Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 2/15 kur. 23-26
  • Kuwatunza Waliozeeka Magumu na Thawabu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwatunza Waliozeeka Magumu na Thawabu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wajibu wa Kiadili na wa Kimaandiko
  • Kushughulikia Magumu Yanayokabiliwa
  • Kupoteza Uhuru
  • Kuwadumisha Wakiwa Wenye Kutenda
  • Kushughulikia Udhaifu wa Akili wa Uzeeni
  • Mahitaji ya Kihisiamoyo Kutoshelezwa
  • Watunzi Wanahitaji Utunzi Pia
  • Kuna Thawabu Pia
  • Utunzaji wa Wazee-Wazee Tatizo Lenye Kukua
    Amkeni!—1991
  • Kuwaheshimu Wazazi Wetu Wazee-Wazee
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Familia ya Kikristo Huwasaidia Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Kuzoea Bidii ya Kujitolea Mungu Kuhusiana na Wazazi Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 2/15 kur. 23-26

Kuwatunza Waliozeeka Magumu na Thawabu

SHINETSU, mhudumu Mkristo, alikuwa akifurahia sana mgawo wake. Familia yake ya watoto watatu ilitia ndani mama ya mke wake. Walikuwa wakifanya kazi kwa furaha pamoja na kutaniko ndogo la Mashahidi wa Yehova, wakiwafundisha watu Biblia, mpaka siku moja alipoombwa kufikiria kusafiri pamoja na mke wake ili kuzuru makutaniko mengine. Hilo lingehitaji badiliko la makao kila juma. Alifurahia taraja hilo lakini ni nani angemtunza Mama?

Familia nyingi zitakabili ugumu uo huo hatimaye—namna bora zaidi ya kuwatunza wazazi wanaozeeka. Kwa kawaida jambo hilo halifikiriwi sana wakati wazazi ni wenye afya nzuri na wanafanya kazi. Hata hivyo, mambo madogo-madogo huenda yakafunua kwamba wanaanza kuzeeka, kama vile mikono yenye kutetemeka wanapojaribu kutia uzi kwa sindano au kusahau-sahau wanapojaribu sana kukumbuka wakati wa mwisho walipoona kitu fulani ambacho kimewekwa mahali pasipo pake. Lakini, mara nyingi ni aksidenti au ugonjwa wa ghafula unaomfanya mtu atambue mahitaji yao. Lazima jambo fulani lifanywe.

Katika nchi nyingine wazazi wenye afya nzuri kwa kulinganisha hupendelea kuishi miaka yao ya uzee pamoja na wenzi wao pekee kuliko kuwa pamoja na watoto wao. Katika nchi nyingine, kama vile katika nchi za Mashariki na za Afrika, ni jambo la kidesturi kwa wazee-wazee kuishi pamoja na watoto wao, hasa yule mwana mkubwa zaidi. Hilo ni kweli hasa ikiwa mzazi mmoja ni mgonjwa kitandani. Kwa kielelezo, katika Japani, kati ya wale walio na miaka 65 na zaidi na ni wagonjwa kitandani kwa kadiri fulani, karibu 240,000 wao hutunzwa nyumbani na familia zao.

Wajibu wa Kiadili na wa Kimaandiko

Ingawa tunaishi katika kizazi ambacho wengi wamekuwa “wenye kujipenda wenyewe,” “wasiopenda wa kwao,” kwa wazi sisi tuna wajibu wa kiadili na wa Kimaandiko kuelekea wazee-wazee. (2 Timotheo 3:1-5) Tomiko, anayemtunza mama yake mzee-mzee, mwenye ugonjwa wa Parkinson, alieleza juu ya wajibu wa kiadili aliohisi aliposema hivi juu ya mama yake: “Alinitunza kwa miaka 20. Sasa ninataka kumfanyia vivyo hivyo.” Mfalme Sulemani mwenye hekima alionya hivi kwa upole: “Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako akiwa mzee.”—Mithali 23:22.

Wala chuki ya kidini wala uadui kwa upande wa mzazi asiyeamini haufuti amri hiyo ya Kimaandiko. Mtume Mkristo Paulo alipuliziwa kuandika hivi: “Mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.” (1 Timotheo 5:8) Yesu alituwekea kielelezo wakati alipopanga ili mama yake atunzwe, likiwa mojayapo matendo yake ya mwisho kabla ya kufa.—Yohana 19:26, 27.

Kushughulikia Magumu Yanayokabiliwa

Marekebisho mengi yanahitaji kufanywa na wote wakati familia zinapounganika tena baada ya kuishi mbalimbali kwa miaka nyingi. Mabadiliko hayo yanataka kadiri kubwa ya upendo, saburi, na kuelewana. Ikiwa mwana mkubwa zaidi, au mwana au binti mwingine, anahamisha familia yake kwenye nyumba ya wazazi wake, aina mpya kabisa ya hali hujitokeza. Huenda kukawa kazi mpya, shule mpya kwa watoto, na ujirani mpya kuzoelea. Mara nyingi itamaanisha wajibu wenye kuongezeka kwa mke.

Itakuwa vigumu vilevile kwa wazazi kufaana na hali. Huenda ikawa wamezoea kadiri fulani ya faragha, ukimya, na uhuru; sasa watakuwa na makelele ya wajukuu wenye nishati nyingi pamoja na marafiki wao. Wamezoea kujifanyia maamuzi yao wenyewe na huenda wakachukia majaribio yoyote ya kuwaelekeza. Wazazi wengi, wakiona kimbele wakati familia za wana wao watakapokuja kuishi nao, wamejenga nyumba mbalimbali karibu au wameongezea nyumba zao kwa kumbi zenye kuunganisha, wakiandaa kujitegemea kwa kadiri fulani kwa wote.

Mahali ambapo nyumba ni ndogo, marekebisho makubwa zaidi huenda yakahitajiwa ili kuandalia nafasi wapya. Mama mmoja alicheka alipokumbuka jinsi mabinti wake wanne walivyoudhika wakati fanicha zaidi na vyombo vinginevyo vya nyumba vilipoendelea kuletwa vyumbani mwao ili kumwandalia nafasi nyanya yao wa miaka 80. Bado, mengi ya matatizo hayo husuluhishwa wote wanapokuja kutambua uhitaji wa kufanya marekebisho na kukumbuka lile himizo la Biblia kwamba upendo “hautafuti mambo yake.”—1 Wakorintho 13:5.

Kupoteza Uhuru

Tatizo lenye uzito kwa mwanamke Mkristo laweza kutokea ikiwa mume wake hashiriki imani yake na aamua kuhamisha familia iishi pamoja na wazazi wake. Wajibu wa kuitunza familia huenda ukafanya ionekane kuwa vigumu sana kwake kusawazisha wajibu wake wa Kikristo na wajibu wake mwingine. Setsuko alisema hivi: “Mume wangu alihisi kwamba lilikuwa jambo la hatari kumwacha nyumbani peke yake mama yake aliyekuwa amerukwa na akili kwa kadiri fulani, na alinitaka niwe nyumbani nyakati zote. Nilipojaribu kwenda mikutanoni, angekasirika na kulalamika. Mwanzoni, kwa sababu ya malezi yangu ya Kijapani, mimi pia nilihisi lilikuwa jambo lisilo sawa kumwacha peke yake. Lakini, baadaye, nilitambua kwamba matatizo hayo yangeweza kusuluhishwa.”

Hisako alikuwa na tatizo lilo hilo. “Tulipohama kuishi pamoja na familia ya mume wangu,” yeye aripoti, “mume wangu, kwa sababu ya kuhofu lile ambalo watu wa ukoo wangefikiri, alitaka nibadilishe dini yangu na kuacha utendaji mbalimbali wa kidini. Kwa ubaya hata zaidi, kila Jumapili watu wa ukoo walioishi karibu walikuwa wakija kututembelea, wakiifanya iwe vigumu kwangu kwenda mikutanoni. Zaidi ya hayo, watoto walitaka kucheza pamoja na binamu zao kuliko kwenda mikutanoni. Niliona kwamba hali yetu ya kiroho ilikuwa inaathiriwa. Nililazimika nichukue msimamo imara na kumweleza mume wangu kwamba dini yangu haikuwa jambo la kubadilishwa kama mavazi lakini ilikuwa ya maana kwangu. Baadaye, familia ilifaana na hali.”

Wengine wamesuluhisha tatizo hilo la kupata wakati zaidi kwa kuwa na mfanyakazi nyumbani ili asaidie siku moja au mbili kwa juma. Wengine wamepata kadiri fulani ya uhuru kwa ajili ya shughuli za kibinafsi na utendaji wa Kikristo kwa kutafuta msaada wa watoto wao, watu wa ukoo walio karibu, na hata marafiki kutanikoni. Waume pia wameweza kusaidia usiku na miisho-juma wanapokuwa nyumbani.—Mhubiri 4:9.

Kuwadumisha Wakiwa Wenye Kutenda

Kuwadumisha wazee-wazee wakiwa wenye kutenda ni ugumu mwingine wenye kukabiliwa. Baadhi ya watu wazee-wazee wanafurahi kushiriki katika upishi na kazi nyinginezo za nyumbani. Wanahisi wanahitajiwa wanapoombwa wawatunze watoto na wanapata uradhi katika kutunza shamba ndogo, kutunza maua, au kushiriki katika utendaji fulani wenye kujipendeza.

Hata hivyo, wengine wanataka kulala karibu siku nzima na wanatazamia kutumikiwa. Lakini kuwadumisha wakiwa wenye kutenda kwa kadiri iwezekanavyo kwaonekana kuwa jambo la maana kwa afya yao njema, kuishi kwao kwa muda mrefu zaidi, na kubaki timamu kiakili. Hideko alipata kwamba ingawa mama yake alikuwa katika kiti cha magurudumu, kumpeleka mikutanoni kulikuwa ndicho kichocheo ambacho mama yake alihitaji. Alikaribishwa na wote kwa uchangamfu na kutiwa ndani katika mazungumzo. Uangalifu aliopewa uliongoza hatimaye kwenye kukubali kwake kujifunza Biblia pamoja na mwanamke mwenye umri mkubwa zaidi. Wenzi wa ndoa wanaomtunza mzazi anayeugua ugonjwa wa Alzheimer, huenda pamoja naye kwenye mikutano yao ya Kikristo. “Kwa kawaida yeye hataki kufanya chochote,” wakaonelea. “lakini anafurahi mikutanoni. Anakaribishwa kwa uchangamfu, kwa hiyo yeye huja kwa hiari. Tunahisi hilo linamnufaisha sana.”

Shinetsu, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, alisuluhisha tatizo lake kwa kumtafutia mama wa mke wake nyumba katikati ya eneo alikotumikia akiwa mhudumu anayesafiri. Hivyo yeye na mke wake wangekaa pamoja na yeye kati ya ziara zake kwenye makutaniko tofauti-tofauti kila juma. Mke wake, Kyoko, alisema hivi: “Mama yangu huhisi kwamba yeye ni sehemu ya maana ya kazi yetu na anahisi kuhitajiwa. Anafurahi wakati mume wangu anapomwomba apike mlo fulani wa pekee.”

Kushughulikia Udhaifu wa Akili wa Uzeeni

Wazazi wanapozeeka, kadiri mbalimbali za udhaifu wa akili huenda zikatokea, kwa hiyo wanahitaji uangalifu zaidi na zaidi. Wanasahau siku, nyakati, majira, na ahadi. Huenda wakashindwa kukata nywele zao na kufua nguo zao. Huenda hata wakasahau namna ya kujivika nguo na kuoga. Wengi hutatanika, hali wengine huwa na ugumu wa kulala usingizi usiku. Kuna mwelekeo wa kujirudia-rudia wenyewe na kuudhika ikiwa wanajulishwa hilo. Akili huwadanganya na kuwatatanisha. Huenda wakasisitiza kwamba wameibiwa kitu fulani au kwamba wanyang’anyi wanajaribu kuvunja nyumba. Familia moja yenye mabinti wanne ilihitaji kuvumilia mashtaka ya daima yasiyo na msingi juu ya utendaji kosa la kingono. “Halikupendeza,” wakasema, “lakini tulijifunza tu kuvumilia mashtaka hayo na kujaribu kubadili habari. Kugombana na nyanya kulikuwa bure.”—Mithali 17:27.

Mahitaji ya Kihisiamoyo Kutoshelezwa

Umri huwaletea wazee-wazee majaribu. Kuna magonjwa yenye kuhuzunisha, kupoteza uwezo wa kwenda huku na huku, na maumivu makali ya kiakili ya kuvumiliwa. Wengi huhisi kwamba maisha zao hazina mwelekezo au kusudi. Huenda wakahisi kwamba wao ni mzigo na kusema wanatamani kufa. Wanahitaji kuhisi wanapendwa, kustahiwa, na kutiwa ndani katika mambo. (Mambo ya Walawi 19:32) Hisako alisema hivi: “Sisi hujaribu sikuzote kumtia ndani mama katika mazungumzo yetu anapokuwako, tukimfanya awe kichwa cha mazungumzo inapowezekana.” Familia nyingine hujaribu kukuza kujistahi kwa babu yao kwa kumwomba aongoze mazungumzo ya kila siku ya andiko la Biblia.

Ni lazima mtu ajitahidi daima kudumisha maoni yafaayo juu ya wazee-wazee. Wagonjwa wa kitandani huchukizwa wanapohisi kwamba wanaambiwa mambo kwa dharau au kutendwa bila staha. “Mama alikuwa chonjo,” akaeleza Kimiko, aliyeishi pamoja na mama mkwe wake asiyejiweza, “na alijua wakati nisipomtunza kwa moyo wangu wote au nilipokuwa mwenye kudharau-dharau.” Hideko pia alihitaji kurekebisha mtazamo wake. “Mwanzoni nilifadhaika nilipohitaji kumtunza mama mkwe wangu. Nilikuwa nimekuwa painia [mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova], na niliikosa huduma. Kisha nikaona kwamba nilihitaji kurekebisha kufikiri kwangu. Ingawa huduma ya nyumba kwa nyumba ni ya maana, hiyo pia ilikuwa sehemu ya maana ya kutii amri za Mungu. (1 Timotheo 5:8) Nilitambua kwamba nilihitaji kusitawisha upendo na hisia-mwenzi zaidi ikiwa ningekuwa na shangwe. Dhamiri yangu ilikuwa ikinisumbua nilipofanya mambo tu kwa ajili ya kuhisi wajibu. Nilipopata aksidenti na kuwa na maumivu, nilimfikiria mama mkwe wangu na maumivu aliyokuwa nayo. Na baada ya hiyo ilikuwa rahisi zaidi kwangu kuonyesha uchangamfu na hisia-mwenzi zaidi.”

Watunzi Wanahitaji Utunzi Pia

Jambo lisilopasa kupuuzwa ni uhitaji wa kuonyesha uthamini kwa yule mwenye ule mzigo wa kumtunza aliyezeeka. (Linganisha Mithali 31:28.) Wanawake wengi huendelea kutunza wajibu wao mbalimbali wakisikia au bila kuyasikia maneno ya uthamini. Hata hivyo, tunapofikiria yale ambayo kazi zao huhusisha kwa hakika maneno hayo yanastahili. Yaelekea watakuwa na kazi zaidi ya kufanya ya kusafisha, kufua, na kupika. Pia, fikiria safari za kwenda hospitalini au kwa daktari, pamoja na kumlisha na kumwogesha mgonjwa aliye mzee-mzee. Mwanamke mmoja, aliyemtunza mama mkwe wake kwa muda mrefu, alisema hivi: “Najua ni vigumu kwa mume wangu kuonyesha uthamini wake kwa maneno, lakini yeye huonyesha katika njia nyinginezo kwamba anathamini yale ninayofanya.” Maneno sahili ya shukrani yaweza kufanya hayo yote yaonekane kuwa yenye kustahili.—Mithali 25:11.

Kuna Thawabu Pia

Familia nyingi ambazo zimewatunza kwa miaka mingi wazazi wanaozeeka zimesema kwamba hilo limewasaidia wasitawishe sifa za Kikristo za maana: uvumilivu, kujidhabihu, upendo usio na ubinafsi, bidii-nyendelevu, unyenyekevu, na wororo. Familia nyingi zimekaribiana pamoja kihisiamoyo. Bakshishi nyingine ni nafasi ya kuzungumza zaidi pamoja na wazazi na kupata kuwajua zaidi. Hisako alisema hivi juu ya mama mkwe wake: “Alikuwa na maisha yenye kupendeza. Alipatwa na magumu mengi. Nimekuja kumjua vema zaidi na kujifunza kuthamini sifa ndani yake ambazo sikuwa nimetambua kabla ya hapo.”

“Kabla ya mimi kujifunza Biblia kulikuwako wakati nilipotaka kutaliki na kuikimbia hali hiyo,” akaeleza Kimiko, aliyewatunza wazazi wa mume wake na nyanya yake aliyekuwa mgonjwa kitandani. “Halafu nikasoma kwamba tunapaswa ‘kuwatazama . . . wajane katika dhiki yao.’ (Yakobo 1:27) Ninafurahi kwamba nilifanya bora niwezavyo, kwani sasa hakuna yeyote katika familia awezaye kulalamika ifaavyo juu ya imani zangu. Dhamiri yangu ni safi.” Mwingine alisema hivi: “Nimejionea kwa macho yangu mwenyewe matokeo mabaya ya dhambi ya Adamu na sasa ninathamini hata zaidi uhitaji wa fidia.”

Je! hivi karibuni utamkaribisha mshiriki mwingine wa familia yako nyumbani kwako? Au labda utahama kuishi pamoja na wazazi wako waliozeeka? Je! unahisi hangaiko fulani? Hilo laeleweka. Kutakuwako marekebisho ya kufanywa. Lakini utathawabishwa sana katika kushughulikia jambo hilo kwa mafanikio.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Waliozeeka wanahitaji kuhisi wanapendwa na kustahiwa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki