Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 11/15 kur. 10-15
  • Useja—Faida na Nafasi Zake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Useja—Faida na Nafasi Zake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nafasi Kubwa Zaidi
  • Sababu Gani Kuna Tamaa Hiyo Yenye Nguvu?
  • Faidika kwa Kutiana Moyo na Mwenzako
  • Faidika na Nguvu Kutoka Juu
  • Kujiweza
  • Jitihada Hiyo Inastahili!
  • Tumia Vizuri Kabisa Useja Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Kuna Faida za Kukaa Bila Kuoa au Kuolewa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Useja—Mlango Uelekeao Kwenye Utendaji Pasipo Kukengeushwa Fikira
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Mashauri ya Hekima Kuhusu Useja na Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 11/15 kur. 10-15

Useja—Faida na Nafasi Zake

1. Ni nini maoni ya wengi juu ya useja, na kwa sababu gani wengine wana maoni hayo?

MWALIMU mmoja wa shule mwenye umri wa miaka 21 aliulizwa na rafikiye msichana aliyekuwa mkubwa zaidi: “Je! wewe hutaki kuolewa?” Mwalimu huyo mwanamke kijana, ambaye alithamini faida za useja wake, alijibu hivi: “Nadhani sijafikiria jambo hilo kwa uzito.” Kwa kushangazwa na jibu hilo, rafiki huyo alisema hivi: “Haya, utakapokuwa mkubwa zaidi utajuta hukufanya hivyo. Kila mtu apasa kufunga ndoa.” Unapochunguza juu ya umati wa watumishi wa Mungu ambao wameoa (au kuolewa) unaweza kufahamu ni sababu gani wengi, kama rafiki huyu mwenye kusudi jema, wanaona kwamba useja ni hali isiyotamanika, inayofanya maisha ya mtu yasiwe kamili.

2. Kwa sababu gani Wakristo waseja na waliofunga ndoa, wote wawili, wanapaswa kupendezwa na hii habari yetu?

2 Mtu anaweza kuwa mseja kwa sababu ya kuwa mchanga mno au kama sivyo kwa kutoweza kuchukua madaraka ya ndoa. Wengine wamepoteza mwenzi kupitia talaka au kifo. Katika Marekani nyumba moja kati ya kila tatu kwa sasa inaongozwa na mseja. Kumekuwa ongezeko la asilimia 64 la watu wanaoishi peke yao kwa muda wa miaka 10 tu. Kwa hiyo inaelekea sana kwamba hata ikiwa wewe si mseja, mtu fulani aliye karibu nawe ni mseja. Wewe ukiwa Mkristo aliyeoa (au kuolewa) unawezaje kuhurumia ipasavyo waseja ambao wanafanyiza sehemu kubwa ya nyumba ya Mungu? Bila shaka ikiwa wewe ni mseja unajua magumu ya kuwa na furaha na katika ujamii unaoona ndoa kuwa jambo la kawaida linalopasa kufanywa. Unapaswa kuuonaje useja wako?​—1 Petro 3:8.

3. (a) Siku za Yesu, useja ulikuwa unaonwaje? (b) Yesu alikuwa na maoni gani juu ya useja “kwa ajili ya ufalme”?

3 Yesu Kristo alifunua kwamba useja “kwa ajili ya ufalme wa mbinguni” ulikuwa ni kipawa kutoka kwa Mungu. Hilo lilikuwa wazo jipya kabisa, kwa maana kati ya Wayahudi wa siku zake ndoa ilionwa kuwa “takwa kwa watu wote ulimwenguni” na useja kuwa suto. “Yeye asiye na mke si mwanamume kamili,” ulikuwa mmojawapo wa semi za marabi Wayahudi. Hata hivyo, Yesu alitia moyo wanafunzi wake ‘wakipatie nafasi’ kipawa cha useja wala wasijione kuwa na lazima ya kufunga ndoa.​—Mathayo 19:10-12, NW.

4. Mwendo wa Wakristo wengi umekuwa nini, na wao wana maoni gani juu ya hali zao?

4 Kwa hiyo ndoa na useja yote mawili ni zawadi kutoka kwa Mungu. Wakati wa siku za mapema za Ukristo, pia katika siku zetu, wengi wamefuatia maisha ya useja, “kwa ajili ya ufalme.”a Badala ya kusikitikia hali zao, wengi wa hao wana maoni sawa na yale ya mwanamke Mkristo mwenye umri wa miaka 41 ambaye hajapata kuolewa aliyesema juzi-juzi hivi: “Singeweza kukubali jambo lo lote lichukue mahali pa miaka ambayo nimetumia nikiwa mseja.” Kwa sababu gani wengi wana maoni hayo?

Nafasi Kubwa Zaidi

5. Wakristo ambao hawajafunga ndoa wanawezaje kutumia kwa faida nafasi zinazotokezwa na hali zao?

5 Mifano ya Wakristo waliofunga ndoa kama mitume wa Yesu, pamoja na Akila na Prisila, inaonyesha kwamba wenzi wanaweza kutoa sehemu yenye thamani katika utumishi wa Mungu. (Matendo 18:26-28; 1 Wakorintho 9:5) Hata hivyo mtume Paulo alionyesha kwamba mseja ana nafasi kwa ajili ya sehemu kubwa zaidi ya utumishi. Yeye aliandika hivi: “Yeye asiyeoa [au kuolewa] hujishughulisha na mambo ya Bwana, ampendezeje Bwana; bali yeye aliyeoa [au aliyeolewa] hujishughulisha na mambo ya dunia hii, jinsi atakavyompendeza mkewe [au mumewe, naye amegawanyika].” (1 Wakorintho 7:32-34) Mseja ‘hajagawanyika’ (NW) kwa sababu ya madaraka ya ndoa, ambayo huleta “dhiki katika mwili,” na kwa hiyo aweza ‘kujishughulisha’ au kuhangaikia mambo ya kiroho. Angalia katika kisanduku hiki kadiri ambayo matendo matakatifu yalijaza maisha ya wale waliotajwa. Kuweza kushiriki katika utumishi wa Mungu, unaotia kwanza kazi ya kuhubiri, “pasipo kuvutwa na mambo mengine,” ni hazina kubwa. Mara nyingi waseja wana wakati mwingi zaidi wa kujifunza na kutafakari. Jambo hilo linaweza kufanya “roho,” au kichocheo cha ndani kiwe bora zaidi, na kumleta mtu huyo karibu zaidi na Yehova wakati yeye anakaza fikira kuwa ‘mtakatifu katika mwili na roho.’ Kwa kutokuwa na mwenzi wa ndoa, wengi wanajifunza kutegemea sana Mungu, wakimtazamia awape uongozi na shauri. Wakristo ambao hawajafunga ndoa mara nyingi wanaweza kukubali mapendeleo ya utumishi ambayo wenzi waliofunga ndoa hawawezi. Haishangazi, basi, kwamba Yesu aliliita pendeleo hilo la kuendelea kuwa Mkristo mseja kuwa “kipawa” (NW)!—Mathayo 28:19, 20; 1 Wakorintho 7:28, 35.

6, 7. (a) Je! kuwa na kipawa cha useja kunamaanisha kwamba mtu havutiwi tena na wanawake (au wanaume) na hatafunga ndoa kamwe? (b) Maana yake nini ‘mtu kufanya uamuzi katika moyo wake’? (c) Huenda ulizo gani likawa katika akili za waseja fulani?

6 Wale ‘wanaopatia nafasi kipawa hicho’ (NW) kwa lazima wao si watu wenye kipawa cha pekee katika umbo lao la maono ya moyoni kwamba hawawezi kuvutwa na wanawake (au wanaume). Wao hawajatoa nadhiri ya kutokufunga ndoa (ubikira), kama kwamba hawajapata hata siku moja kukusudia kuoa (au kuolewa), bali ‘wamekusudia’ (‘kufanya uamuzi,’ NW), au kukata hukumu, katika mioyo yao wafanikishe hali yao ya useja.b (1 Wakorintho 7:37) Watu hao wamepima mioyoni mwao faida za useja. Kwa msingi wa ‘ushuhuda’ huo mioyo yao inaanza ‘kukata hukumu’ kwamba useja ni “kipawa” nao ‘wanaupatia nafasi.’​—1 Wakorintho 7:38.

7 Lakini vipi ukiwa na tamaa yenye nguvu ya kutaka kufunga ndoa? Je! Paulo hakusema ilikuwa afadhali kufunga ndoa kuliko kuwashwa na nyege?​—1 Wakorintho 7:9.

Sababu Gani Kuna Tamaa Hiyo Yenye Nguvu?

8. (a) Kwa sababu gani huenda vijana wengine waseja wakawa na tamaa yenye nguvu ya kutaka kufunga ndoa? (b) Kuna faida gani kuahirisha ndoa mpaka mtu ‘apite ukamilifu wa ujana’?

8 Ni jambo la asili kutaka kufunga ndoa. Mungu alituumba tukiwa na tamaa hiyo. (Mwanzo 2:18) Lakini je, tamaa hiyo yenye nguvu inakuwapo kwa sababu mtu yuko katika “ukamilifu wa ujana,” wakati ambapo kuna kichocheo cha kwanza cha kutaka kufanya ngono? Paulo alipendekeza kwamba mtu akawize ndoa mpaka kipindi hicho ‘kipite.’ Huenda kungojea huko kukaonekana kusikowezekana kwa kijana. Wengine katika karne ya kwanza pia walijisikia ilikuwa lazima wafunge ndoa. Hata hivyo, ingawa wao walikuwa ‘wakitafuta wake’ wengine waliokuwa wamekwisha kufunga ndoa walikuwa ‘wanatafuta kuwekwa huru’ kutoka hali yao! Ingawa ndoa inaweza kuwa ulinzi wa kuepuka kufanya uasherati, haitatui matatizo yote. Mkristo mmoja mseja mwenye umri wa miaka 35 alisema: “Nikiwa mzee ninapoona maisha ya watu yakiharibiwa na ndoa mbaya, inanifanya kuwa na akili timamu. Mimi sipingi ndoa lakini naonelea hakuna haja ya kuikimbilia.” Uchunguzi unaonyesha kwamba wanawake Wamarekani walioolewa kabla ya miaka 18 wana maelekeo mara tatu ya kutalikana zaidi ya wale waliongojea mpaka walipokuwa wenye miaka 24! Hesabu za talaka za waume tineja katika Marekani ni mara tatu zaidi ya zile za watu wengine kwa ujumla. Miaka ya kijana ya useja yaweza kutumiwa kwa njia ya hekima katika kusitawisha uhusiano mwema na Yehova pamoja na sifa na ujuzi unaohitajiwa ili kuwa mwenzi mwema.​—1 Wakorintho 7:27, 36, NW.

9. (a) Wengine wamefanya nini kwa sababu ya kutamani mwenzi, na mara nyingi matokeo yakawa nini? (b) Ni ulizo gani linalokabili waseja hapa?

9 Wakristo wengi wamekuwa wakubwa zaidi pasipo kufunga ndoa. Baada ya muda, baadhi yao, kwa sababu ya tamaa yenye nguvu ya kutaka mwenzi, wamekimbilia ndoa pamoja na mtu asiye mwamini, wakiwaza kwamba mwenzi ye yote ni afadhali kuliko kukosa mmoja. Hata hivyo huenda ukawa unajua juu ya wengine waliofanya hivyo ndipo tu wakajikuta wakiwa wapweke kwa kuwa na mwenzi ambaye hawangeweza kupashana habari naye. Hata hivyo, mseja anawezaje kuendelea ‘kutulia moyoni’?​—1 Wakorintho 7:28, 37, 39.

Faidika kwa Kutiana Moyo na Mwenzako

10. Kulingana na Warumi 1:11, 12, mtume Paulo alitamani nini, naye alipataje faida?

10 Wakristo waseja wenye kufanikiwa ni wenye kupenda watu. Mtume Paulo, yeye mwenyewe akiwa mseja, aliandika hivi: “Ninatamani sana kuwaona, nipate kuwapa karama ya rohoni, ili mfanywe imara; yaani, [tutiane moyo] mimi na ninyi.” (Warumi 1:11, 12) Paulo alipendezwa sana na watu naye alitaka kuwapa waamini wenzake ‘karama ya kiroho.’ Kwa kufanya hivyo naye pia alitiwa moyo. Ni hali moja na hiyo leo.

11. Ni jambo gani linaloonyesha jinsi mtu anavyoweza kutiwa moyo kupitia utoaji wa ‘karama ya kiroho’?

11 Mwanamke mmoja mseja Mkristo alialika dada wengi vijana katika kundi nyumbani mwake kwa chai (mkusanyo) mdogo, akiwa na tamaa ya kushiriki ‘karama ya kiroho’ kupitia ushirika wenye kufaa. Siku iliyofuata tineja mmoja (msichana) alimkumbatia dada huyo akasema: “Nakuambia chai hiyo imekuwa na maana sana kwangu nami nilihitaji sana kitia-moyo hicho. Nilikuwa nawaza kwamba singeweza kuvumilia zaidi matatizo yangu nyumbani na mama yangu wa kambo. Sasa nahisi naweza kuyakabili.” Dada mseja huyo alipokuwa akisimulia jambo hilo, alisema hivi, macho yakiwa na machozi: “Sikusahau jambo hilo kamwe. Baadaye mimi nilisaidiwa sana na pongezi la msichana huyo, kwa sababu nilifurahishwa sana na aliyosema.” Kusitawisha kupendezwa na wengine wa ‘jamaa yetu ya kiroho,’ kwafaa, kwaweza kusaidia kushinda upweke. Lakini, jitihada inahitajiwa ili kusitawisha urafiki wa maana.c—Marko 10:29, 30.

12. Kazi ya kufanya wanafunzi inatokeza nafasi gani?

12 Hata hivyo, licha ya nafasi zilizo ndani ya kundi la Kikristo za kutoa ‘karama za kiroho,’ kuna nafasi zinazotokezwa na kazi ya kufanya wanafunzi. Yule anayetoa mara nyingi anaburudishwa kuona maendeleo ya mwanafunzi na kuona faraja ya kudumu ambayo kweli ya Biblia inaweza kuleta. Kwa hiyo unapoongoza katika kuonyesha upendo wale walio ndani na nje ya nyumba ya Mungu, maisha yako mwenyewe yatakuwa mazuri zaidi na utaliona likiwa jambo rahisi zaidi kuendelea ‘kutulia moyoni.’​—Warumi 12:2; Mhubiri 11:1; Luka 6:38.

Faidika na Nguvu Kutoka Juu

13. 2 Timotheo 4:17 inawezaje sana sana kuwatia moyo Wakristo waseja?

13 Alipokuwa amefungwa katika Roma, mtume Paulo alilazimika kukabili hali ngumu akiwa peke yake. Yeye aliandika hivi: “Lakini Bwana alisimama pamoja nami akanitia nguvu.” (2 Timotheo 4:17) Kupitia nguvu hiyo Paulo alikuwa mwaminifu akaokolewa ama kwa njia halisi ama kwa njia ya mfano kutoka “kinywa cha simba.” “Simba” wa mfano wanapoingia maishani mwako, je, unamwendea Baba yako mwenye kuhurumia akupe msaada? Je! unamfunulia moyo wako, ukijua kwamba hata ikiwa hakuna mtu mwingine anayefahamu, yeye anafahamu mahitaji yako na atasimama karibu nawe?​—1 Petro 5:6-9.

14. (a) Dada mmoja mseja alikuwa anakabiliwa na mkazo gani, naye alibarikiwaje? (b) 1 Wakorintho 10:13 inapasa kutupa uhakika gani?

14 Dada mmoja mseja mwenye umri wa miaka 53 alishuka moyo sana alipopoteza kazi yake ya kuajiriwa. “Nilimwomba Yehova anisaidie nipate kazi fulani ya kuajiriwa ili nijiruzuku tu. Kabla juma halijakwisha nilikuwa nimeajiriwa kazi nyingine! Tangu siku hiyo kuendelea niliazimu kutenganisha siku moja moja nitegemee uangalizi wa Yehova. Yeye hajaniacha kamwe.” Katika mwaka 1982, baada ya kupainia miaka 26, sala yake ya kutaka mwenzi anayestahili kiroho ilijibiwa alipokuwa mke wa mwangalizi asafiriye aliyekuwa amefiwa. Kweli kweli, sikuzote Yehova hajibu sala zetu kwa njia hizo hizo kabisa, hata hivyo yeye atatutia nguvu tukabili matatizo yo yote ambayo huenda yakaendelea kuwapo.​—1 Wakorintho 10:13.

Kujiweza

15. (a) Ili kuzuia nyege mtu anapaswa kutambua nini? (b) Jambo hilo linaonyeshwaje katika Mithali sura ya 7?

15 “Nahisi siwezi tena kuendelea kuvumilia nikiwa peke yangu.” akaandika mwanamke mmoja Mkristo. “Najiona mwenyewe nikiwa na tamaa yenye nguvu ya kutaka kufanya ngono na kwa miaka mingi nimeshindwa kupata mume Mkristo anayefaa. Nimeambiwa-ambiwa tu niende nyumbani nikajiweze. Lakini namna gani?” Kukabili maono hayo ya moyoni si rahisi. Ili kuzuia nyege lazima mseja atambue ni wakati gani anapopaswa kuanza kuzishinda kwa kujiadibu. Kwa mfano, katika Mithali 7:6-23, mwanamume mmoja kijana anapoteza kujiweza kwake na kuwa na msisimuko mwingi wa nyege na kumfuata malaya. Hata hivyo, yeye hakufikia hatua hiyo kwa ghafula. Hatua za kwanza zilikuwa ni (1) kutembea kwenye barabara ya malaya wakati wa usiku, (2) kuruhusu malaya huyo ampige busu, na (3) kusikiliza utongozi wake. Kila hatua ilifanya iwe vigumu zaidi na zaidi kujiweza mpaka kugeuka kukawa hakuwezekani. Mara kijana huyo alipojiona akifuatia hatua ya kwanza, alipaswa kuacha! —Wagalatia 5:22, 23.

16. Ingawa hakuna Mkristo wa kweli ambaye angefuata mwendo wa mwanamume huyo mwasherati, yawezekana akafanya nini?

16 Hakuna Mkristo halisi ambaye angefuata hatua za mwanamume huyo kwa halisi, lakini namna gani mawazo ya mtu? Je! kwa akili mtu angeweza ‘kuishika njia iendayo nyumbani kwa mwanamke huyo’ kwa kudumu kwenye mawazo ya uasherati? Papo kwa hapo kanyaga breki! Kukosa kufanya hivyo kwaweza kumfanya mtu azidi kuchukua akilini mwake hatua kama kupiga punyeto au hatimaye uasherati.

17. (a) Kwa sababu gani ni lazima kuutundika mwili pamoja na nyege zake? (b) Mkristo anawezaje kufanya hivyo?

17 Kwa sababu tamaa mbaya zinapendeza miili yetu isiyokamilika, haziondoleki kwa urahisi. “Na hao walio wa Kristo Yesu [wametundika] mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake.” (Wagalatia 5:24) Kutundikwa kulikuwa kuuawa kwa njia yenye uchungu mkali. Kwa hiyo jichukulie mwenyewe hatua kali-kali ili kufisha au “kuua” tamaa hizo zisizofaa—pale pale mwanzoni kabla hazijatia sana mizizi. Ikiwa programu ya televisheni inaanza kuamsha nyege zako, basi izime au ufungue programu nyingine mara moja. Jihadhari sana na sinema unazotazama au vitabu unavyosoma. Angalia mazungumzo yako na jinsi unavyowaona wanawake (au wanaume).​—Mathayo 5:28-30; Wakolosai 3:5.

18. Baadhi ya waseja Wakristo wamefanya nini ili kafisha nyege zisizofaa, na matokeo yakawa nini?

18 Unapokuwa ni wakati wa funzo la Biblia la kibinafsi au la kundi, je, tunapinga kishawishi cho chote cha kupuza mambo haya? Mkristo mmoja, kwa kufanya jitihada ya kutundika nyege zisizofaa wakati maono hayo ya moyoni yalipokuwa yenye nguvu sana, alijilazimisha mwenyewe atoke kitandani wakati wa usiku na kusoma kwa sauti kuu maneno ya Biblia kisha ya kila fungu mpaka vishawishi hivyo vilipopungua. Nyakati nyingi Wakristo wamejilazimisha kumwomba Yehova kwa bidii awape msaada papo kwa hapo. Maadamu Mkristo anajitahidi kwa unyofu kutundika “nyege” (NW) haielekei atasonga mbele akafanye uasherati.​—Waebrania 4:16.

Jitihada Hiyo Inastahili!

19. Je! uhusiano wetu pamoja na Mungu unategemea kama sisi tumefunga ndoa au tu waseja?

19 Useja ‘kwa ajili ya Ufalme’ na ndoa—mambo hayo mawili ni vipawa kutoka kwa Mungu. Hata hivyo yote mawili yanahitaji jitihada iwapo Mkristo atafanikiwa. Tuwe tu waseja au waliofunga ndoa, tunaweza kusitawisha uhusiano wa karibu na Mungu wetu na kupata uradhi maishani. Hata ‘ukipatia nafasi’ kipawa cha useja kwa muda mfupi tu, jambo lililo la maana ni kwamba uutumie kwa hekima.

20. (a) Wakristo wote waliokomaa wanapaswa kuuonaje useja? (b) Waseja wanaweza kuwa na uhakika gani juu ya wakati ujao?

20 Tambua kwamba Yesu alikipa heshima kubwa kipawa cha useja. Kila Mkristo aliyekomaa apaswa kuuona kama Yesu wala asifikiri useja ni hali ya kuhurumiwa. Yehova anathamini sana kujinyima kwa waseja ambao wamechagua kufanya anayoyafurahia. (Linganisha Isaya 56:4, 5.) Yehova hatawasahau. Wengine watakaookoka waingie katika dunia mpya huenda wakafurahia mapendeleo ya ndoa, na sawa na watoto wa Noa baada ya gharika ya dunia yote, wawe na nafasi za kushiriki katika agizo la kimungu la ‘kuijaza nchi.’ (Mwanzo 9:1) Huenda hizo zikawa ndizo baraka kuongezea zile ambazo tayari Wakristo waseja wanafurahia. Katika mfumo mpya wa Mungu yeye ‘atatosheleza tamaa ya kila kilicho hai’ na kuwapa wote ‘haja za moyo wao.’ Kwa hiyo uwe na hakika kwamba wote watapata furaha kamili kwa kupatana na mapenzi ya Mungu kwa wakati huo.​—Zaburi 37:3, 4; 145:16, NW.

21. (a) Mwalimu wa shule aliyetangulia kutajwa ametumiaje maisha yake ya useja? (b) Wale Wakristo wengine waseja wanawezaje kuona vivyo hivyo?

21 Huyo aliyekuwa mwalimu wa shule aliyetajwa katika fungu la kwanza la makala hii sasa ni mwenye umri wa miaka 83 na angali mseja. Mwanamke huyo ametumia miaka 57 katika utumishi wa wakati wote wa Ufalme, kutia miaka 56 kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova. Yeye anaonaje kuhusu maisha yake? “Nimeridhika kabisa na maisha yangu na kazi yangu. Sasa nina shughuli zaidi ya wakati mwingine wote katika kazi ninayoipenda sana,” akasema mwanamke huyo Mkristo mwenye kusisimuka. “Sina masikitiko yo yote. Ningeweza kufanya uamuzi huo huo tena.” Ndiyo, wewe, pia, ikiwa wewe ni mseja, unaweza kuwa na uradhi huo kwa kufanikisha useja—kupata faida na nafasi zake zote.​—Kutoka The Watchtower, June 15, 1982.

□ Useja ‘kwa ajili ya Ufalme’ unapasa kuonwaje?

□ Wakristo waseja wana nafasi gani kubwa?

□ Kwa sababu gani ni bora zaidi mtu kutokuacha useja haraka-haraka?

□ Ili kuendelea ‘kutulia moyoni,’ mseja anahitaji mambo gani matatu?

[Maelezo ya Chini]

a Athenagorasi mwenye kudai kuwa Mkristo aliandika hivi wapata mwaka 175 W.K.: “Utaona wengi kati yetu, wanaume na wanawake pia, wakizeeka bila kufunga ndoa, kwa tumaini la kuishi katika ushirika wa karibu zaidi na Mungu.”​—A Plea for the Christians, sura ya 33.

b Neno la awali la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “uamuzi,” krino, linamaanisha “kukata hukumu, kutangaza maoni.” Neno hilo linatumiwa katika Yohana 7:51 ambapo Nikodemo anasema kabla mtu hajahukumiwa, ni lazima kusikiliza ushahidi. Jambo hilo lingechukua wakati.

c Tafadhali ona makala “Sasa Nitasemaje—kusitawisha Ufundi wa Kuzungumza” na “Nawezaje kuwa na Rafiki za Kweli?” katika matoleo ya gazeti mwenzi wa hili, Amkeni! matoleo ya Januari na Machi 1983.

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

BAADHI YA WASEJA WANAOTAJWA KATIKA BIBLIA

Yesu: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.”-—Yohana 4:34.

Paulo: ‘Nilimtumikia Bwana nikatoa ushuhuda kikamilifu. Sikuifanya nafsi yangu kuwa yenye thamani.’​—Matendo 20:19-24, NW.

Yeremia: “Ee [Yehova], nguvu zangu, ngome yangu, na kimbilio langu siku ya taabu.”​—Yeremia 16:19.

Binti ya Yeftha: ‘Hakufanya ngono kamwe na mwanamume. Kila mwaka, wanawake wa Israeli walikuwa wakimwendea kwenye hekalu kumsifu.’​—Waamuzi 11:39, 40.

Ana: ‘Alikuwa mjane sasa mwenye umri wa miaka themanini na minne, naye hakuwa akikosa hekaluni, akitoa utumishi mtakatifu usiku na mchana pamoja na kufunga kula na maombi.’​—Luka 2:37, NW.

Dorkasi: “Alikuwa amejaa matendo mema na [mwenye kutoa zawadi za rehema].”​—Matendo 9:36.

[Picha katika ukurasa wa 13]

ILI KUENDELEA KUTULIA MOYONI

1. Jitoe utumikie wengine kiroho

2. Faidika na nguvu kutoka juu matatizo yanapolemea

3. Pinga upesi tamaa zisizofaa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki