Thamani ya Mafunjo ya Nash
UNAWEZAJE kwa usahihi kuwekea tarehe hati-mkono ya zamani ya Biblia ya Kiebrania? Hilo ndilo lililokuwa tatizo lililomkabili Dakt. John C. Trever katika 1948 alipoona kwa mara ya kwanza ile Hati-Kunjo ya Bahari ya Chumvi ya Isaya. Namna ya herufi za Kiebrania zilimsisimua. Naye alijua herufi hizo ndizo zilizokuwa na ufunguo wa kupata umri wa hati-kunjo hizo, lakini angeweza kuzilinganisha na nini? Kwa usahihi, alifikia mkataa huu: Na hati ya mafunjo ya Nash tu. Kwa nini? Hati-mkono hiyo ni nini, nayo ilitoka wapi?
Mafunjo ya Nash yanatia ndani vijipande vinne tu vya mistari 24 ya maandishi-awali ya Kiebrania, vyenye ukubwa wa sentimeta 7.5 kwa 12.5. Yalipewa jina la W. L. Nash, katibu wa Society of Biblical Archaeology, aliyeyapata kutoka kwa mfanya biashara mmoja kutoka Misri katika 1902. Yalitangazwa kwa chapa na S. A. Cooke katika mwaka uliofuata katika kichapo cha sosaiti hiyo kiitwacho Proceedings na yakatolewa kwa Cambridge University Library, Uingereza, ambamo yamekaa. Thamani ya kijipande hicho cha mafunjo inalinganika na umri wacho. Wanachuo walikipatia tarehe ya karne ya pili au ya kwanza K.W.K., kwa hiyo ulikuwa ndio ukurasa wa hati-mkono wa Kiebrania wa mapema zaidi kupatikana.
Wakati Dakt. Trever alipolinganisha slaidi yenye rangi ya Mafunjo ya Nash pamoja na ile hati-kunjo iliyokuwa mbele yake, aliangalia kwa makini sana namna na maumbo ya herufi moja moja. Bila shaka yoyote, yalifanana sana. Ingawa hivyo, lilionekana kuwa jambo lisiloweza kuaminika kwake kwamba ile hati-mkono kubwa, iliyovumbuliwa karibuni ingeweza kwa vyovyote kuwa ya tarehe ya mapema kama mafunjo ya Nash. Hata hivyo, baadaye, kusababu kwake kulithibitika kuwa sahihi. Hati-Kunjo ya Bahari ya Chumvi ya Isaya ilikuwa ya karne ya pili K.W.K.!
Yaliyomo Katika Mafunjo ya Nash
Mchanganuo wa maandishi-awali ya Mafunjo ya Nash unafunua kwamba mistari yayo 24 yote si kamili, yakiwa yanakosa neno au herufi kwenye miisho yayo yote miwili. Yanatia ndani sehemu za zile Amri Kumi kutoka kitabu cha Kutoka sura 20, pamoja na baadhi ya mistari kutoka Kumbukumbu la Torati sura 5 na 6. Kwa hiyo haikuwa hati-mkono ya Biblia ya kawaida bali ulikuwa mchanganyiko wa maandishi-awali wenye kusudi la pekee. Yaonekana ilikuwa sehemu ya mkusanyiko wa mafundisho ya kumkumbusha Myahudi juu ya wajibu wake kwa Mungu. Sehemu ya andiko inayoanza na Kumbukumbu la Torati 6:4, iitwayo Shema, ilirudiwa mara nyingi. Mstari huo husema hivi: “Ee Israeli; BWANA [Yehova, NW], Mungu wetu, BWANA [Yehova, NW] ndiye mmoja.”
Tetragramatoni, YHWH, “Yehova,” katika andiko hilo inaonekana mara mbili kwenye mstari wa mwisho wa mafunjo hayo, na inatokea katika mahali pengine patano. Pia inatokea mara moja herufi yayo ya kwanza ikiwa inakosekana.
Shema ilikusudiwa hasa kukazia “utu mmoja wa Mungu.” Kulingana na Talmud ya Kiyahudi (Berakoth 19a), neno la kumalizia, ʼE·chadhʹ (“Mmoja”), “lilipasa kukaziwa hasa wakati lilipokuwa likitamkwa kwa kutaja kila silabi.” (W. O. E. Oesterley na G. H. Box) Kuhusiana na Mungu, neno ʼE·chadhʹ lililorefushwa lilipiga mbiu pia juu ya kutokuwa kwake na kifani.
Leo, Mafunjo ya Nash yana marika mengi, hasa miongoni mwa hati-kunjo yaliyopatikana katika mapango yaliyo kwenye ukingo wa bahari ya Chumvi karibu na Kwumran. Mchanganuo wenye mambo mengi madogomadogo umethibitisha kwamba nyingi za hati-mkono hizo ni za tarehe ya karne ya kwanza na ya pili K.W.K.a Ingawa Mafunjo ya Nash si hati-mkono ya Kiebrania ya mapema zaidi kujulikana, bado ni yenye kupendeza sana. Inabaki kuwa hati-mkono ya Biblia ya Kiebrania pekee ya tarehe hiyo ya mapema iliyovumbuliwa Misri.
[Maelezo ya Chini]