“Mkabidhi Yehova Kazi Zako”
“Mkabidhi [Yehova] kazi zako, Na [mipango] yako [i]tathibitika.”—Mit. 16:3.
1. Mitume walifahamu mojawapo uhitaji mkubwa sana kwa Wakristo kuwa nini?
MOJAWAPO ya mambo yanayohitajiwa sana na watu leo ni kutiwa moyo. Kila mtu anavunjika moyo mara kwa mara kwa sababu ya mikazo ya ulimwengu huu na kwa sababu ya kupungukiwa kwake. Hiyo ni kutia na Wakristo. Mtume Paulo alieleza kusudi la kulitembelea kundi moja “yaani, tufarijiane mimi na ninyi, kila mtu kwa imani ya mwenzake, yenu na yangu.” (Rum. 1:12) Wakati wanaume Wakristo kutoka Yerusalemu walipotembelea miji mingine, ‘waliwatia ndugu moyo kwa hotuba nyingi, wakawatia nguvu.’ (Matendo 15:32, NW; 20:1) Huu ni mfano mzuri wa kufuatwa na wazee na waangalizi wasafirio leo.—Linganisha Wafilipi 2:1.
2. Biblia inashauri tufanye nini tunapokuwa na kazi au tatizo (gumu) kubwa?
2 Nyakati nyingine huenda ukawa na gumu au kazi inayoonekana kuwa kubwa sana. Au, huenda ukakutana na hali mbaya sana katika maisha. Unapaswa kufanya nini? Mahali pa kuvunjika moyo au kukata tamaa, unapaswa kumgeukia “Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote.” (2 Kor. 1:3, 4) Ndiyo, “mkabidhi [Yehova] kazi zako, na [mipango] yako [i]tathibitika.” Mit.—16:3.
3. ‘Kumkabidhi Yehova kazi zako’ kunamaanisha nini?
3 Hata hivyo, ‘kumkabidhi Yehova kazi zako’ kunamaanisha nini? Kunamaanisha uutoe mzigo wako begani mwako umtwike yeye. Bila shaka, mipango au tamaa ulizo nazo lazima ziwe zinafaa, njema, zinazopatana na Neno la Mungu la kweli, si zile za kutosheleza choyo, kisasi, na vivyo hivyo. Mahali pa kuona kwamba mzigo unakulemea wewe, mweleze Yehova kila kitu, ukimwachia kabisa jambo hilo. Kisha, kupitia kwa sala na kwa kufuata shauri la Biblia namna uwezavyo, umtazamie yeye atimize jambo ulilomwomba.—Yak. 1:2, 5; Mt. 7:7, 8.
UKUZI NA UFANISI WATOKA KWA MUNGU
4. Ni kwa sababu gani ni jambo la maana Mkristo akumbuke ‘kumkabidhi Yehova kazi zake’?
4 Hili ni jambo zito sana. Mkristo akikosa kufanya hivyo, huenda akaanza kujitegemea sana, akifikiria, hata bila kujua, juu ya ukuu au uwezo wake. Mipango yake ikielekea kufanikiwa, huenda akajisifu, halafu baadaye aone kwamba ‘kufanikiwa’ kulikuwa kwa muda tu au kwa juujuu tu. Kufanikiwa kama huko hakumtukuzi Mungu na hakuwasaidii wengine. Kwa kuwa, “[Yehova] asipoijenga nyumba waijengao wafanya kazi bure. [Yehova] asipoulinda mji yeye aulindaye akesha bure.”—Zab. 127:1.
5. Mtume Paulo alionyeshaje kwamba haifai kujitukuza au kutukuza wanadamu wengine?
5 Kanuni hii ilikaziwa na mtume Paulo alipoliandikia kundi la Kikristo la Korintho. Wengi katika kundi hili walikuwa wakifuata au kutukuza wanaume wenye kujitafutia makuu. (2 Kor. 11:4, 5, 13) Vilevile, huenda wengine walikuwa wakiwaheshimu Paulo na Apolo kupita kiasi. (1 Kor. 1:12) Walakini Paulo alitumia mfano wake yeye mwenyewe na wa Apolo na Kefa ili aonyeshe namna isivyofaa kujitukuza au kujitegemea au kutegemea mwanadamu mwingine ye yote. (1 Kor. 4:6) Alisema hivi: “Kwa vyo vyote, Apolo ni nini? Paulo ni nini? Sisi tu mawakili [au, watumishi] tu wa Mungu katika kumleta katika imani. Kila mmoja wetu alifanya ile kazi ambayo aligawiwa na Bwana: Mimi nilipanda mbegu, naye Apolo akaimwagilia maji; lakini Mungu aliifanya ikue. Hivyo si wakulima walio wa maana pamoja na kupanda na kumwagilia maji, bali Mungu, aifanyaye ikue.”—1 Kor. 3:5-7, New English Bible.
6. Matokeo kwa Mkristo ambaye ‘hamkabidhi Yehova kazi zake’ yatakuwa nini?
6 Ndipo Paulo alipowaambia kwamba walipaswa kuwa wakifanya kazi kwa bidii wajenge juu ya msingi unaofaa, ambao ni Yesu Kristo. Walakini, wakishindwa kujenga vizuri—wakose ‘kumkabidhi Yehova kazi zao’ hivyo wawe hawamtegemei awafanikishe—wangeona kwa aibu yao kwamba, walikuwa wamejenga vitu visivyo na maana, vitu visivyoweza kustahimili jaribu la Mungu.—1 Kor. 3:10-15.
7. Kwa sababu gani lazima Mkristo ajiangalie asijitegemee au kujisifu?
7 Sababu ya Wakristo kujiangalia ni kwamba maelekeo ya kibinadamu ni kujitegemea, na kujisifu. Upesi baada ya siku za Nuhu, Mungu alisema hivi: “Mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana.” (Mwa. 8:21) Sisi sote tumeyarithi maelekeo haya kutoka kwa Adamu, aliyechukua mwendo wa kujitegemea, afanye mambo kwa kujitegemea, kulingana na anavyojiongozea mambo. Lakini kwa kweli yeye alikuja chini ya utawala wa Ibilisi.—Mwa. 3:5.
TUTUKUZE JINA LA MUNGU, TUSIJITUKUZE WENYEWE
8. Sababu ya msingi ya mambo yote tuyafanyayo inapaswa kuwa nini?
8 Jina la Mungu na la Mwanawe ni lazima yatakaswe na yale yanayofanywa na Wakristo. Hii inamaanisha kwamba lengo letu lazima liwe kuijulisha na kuitukuza enzi kuu ya Mungu, haki yake, rehema zake pamoja na sifa nyingine bora zake. (1 Pet. 3:15) Tusipofanya hivyo, ama sisi wenyewe au mtu mwingine atapewa sifa kwa yale yanayofanywa, bila matokeo mema. Mfano ambao Mungu aliandikisha, ukionyesha uhakika huu, unaonekana katika hali iliyotokea baada ya Israeli kukalia nchi ya Ahadi.
9. Waisraeli waliyaonaje matokeo ya ‘kumkabidhi Yehova kazi zao’?
9 Katika wakati huo, Samweli nabii mwaminifu ndiye aliyekuwa akihukumu Israeli. Kwa sababu watu walikuwa wakisita-sita kati ya ibada ya Yehova na ile ye miungu mingine, walikuwa wametaabishwa sana na adui zao. Walakini Samweli aliwaongoza katika njia inayofaa, Aliwaomba waitupilie mbali miungu ya uongo iliyokuwa katikati yao. Walitii wakaanza kumtumikia Yehova peke yake. Hivyo, ‘wakimkabidhi Yehova kazi zao,’ walipewa ushindi mkubwa juu ya adui zao, Wafilisti.—1 Sam. 7:3, 4, 10-14.
10, 11. Hata baada ya Yehova kuwaongoza vizuri sana Waisraeli walishindwaje kumtukuza na kumtumaini?
10 Hata hivyo, baada ya kuona kutoweza kwao kitu na kuona kwamba walipaswa wamtegemee Yehova kwa baraka, baadaye, Samweli alipokuwa mzee, waliomba wawe na mfalme. Walisema hivi: “Tufanyie mfalme atuamue, mfano wa mataifa yote.” Samweli aliposali juu ya jambo hilo, jibu la Yehova lilikuwa: “Hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi, nisiwe mfalme juu yao.”—1 Sam. 8:4-7.
11 Ndipo Samweli alipowaonya juu ya maonezi ambayo wangeyapata chini ya utawala wa mfalme wa kibinadamu, lakini walijibu: “Sivyo, hivyo; lakini tunataka kuwa na mfalme juu yetu. Ili sisi nasi tufanane na mataifa yote; tena ili mfalme wetu atuamue, tena atoke mbele yetu na kutupigia vita vyetu.”—1 Sam. 8:10-20.
12. Kwa sababu ya kushindwa ‘kumkabidhi Yehova kazi zao,’ Waisraeli walipatwa na nini?
12 Hapa watu wa Israeli walifunua hali yao ya kweli ya moyoni, wakiwatazamia wanadamu wafanikishe mipango yao. Hawakuwa na imani ‘wamkabidhi Yehova kazi zao.’ Baadaye kidogo, Mungu alionyesha kuchukizwa kwake kwa kuifanya mvua inyeshe siku ile ile waliyotazamia kuvuna ngano yao. (1 Sam. 12:17, 18) Kufuata hapo, Israeli walitaabika sana chini ya utawala wa wafalme wao, kuondoa wanaume wachache waliokuwa waaminifu, kama Mfalme Daudi, Yosia na Hezekia. Haya yalikuwa matokeo ya kutokubali kwamba Yehova ndiye kweli alikuwa Mfalme wao.
WEKA MAMBO YOTE MIKONONI MWA MUNGU
13. Jambo lo lote tulifanyalo sisi kama watumishi wa Mungu, tunapaswa kulifanyaje?
13 Kutokana na mfano huu tunaweza kuona kwamba, Yehova anapaswa na kila gumu linalowapata watumishi wake na katika shughuli (kazi) zao zote. Kwanza ni lazima tukumbuke mapenzi na jina la Yehova. Ndipo tunapoweza kuweka mambo yote mbele zake tukijua kwamba kuthibitishwa kwa mipango yetu kuko mikononi mwake. Ikifanikiwa, Mungu anapata sifa. Ikitokea vingine kuliko tulivyokuwa tumepanga, bado tunaweza kujua kwamba yeye anafanya au anaruhusu yanayotufaa zaidi.—Rum. 8:28.
14. Kuna ubaya gani wakati sisi kama Wakristo tunaposifu uwezo au ujuzi wetu kwa sababu ya jambo ambalo limetimizwa?
14 Katika ulimwengu, kufanikiwa kwa mtu mara nyingi kunalingana na uwezo na ujuzi wake, hivi kwamba watu wanajisifu kwa sababu ya mambo waliyoyatimiza. Walakini katika utumishi wa Mungu sivyo ilivyo. Kama sivyo, kadiri ya uhusiano wa mtu na Mungu ungekuwa kulingana na uwezo na utu wake. Kwa kweli, mtu ambaye hajitegemei mwenyewe wala uwezo wake ndiye anabarikiwa na Yehova. Mtume alisema hivi: “Lakini tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si kutoka kwetu.” (2 Kor. 4:7; linganisha 2 Wakorintho 12:9.) Wakristo wanapaswa kuwa macho nyakati zote ili wasiyarudie maelekeo ya asili ya mwili usiokamilika, wakisahau kwamba ‘wao ni watumishi tu wa Mungu,’ wapandao na kumwagilia mbegu maji, lakini kwamba Mungu ndiye azikuzaye.—1 Kor. 3:6, 7.
15. Yanayotimizwa katika utumishi wa Mungu yanategemeaje kanuni ile ile ya namna miili yetu inavyofanya kazi kwa kufaa?
15 Sehemu ambayo Mungu anashiriki tunapomtumikia inaweza kulinganishwa na namna miili yetu inavyofanya kazi. Viungo ambavyo Mungu alitupa vinafanya kazi bila ya sisi kujua namna vinavyofanya kazi. Tunaweza kueleza kidogo tu namna vinavyofanya kazi. Vilevile chakula ambacho tunapata sisi kinakua bila ya sisi kujitaabisha sana, na mara nyingi hata bila ya sisi kujitaabisha hata kidogo, hata hivyo, kinavyo vitu vyote vinavyohitajika kutia mwili nguvu. Jua, mvua, udongo na mbegu ndizo zinazofanya kazi zilizo kubwa zaidi. Hivyo, kwa kweli, maisha yetu yanategemea kabisa mambo ambayo Mungu anatoa. Yeye anafanya kazi yote. Utumishi wetu kwa Mungu unafuata kanuni iyo hiyo. Asema mtume Petro: “Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo.”—1 Pet. 4:11, linganisha Mathayo 6:25-31.
MFANO BORA WA IBRAHIMU
16. Ibrahimu alilazimikaje ‘amkabidhi Yehova kazi zake’ kuhusiana na uzao ulioahidiwa?
16 Ibrahimu ni mfano bora wa mtu ‘aliyemkabidhi Yehova kazi zake’ bila kuacha cho chote. Yeye alikuwa na neno la ahadi ya Yehova tu kwamba Mungu angefanya taifa kubwa kutoka kwake na kwamba jamaa zote za dunia zingebarikiwa kupitia kwake. (Mwa. 12:2, 3) Mtume Paulo anavuta fikira kwenye imani ya Ibrahimu, akisema:
“[Yeye] Ibrahimu; aliye baba yetu sisi sote; (kama ilivyoandikwa, Nimekuweka kuwa baba wa mataifa mengi); mbele zake yeye aliyemwamini, yaani Mungu, mwenye kuwahuisha wafu, ayatajaye yale yasiyokuwako kana kwamba yamekuwako. Naye aliamini kwa kutarajia yasiyoweza kutarajiwa, ili apate kuwa baba wa mataifa mengi, kama ilivyonenwa, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako. Yeye asiyekuwa dhaifu wa imani, alifikiri hali ya mwili wake uliokuwa umekwisha kufa, (akiwa amekwisha kupata umri wa kama miaka mia), na hali ya kufa ya tumbo lake Sara. Lakini akiiona ahadi ya Mungu hakusita kwa kutokuamini, bali alitiwa nguvu kwa imani, akimtukuza Mungu; huku akijua hakika ya kuwa Mungu aweza kufanya aliyoahidi. Kwa hiyo ilihesabiwa kwake kuwa ni haki.”—Rum. 4:16-22.
17. Ibrahimu ‘alimkabidhije Yehova kazi zake’ wakati Mungu alipomwuliza amtoe dhabihu yule ambaye kupitia kwake uzao ungetokea?
17 Ibrahimu alijua kwamba, ili mwana atoke kwake na kwa mkewe Sara, ni lazima Mungu aingilie jambo hilo. Yeye alijua kwamba hakuwa na uwezo hata kidogo. Walakini hilo halikumfanya Ibrahimu akate tumaini. Mwana alipozaliwa kwake, Ibrahimu alijua kwamba ilikuwa katika njia ya mwujiza wa Yehova, akizirudisha nguvu zake za uzazi na zile za Sara. Jambo hili likatia imani yake nguvu zaidi. Sasa, alijua kwamba kupitia kwa mwana huyu uzao ungekuja. Yeye alifanya nini Mungu alipomwuliza amtoe dhabihu mwana huyo? Bila shaka jambo hilo lilimshangaza sana Ibrahimu. Angeweza kuona jambo hili kuwa gumu sana. Lakini yeye alijiacha kabisa mikononi mwa Yehova, kama inavyoelezwa katika kitabu cha Biblia cha Waebrania:
“Kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe, mzaliwa wa pekee; naam, yeye aliyeambiwa, Katika Isaka uzao wako utaitwa, akihesabu ya kuwa Mungu aweza kumfufua hata kutoka kuzimu; akampa tena kutoka huko kwa mfano.”—Ebr. 11:17-19.
YEHOVA ANAWEZA KUFANIKISHA NJIA YAKO
18, 19. Kwa kuona mambo hayo, kwa sababu gani inatupasa tupambane na kazi ngumu au matatizo kwa uhodari na kwa kutumaini?
18 Baada ya kusoma habari kama hiyo, inawezekanaje mmoja wetu afikiri, wakati wo wote, kwamba inatupasa tutegemee nguvu zetu, cheo au uwezo kutimiza jambo fulani katika utumishi wa Mungu? Inatia moyo sana na kuburudisha kujua kwamba tukimtumaini Yehova kabisa na kumtii, kama alivyofanya Ibrahimu, haitupasi kuhangaikia matokeo, hata kazi au gumu lililoko mbele yetu liwe kubwa namna gani. Huenda liwe ni lile la kuruzuku jamaa zetu. Au, mjane mwenye watoto wachanga huenda akawa na kazi nyingi akijaribu kuwalea katika “adabu na rekebisho la moyoni la Yehova.” (Efe. 6:4, NW) Au, huenda tatizo (gumu) likawa kupata wakati wa utumishi wa shambani. Wengine huenda wakaona wasiwasi kwenda mlango kwa mlango na kufundisha watu Biblia. Kumbuka kwamba ‘unayaweza mambo yote katika yeye akutiaye nguvu.’ (Flp. 4:13) Kumbuka kwamba Yehova Mungu na Yesu Kristo wanakusaidia. Unaweza kuvumilia ‘kama kwamba unamwona Yeye asiyeonekana,’ kama alivyofanya Musa alipokuwa na kazi kubwa sana ya kuwaongoza Waisraeli watumwa kutoka Misri, kupitia katika jangwa—kazi ambayo haingewezekana kwa uwezo wa binadamu. (Ebr. 11:27-29) Ilimpasa Musa ‘amkabidhi Yehova kazi yake yote.’ Kisha Yehova akaifanya. Bila shaka matatizo yetu si makubwa kama aliyokuwa nayo Musa.
19 Ndiyo sababu Biblia inatushauri “ombeni bila kukoma” na ‘dumuni katika sala.’ Katika njia hii tunaweza ‘kumkabidhi Yehova kazi zetu,’ tukiendelea kumtazamia aimarishe mipango yetu. (1 The. 5:17; Rum. 12:12) Kama alivyofanya Yesu, sisi vilevile tutalitakasa jina la Yehova na tukubali kwamba yeye ndiye aletaye matokeo, tukimsifu na kumtukuza kwa yale yanayotimizwa.
—Kutoka The Watchtower May 1, 1978.
[Picha katika ukurasa wa 22]
Mungu anafanya miili yetu ifanye kazi na chakula kikue bila sisi kujitaabisha sana
[Picha katika ukurasa wa 23]
Vivyo hivyo, Mungu ndiye aletaye ukuzi wa kiroho