Maoni ya Biblia
Wakati Useja Ni Zawadi
‘MIMI ni mpweke,’ aomboleza mwanamke Mkristo ambaye amekuwa mjane kwa miaka mingi. ‘Nimekuwa nikitumainia kupata mwenzi wa ndoa. Kufuliza kujishughulisha husaidia. Kuwa na marafiki husaidia. Lakini nataka kuolewa.’
Wakati utamanipo kwa moyo mweupe kufunga ndoa lakini utafutaji wako wa mwenzi wa ndoa haujafanikiwa, bila shaka useja hauonekani kuwa zawadi (karama)—huenda ukahisi ni kama umehukumiwa kifungo cha gereza la hisia-moyo hasi zikuachazo ukiwa umenyong’onyea na kushuka moyo. Au ikiwa tayari una familia yako mwenyewe lakini u mseja, huenda ikawa ni wewe tu uliye na daraka la kuandalia mahitaji yote ya watoto wako.
Hivyo basi, huenda usiione hali ya useja kuwa zawadi. Ingawa hivyo, wengine huchukua useja kuwa kitu cha thamani sana, nao huchagua kuishi peke yao. Kwa hiyo je, useja ni zawadi, na ikiwa ndivyo, wakati gani na kwa nini? Biblia yasema nini?
Ni Kipingamizi cha Furaha?
Ndoa yaweza kuwa chanzo cha upendezo mkubwa. (Mithali 5:18, 19) Watu fulani ‘wamesadikishwa kwamba kuiteremkia njia ya pingu za maisha ndio mwendo pekee wa kupata furaha na utimizo,’ laeleza Los Angeles Times. Je, leseni ya ndoa ndiyo “tiketi” pekee ya kupata furaha?
Mtaalamu mmoja wa afya ya kiakili, Ruth Luban, asema hivi, kulingana na Los Angeles Times: “Wanawake [na wanaume] watashangaa juu ya kadiri ya utimizo wawezao kuupata waachapo kuishi maisha ya utimizo kwa kutumainia kwamba mwanamume [au mwanamke] fulani atawaokoa kutoka kwenye maisha ya useja.” Ndiyo, useja si kitu kizuiacho maisha yenye furaha, yenye utimizo. Watu wengi waliopata talaka wangetoa usiri wa kwamba ndoa si barabara ya kuelekeza kwenye furaha moja kwa moja tu. Furaha ya kweli ni tokeo la uhusiano mwema pamoja na Mungu. Hivyo, Mkristo aweza kuwa mwenye furaha ama akiwa mseja ama akiwa amefunga ndoa.—Zaburi 84:12; 119:1, 2.
Zaidi ya kutaja vizuizi vya kujiletea, Marie Edwards na Eleanor Hoover, katika kitabu chao The Challenge of Being Single, watokeza kipingamizi kingine kiwezacho kuzuia furaha—msongo wa kijamii. Wao wasema “dhana ni ya kwamba ikiwa wewe hujafunga ndoa una ugonjwa fulani wa kihisia-moyo, wa kina kirefu, wenye kuhuzunisha. . . . Wewe una kasoro fulani, pasipo shaka.”
Hata marafiki wenye kusudio jema waweza kuweka bila kujua msongo mkubwa juu ya watu waseja kwa kuwauliza hivi kwa kuchokora-chokora, ‘Utafunga ndoa lini?’ au, ‘Ikawaje mwanamume mwenye haiba kama wewe bado hujapata mke?’ Ingawa maelezo kama haya huenda yakasemwa kwa mzaha, huenda ‘yakachoma kama upanga,’ yakitokeza hisia zenye maumizo au aibu.—Mithali 12:18.
Zawadi ya Kila Mmoja
Mtume Paulo alikuwa asiyefunga ndoa wakati aliposafiri akiwa mishonari. Je, hii ilikuwa kwa sababu alipinga ndoa? Hata. Mtume Paulo alikuwa mseja kwa sababu alichagua kubaki bila kufunga ndoa “kwa ajili ya Injili [“habari njema,” NW].”—1 Wakorintho 7:7; 9:23.
Paulo alikuwa na uwezo wa kujizuia asifunge ndoa, na bado alitambua kwamba si kila mtu awezaye kuwa kama yeye. Alisema hivi: “Kila mtu ana karama yake mwenyewe itokayo kwa Mungu, huyu hivi, na huyu hivi.”—1 Wakorintho 7:7.
Useja waweza kuwa barabara ielekezayo kwenye furaha, hata ingawa huenda ikawa siyo uliyokuwa umekusudia kusafiria. Hakika, ndoa imetiwa miongoni mwa zawadi nyingi zilizopokewa kutoka kwa Yehova. Lakini Biblia yaonyesha kwamba useja waweza pia kuwa “karama”—ikiwa wewe ‘waweza kulipokea neno hili.’ (Mathayo 19:11, 12; 1 Wakorintho 7:36-39) Basi, ni nini baadhi ya manufaa za useja?
Paulo alisema kwamba wenzi waliofunga ndoa huhangaikia ‘watakavyopendeza’ wenzi wao wa ndoa, hali wasiofunga ndoa “hujishughulisha na mambo ya Bwana.” Hii yakazia mojapo manufaa kubwa zaidi za useja—fursa ya kumtumikia Yehova “pasipo kuvutwa na mambo mengine.”—1 Wakorintho 7:32-35.
Biblia haisemi kwamba mtu mseja huishi pasipo vikengeusha-fikira. Hata hivyo, mtu anayeishi peke yake kwa jumla ana vikengeusha-fikira vichache kuliko yule anayetunza familia, kwa kuwa yeye pekee ndiye wa kujifikiria afanyapo uamuzi. Kwa kielelezo, wakati Mungu alipomwelekeza Abrahamu aondoke Harani ahamie bara la Kanaani, Biblia yasema hivi: “Abramu akamchukua Sarai mkewe, na Lutu mwana wa nduguye, na vitu vyao vyote walivyokuwa wamejipatia, na hao watu waliowapata huko Harani, wakatoka ili kwenda.” (Mwanzo 12:5) Ingawa hali ya familia ya Abrahamu haikumzuia, bila shaka alitumia wakati mwingi akipanga mambo ya nyumba yake kitengenezo kwa ajili ya utume huo.
Linganisha mwondoko wa Abrahamu na ule wa mtume Paulo. Paulo na Sila wakiwa wangali wakihubiri ile habari njema katika jiji la Thesalonike, kundi la watu wenye hasira lilikusanyika dhidi yao. Usiku uohuo, akina ndugu waliwatuma wote wawili Paulo na Sila kwenda Beroya mara hiyo. Katika pindi nyingine, Paulo akiwa katika Troa, alipokea njozi ya “vuka, uje Makedonia u[wa]saidie.” Mara tu alipokuwa ameona njozi hiyo, aliondoka kwenda Makedonia. Kwa wazi, kutokuwa kwa Paulo na mke kuliruhusu uhuru mkubwa wa kuhama kwa kipindi kifupi, jambo ambalo lingalikuwa gumu akiwa na familia.—Matendo 16:8-10; 17:1-15.
Manufaa nyingine ambayo useja hutoa ni uhuru mkubwa zaidi wa chaguo la kibinafsi. Uishipo peke yako, kwa kawaida huwa ni rahisi zaidi kuamua mahali pa kuishi, kitu cha kula na wakati wa kukila, au hata wakati wa kwenda kulala. Pia uhuru huu hutanda kufikia utendaji mbalimbali wa kiroho. Kuna wakati mwingi zaidi wa kujitia katika funzo la kibinafsi la Neno la Mungu, kushiriki katika huduma ya peupe, na kujifaidi na fursa za kusaidia watu wengine.
Kwa hiyo, iwe wewe u mseja kwa sababu ya kujichagulia hivyo au kwa sababu ya hali, azimia kutumia wakati wako kwa hekima. Utakuwa na maisha yenye furaha zaidi wakati useja wako utumiwapo katika kusaidia wengine. (Matendo 20:35) Ikiwa watamani kufunga ndoa, usijifunge katika gereza la hisia-moyo hasi wala usiishi maisha yako kama kwamba wewe ni mtu-nusu tu kwa sababu yule ‘mtu murua’ bado hajapita janibu zako. Jishughulishe katika utumishi wa Mungu, na kama vile Paulo alisema, huenda ukapata kwamba useja waweza kuwa zawadi.