Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
Kushinda Magumu Katika “Nchi ya Yasiyotarajiwa”
MTUME Paulo aliuliza Wakristo wa karne ya kwanza katika Korintho hivi: “Tarumbeta ikivuma wito usio dhahiri, nani atajitayarisha kwa ajili ya pigano? Katika njia hiyohiyo pia, nyinyi msipotamka usemi wenye kueleweka kwa urahisi kupitia hiyo lugha, linalosemwa litajulikanaje?”—1 Wakorintho 14:8, 9.
Katika Papua New Guinea, iitwayo nyakati nyingine Nchi ya Yasiyotarajiwa, Mashahidi wa Yehova hukabili vizuizi vya kutisha katika kuvumisha ujumbe wa Biblia ulio wazi. Wao huwahubiri watu wasemao lugha tofauti zaidi ya 700 na walio na desturi za namna nyingi. Mashahidi pia hupambana na maeneo yenye milima-milima, ukosefu wa barabara, na uhalifu wenye kuongezeka. Mbali na magumu hayo yote, kuna upinzani kutoka makundi fulani ya kidini na, nyakati nyingine, hata kutoka kwa maofisa wa shule.
Hata hivyo, maagizo mazuri ya kiroho na maktaba inayokua ya misaada ya kujifunza Biblia katika lugha za kienyeji zinawaandalia vifaa Mashahidi kuwasilisha habari njema ikiwa mwito wa tarumbeta ulio dhahiri. Mara nyingi itikio ni lenye kufaa, kama ripoti zenye kufuata zionyeshavyo:
• Mwanzoni mwa mwaka mpya wa shule, mwalimu fulani alitaka kujua kwa sababu gani watoto wa Mashahidi wa Yehova hawasalimu bendera au kuimba wimbo wa taifa. Alimwuliza Maiola, mwanafunzi mwenye umri wa miaka 13 ambaye ni Shahidi aliyebatizwa. Maiola alitoa ufafanuzi wazi, wenye kutegemea Maandiko. Mwalimu alikubali kusababu kwake kwa kuwa kulitoka katika Biblia. Wafanyakazi wengine pia wa shule walijulishwa juu ya ufafanuzi wake.
Baadaye, wanafunzi walipopewa mgawo wa kuandika insha, Maiola alichagua kuandika juu ya Utatu. Insha yake ilipata alama za juu zaidi darasani, na mwalimu alimwuliza alikokuwa amepata hiyo habari. Alimwonyesha kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani katika lugha ya Kiingereza. Kisha huyo mwalimu akakitoa hicho kitabu kwa darasa nzima, na wengi walitaka nakala yao wenyewe. Siku iliyofuata, Maiola aliangushia wanashule wenzake vitabu 14 na magazeti 7, na kuanzisha mafunzo ya Biblia pamoja na watatu kati yao. Mradi wa Maiola ni kuwa mhudumu wa wakati wote.
• Kikundi kilicho pekee cha Mashahidi wa Yehova katika kijiji kilicho karibu na Port Moresby, kimekabili upinzani tangu miaka ya mapema ya 1970. Hata hivyo, hivi majuzi walipokea msaada kutoka chanzo kisichotarajiwa. Siku moja, askofu wa kanisa liitwalo United Church la huko, mzaliwa wa Papua New Guinea aliyeelimishwa katika nchi za kigeni, alialika maswali kutoka kwa wasikilizaji kanisani. Mtu fulani aliuliza hivi: “Kuna dini mbili katika kijiji chetu—United Church na Mashahidi wa Yehova. Twapaswa kufanya nini Mashahidi wajapo milangoni petu?” Baada ya kutua kwa muda mrefu, huyo askofu alijibu hivi: “Wajua, kwa kweli sijui nikwambie nini. Hivi majuzi, Mashahidi wawili wachanga walikuja mlangoni pangu. Waliniuliza swali, na nikiwa na elimu yangu yote ya chuo kikuu, sikujua jibu. Lakini walinitolea jibu kwa urahisi kutoka kwenye Biblia. Hivyo sitakuambia utakalofanya—jifanyie uamuzi. Si lazima uwasikilize ikiwa hutaki kufanya hivyo, lakini usiwe mwenye jeuri nao.”
Mwakilishi asafiriye wa Watch Tower Society ambaye baadaye alikitembelea kikundi hicho cha Mashahidi aliripoti hivi: “Karibu kila mtu kijijini aliwasikiliza Mashahidi walipoenda kuhubiri. Baadhi yao hata waliwakaribisha nyumbani mwao. Sasa kijiji hicho ni paradiso kwa ajili ya kuhubiri.”y