‘Kunyakuliwa Ili Kumlaki Bwana’—Jinsi Gani?
WAKATI unaoelekea mwisho wa mfumo mbovu uliopo unaendelea kupungua kwa kasi. Kila saa, kila dakika, kila sekunde ipitapo, tunakaribia matukio yenye kutokeza yaliyotolewa unabii zamani. Je! kuchukuliwa kimwili kutoka duniani ni moja yayo? Ikiwa ndivyo, kutatukia wakati gani na jinsi gani?
Neno la Kiingereza “rapture” (kuchukuliwa kimwili kutoka duniani) halionekani katika Biblia. Lakini wale wanaoamini jambo hilo hutaja maneno ya mtume Paulo kwenye 1 Wathesalonike 4:17 likiwa msingi wa imani yao. Acheni tulichunguze andiko hilo katika muktadha walo. Paulo aliandika hivi:
“Lakini, ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini. Maana, ikiwa twaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye. Kwa kuwa twawaambieni haya kwa neno la Bwana, kwamba sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake [kuwapo kwa, New World Translation] Bwana, hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti. Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. Kisha sisi tulio hai, tuliosalia; tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele. Basi farijianeni kwa maneno hayo.”—1 Wathesalonike 4:13-18.
Kundi katika Thesalonike lilikuwa jipya kwa kadiri fulani wakati Paulo alipoandika barua yake ya kwanza kwa Wakristo huko katika yapata 50 W.K. Washiriki wa kundi hilo walitaabika kwamba baadhi yao walikuwa ‘wamelala mauti.’ Hata hivyo, yale Paulo aliandika yaliwafariji Wathesalonike kwa tumaini la ufufuo.
“Kuwapo kwa” Kristo
Alipokuwa akithibitisha kwamba Wakristo waaminifu waliokuwa wamekufa wakati huo wangefufuliwa, Paulo alisema hivi pia: “Sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake [kuwapo kwa, NW] Bwana, hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti.” (Mstari 15) Lenye kutokeza kwelikweli, ni rejezeo la mtume huyo kwenye “kuwapo” kwa Bwana. Hapo maandishi ya lugha ya awali hutumia neno la Kigiriki pa·rou·siʹan, linalomaanisha kihalisi “kuwa kando ya.”
Rais wa nchi ya kigeni anapozuru nchi, kwa ukawaida tarehe za kuwapo kwake huko hutangazwa. Ndivyo imekuwa na kuwapo kwa Bwana Yesu Kristo. Mnara wa Mlinzi limewatokezea kwa uthabiti wanafunzi wa unabii wa Biblia wenye mioyo myeupe uthibitisho wa kwamba kuwapo kwa Yesu katika mamlaka ya Ufalme wa kimbingu kulianza katika 1914. Matukio ya tangu mwaka huo yanashuhudiza kuwapo kwa Yesu kusikoonekana. (Mathayo 24:3-14) Kwa hiyo kwa kusema kwamba Wakristo fulani ambao wangeishi wakati wa kuwapo kwa Bwana ‘wangenyakuliwa katika mawingu, ili kumlaki Bwana,’ Paulo alimaanisha kwamba waokokaji hao wangemlaki Kristo, si katika angahewa ya dunia, bali katika makao ya kimbingu yasiyoonekana ambako Yesu aketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu. (Waebrania 1:1-3) Lakini hao ni akina nani?
“Israeli wa Mungu”
Maandiko husema mengi kuhusu Waisraeli wa kimwili na pia husema juu ya “Israeli wa Mungu” wa kiroho. Waamini Wayahudi na Wasio Wayahudi wangejumulika kufanya idadi kamili ya kikundi hicho cha wapakwa-mafuta kwa roho takatifu au kani ya utendaji ya Mungu. (Wagalatia 6:16; Warumi 11:25, 26; 1 Yohana 2:20, 27) Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha kwamba idadi kamili ya Israeli wa kiroho ni 144,000, wote ambao huonyeshwa pamoja na Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, wakiwa kwenye Mlima Sayuni wa kimbingu. Pamoja na Kristo, wangekuwa wafalme na makuhani mbinguni. (Ufunuo 7:1-8; 14:1-4; 20:6) Waliotiwa miongoni mwao ni watu mmoja mmoja waliokuwa wameshiriki na makundi katika Thesalonike na kwingineko, bila kujali yaliyokuwa malezi yao ya kijamii na ya kitaifa.—Matendo 10:34, 35.
Kabla ya washiriki waaminifu wowote wa Israeli wa kiroho kuweza kupokea thawabu ya kimbingu, wangalipaswa washiriki ono fulani. Kama vile kifo cha Yesu juu ya mti wa mateso kilitangulia ufufuo wake kwenye uhai mbinguni, ndivyo ilivyo lazima Wakristo wenye tumaini la kimbingu wafe kabla ya kupokea thawabu yao. (1 Wakorintho 15:35, 36) Ndivyo ingekuwa kwa washiriki wa Israeli wa kiroho walioishi katika karne ya kwanza na kwa watu wa jinsi hiyo mmoja mmoja walio hai leo.
Baada ya kutaja “kuja kwake [kuwapo kwa, NW] Bwana,” Paulo alielekeza kwenye wakati ambapo Waisraeli wa kiroho waaminifu waliokuwa wamekufa wangepokea thawabu yao ya kimbingu. Aliandika hivi: “Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza.” (Mstari 16) Kwa hiyo, mara kuwapo kwa Yesu akiwa Mfalme kungeanza, tungetazamia ufufuo wa kimbingu uanze, ukianza na wale wa Israeli wa kiroho waliokuwa tayari wamekufa wakiwa washika uaminifu-maadili. (1 Wakorintho 15:23) Sasa wao wanatumika kando ya Yesu mbinguni. Lakini namna gani wale Wakristo wachache kwa kulinganisha walio hai bado duniani? Je! wao hungojea kuchukuliwa kimwili kutoka duniani?
‘Kunyakuliwa’—Jinsi Gani?
Baada ya kuwataja Wakristo wapakwa-mafuta waliokuwa wamekufa, Paulo aliongezea hivi: “Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele.” (Mstari 17) ‘Walio hai’ wangekuwa wale walio hai wakati wa kuwapo kwa Kristo. ‘Wangenyakuliwa’ ili kumlaki Bwana Yesu. Kama vile katika kisa cha Wakristo waaminifu wa mapema, kifo wakiwa wanadamu ni cha lazima ili waweze kuungana na Kristo mbinguni.—Warumi 8:17, 35-39.
Alipowaandikia Wakristo katika Korintho, Paulo alitaarifu hivi: “Ndugu zangu, nisemayo ni haya, ya kuwa nyama na damu haziwezi kuurithi ufalme wa Mungu; wala uharibifu kurithi kutokuharibika. Angalieni, nawaambia ninyi siri; hatutalala sote, lakini sote tutabadilika, kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho; maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika.” (1 Wakorintho 15:50-52) Anapokufa kwa uaminifu wakati wa kuwapo kwa Kristo, kila mmoja wa mabaki ya Israeli wa kiroho anapokea thawabu yake ya kimbingu mara hiyo hiyo. Kwa “kufumba na kufumbua,” anafufuliwa akiwa kiumbe cha roho na ‘ananyakuliwa’ ili kumlaki Yesu na kutumika akiwa mtawala mwenzake katika Ufalme wa mbinguni. Lakini namna gani wengine wote wanaomwabudu Yehova? Mwisho wa mfumo mbovu huu ukaribiapo, je, wao pia watanyakuliwa ili kwenda mbinguni?
Wokovu—Lakini Si kwa Kuchukuliwa Kimwili Kutoka Duniani
Kwa kuwa kuwapo kwa Yesu kwa kifalme kulianza katika 1914, sasa sisi tumo ndani sana ya “wakati wa mwisho” wa ulimwengu huu. (Danieli 12:4) Paulo alionya hivi: “Lakini, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie. Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku. Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba wala hakika hawataokolewa.” (1 Wathesalonike 5:1-3) Lakini Wakristo walio macho wataokoka. Jinsi gani?
Kilio cha “amani na salama” ndicho kitangulizi cha kipindi ambacho Yesu aliita “dhiki kubwa.” Kikisimulia “mkutano mkubwa” wa waaminifu walio na tumaini la kuishi milele katika paradiso ya kidunia, kitabu cha Ufunuo kinasema hivi: “Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 7:9, 14; Luka 23:43) La, taraja lao si la kuchukuliwa kimwili kutoka duniani. Bali, wana tumaini la kuokoka hapa hapa duniani. Ili wajitayarishe kwa ajili yalo, ni lazima wabaki wakiwa macho kiroho. Wewe unaweza kufanyaje hivyo na kuokoka mwisho wa mfumo huu?
Unahitaji ‘kuwa na kiasi na kujivika kifuani na imani na upendo, na chapeo yako iwe tumaini la wokovu.’ (1 Wathesalonike 5:6-8) Sasa ndio wakati wa kukazia fikira Neno la Mungu la kiunabii, Biblia. Wakati upitapo hadi mwisho wa mfumo huu, tii shauri hili la Paulo: “Msitweze unabii; jaribuni mambo yote; lishikeni lililo jema.” (1 Wathesalonike 5:20, 21) Hivyo Mashahidi wa Yehova wanakukaribisha kwenye Majumba ya Ufalme yao, ambako unaweza kushiriki nao katika kujifunza unabii mwingi wa Biblia na sehemu nyinginezo za Neno la Mungu lililopuliziwa.
Unapokua katika maarifa sahihi na imani, utatambua utimizo wa kusudi la Yehova Mungu la kuondolea mbali maadui wake kutoka ulimwengu wote mzima na kuirudisha dunia kuwa paradiso. Kwa kuzoeza imani, huenda ukawa miongoni mwa waokokaji wa dhiki kubwa, wenye pendeleo la kukaribisha tena mamilioni watakaofufuliwa kwenye uhai duniani. Na itakuwa shangwe iliyoje kuishi chini ya Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Yesu Kristo na watawala wenzake, watakaokuwa ‘wamenyakuliwa ili kumlaki Bwana’ kwa kufufuliwa kwenye uhai katika makao ya kimbingu!
Basi, ni nini lililo tumaini la Kimaandiko la kweli kwa ainabinadamu tiifu kwa ujumla? Si kuchukuliwa kimwili kutoka duniani. Bali, ni uhai wa milele duniani chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Waokokaji wa dhiki kubwa watawakaribisha wale watakaofufuliwa kwenye uhai duniani chini ya utawala wa Yesu pamoja na wale ‘watakaonyakuliwa’ ili kwenda mbinguni