“Habari za Asubuhi! Je, Walijua Jina la Mungu?”
IFUATAYO ni barua iliyopokewa kwenye ofisi ya tawi la Mashahidi wa Yehova katika Brazili, kutoka kwa dada wawili walio mapacha wenye miaka 12 katika jiji la Fortaleza:
“Nyuma katika 1990 tulipokuwa katika darasa la tano, shule yetu ilipanga tamasha ya maonyesho ya kisayansi, kisanii, na kitamaduni. Tulimweleza mwalimu wetu kwamba tulitaka wonyesho wetu uwe tofauti na ule ambao wanafunzi wengine walikuwa wanapanga kutayarisha. Kwa kuwa alikuwa ametusikia tukiongea juu ya Yehova na Biblia kabla ya hapo, alidokeza hivi: ‘Basi mwaweza kuandika juu ya Mungu wenu!’
“Tuliona kwamba hiyo ilikuwa fursa ya kutoa ushahidi tukaamua kutayarisha wonyesho wa fasihi ya Biblia inayokazia jina la Yehova. Tulitayarisha nakala kubwa ya maneno ya Zaburi 83:18 tukaiambatisha kwa gundi kwenye picha ya Biblia iliyofunguliwa. Pia, tuliweka kwenye meza tafsiri za Biblia tofauti-tofauti zenye jina la Yehova. Kwenye meza iyo hiyo, tulionyesha fasihi tofauti-tofauti za Biblia. Kwenye mwisho wa meza, tuliweka TV na vidiorekoda ili kuwaonyesha wageni kielelezo kimoja cha mahali ambapo jina la Yehova lilitumiwa katika sinema moja iliyopendwa sana.
“Wakati wa tamasha hiyo ya maonyesho, mtu alipokuja kwenye meza yetu, tulikuwa tukisema: ‘Habari ya asubuhi! Je, walijua jina la Mungu?’ Baada ya kumpa mgeni fursa ya kujibu, tuliendelea hivi: ‘Tazama hapa! Tafsiri kadhaa za Biblia huonyesha kwamba jina lake ni Yehova,’ tukielekeza kwenye jina hilo katika tafsiri tofauti-tofauti, kama zile za João Ferreira de Almeida, The Jerusalem Bible, na New World Translation. Kisha tulichezesha ile mandhari ambayo mwigizaji mkuu wa sinema akazia Yehova kuwa ndilo jina la Mungu. Watu walipoonyesha kupendezwa, tuliwapa gazeti au trakti yenye habari zaidi.
“Mmoja wa vijana waliokuja kwenye meza yetu aliomba kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. Mwalimu wetu alichunguza kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha alipaaza sauti hivi: ‘Mamawee! Hiki ni kitabu chenye kupendeza kama nini!’ Kufikia mwisho wa tamasha hiyo ya maonyesho, tulikuwa tumeangusha vitabu 7, trakti 18, na magazeti 67. Tulijishindia mahali pa tatu katika tamasha hiyo ya maonyesho. Lakini zaidi ya hayo yote, tulifurahi sana kuwa na pendeleo la kulijulisha jina la Mungu, Yehova.”