Mungu Ndiye Akuzaye—Je! Wewe Hufanya Sehemu Yako?
EBU wazia mandhari hii. Umo katika bustani nzuri, ukiwa umezungukwa na miti yenye fahari, vichaka vyenye kusitawi, na maua mengi sana yenye rangi nyangavu. Bustani zenye nyasi za rangi ya kijani kibichi zateremka kuelekea kingo zenye kutunzwa kwa uangalifu za kijito chenye kububujika na maji safi. Hakuna chochote kinachoharibu mandhari hiyo. Ukiwa umevutiwa, wauliza ni nani aliyepafanya mahali hapo pazuri. Kwa kujibu mtunza bustani asema kwa unyenyekevu kwamba Mungu ndiye akuzaye vitu vyote.
Bila shaka ulikuwa umejua hilo. Na wakumbuka maneno ya mtunza bustani huyo unaporudi nyumbani na kuona bustani yako mwenyewe isiyotunzwa vizuri, ambapo hakuna chochote chenye kuvutia kinachokua, takataka zalimbika, na maji ya mvua yajaza mashimo yasiyopendeza ardhini. Watamani sana kuwa na bustani kama ile uliotoka kuzuru. Kwa hiyo, ukiamini kwa uthabiti maneno ya mtunza bustani huyo, wapiga magoti na kusali kwa bidii ukimwomba Mungu afanye maua mazuri yakue katika bustani yako. Ni nini chatokea? Bila shaka, hakuna chochote.
Namna gani ukuzi wa kiroho? Huenda ukatamani sana kuona mambo yakikua kiroho, kama vile kuona wanafunzi wapya wakiitikia kweli ya Neno la Mungu au kuona maendeleo yako mwenyewe ya kiroho. Na huenda ukasali kwa bidii ukimwomba Yehova atokeze ukuzi huo, ukiwa na usadikisho wenye kina wa kwamba ana nguvu za kufanya hivyo. Lakini je, kutamani kwako sana, kusali kwa bidii, na uhakika katika nguvu za Mungu vyenyewe vyaweza kutokeza ukuzi?
Mungu Ndiye Akuzaye
Labda wahisi kwamba sehemu yako katika kutokeza ukuzi wa kiroho si ya maana sana, hata haina maana yoyote. Je! mtume Paulo hakudokeza hilo kwenye 1 Wakorintho 3:5-7? Aliandika hivi: “Basi Apolo ni nani? na Paulo ni nani? Ni wahudumu ambao kwao mliamini; na kila mtu kama Bwana alivyompa. Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye.”
Paulo akiri ifaavyo kwamba mambo yanapokua, sifa zote humwendea Mungu. Mtunza bustani aweza kutayarisha ardhi yake, apande mbegu yake, na kutunza mimea kwa uangalifu, lakini mwishoni ni kwa sababu ya nguvu nzuri ajabu za uumbaji za Mungu kwamba vitu hukua. (Mwanzo 1:11, 12, 29) Lakini, Paulo amaanisha nini anaposema “apandaye si kitu, wala atiaye maji”? (“Si watunza bustani kwa kupanda na kutia maji kwao walio na maana,” The New English Bible.) Je! anapunguza umaana wa sehemu ya mhudumu mmoja mmoja katika kufanya wanafunzi wapya, akidokeza kwamba mwishoni si jambo la maana sana namna tunavyofanya huduma yetu?
“Apandaye Si Kitu”
Kumbuka kwamba katika sehemu hiyo ya barua yake, Paulo hazungumzi juu ya huduma ya Kikristo bali azungumza juu ya upumbavu wa kufuata watu badala ya kumfuata Yesu Kristo. Wengine katika Korintho walikuwa wakiwapa watumishi mashuhuri wa Yehova, kama vile Paulo na Apolo, umaana usiofaa. Wengine walikuwa wakianzisha madhehebu na kuwainua watu waliofikiri walikuwa wakuu zaidi ya ndugu zao wa Kikristo.—1 Wakorintho 4:6-8; 2 Wakorintho 11:4, 5, 13.
Kuwatukuza watu katika njia hiyo si jambo linalofaa. Ni kufikiri kimwili, nako kwatokeza wivu na ugomvi. (1 Wakorintho 3:3, 4) Paulo aonyesha matokeo ya kufikiri huko. Asema hivi: “Iko fitina kwenu. Basi, maana yangu ni hii, ya kwamba kila mtu wa kwenu husema, Mimi ni wa Paulo, na, Mimi ni wa Apolo, na, Mimi ni wa Kefa, na, Mimi ni wa Kristo.”—1 Wakorintho 1:11, 12.
Kwa hiyo, anapoandika, “mpandaji na mtia maji si kitu” (Phillips), mtume anashindana na kufikiri huko kwa kimwili, akikazia uhitaji wa kumtegemea Yesu Kristo kuwa Kiongozi na kukiri kwamba utukufu wote kwa ajili ya ukuzi katika kundi humwendea Mungu. Mitume na wazee wengine walikuwa watumishi wa kundi tu. Hakuna aliyepaswa kuinuliwa wala wao wenyewe hawakupaswa kutafuta fahari au umashuhuri. (1 Wakorintho 3:18-23) Kwa hiyo mpandaji na mtia maji si kitu, asema Paulo, “wakilinganishwa na yeye atoaye uhai kwa mbegu.”—1 Wakorintho 3:7, Phillips.
Wafanya Kazi Pamoja na Mungu
Kwa hiyo, katika kusema hivyo, mtume Paulo hakuwa akipunguza umaana wa sehemu yetu katika kupanda na kutia maji. Hakutaka tuanze kufikiri kwamba, “Mungu ndiye atakayekuza mambo kwa wakati wake mwenyewe,” na kisha tuketi kitako tu na kumngojea afanye hivyo. Alijua kwamba lile tunalofanya na jinsi tunavyolifanya lina matokeo juu ya jinsi mambo yanavyokua.
Ndiyo sababu Paulo aliwatia moyo Wakristo sikuzote wajitahidi katika huduma yao na kufanyia maendeleo stadi zao wakiwa walimu. Fikiria lile shauri analompa kijana Timotheo. “Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako. Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.” (1 Timotheo 4:16) “Nakuagiza . . . , lihubiri neno, uwe tayari . . . , kwa uvumilivu wote na mafundisho [ufundi wa kufundisha, NW]. . . . Timiliza huduma yako.” (2 Timotheo 4:1, 2, 5) Kusingekuwako maana yoyote katika Timotheo kujitahidi kufanyia maendeleo stadi zake ikiwa kupanda na kutia maji kwake kusingekuwa na matokeo juu ya kukuza mambo.
Kama vile Paulo na Apolo, wewe pia waweza kuwa na pendeleo lisilokadirika la kutumikia ukiwa mmoja wa wafanya kazi pamoja na Mungu. (1 Wakorintho 3:9; 2 Wakorintho 4:1; 1 Timotheo 1:12) Hivyo, kazi yako ni ya maana. Mtunza bustani hamtazamii Mungu atokeze bustani nzuri kimuujiza bila jitihada kwa upande wa mtunza bustani. Je! iwe vingine kwa habari ya ukuzi wa kiroho? Bila shaka sivyo. Kama vile mkulima angojeaye kwa saburi “mazao ya nchi yaliyo ya thamani,” ni lazima kwanza tujikakamue wenyewe katika kupanda na kutia maji, tukingoja huku Mungu akikuza mambo.—Yakobo 1:22; 2:26; 5:7.
Fanya Sehemu Yako
Kwa kuwa, kama mtume Paulo asemavyo, “kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu [kazi ya jasho, NW] yake mwenyewe,” twafanya vema kujiuliza wenyewe jinsi tunavyofanya kazi ya jasho.—1 Wakorintho 3:8.
Mstadi wa kazi za bustani Geoffrey Smith asema hivi: “Hakuna sifa za ustahili za pekee zinazohitajiwa ili kuwa mtunza bustani, kinachohitajiwa tu ni kupendezwa na mimea.” (Shrubs & Small Trees) Vivyo hivyo, hakuna sifa za ustahili za pekee za asili zinazohitajiwa ili sisi tuwe wafanya kazi pamoja na Mungu, kinachohitajiwa tu ni kupendezwa kikweli na watu na kuwa na nia ya kutumiwa na Mungu.—2 Wakorintho 2:16, 17; 3:4-6; Wafilipi 2:13.
Fikiria baadhi ya mashauri mazuri yanayotolewa na watunza bustani wastadi. Mamlaka yasema, mtunza bustani mpya akiwa na nia ya kuwasikiliza wale wenye ujuzi zaidi ya yeye, “mwanafunzi huyo aweza kuwa mstadi upesi.” Na mamlaka iyo hiyo yasema, “mstadi sikuzote hupata jambo jipya la kujifunza.” (The Encyclopedia of Gardening) Je! wewe hukubali kwa utayari msaada na mazoezi ambayo Yehova huandaa ili uweze kupanda na kutia maji kwa matokeo? Ikiwa wafanya hivyo, iwe wewe ni mpya katika kazi hiyo au ni mwenye ujuzi, waweza kusitawisha stadi zaidi ukiwa mfanya kazi pamoja na Mungu na hivyo kuwa na “sifa za kustahilisha vya kutosha ili kuwafundisha wengine.”—2 Timotheo 2:2, NW.
Ikiwa ana nia ya kusikiliza na kujifunza, asema Geoffrey Smith, “yeye anayeanza [kuwa mtunza bustani] ataepuka mitego mibaya zaidi.” Tukisikiliza mwelekezo ambao Yehova hutoa kupitia Neno lake na tengenezo lake, tutafanya mambo njia yake. Hivyo tutaepuka, kwa kielelezo, mitego kama vile kubishana kipumbavu na wale wanaotaka tu kugombana na kupigana juu ya maneno.—Mithali 17:14; Wakolosai 4:6; 2 Timotheo 2:23-26.
Shauri jingine zuri la utunzaji wa bustani ni kufikiria mambo kwa uangalifu kabla ya kwenda mbio kulima. “Kabla ya kuanza kulima,” yasema The Encyclopedia of Gardening, “tumia wakati ukikadiria [mataraja yako].” Je! wewe hutumbukia katika mtego wa kwenda mbio katika huduma ya Kikristo bila kufikiria kwanza kwa uangalifu na kwa sala lile unalotaka kutimiza na jinsi utakavyolitimiza bora zaidi? Tambua wazi miradi yako kabla ya kuanza. Kwa kielelezo, fikiri juu ya watu ambao huenda ukakutana nao na matatizo ambayo huenda ukakabili, na ujitayarishe kuyashughulikia. Hilo litakuruhusu “[uwapate] watu wengi zaidi. [unapokuwa] hali zote kwa watu wote.”—1 Wakorintho 9:19-23.
“Usiuzuie Mkono Wako”
Tukithamini pendeleo la kutumikia tukiwa wafanya kazi pamoja na Mungu, hatutakuwa wanyimivu katika upande wetu wa ushirika huo. “Asubuhi panda mbegu zako, wala jioni usiuzuie mkono wako. Kwa maana wewe hujui ni zipi zitakazofanikiwa, kama ni hii au hii, au kama zote zitafaa sawasawa.” (Mhubiri 11:6) Matokeo ya mwisho yamo mikononi mwa Yehova, lakini tutavuna tu ikiwa twapanda kwanza kwa bidii nyendelevu.—Mhubiri 11:4.
Hakuna bustani yoyote iliyofanywa nzuri kwa kulima na kutawanywa kwa mbegu ki-vivi-hivi tu, kulikofanywa kizembe. Vivyo hivyo, mengi zaidi yanatakwa katika huduma ya Kikristo kuliko ushiriki wa ki-vivi-hivi tu katika ugawanyaji wa fasihi ya Biblia. Tukiwa wafanya kazi pamoja na Mungu, tunahitaji kujulisha habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu kwa bidii nyendelevu na kikamili, tukiwatafuta wale wenye mwelekeo ufaao. (Matendo 13:48) Kumbuka ile kanuni katika maneno ya mtume Paulo kwenye 2 Wakorintho 9:6: “Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu.”
Kama vile watunza bustani wote wazuri, sisi hujaribu kupanda katika udongo mzuri. Hata hivyo, mara kitu kinapopandwa hata katika udongo ulio mzuri zaidi, huo si mwisho wa jambo hilo. Asema Geoffrey Smith: “Hilo halimaanishi kwamba mara kitu kinapopandwa hakuna jambo jingine linalotakwa kutoka kwa mtu mwenye daraka hilo ila kupumzika.” La, ili vitu vikue, jitihada inatakwa katika kutia maji na kuilinda mimea.—Linganisha Mithali 6:10, 11.
Kwa kweli, huenda huduma ya Kikristo ikamaanisha vipindi virefu vya kazi ngumu wakati ambapo hakuna lolote linaloonekana kutukia. Lakini kwa ghafula, na nyakati nyingine bila kutazamiwa, matokeo mazuri ajabu huenda yakafuata. Geoffrey Smith asema hivi: “Kutunza bustani huahusisha vipindi virefu vya kazi ngumu ya kawaida vikichanganyika na wasaa wa uzuri wa ajabu hivi kwamba kulima kote, kupalilia kote, na wasiwasi mwingi sana vinasahauliwa.” Wewe pia waweza kuwa na wasaa wa uradhi wa ajabu wakati moyo wenye kukubali wapokea ujumbe wa kweli—maadamu una nia ya kulima, kupanda, kupalilia, na kutia maji mwanzoni.—Linganisha Mithali 20:4.
Paulo na Apolo walijua kwamba kazi yao ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi hakukuwapa umashuhuri fulani wa pekee katika kundi la Kikristo. Walielewa kwamba ni Mungu ndiye akuzaye mambo. Bado, walipanda na kutia maji—kwa bidii nyendelevu. Sisi na tufuate kielelezo chao na tujitolee kwa Mungu tukiwa ‘wahudumu ambao kwetu wengine wanakuwa waamini.’—1 Wakorintho 3:5, 6.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mungu ndiye akuzaye vitu vyote—lakini mtunza bustani hufanya sehemu yake pia