kunatukiaje na kwa nini?

Watu hao mmoja mmoja wamebatizwa katika maji wakiwa wafuasi wa Kristo. Mungu amewasamehe dhambi zao kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu, amejulisha rasmi kuwa ni waadilifu, na amewafanya kuwa wana wa kiroho. (Warumi 3:23-26; 5:12-21; Wakolosai 1:13, 14) Kwa hao mtume Paulo asema hivi: “Mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, Aba, yaani, Baba. Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu; na kama tu watoto, basi, tu warithi; warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo; naam, tukiteswa pamoja naye ili tupate na kutukuzwa pamoja naye.”—Warumi 8:15-17.

Wakiwa wafuasi wa Kristo, hao wamekuwa na uzaliwa mpya, au kuwa na mwanzo mpya, maishani. Tokeo limekuwa usadikisho wa kwamba wangeshiriki urithi wa Yesu wa kimbingu. (Luka 12:32; 22:28-30; 1 Petro 1:23) Mtume Petro alifafanua kuzaliwa upya huko katika njia hii: “Kwa rehema zake nyingi [Mungu] alituzaa mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa kufufuka kwake Yesu Kristo katika wafu; tupate na urithi usioharibika, usio na uchafu, usionyauka, uliotunzwa mbinguni kwa ajili yenu.” (1 Petro 1:3, 4) Maisha hayo mapya mbinguni huwezekana kwa watu hao mmoja mmoja kwa sababu Mungu anawafufua kama alivyomfufua Yesu.—1 Wakorintho 15:42-49.

Namna Gani Dunia?

Hilo halimaanishi kwamba hatimaye ainabinadamu yote tiifu itazaliwa mara ya pili ili itoke duniani kwenda mbinguni. Wazo hilo lenye kosa lilifanana na lile la wanafalsafa kama Filo, waliofikiri kwamba “maisha katika mwili si kitu bali ni kipindi kifupi, ambacho mara nyingi ni chenye kusikitisha.” Lakini hakukuwa kasoro yoyote na uumbaji wa kidunia wa awali wa Yehova Mungu.—Mwanzo 1:31; Kumbukumbu la Torati 32:4.

Uhai wa kibinadamu haukupaswa kamwe uwe mfupi na wenye maumivu. Yesu Kristo na wale wanaozaliwa mara ya pili ili kutumikia wakiwa wafalme na makuhani pamoja naye mbinguni wataondolea mbali matokeo yote yenye kudhuru ya uasi wa Shetani. (Waefeso 1:8-10) Kupitia wao wakiwa ‘mbegu ya Abrahamu’ iliyoahidiwa, “mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Wagalatia 3:29; Mwanzo 22:18) Kwa ainabinadamu tiifu hilo litamaanisha uhai juu ya dunia-paradiso, tofauti kabisa na kuwako kwa leo kuliko kufupi, kwenye kujawa na maumivu.—Zaburi 37:11, 29; Ufunuo 21:1-4.

Ni Nani Watakaonufaika?

Miongoni mwa wale wanaonufaika kutokana na uandalizi wa Mungu wa kuwabariki ainabinadamu ni wafu watakaofufuliwa wanaozoea imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Wengi wao hawajapata kujifunza juu ya Mungu na Kristo na kwa hiyo wasingeweza kuonyesha imani katika Yesu. Wale watakaofufuliwa watatia ndani pia watu waaminifu kama vile Yohana Mbatizaji, aliyekufa kabla ya kifo cha Yesu kufungulia njia ya uhai wa kimbingu. (Mathayo 11:11) Licha ya hao, ‘mkutano mkubwa sana kutoka kila taifa wamefua mavazi yao na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,’ Yesu Kristo. Wanaitikia ifaavyo kazi ya kuhubiri Ufalme inayoongozwa na “ndugu” za Yesu waliozaliwa mara ya pili na watakaookoka vita ya Mungu ya Har–Magedoni kuishi juu ya dunia iliyosafishwa. (Ufunuo 7:9-14; 16:14-16; Mathayo 24:14; 25:31-46) Kwa hiyo, katika mpango wa Mungu, mamilioni wataokolewa, ingawa hawazaliwi mara ya pili ili kutawala na Kristo mbinguni.—1 Yohana 2:1, 2.

Je! wewe utakuwa miongoni mwa wale watakaorithi uhai juu ya dunia-paradiso? Wewe waweza kuwa miongoni mwao ukizoea imani katika dhabihu ya Yesu Kristo na kushirikiana kwa bidii na kundi la Kikristo la kweli. Halijapata kufisidiwa na falsafa bali limebaki likiwa “nguzo na msingi wa kweli.” (1 Timotheo 3:15; linganisha Yohana 4:24; 8:31, 32.) Kisha waweza kutazama mbele kwenye wakati ujao mzuri ajabu wakati ambapo wana wa Mungu waliozaliwa mara ya pili wanatawala mbinguni na watoto wa Mungu wote wa kidunia wamerudishwa kwenye ukamilifu juu ya dunia-paradiso ya ajabu. Kwa hiyo twaa fursa yako ya uhai katika ulimwengu mpya wenye baraka za milele.—Warumi 8:19-21; 2 Petro 3:13.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Adamu hakupewa kamwe hiari ya ama uhai mbinguni ama kuteseka milele katika moto wa helo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki