Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Mkristo afanyeje asipoweza kupata mwenzi wa ndoa anayefaa?
Ingawa sisi ni Wakristo wenye kujitoa, tunaweza kuvunjika moyo sana tunapotumainia sana kupata kitu fulani maishani na hatukipati. Hisi zetu zinaelezwa vema kwenye Mithali 13:12 ambalo husema hivi: “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua.” Hivyo ndivyo Wakristo fulani wamehisi wakati ambapo wametamani kuoa au kuolewa lakini hawakuweza kupata mwenzi wa ndoa anayefaa. Na hasa hilo linaweza kuwa kweli kwa wale ambao mtume Paulo anaeleza kuwa hujiruhusu ‘wawake tamaa.’—1 Wakorintho 7:9.
Yehova aliweka katika wanadamu tamaa ya kupata kikamilisho cha kweli katika mtu wa jinsia tofauti. Kwa hiyo, si jambo la kushangaza kwamba Wakristo wengi waseja huwa na hisi za moyoni kama hizo. (Mwanzo 2:18) Hisi hizo za kawaida zinaweza kuchochewa katika tamaduni zinazokazia sana kufunga ndoa (au kufunga ndoa kufikia umri fulani) au wakati Wakristo waseja wanapozungukwa na wenzi waliooana kwa furaha kundini. Hata hivyo, haifai kuruhusu hangaiko liendelee kwa kipindi kirefu cha wakati. Kwa hiyo Wakristo wenye mioyo myeupe wanaweza kushughulikaje na hali hiyo bila kuhangaika mno?
Hilo si rahisi, na wengine hawapaswi walione hangaiko hilo kana kwamba ni kutilia mambo chumvi tu au kuwa jambo dogo tu lisilofaa. Lakini kwa kadiri kubwa, uwezo wa kukabiliana nalo au kulisuluhisha linategemea zile hatua ambazo mseja aweza kuchukua.
Tunapata ufunguo katika kanuni hii ya Biblia yenye kutumika: “Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35, NW) Hayo yalisemwa na mwanadamu mseja Yesu Kristo, na alistahili kusema kuhusu jambo hilo. Kuwatumikia wengine, tukiwa na nia isiyo na ubinafsi, ndiyo njia nzuri ya kusaidia yeyote kati yetu kushinda hisi zinazotokana na taraja lililokawizwa. Hilo linamaanisha nini kwa habari ya Mkristo mseja?
Jitoe kufanya matendo ya fadhili kwa ajili ya familia yako mwenyewe na kwa ajili ya wengine ndani ya kundi, na uongeze utendaji wako katika huduma. Shauri hilo si njia tu ya kusema, ‘Endelea kujishughulisha, na utasahau juu ya kutaka kufunga ndoa.’ La. Kwa kujishughulisha katika ufuatiaji huo wa Kikristo wenye matokeo, huenda ukaona kwamba‘unasimama ukiwa umetulia moyoni mwako, ukiwa na mamlaka juu ya mapenzi yako mwenyewe’ na waweza kutumia hali yako ya sasa katika njia yenye manufaa.—1 Wakorintho 7:37, NW.
Wengine ambao wametamani sana kufunga ndoa wameruhusu tamaa hiyo kuwa jambo kuu la kufikiriwa kila wakati. Hata wamefikia hatua yenye kupita kiasi ya kutoa matangazo magazetini ili kupata wenzi wa ndoa. Lakini, jinsi ilivyo bora zaidi kukaza fikira juu ya kuthamini manufaa ziwezazo kupatikana kutoka kwa wakati wa useja.—Tafadhali ona makala “Asiyefunga Ndoa Lakini Kamili kwa Utumishi wa Mungu” na “Useja—Njia ya Maisha Yenye Kuthawabisha” katika Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1987, na “Je! Ndoa Ndiyo Ufunguo wa Pekee wa Kupata Furaha?” katika Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1992.
Sali kwa Yehova akupe msaada wa kudumu katika hali ya useja. (Wafilipi 4:6, 7, 13) Wakristo wengi wasiofunga ndoa wameona kwamba kwa kutumia wakati wao ili kujifunza na kutafakari Neno la Mungu na kuhudhuria na kushiriki katika mikutano ya Kikristo, wamepata ‘raha [burudisho, NW] [zaidi] nafsini mwao,’ kama vile Yesu alivyowaahidi wale waliomfuata. (Mathayo 11:28-30) Hilo limewasaidia wasitawishe hali ya kiroho, ili wawe waume au wake bora zaidi ikiwa baadaye wangepata mwenzi wa ndoa anayefaa.
Usisahau kamwe kwamba Yehova anaielewa hali ya waseja wote wanaomtumikia. Anajua ya kwamba huenda usihisi kwamba hali yako ya sasa ndiyo hali ambayo ungependelea. Baba yetu wa kimbingu anajua pia kile kilicho bora zaidi kwako, kiroho na kihisia-moyo pia. Na wewe pia waweza kujua hili kwa hakika: Kwa kumngojea Yehova kwa subira na kwa kutumia kanuni za Neno lake katika maisha ya kila siku, unaweza kuwa na uhakika kwamba atatosheleza mahitaji yako ya maana zaidi katika njia iliyo ya manufaa yako ya milele.—Linganisha Zaburi 145:16.