“Waliokufa Katika Kristo Watafufuliwa Kwanza”
1. Sababu gani kwapaswa kuwapo ufufuo wa wanadamu wafu iwapo wataishi tena mahali po pote, na Mungu aliwekaje msingi wa ufufuo huo unaohitajiwa?
KUNGEKUWAKO tumaini gani kwa wanadamu wafu kama isingekuwa kwa sababu ya ufufuo ulioahidiwa? Kufufuliwa kwa wafu ni uhitaji wa lazima kabisa kwa kuwa nafsi ya mwanadamu inakufa. Hivyo, mwili unapokufa isingeweza kuingia kwenye uzima ulio kamili zaidi wa hali ya juu zaidi katika ulimwengu usioonekana. (Eze. 18:4, 20; Isa. 53:12) Ili wanadamu wafu waishi tena po pote ni lazima kuwepo ufufuo. Hiyo ndiyo sababu Mungu ameweka msingi wa ufufuo wa namna hiyo utukie katika wakati wake unaokuja. Wakati alipomfufua kutoka kwa wafu Mwana wake mwenye kujinyima katika siku ya tatu, alimfungulia njia Mwana huyu mwenye kustahili ili apae arudi alikokuwa hapo kwanza, mbinguni. Mwana huyo alienda pamoja na thamani kamili yenye kukomboa ya dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu. Yesu Kristo hatakufa tena. Yeye alitoa dhabihu moja ya kibinadamu kwa ajili ya dhambi za wanadamu milele. Kwa hiyo, atakapokuja mara ya pili, haimaanishi kuelekeana kwake na kifo.—Ebr. 9:28; Rum. 6:9.
2. 1 Wakorintho 15:22, 23 linaonyeshaje kwamba Mungu hufuata taratibu fulani kuhusiana na ufufuo?
2 Yehova Mungu anafuata utaratibu fulani kuhusiana na kufufuliwa kwa wafu. Jambo. hili linavutwa kwa fikira zetu na mtume Paulo, ambaye yeye mwenyewe aliona utukufu wa Yesu aliyefufuliwa na kuzungumza naye. Yapata miaka 18 baada ya hilo, Paulo aliandikia kundi la Kikristo katika Korintho, Ugiriki, akatokeza ulizo hili: “Basi, ikiwa Kristo anahubiriwa ya kwamba amefufuka katika wafu, mbona baadhi yenu husema kwamba’ hakuna [ufufuo wa] wafu?” (1 Kor. 15:12) Akifuatia ulizo hili, Paulo aliendelea kuonyesha jibu lililoongozwa kwa roho. Anapoendelea, yeye anasema hivi: “Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote wahuishwa. Lakini kila mmoja mahali pake; limbuko ni Kristo; baadaye walio wake Kristo, [wakati wa kuwapo kwake: Kigiriki: Parousia].” (1 Kor. 15:22, 23) Mungu peke yake ndiye aliyehusika na ufufuo wa Yesu.
3. Yesu alipataje kuwa wa “kwanza” kwa habari ya kufufuliwa?
3 Yesu Kristo alifufuliwa katika Nisani 16, 33 W.K., siku ambayo kuhani mkuu wa Kiyahudi alitoa malimbuko ya mavuno ya shayiri. Kwa usahihi hili linapatana na Yesu kuwa “malimbuko” katika ufufuo wa wanadamu wafu. (1 Kor. 15:20) Jambo hili linamweka Yesu Kristo katika “mahali” pa kwanza. Kama vile mavuno ya Wayahudi ya shayiri kulikuwako mavuno ya baadaye ya kuvunwa, vivyo hivyo pia ni lazima kuwepo mavuno ya baadaye katika ufufuo wa wafu. Walakini kwa kuwa Yesu Kristo anachukua pahali pa kwanza, Paulo alimwita “mzaliwa wa kwanza katika wafu, ili kwamba awe mtangulizi katika yote.”—Kol. 1:18.
4. Hata kufufuliwa kwa wale wa kwanza wa wanadamu wafu kulipaswa kungojea mpaka tukio gani rasmi lianze, na lilianza wakati gani?
4 Kwa kifo chake cha dhabihu Yesu Kristo alinunua au alikomboa jamii yote ya kibinadamu inayokufa “katika Adamu.” Hivyo, wote hao ni “wake Kristo.” Walakini, hata kufufuliwa kwa walio wa kwanza wa wanadamu wafu lazima kungengoja mpaka baada ya ‘kuwapo,’ au parousia, kwa Yesu Kristo kuanze. Kuwapo huku kwa rasmi kunaanza na kuja kwake kwa pili. Kulingana na “dalili” aliyotabiri Yesu na vilevile kulingana na vipimo fulani vya wakati vya Biblia, ‘kuwapo’ kwake kusikoonekana, au parousia, kulianza katika vuli ya mwaka 1914 W.K.—Mt. 24:3, NWa
5, 6. 1 Wathesalonike 4:13-17 linaonyeshaje kwamba Mungu atafuata orodha ya utaratibu na “mahali” katika kuvuna wale wanaokufa “katika Adamu”?
5 Yehova Mungu atafuata orodha ya utaratibu na “mahali” kuhusiana na ufufuo wa wale wanaokufa “katika Adamu” na wanaovunwa kama mavuno ya kwanza ya ufufuo. Sana sana ili afariji Wakristo wa karne ya kwanza waliofiwa na wale “waliolala [katika mauti] katika Yesu,” mtume Paulo aliandika hivi:
6 “Kwa kuwa twawaambieni haya kwa neno la [Yehova], kwamba sisi tulio hai [Wakristo waliozaliwa kwa roho], tutakaosalia hata wakati wa [kuwapo] kwake Bwana, hakika hatutawatangulia wao [Wakristo waliozaliwa kwa roho] waliokwisha kulala mauti. Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, [na sauti kubwa, ZSB] na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele.”—1 The. 4:13-17.
7. Paulo alikuwa akizungumza juu ya wafu gani hasa, na Ufunuo 14:12, 13 unaonyeshaje wakati ulio wa pekee kwao kufufuliwa?
7 Hapa mtume Paulo anazungumza, si juu ya wanadamu wafu kwa ujumla, bali juu ya wale “waliolala [katika mauti] katika Yesu.” Katika kitabu cha Biblia mtume Yohana analo jambo la kusema juu ya wakati ambao Wakristo hao waliokufa watafufuliwa kutoka kulala kwao katika mauti. Katika Ufunuo 14:12, 13 Yohana anaandika hivi: “Hapa [kuhusiana na tengenezo la ulimwengu la amani na usalama wa mataifa yote] ndipo penye subira ya watakatifu, hao wazishikao amri za Mungu, na imani ya Yesu. Nikasikia sauti kutoka mbinguni ikisema, Andika, Heri wafu wafao katika Bwana tangu sasa. Naam, [y]asema [roho], wapate kupumzika baada ya taabu zao; kwa kuwa matendo yao yafuatana nao.” Kwa hiyo, basi, “tangu sasa” ni kuanzia wakati gani?
8. Sababu gani “tangu sasa” ingemaanisha wakati wa kuwapo kwa Bwana katika roho, na je! kufa kwao kunakomesha matendo yao?
8 Kulingana na maelezo anayoandika mtume Paulo katika 1 Wathesalonike 4:16, 17, lazima iwe wakati wa ‘kuwapo,’ au parousia, kwa Yesu Kristo, si kabla hakujaanza, walakini baadaye. Hata wakati wa kuwapo kwake kusikoonekana katika roho kutakuwako duniani Wakristo waliozaliwa kwa roho ‘watakaokufa katika Bwana’. Sana sana hawa wapaswa ‘kufurahia’ kufa wakati wa ‘kuwapo’ kwake. Kufa kwao katika mwili hakukomeshi “matendo” yao, kwa muda wo wote. Sababu gani hivyo? Kwa sababu ‘matendo waliyofanya yako nao,’ au, kwa halisi, kulingana na andiko la Kigiriki, “yafuatana nao.”
9. Sababu gani, basi, “watakatifu” wanaokufa wakati huo ni ‘wenye furaha, ‘ kulingana na Ufunuo 14:13?
9 Hii inahitaji badiliko la utendaji, kutoka kwa matendo katika mwili duniani, kwenye matendo katika roho katika utawala wa mbinguni. Kuhusu wale “wafao katika Bwana,” mtume Paulo asema hivi: “Kadhalika na [ufufuo wa] wafu. Hupandwa katika uharibifu; hufufuliwa katika kutokuharibika; hupandwa katika aibu; hufufuliwa katika fahari; hupandwa katika udhaifu; hufufuliwa katika nguvu; hupandwa mwili wa asili; hufufuliwa mwili wa roho. Ikiwa uko mwili wa asili, na wa roho pia uko.” (1 Kor. 15:42-44) Kwa hiyo hawa wenye ‘furaha’ waliofufuliwa, “taabu zao” za dunia hufuatwa na matendo katika miili ya kiroho katika makao ya kiroho. Hawalali katika mauti wakingoja kuwapo kwa Kristo.
ANACHOSHUKA NACHO BWANA KUTOKA MBINGUNI
10. Wakati wa kufufua wanafunzi wake waliozaliwa kwa roho Bwana Yesu Kristo atashuka kutoka mbinguni pamoja na nini?
10 Mtume Paulo anatuambia kinachofuatana na kushuka kwa kiroho kwa Bwana kutoka mbinguni, akisema: “Sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa [kuwapo au parousia] kwake Bwana, hakika hatutawatangulia [katika kupata ufufuo wa kiroho] wao waliokwisha kulala mauti. Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza.”—1 The. 4:15,16.
11. Ni nani wanaosikia ‘mwaliko wenye kuamuru’ wa Bwana Yesu Kristo na kutii anaposhuka kutoka mbinguni?
11 Ni nani anayesikia ‘mwaliko wa kuamuru’ anaokuja nao Bwana Yesu Kristo kutoka cheo chake cha kimbinguni kwenye mkono wa Mungu wa kuume? Kwa wazi Wakristo waliozaliwa kwa roho ambao, mpaka wakati huo, wamekufa “katika Bwana.” Twajua kwamba hakuna wanadamu wanaoishi duniani waliopata kusikia sauti yake moja kwa moja tangu ashuke kiroho, yaani, tangu ‘kuwapo’ kwake kusikoonekana, au parousia, kuanze mwanzoni mwa vuli mwaka 1914. Walakini “wafu katika Kristo” walimsikia na kumtii.
12. (a) “Siku ya mwisho” aliyotaja Yesu katika Yohana 6:53. 54 inaanza lini, na wanafunzi hao wanaingiaje kwenye “uzima wa milele”? (b) Hii inatofautiana na siku gani nyingine inayoitwa “siku ya mwisho’?
12 Wale waliofufuliwa na Yesu Kristo namna hiyo ni sehemu ya wanafunzi ambao Yesu alisema hivi kuwahusu: “Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele [kuanzia na wakati wa kufufuliwa kwake kutoka kwa wafu]: nami nitamfufua siku ya mwisho.” (Yohana 6:53, 54) Wakati wa hiyo “siku ya mwisho” katika mwaliko wake wenye kuamuru una uwezo wa kuwainua kutoka katika usingizi wa kifo wanafunzi wake walioshiriki katika pendeleo hili la pekee kuhusiana na mwili na damu yake. Kwa wanafunzi hawa walio na pendeleo, “siku ya mwisho” inaanza wanapoingia kwenye “uzima wa milele” mbinguni kwa kufufuliwa katika ‘mwili wa roho’ kama ule wa Kristo. Kwa kuwa hii “siku ya mwisho” inatumika kwa kufufuliwa kwa Wakristo waaminifu waliozailwa kwa roho walio na tumaini la kimbinguni, inatofautiana na “siku ya mwisho” ambayo Martha wa Bethania alikuwa akifikiria, kwa kuwa wakati huo hakuwa na wazo lo lote la ufufuo wa kiroho kwenye mbingu.
13. (a) Ni sauti ya nani ambayo “wafu katika Kristo” wanasikia, na “malaika mkuu” ni nani? (b) Tuna ushuhuda gani wa Kimaandiko kwa jambo hili?
13 Vilevile Bwana Yesu Kristo aliyetukuzwa anashuka “na sauti ya malaika mkuu.” Hii ni sauti yake mwenyewe. Yeye ndiye “malaika mkuu.” Katika mfano wake wa kondoo na mbuzi Yesu alijitaja katika cheo hiki cha malaika mkuu kwa kusema hivi: “Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake; na mataifa yote watakusanyika mbele zake.” (Mt. 25:31, 32) Katika hali yake ya mbinguni kabla ya ‘kuwa mwanadamu jina lake lilikuwa Mikaeli. Hakuna shaka kwamba ndiye anayemaanishwa katika unabii wa kabla ya Ukristo wa Danieli 12:1, 2: “Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako [wa Danieli]; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo; na wakati huo watu wako wataokolewa; kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu kile. Tena, wengi wa hao walalao katika mavumbi ya nchi wataamka, wengine wapate uzima wa milele, wengine aibu na kudharauliwa milele.”
14. Ufunuo 12:7 unalitoa jina la malaika huyu mkuu kuwa gani, na Yuda 9 linatajaje shindano lake huyu la wakati uliopita?
14 Vilevile, Ufunuo 12:7 huonyesha malaika kuwa wadogo kuliko Mikaeli, ukisema: “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake [siyo Wakristo waliozaliwa kwa roho waliofufuliwa] wakapigana.” Zaidi ya hayo, Yuda 9 humsema kuwa malaika mkuu, likisema hivi: “Mikaeli, malaika mkuu, aliposhindana na Ibilisi, na kuhojiana naye kwa ajili ya mwili wa Musa.” Ibilisi hakupata mwili huo.
15. Shetani Ibilisi alipata matokeo gani katika vita na malaika mkuu Mikaeli, na je! anaweza kuzuia kufufuliwa kwa wanafunzi wa Kristo na kupaa kwao mbinguni ili wawe pamoja na Yesu Kristo?
15 Wakati wote katika shindano hilo la muda mrefu Shetani Ibilisi ameshindwa. Katika vita mbinguni alishindwa naye pamoja na malaika zake mashetani walivurumishwa chini kwenye ujirani wa dunia, huku malaika mkuu Mikaeli, yaani, Bwana Yesu Kristo, na malaika zake walibaki mbinguni wakiwa washindi. Kwa kuwa Yesu Kristo mshindi hutumia “sauti ya malaika mkuu” anapowaamuru wale waliokufa katika umoja na Kristo watoke, ‘mwaliko wake wenye kuamuru’ una mamlaka zaidi na matokeo yenye nguvu zaidi. Pamoja na hayo, Shetani Ibilisi aliyeshindwa hatakuwa na uwezo wa kutosha kuzuia ufufuo wa kiroho wa wale waliokufa katika umoja na Kristo na hataweza kuzuia wasiingie katika makao ya kiroho wala kupaa kwao mbinguni ili wawe na Yesu Kristo mshindi.
16. “Parapanda ya Mungu” inalia kwa kusudi gani wakati wa kushuka kwa Bwana kutoka mbinguni, na ni nani watakuwa wa kwanza kuiitikia?
16 Kitu kingine kinachofuatana na kushuka kwa Kristo kutoka mbinguni ni sauti ya “parapanda ya Mungu.” (1 The. 4:16) Katika habari hii parapanda hii siyo ishara ya vita ya kukusanya majeshi kusudi yapigane na kumwua adui. Mahali pake, kupigwa kwa “parapanda ya Mungu” ni kwa amani ili kukusanya watu wa Yehova, kama ilivyokuwa wakati parapanda mbili za fedha zilipopigwa katika siku za Musa ili kukusanya makabila 12 ya Israeli. (Hes. 10:1-10) Mahali pengine, katika 1 Wakorintho 15:52, mtume Paulo anahusianisha “parapanda” ya namna hiyo ya kukusanya na kufufuliwa kwa wafu Wakristo, anaposema hivi: “Wakati wa parapanda ya mwisho; maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika.” Ni nani wa kwanza kuiitikia hiyo “parapanda ya mwisho,” wakati hiyo, ikiwa “parapanda ya Mungu,” itakapolia kwa ajili ya kukusanya wafu warudi kwenye uzima? Katika kujibu, 1 Wathesalonike 4:16 lasema hivi: “Nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza.”
17. Sababu gani kufufuliwa kwa “waliokufa katika Kristo” hakuonekani kwa macho ya kibinadamu?
17 Hata hivyo, kufufuliwa kwa wale “waliokufa katika Kristo” hakuonekani kwa wanadamu duniani. Sababu gani sivyo? Kwa sababu wamebarikiwa na ufufuo wa kiroho, kila mmoja ‘akifufuliwa mwili wa roho.’ (1 Kor. 15:44) Kwa sababu macho ya kibinadamu hayana nguvu za kutosha kuweza kuona miili ya kiroho, kufufuliwa kwa “waliokufa katika Kristo” hakuonekani na wanadamu. Hiyo ndiyo sababu, tangu kuanza kwa ‘kuwapo,’ au parousia, kwa Kristo kuanzia mwaka 1914 kuendelea, wanadamu hawajapata kumwona wala kuona kufufuliwa kwa wanafunzi wake.
18, 19. (a) Kwa yale aliyosema Paulo katika 1 Wathesalonike 4:17, je! alimaanisha kwamba Wakristo hao wasingekufa kabla ya ‘kunyakuliwa’? (b) Kwa hiyo, ni katika maana gani, wao ‘wananyakuliwa,’ na wanapaa wakiwa na miili gani ili wakutane na Bwana katika furaha?
18 Mtume Paulo anajitaja kama akiendelea kuwapo duniani mpaka wakati wa tukio hilo lenye furaha kwa Wakristo waliozaliwa kwa roho, anaposema hivi: “Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele.”—1 The. 4:17.
19 Hapa mtume Paulo hakumaanisha kwamba Wakristo waliozaliwa kwa roho kama yeye hawatakufa bali ‘wangenyakuliwa,’ mwili wa kibinadamu na kila kitu, kwenye mbingu katikati ya mawingu halisi. Paulo alikufa. Wakristo waliozaliwa kwa roho walioko leo wakati wa ‘kuwapo,’ au parousia, kwa Kristo nao lazima wafe pia. Kama vile mbegu zilizopandwa katika ardhi, lazima kila mmoja wao ‘apandwe mwili wa asili’ kwa kufa kifo cha kibinadamu. (1 Kor. 15:44) Hivyo, basi, ‘wananyakuliwaje katika mawingu’ pamoja na wale “waliokufa katika Kristo” ambao walifufuliwa kwanza? Katika njia hii: Wanapopandwa kama miili ya asili, hawaingii katika usingizi wa mauti. Mara iyo hiyo wanapata ufufuo wa kiroho, wakiacha miili yao ya kibinadamu nyuma duniani na kila mmoja akifufuliwa “mwili wa roho.” Wanapaa kama miili ya kiroho ili kukutana na Bwana wao wa kimbinguni. Kwa sababu hizi sana sana wao waweza kuhesabiwa ‘wenye furaha,’ kulingana na Ufunuo 14:13.
20. Ni katika “mawingu” ya namna gani ambayo katika hayo Wakristo waliobaki wanaoishi ‘wananyakuliwa,’ nako ‘kunyakuliwa’ huko kunaonyesha nini juu ya kupaa kwao?
20 Hata hivyo, kunyakuliwa kwao “katika mawingu” kunamaanisha nini? Bila shaka, mawingu huelea katika mbingu na hufananisha hali ya kuinuliwa. Vilevile yanatuficha sisi tulio duniani yale yaliyomo ndani yake au juu yake. Miili ya kiroho haihitaji mawingu yetu ya halisi ili yaifanye isionekane nasi. Kwa hiyo yanayomaanishwa katika 1 Wathesalonike 4:17 ni mawingu ya mfano, ambayo, kama ilivyo, huficha maono ya kidunia yasione kunyakuliwa kwa Wakristo waliofufuliwa kusudi wakutane na Bwana wao aliyenyanyuliwa juu sana. Ebu na tukumbuke namna, wakati wa siku ya 40 toka afufuliwe, alivyopaa kurudi mbinguni Yesu Kristo na, wakati wa kupaa kwake, “wingu likampokea kutoka machoni pao [wanafunzi waliokuwa wakitazama].”—Matendo 1:9.
21. Je! kushuka kwa Bwana kutoka mbinguni kunakoma kwa yeye binafsi, kuja katika uhusiano wa moja kwa moja na dunia yetu, nayo “siku ya mwisho” ambayo katika hiyo anafufua wanafunzi wake waliozaliwa kwa roho inamalizika lini?
21 Yote haya yanathibitisha nini? Hili: Bwana Yesu Kristo mwenye kushuka hatakuja kwa uhusiano wa moja kwa moja na dunia yetu. Mawingu, ambayo katika hayo Wakristo waliofufuliwa wanafananishwa kama wakikutana na Bwana wao wa kimbinguni, huelea juu juu ya uso wa dunia. Pamoja na hayo, Wakristo waliofufuliwa wanakutana na Bwana wao “hewani,” si hapa ardhini, wala si katika Yerusalemu, Mlima wa Mizeituni wala mahali po pote duniani yetu. Zaidi ya hapo, “siku ya mwisho” ambayo katika hiyo kunyakuliwa huku kunatokea si siku yenye saa 24 ya kidunia. Ni kipindi cha wakati ambacho kinafikia utimilifu wake kwa mara ya kwanza wakati Mkristo wa mwisho wa wale waliozaliwa kwa roho wanaoshiriki katika “ufufuo wa kwanza” anapofufuliwa kwenye uzima wa kimbinguni. (Ufu. 20:4, 6; Yohana 6:54) Kutimizwa kwa unabii wa Biblia kunaonyesha kwamba tayari tunaishi katika hiyo “siku ya mwisho.”
[Maelezo ya Chini]
a Tazama Our Incoming World Government—God’s Kingdom, sura 9.