Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Kuwaridhisha Wenye Njaa ya Kiroho—Shuleni
“Wenye furaha ni wale wanaofahamu uhitaji wao wa kiroho,” akasema Yesu katika Mahubiri yake ya Mlimani. (Mathayo 5:3, NW) Watoto wengi wa shule wana kiu ya kupata ujuzi wa Mungu na makusudi yake mazuri ajabu. Wao hutaka majibu kwa maswali juu ya maisha na hutaka kujua jinsi wapaswavyo kuishi ili kupokea kibali cha Mungu na kuwa wenye furaha. Hilo lilionekana wazi katika shule moja katika British Virgin Islands. Mmoja wa Mashahidi wa Yehova huko asimulia hivi:
◻ “Nilihudhuria mkutano wa wazazi na walimu kwenye shule ya mahali hapa, na mengi yalisemwa juu ya dawa za kulevya, kunywa vileo, kufanya miadi ya kimapenzi, kutazama TV, maksi, na mambo mengine, kwa hiyo niliamua kuchukua kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi na kukitoa kwa mwalimu mkuu. Baada ya yeye kukichunguza kitabu hicho, alisema kwamba kilikuwa ndicho kitu walichohitaji hasa akaomba kama shule ingeweza kupata nakala kwa ajili ya kila mmoja wa wale wanafunzi 120. Jambo hilo lilizungumziwa pamoja na wazee wa kundi, nao wakaamua kutoa upaji wa vitabu hivyo kwa shule. Tulipotaja hilo, walimu walituomba tuwatolee wanafunzi vitabu hivyo. Mashahidi wawili walienda, na chumba kilikuwa kimejaa wanafunzi wakiwangojea. Akina ndugu walisema kwa muda wa nusu saa, na maono yenye kuonyesha jinsi ambavyo kitabu hicho kimewasaidia wachanga na wazee yalisomwa kutoka kwa magazeti ya Watch Tower Society. Kisha vitabu vikatolewa kwa wanafunzi hao wenye hamu.”
Ni shangwe kujua kwamba shule hiyo imeamua kutumia kitabu hicho kikiwa sehemu ya kawaida ya mtaala wa darasa la nne na la tano. Kwa kweli kitajibu maswali mengi ambayo wanafunzi hao wanayo kuhusu maisha na wakati ujao.
Kuwaridhisha Wenye Njaa ya Kiroho —Katika Papua New Guinea
Ono lifuatalo lilipokewa kutoka kwa mwangalizi asafiriye. Linatoa kielezi cha jinsi watu walivyo na njaa ya kiroho katika nchi hiyo na jinsi vichapo vyetu vyenye msingi wa Biblia vilivyo vyenye kuridhisha njaa yao.
◻ “Kwa kuwa sikuweza kutembelea kijiji cha Kamberatoro,” akasema mwangalizi huyo, “nilitumia wakati wangu nikifanya kazi pamoja na lile kundi dogo katika Vanimo. Kuna kupendezwa kwingi huko. Watu kadhaa kutoka Bewani walikubali fasihi. Mwanamume mmoja aliniomba nije nitembelee kijiji hicho, naye angenipa mahali pa kukaa. Watu wengi wanafahamu fasihi yetu. Kila wakati ambapo tumeenda mji wa Vanimo, tumemaliza fasihi ijapokuwa tumechukua boksi tatu za vitabu. Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kinaonwa kuwa chenye thamani sawa na dhahabu. Watu wanakitafuta. Vitabu nilivyochukua viliangushwa upesi sana. Tulipowaonyesha watu fasihi yetu, wengine walikuwa wakiuliza hivi: ‘Kiwapi kile kitabu cha rangi ya manjano?’ Mtu mmoja aliagiza sita. Alinipa jina na anwani yake akaniomba nitangaze kupitia redio nilipovipokea. Kisha angekuja kutoka kijiji chake kuvichukua.” Mwangalizi huyo asafiriye aongeza hivi: “Nilipata kwamba watu wengi katika Vanimo walichukua vitabu Jitahada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu na Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi.”
Hilo latoa kielezi cha jinsi watu wenye moyo mweupe walivyo na njaa ya kupata chakula cha kiroho kinachopatikana katika Biblia na vichapo ambavyo Yehova ameandaa kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45-47) Mashahidi wa Yehova ni wenye furaha kama nini kuweza kuwasaidia watu hao wenye njaa ya kupata kweli!
[Picha katika ukurasa wa 19]
Kutoa ushahidi katika Papua New Guineay