Kuna Faida za Kukaa Bila Kuoa au Kuolewa
“Wako matowashi waliojifanya kuwa matowashi kwa ajili ya ufalme wa mbinguni. Awezaye kulipokea neno hili, na alipokee.”—Mt. 1 9:12.
1. Watumishi wa Yehova wa kale waliionaje ndoa na uzazi ikilinganishwa na kukaa pekee?
WATU wengi wanaona kwamba ni vigumu maisha kupendeza bila kuoa au kuolewa. Tangu Yehova Mungu alipowaoza mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, wanadamu wengi wamechagua kuoa au kuolewa badala ya kukaa peke yao. Nyakati za kale pia, ilikuwa vigumu kuona mtu asiyeoa au asiyeolewa kati ya watumishi wa Mungu. Wakati binti ya Yeftha alipopoteza haki ya kuolewa ili kutimiza nadhiri ya baba yake, kwanza alihuzunika. Baba yake alimruhusu kwenda na wasichana wenzake milimani muda wa miezi miwili, “akauombolea uanawali wake huko.” (Amu. 11:38) Naam, ndoa na uzazi ndiyo mambo yaliyoonekana kuwa baraka kubwa, si kuwa pekee.—Ruthu 4:13-17; Zab. 127:3-5; Mit. 5:18; 18:22; 31:10; Mhu. 9:9.
2. Kulitokea mabadiliko gani juu ya maoni ya kudumu kwa ndoa, Yesu alipokuja duniani?
2 Miaka 4,000 baada ya ndoa ya kwanza kufanywa, ndipo ilipoonyeshwa kwamba kukaa bila kuoa au kuolewa kunawafaa wanaume na wanawake fulani. Wakati mpya, wakati wa Kikristo, ulikuwa umeanza. Mabadiliko yaliyotokea yaligeuza maoni ambayo Waisraeli walikuwa wamekuwa nayo muda mrefu chini ya agano la zamani la Torati, juu ya upweke na ndoa. Mwanzishi wa Ukristo, Yesu, alionyesha wazi kwamba kanuni ya Mungu iliyotumika mwanzoni kuhusu ndoa ingerudishwa, alipokuwa akijibu ulizo juu ya talaka. Watu wasingeoa wake wengi wala kutalikiana tena isipokuwa kwa sababu ya ukosefu wa uaminifu katika ndoa.—Mt. 19:4-9.
3. (a) Wanafunzi wa Yesu walionaje aliposema ndoa ni yenye kudumu? (b) Je! wanafunzi walikata maneno vizuri juu ya kukaa bila kuoa? (c) Yesu alisema watu wengine ni matowashi kwa sababu gani?
3 Wanafunzi wa Yesu walionaje aliposema kwamba ndoa ni jambo lenye kudumu? Walisema, “Mambo ya mtu na mkewe yakiwa hivyo, haifai kuoa.” (Mt. 19:10) Waliona kwamba ilifaa kutooa badala ya kujitia katika uhusiano mbaya usioweza kuvunjwa hata mtu akitaka. Lakini, ikiwa mtu anajaribu kukaa bila kuoa au kuolewa kwa sababu ya kuogopa kuingia katika ndoa isiyopendeza au kwa sababu hataki kujitoa bila choyo awe na mwenzi, hana sababu nzuri. Hiyo ni wazi kutokana na maneno ambayo Mwana wa Mungu aliwaambia wanafunzi wake baada ya hapo: “Si wote wawezao kulipokea neno hili [la kukaa peke yao], ila wale waliojaliwa. Maana wako matowashi waliozaliwa hali hiyo toka matumboni mwa mama zao; tena wako matowashi waliofanywa na watu kuwa matowashi; tena wako matowashi waliojifanya kuwa matowashi kwa ajili ya ufalme wa mbinguni. Awezaye kulipokea neno hili, na alipokee.”—Mt. 19:11, 12.
SABABU YA KIROHO
4. Sababu bora zaidi ya kukaa bila kuoa au kuolewa ni nini, na kwa nini?
4 Kwa hiyo, sababu bora kabisa ya kukaa pekee ni ya kiroho. Kusudi bora kupita yote ambayo mwanamume au mwanamke ye yote anaweza kuwa nalo ni kujitoa afanye kazi ya Ufalme, asaidie wanadamu wenzake waipate thawabu nzuri sana ya uzima wa milele, na kuishika sana. Kwa kuwa mtu aliye pekee hana shughuli na masumbufu ya kutunza mwenzi wa ndoa na watoto, anaweza kumtumikia Mungu zaidi. Jambo hilo linaweza kupendeza na kuleta faida kweli kweli!
5. Je! watu wote wanaweza kukaa bila kuoa, na hilo linaonekanaje wazi kutokana na maagizo yanayohusu wanaume wanaostahili kuwa watumishi wa huduma na wazee?
5 Lakini, wale wanaoweza “kulipokea neno hili” peke yao ndio wanaopaswa kuchagua kukaa bila kuoa au kuolewa. Ni wachache tu kati ya Wakristo wa karne ya kwanza walioweza kufanya hivyo. Hiyo yaonyeshwa wazi na maagizo yaliyotolewa juu ya wanaume ambao wangestahili kuwa watumishi wa huduma na wazee. Njia yao ya kusimamia jamaa zao ilipaswa kufikiriwa, kuonyesha kwamba kwa kawaida wanaume wenye umri wa kuweza kuwekwa walikuwa wameoa, na walikuwa na watoto.—1 Tim. 3:2, 12; Tito 1:6.
6, 7. Mtu anawezaje kuwa na hakika kwamba anaweza kukaa bila kuoa au kuolewa?
6 Kwa kuwa karne zote watumishi wengi wa Mungu wameoa au wakaolewa, huenda mtu akauliza, Nawezaje kuwa na hakika kama mimi ni mmoja wa watu wachache wanaoweza kukaa peke yao? Mtume Paulo anatoa jibu lililoongozwa na Mungu: “Ikiwa mtu ye yote ametulia moyoni mwake, hana haja yo yote, lakini anatawala mapenzi yake mwenyewe na amefanya uamuzi huu moyoni mwake mwenyewe, kuendeleza ubikira wake mwenyewe, atafanya vizuri.”—1 Kor. 7:37, NW (Kiingereza).
7 Kwa hiyo, mtu aliye na “karama” ya kukaa peke yake anapaswa kujionea mwenyewe kwamba kuendelea kukaa hivyo kwa sababu za kiroho ni bora. Hiyo maana yake si kunyamazisha-nyamazisha tamaa za moyoni anapojisikia akitaka ndoa na maisha ya jamaa. Inampasa asadiki kabisa moyoni kwamba anafaa kukaa peke yake, tena inampasa ajitahidi awezavyo akae katika hali ya usafi wakati huo. Hataona wasiwasi wo wote akiendelea kukaa bila kuoa au kuolewa milele.
8. (a) Je! mtu anakuwa bora kuliko wengine ati kwa sababu hajaoa wala kuolewa? (b) Kulingana na Warumi 12:3-8, ni maoni gani ya kiasi tunayopaswa kuwa nayo juu ya “karama,” nazo zinapaswa kutumiwaje?
8 Bila shaka, mtu anayeweza kukaa peke yake kwa ajili ya Ufalme hapaswi kudharau Wakristo waliooa au kuolewa. Kulingana na maoni ya Mungu, yeye hawi bora kuliko wao ati kwa sababu yuko peke yake. Inampasa afahamu kwamba yuko alivyo kwa sababu ya fadhili zisizostahilika za Yehova. Mtume Paulo anaonyesha maoni ya kiasi ambayo Wakristo wanapaswa kuwa nayo juu ya “karama” zo zote walizo nazo, katika Warumi 12:3-8:
“Namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa kunia; bali awe na nia ya kiasi, kama Mungu alivyomgawia kila mtu kiasi cha imani. Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake. Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema tuliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia, kwa bidii; mwenye kurehemu, kwa furaha.”
Kwa hiyo, karama hazipaswi kutumiwa ili kujitukuza, bali kulifaidi kundi, kuwajenga washiriki wake.
WALE WASIO NA “KARAMA” HIYO
9. Kwa sababu gani watu wazima wasioweza kukaa bila kuoa au kuolewa wanaweza kupata faida wakingojea miaka kadha?
9 Lakini namna gani Mkristo anayetaka ndoa kikweli? Ingawa hana karama ya kukaa peke yake, hiyo haimaanishi afanye ndoa haraka haraka. Hasa wakati mtu anapokuwa bado na miaka ishirini na kitu, ana mengi ya kujifunza juu ya maisha, tena anaweza kuwa na ujuzi katika uhusiano wa kibinadamu kwa kushirikiana na vijana, watu waliooana na watoto wa umri wote. Mtu mzima aliye peke yake anaweza kupata ujuzi na busara inayohitajiwa ili kuchagua vizuri mwenzi wa maisha na kutimiza vizuri madaraka ya ndoa.
10. Maandiko kama Kumbukumbu la Torati 7:3, 4 na 1 Wakorintho 7:39 yanaonyeshaje kwamba Yehova anapendezwa na ndoa za watumishi wake?
10 Mkristo asisahau kamwe kwamba Aliye Juu Zaidi anapendezwa na ndoa za watumishi wake waaminifu. Aliye Juu Zaidi anajua sana kwamba ndoa isiyofaa inaweza kuleta msiba wa kiroho, kwa hiyo aliagiza Waisraeli wasifanye maagano ya ndoa na waabudu wa miungu mingine. (Kum. 7:3, 4) Vivyo hivyo, mtume Paulo alionyesha kwamba mjane Mkristo “yu huru kuolewa na mtu ye yote amtakaye; katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Kwa hiyo, ikiwa Yehova Mungu anaona kwamba mmojawapo watumishi wake anahitaji mwenzi kikweli, je! si busara kukata maneno kwamba atamjibu sala zake apate mwenzi mwema wa ndoa? Bila shaka, ikiwa kweli anahitaji mwenzi!
11. (a) Wakristo ambao kweli wanahitaji kuoa au kuolewa lakini hawajapata mwenzi anayewafaa wanaweza kufanya nini? Kwa sababu gani? (b) Ni mifano gani ya Biblia inayoonyesha kwamba Yehova anaweza hata kuwana watu wenzi wa ndoa ikiwa wanawahitaji kweli kweli?
11 Hiyo haimaanishi ndoa zinatayarishiwa mbinguni na kwamba kila Mkristo ana mwenzi mmoja tu wa kumfaa kati ya watumishi wengi wa Yehova. Hapana, maana ni kwamba Yehova anaweza kuhakikisha kwamba watumishi wake waaminifu wamepata wanachohitaji, kutia na mwenzi wa ndoa ikiwa wanatatizwa sana kukaa peke yao katika hali ya usafi. (Mit. 19:14) Aliye Juu Zaidi alimpa Isaka mke, tena alimpa Ruthu mume mwema. Wote wawili walibarikiwa sana kwa sababu walitanguliza mapenzi ya Yehova. (Mwa. 24:2-4, 12-27, 50, 51, 67; Ruthu 1:16, 17; 3:10; 4:13-17) Kwa hiyo, Wakristo wanaohitaji kuoa au kuolewa wanapaswa kusali kisha wamsubiri Yehova, wakiwa na hakika kwamba anataka wawe na furaha na hali njema.
FIKIRIA MIFANO MYEMA YA WATU WASIOOA WALA KUOLEWA
12. Kwa sababu gani tunaweza kufaidika na mfano wa wale waliofaulu kukaa bila kuoa au kuolewa?
12 Kama mtu mzima asiyeoa au kuolewa ana karama ya kukaa peke yake au hana, anaweza kufaidika kutokana na mifano ya Biblia ya watu ambao wamefaulu kukaa hivyo. Akiifikiria, maisha yake mwenyewe yanaweza kuwa na faida. Hata watu waliooana wanaweza kufaidika, kwa maana wakati na hali zinaweza kumwondolea mtu mwenzi wake na kumtia katika hali ya kuamua kama ataoa au kuolewa tena.
13. Yesu Kristo alijishughulisha sana kufanya nini akiwa katika hali ya kutooa, naye aliuonaje utumishi wake?
13 Bila shaka Yesu Kristo ndiye mfano bora zaidi wa kukaa bila kuoa. Yeye alijishughulisha sana kufanya mapenzi ya Baba yake. Alisema, “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.” (Yohana 4:34) Mwana wa Mungu alikuwa akiamka asubuhi na mapema na kutumikia mpaka usiku, akifundisha watu, kuponya wagonjwa na kukomboa waliokuwa wamepagawa na mashetani. (Marko 1:32; Luka 21:37, 38) Alitumikia kwa moyo wa kupenda. Hiyo inaonyeshwa na jibu alilompa mwenye ukoma aliyesema hivi, “Bwana, ukitaka, waweza kunitakasa.” Biblia inasema hivi: “Naye akaunyosha mkono wake, akamgusa akisema, Nataka; takasika.”—Luka 5:12, 13.
14. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Yesu alifurahia kushirikiana na wanaume, wanawake na watoto?
14 Linalostahili kuangaliwa pia ni kwamba, Yesu Kristo alifurahi sana kushirikiana na watu wote—wanaume, wanawake na watoto. Alikuwa akikubali kwenda kwa watu walipomkaribisha vyakulani na hata karamuni, akatumia nafasi alizopata kuwapa mafundisho ya kiroho. (Luka 5:29-32; 14:1-24) Alishirikiana sana na wanaume waliooa. (1 Kor. 9:5) Alimpenda sana Lazaro na dada zake Mariamu na Martha, na labda alikuwa akiwatembelea mara kwa mara nyumbani kwao Bethania. (Luka 10:38-42; Yohana 11:1, 5) Yesu alifurahia watoto pia. Wakati mmoja wanafunzi wake walijaribu kuzuia wazazi wasimpelekee watoto wao wadogo awaguse na kusali kwa ajili yao. Maandiko yanatuambia kwamba, “Yesu alipoona alichukizwa sana, akawaambia [wanafunzi], Waacheni watoto wadogo waje kwangu, msiwazuie . . . Akawakumbatia, akaweka mikono yake juu yao, akawabarikia.”—Marko 10:13-16.
15. Mfano wa Yesu Kristo unatuonyesha kwamba ni nini kinachomletea mtu asiyeoa au kuolewa furaha?
15 Mfano wa Yesu Kristo unaonyesha kwamba wanaotaka kufurahia kukaa peke yao lazima wajishughulishe kabisa kutumia wakati, nguvu na uwezo wao wakisaidia wanadamu wenzao kwa moyo wote. Lazima wapendezwe kikweli na watu, wafurahie kushirikiana na wanaume, wanawake na watoto. Inawapasa pia waweze kufurahia sana maisha bila ya kujinyima kupita kiasi, kwa sababu kufanya hivyo ‘hakufai kitu kwa kuzizuia tamaa za mwili.’—Kol. 2:23.
16. (a) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Paulo alisaidia sana watu kwa kukaa bila kuoa? (b) Kulingana na maneno ya mtume katika 2 Wakorintho 11:23-28, ingaliwezekana atimize mambo aliyotimiza kama angalikuwa ameoa?
16 Mtume Paulo alimwiga Yesu Kristo na kufurahia sana utumishi wake mtakatifu akiwa peke yake. Fadhili zisizostahilika za Yehova zilimwezesha kufanya kazi nyingi zaidi kuliko mitume wengine wote, akasafiri maelfu ya maili katika bahari na nchi kavu, na kuanzisha makundi mengi Ulaya na Asia Ndogo. (1 Kor. 15:9, 10) Ni wazi kwamba kama angalikuwa na mke na watoto asingaliweza kufanya kazi nyingi hivyo ya kueneza injili, kwa sababu kazi hiyo ilimwingiza hatarini mara nyingi. Karibu na mwaka 55 W.K., alisema kwamba alikuwa “katika taabu kuzidi sana; katika vifungo kuzidi sana; katika mapigo kupita kiasi; katika mauti mara nyingi.” (2 Kor. 11:23) Kwa kutumikia kwa nafsi yote na bila choyo, Paulo alipata furaha nyingi sana inayotokana na kutoa. Jambo hilo lilimfanya apendwe sana na waamini wenzake pia.—Matendo 20:24-27, 31-38.
17. Ni maisha ya namna gani hasa yanayohusika mtu anapokosa kuoa au kuolewa kwa ajili ya Ufalme?
17 Ni wazi kwamba wakati Paulo alipoongozwa na Mungu kupendekeza watu wakae peke yao, hakuwa akiwatia moyo wajishughulishe na mambo yao peke yao, wajikalie kitako tu au wajitie katika anasa. Hapana, alikuwa akipendekeza wafuate maisha ambayo yangewafanya ‘wajishughulishe na mambo ya Bwana’ bila masumbufu. Mtu mzima asiye na shughuli na masumbufu ya kutunza mwenzi wake na watoto anaweza kumtumikia daima Bwana Yesu Kristo, na wengine. (1 Kor. 7:32-35) Kwa kutegemea ujuzi wake mwenyewe, Paulo alisadiki kwamba wenye karama ya kuendelea kukaa peke yao wangefurahia maisha zaidi wakiyatumia kwa kutoa. (1 Kor. 7:40) Aliandika hivi: “Nipendalo ni kwamba watu wote wawe kama mimi nilivyo; walakini kila mtu ana karama yake mwenyewe itokayo kwa Mungu, huyu hivi, na huyu hivi.”—1 Kor. 7:7.
18. (a) Ana na Dorkasi walitumiaje wakati wao kwa faida? (b) Kulingana na Mathayo 28:19, 20, 1 Timotheo 5:10 na Tito 2:3-5, wanawake wanawezaje kufaidi watu kwa kukaa bila kuolewa?
18 Wanawake pia wamefurahi sana kwa kukaa bila kuolewa. Mfano mwema ni Ana. Baada ya kuolewa muda wa miaka saba tu mumewe alikufa, naye akaendelea kukaa peke yake maisha yake yote. Alifanyaje siku zote hizo? Alitanguliza mambo ya kiroho. Hata alipokuwa na miaka 84 alikuwa “haondoki katika hekalu ila huabudu usiku na mchana kwa kufunga na kuomba.” (Luka 2:36, 37) Baadaye, kundi la Kikristo lilikuwa na wanawake wasioolewa waliosaidia sana wenzao. Bila shaka Dorkasia alikuwa mmoja wao. “Mwanamke huyu alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa.” Alikuwa akishonea wajane wenye shida mavazi ya ndani na nje katika kundi. (Matendo 9:36, 39) Kati ya matendo yake mema, bila shaka alikaribisha wageni Wakristo nyumbani mwake, akafariji na kusaidia waliokuwa na shida yo yote. (Linganisha 1 Timotheo 5:10.) Kwa kuwa alikuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo, bila shaka alikuwa na bidii ya kueleza watu habari za Ufalme.—Mt. 28:19, 20.
19. Kwa sababu gani Wakristo ambao wameweza kukaa bila kuoa au kuolewa wanapaswa wathaminiwe?
19 Leo, kama ilivyokuwa katika kame ya kwanza W.K., wako wanaume na wanawake walio peke yao wanaosaidia sana kundi la Kikristo. Furaha yao nyingi inatokana na kujitoa kabisa wasaidie wenzao, ndani na nje ya kundi. Upweke wao unaleta faida kwa sababu hawatumikii faida zao wenyewe, bali za Bwana wao, Yesu Kristo. Je! karama yao haipaswi ithaminiwe na wengine wote kundini, kwa sababu imewezesha wengi wao wawe na utumishi mzuri sana?
20. Kwa sababu gani Wakristo wenye kujitoa wasiooa au kuolewa wanafurahia sana maisha, nao wanawezaje kutiwa moyo na Isaya 56:5?
20 Maisha yao hayawi ya bure tu kwa sababu ya kujinyima ndoa na uzazi, bali yanaleta faida nyingi na furaha. Ingawa hawana jamaa zao wenyewe, katika kundi la Kikristo wamepata watu wa kuwapenda sana kama mama na baba zao wenyewe, ndugu na dada zao wenyewe, naam, kama wana na binti zao wenyewe. (Marko 10:30) Wanachangamshwa sana na uhakikisho wanaopewa na Yehova: “Nitawapa hawa nyumbani mwangu, na ndani ya kuta zangu, kumbukumbu na jina, lililo jema kuliko kuwa na wana na binti; nitawapa jina lidumulo milele, lisilokatiliwa mbali.”—Isa. 56:5.
[Maelezo ya Chini]
a Hakuna mume anayetajwa kama aliomboleza Dorkasi alipokufa. Hiyo inaonyesha labda hakuwa ameolewa wakati huo.
[Picha katika ukurasa wa 413]
Yesu Kristo, aliyefurahia kushirikiana na watu wote—wanaume, wanawake na watoto—ndiye mfano bora zaidi wa mtu aliyefaulu kukaa peke yake
[Picha katika ukurasa wa 414]
Mtume Paulo, aliyependekeza wenye karama wakae peke yao, aliweka mfano mwema kwa kupendeza dhamiri za watu