Yehova Alinitegemeza Katika Gereza la Jangwa
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ISAIAH MNWE
Sikuwa nimehukumiwa mahakamani, nami sikuwa nimetenda uhalifu wowote. Hata hivyo, nililazimishwa kufanya kazi ngumu yenye jasho katika gereza lililokuwa katikati ya Jangwa la Sahara la Afrika lenye joto jingi. Jambo lililofanya hali iwe mbaya zaidi ni kwamba hakuna yeyote wa marafiki wangu waliojua nilikokuwa. Hilo lilitokea zaidi ya miaka minane iliyopita, katika kiangazi cha 1984. Acha nieleze jinsi nilivyokuja kuwa katika hali hiyo mbaya.
KATIKA 1958, nilipokuwa na miaka 12 tu, kaka yangu alikuja kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, baba na mama yangu waliendelea kuabudu vijimungu vya kikabila vya Jimbo la Abia, tulikoishi.
Katika 1968, nilijiunga na jeshi la Biafra. Nilipokuwa vitani, nilifikiri juu ya ule msimamo wa kutokuwamo wa Mashahidi wa Yehova, nikasali kwa Mungu anisaidie. Niliahidi kwamba ikiwa angeniruhusu niokoke vita hiyo, ningekuwa mmoja wa Mashahidi wake.
Baada ya vita hiyo nilitenda kwa haraka ili kutimiza ahadi yangu. Nilibatizwa katika Julai 1970 na mara hiyo nikachukua huduma ya wakati wote nikiwa painia. Baada ya wakati fulani niliwekwa rasmi kuwa mzee katika kundi la Kikristo. Upesi nilipokea mwaliko kutoka kwa ofisi ya tawi ya Naijeria ya kuchukua mgawo wa umishonari katika nchi ya karibu ambako kazi ya Mashahidi wa Yehova haikuwa imetambuliwa kisheria. Nilikubali, na kufikia Januari 1975, nilikuwa njiani, nikiwa na pasipoti yangu.
Kukamatwa
Katika 1978, nilipewa mgawo wa kuwazuru Mashahidi kotekote nchini. Kwa kuwa walikuwa wachache, nilisafiri sana, nikitembelea majiji yote kulikokuwa makundi, pamoja na maeneo kulikokuwa watu wenye kupendezwa. Mara nyingi nilihojiwa kwenye vituo vya polisi. Mara mbili, kwa muda wa siku nne kila wakati, nilifungwa na kuhojiwa juu ya kazi yetu.
Kisha, katika Juni 1984, tulipokuwa tukitayarisha kwa ajili ya huduma ya shambani Jumapili moja, ofisa mwenye urafiki alitujulisha kwamba polisi walikuwa wakijaribu kuwakamata Mashahidi wa Yehova. Juma moja baadaye Djagli Koffivi, anayetoka Togo, na mimi tukakamatwa. Tulipelekwa kwenye makao makuu ya polisi na kuamuriwa tujulishe majina ya Mashahidi wa Yehova wote katika jiji hilo. “Msipotupatia majina hayo,” wakasema, “hatutawaachilia.”
“Ninyi ndio polisi,” nikajibu. “Ni kazi yenu kuwapata watu mnaowatafuta. Mimi si mjumbe wenu.” Tulibishana kwa karibu muda wa dakika 30, na polisi wakatisha kutupiga. Hata hivyo, hatukuwapa majina ya akina ndugu zetu wa Kikristo. Kisha wakaamua kunyakua maktaba yangu kubwa ya vitabu vya marejezo vya Biblia.
Tulipokuwa Kifungoni
Baada ya kurudi kwenye stesheni ya polisi tukiwa na vitabu, Djagli na mimi tulivipakua. Tulipofanya hivyo, karatasi ilianguka kutoka katika Biblia yangu yenye chapa kubwa. Ilikuwa programu ya mkusanyiko wa wilaya iliyokuwa na majina ya wazee wa Kikristo wote katika nchi hiyo. Niliiokota upesi na kuishindilia mfukoni mwangu. Hata hivyo, polisi mmoja aliniona akaniamuru nimkabidhi. Bila shaka, nilihisi vibaya sana.
Karatasi hiyo iliwekwa kwenye meza katika chumba ambamo Djagli na mimi tulikuwa tukivileta vitabu. Nilipoingia nikiwa na mzigo wangu mwingine, nilikwenda mezani, nikaiokota karatasi hiyo, na kuishindilia mfukoni mwangu. Kisha nikasema kwamba nilitaka kujisaidia. Polisi mmoja akanisindikiza kwenye mahali pa vyoo. Nilipokuwa nimeingia na kufunga mlango, niliirarua-rarua karatasi hiyo na kuipitisha kwa maji ndani ya choo.
Polisi waliposikia kilichokuwa kimetukia, walikasirika sana. Lakini waliogopa kufanya chochote juu yalo, kwa kuwa wakubwa wao wangaliwashtaki juu ya kupuuza mambo kwa kunipa fursa ya kuiharibu karatasi hiyo. Baada ya kutuweka kifungoni kwa siku 17, inspekta mmoja wa polisi alituambia tukusanye vitu vyetu pamoja kwa sababu tulikuwa tunahamishwa kwingineko. Tuliweka mavazi kadhaa katika mfuko wa plastiki, na chini kabisa nikaweka Biblia ndogo ambayo mgeni mmoja alikuwa ametuletea kichini-chini.
Tuliweza kuwajulisha Mashahidi kwamba tulikuwa tunahamishwa lakini kwamba hatukujua ni wapi. Mapema asubuhi iliyofuata, Julai 4, 1984, inspekta huyo wa polisi alituamsha. Alitupekua-pekua, akituomba tuondoe mavazi kutoka katika mfuko na kuyaanika juu ya mikono yetu. Lakini nilipofikia shati ya mwisho, alisema ningeweza kuyarudisha mavazi mfukoni, kwa hiyo Biblia haikugunduliwa.
Gereza la Jangwa
Polisi walitupeleka kwa gari hadi uwanja wa ndege, ambako tulipanda ndege ya kijeshi. Muda wa saa kadhaa baadaye tuliwasili kwenye mji wenye karibu watu 2,000, ambako kuna gereza karibu. Ni mwendo wa karibu kilometa 650 kwa barabara hadi mji ulio karibu zaidi. Tulipelekwa kutoka kwa ndege hadi gereza na kukabidhiwa msimamizi wa gereza. Hakuna yeyote kati ya familia zetu wala marafiki wetu waliojua tulikokuwa tumepelekwa.
Mji tulikokuwa tumepelekwa ni oasisi (mahali penye maji jangwani) katika Sahara. Kuna vichaka, miti michache, na majengo yenye kuta za matope yaliyokauka. Maji yaweza kupatikana kwa kuchimba karibu meta moja au meta moja na nusu tu kuelekea chini. Hata hivyo, mwenyeji mmoja wa huko mwenye umri wa miaka 31 alituambia alikuwa ameona ikinyesha mara moja tu katika muda wa maisha yake! Na eneo hilo lilikuwa lenye joto jingi sana. Mfungwa mmoja alisema kwamba wakati mmoja kipimajoto katika makao ya wafungwa kilionyesha digrii 60 sentigredi! Upepo wenye nguvu ulivuruma daima, ukivurumisha mchanga ulioichoma ngozi na kuumiza macho.
Yeyote aliyewasili mahali hapo angetambua alikuwa kwenye kitovu cha adhabu iliyo mbaya zaidi nchini. Gereza lilizungukwa na kuta ndefu zilizotoa kadiri fulani ya himaya kutoka upepo na jua. Hata hivyo, kuta hazikuhitajiwa ili kuzuia kuponyoka, kwa kuwa hakukuwa mahali pa kwenda. Nje ya oasisi hiyo, hakukuwa hata mti mmoja, hakuna chochote cha kumpa kivuli mtu aliyetaka kuponyoka.
Kabla ya sisi kuingia, msimamizi wa gereza alitupekua-pekua. Alituambia tuondoe kila kitu kutoka mfuko wetu. Nilianza kuondoa shati zetu moja baada ya nyingine. Wakati kitu kilichobaki kilikuwa ile shati moja iliyokuwa ikiifunika Biblia, niliinua mfuko na kumwonyesha shati iliyokuwa ndani na kusema: “Hayo tu ndiyo walioturuhusu tuchukue.” Akiwa ameridhika, alisema tuendelee hadi kwenye ua wa gereza. Biblia ilikuwa ndicho kichapo pekee tulichokuwa nacho.
Maisha Gerezani
Kwa ujumla, kulikuwa karibu wafungwa 34. Walikuwa wahalifu wenye sifa mbaya zaidi na wa hatari zaidi nchini. Wengi walikuwa wauaji wa kimakusudi walioonwa kutoweza kugeuzwa. Sisi sote tulilala katika seli mbili kubwa zilizotenganishwa na msala uliokuwa wazi. Msala huo ulikuwa na pipa lisilokuwa na funiko lililotumiwa kama choo. Ingawa liliondolewa takataka na wafungwa kila asubuhi, ilionekana kana kwamba nzi wote jangwani walikuja huko kufurahia ubaridi na uchafu wa pipa hilo.
Chakula pekee tulichokuwa nacho kilikuwa mtama. Ulipondwa-pondwa na mfungwa mmoja, ukachemshwa, na kugawanywa kwenye sahani, ambazo baadaye ziliwekwa, moja kwenye kila mkeka wa kulalia wa mfungwa. Chakula hakikufunikwa. Kufikia wakati tuliporudi kutoka kazini, kulikuwako mamia ya nzi wakifunika kila sahani ya mlo wa mtama. Tulipoziinua sahani zetu, nzi walirukia mbali kwa kelele. Kwa siku mbili za kwanza, hatukula kitu. Mwishoni, katika siku ya tatu, baada ya kuwafukuza nzi na kuondoa tabaka la juu lililokauka, tulianza kula mlo wa mtama. Tulisali kwamba Yehova aweze kulinda afya yetu.
Tulifanya kazi chini ya jua, tukizivunja kuta za nyua za zamani za gereza na kujenga kuta mpya. Ilikuwa kazi ngumu sana. Tulifanya kazi ya jasho bila pumziko kutoka 12:00 za asubuhi hadi adhuhuri, tukala kitu, halafu tukafanya kazi mpaka 12:00 za jioni. Hakukuwa siku za kupumzika. Hatukuteseka tu kutokana na jua bali katika majira ya baridi tuliteseka kutokana na baridi. Na pia tuliteseka kutokana na walinzi wakatili.
Kuendelea Imara Kiroho
Djagli na mimi tulisoma Biblia kisiri, na tulizungumza pamoja juu ya yale tuliyojifunza. Hatukuweza kusoma waziwazi kwa sababu Biblia ingalichukuliwa na tungaliadhibiwa. Mfungwa mmoja ambaye nilikuwa nimeanzisha funzo la Biblia pamoja na yeye alikuwa na taa ya mkono aliyoshiriki pamoja na mimi. Mara nyingi niliamka saa saba au saa nane za usiku na kusoma mpaka karibu saa kumi na moja. Kwa njia hiyo niliweza kusoma Biblia nzima.
Tuliwahubiri wafungwa wale wengine, na mmoja wao akamwambia mlinzi mkuu juu yetu. Bila kutazamia, mlinzi huyo alimpa mfungwa huyo gazeti la Amkeni! alilokuwa nalo, na mfungwa huyo akalipitisha kwetu. Nililisoma tena na tena. Kusoma na kuhubiri kwetu kulitusaidia tuendelee kuwa imara kiroho.
Kuwasiliana na Marafiki Wetu
Hatukuruhusiwa kuandika au kupeleka barua. Hata hivyo, mtu mmoja aliyekuwa amekuwa mwenye urafiki alisema angenisaidia. Katika Agosti 20, karibu majuma sita baada ya kuwasili, niliandika barua mbili kisiri, moja kwenda kwenye ubalozi wa Naijeria na nyingine kwa marafiki Mashahidi. Nilizizika katika mchanga na kutia alama mahali hapo kwa jiwe kubwa. Baadaye rafiki yangu alikuja na kuzichimbua.
Majuma yalipita, nami sikupata habari yoyote. Polepole nikapoteza tumaini kwamba barua hizo hazikufika. Lakini zilikuwa zimepelekwa, na Mashahidi wenzetu wakaanza kupigania kuachiliwa kwetu. Wizara ya Shughuli za Nje ya Naijeria ilionyesha pia kupendezwa na jambo hilo na ikauliza serikali ya nchi nilikokuwa nimetiwa gerezani kwa nini ilikuwa imenitia katika gereza la jinsi hiyo.
Wakati uo huo, katika asubuhi ya Novemba 15, 1984, tulipelekwa kufanya usafishaji fulani. Walinzi walinipeleka kwenye choo cha shule ya upili ambacho watu walikuwa wakitumia kwa muda wa majuma kadhaa ijapokuwa kilikuwa kimezibika. Kilijaa kinyesi. Walinzi walisema kwamba kazi yangu ilikuwa ni kukisafisha. Vyombo nilivyokuwa navyo tu vilikuwa mikono yangu. Nilipokuwa nikifikiria kwa mshangao namna ya kushughulikia kazi hiyo yenye kuchukiza, mlinzi mkuu alikuja na kusema kwamba afisa wa wilaya wa eneo hilo alitaka kuniona.
Nilipowasili afisa wa wilaya alisema kwamba karibuni alikuwa ameongea na rais wa nchi hiyo, aliyekuwa amepata habari juu ya taabu yangu. Rais alieleza kwamba ikiwa ningetoa majina ya Mashahidi wa Yehova katika nchi hiyo, ningeachiliwa mara hiyo na ningeweza kuondoka kwenye ndege ifuatayo. Tena nikasema kwamba ikiwa walitaka Mashahidi wa Yehova, ilikuwa kazi ya polisi kuwatafuta. Afisa wa wilaya aliniambia kwamba nilipaswa kufikiria toleo lao kwa uzito sana. Angenipa siku nne au tano kulifikiria. Baada ya hayo niliambiwa niondoke, na walinzi wakanisindikiza kurudi kwenye gereza na kwa shukrani, si kurudi kwenye kile choo!
Baada ya siku tano afisa wa wilaya aliniita na kuniuliza lile nililokuwa nimeamua. Nilisema kwamba sababu pekee ya mimi kuwa katika gereza lao lilikuwa kwamba nilishuhudia Mungu wa kweli na kwamba sikuwa nimefanya jambo lolote baya. Nilieleza kwamba nilikuwa na pasipoti na ruhusa ya ukaaji ya kisheria. Hati zangu zote zilikuwa sahihi, na wakati wowote nilipokuwa nimesafiri kwenda kwenye jiji lolote, sikuzote niliwasiliana na polisi kuhakikisha kwamba kila jambo lilikuwa sawasawa. Kwa kuwa sikuwa nimetenda uhalifu wowote, niliuliza hivi: “Kwa nini ninaadhibiwa? Ikiwa sikutakiwa nchini, kwa nini sikuondolewa? Kwa nini nilipewa hukumu ya kuja mahali hapa?”
Niliongea kwa muda wa dakika 15. Nilipomaliza, niliombwa niandike yale niliyotoka tu kusema, nikaambiwa kwamba rais angepewa maelezo yangu. Nilipewa karatasi, nikaandika kurasa nne.
Kuachiliwa Hatimaye!
Sikupata habari zaidi kuhusu jambo hilo mpaka Januari 1985, karibu miezi saba baada ya mimi kufungwa gerezani. Katika pindi hiyo, mlinzi mkuu alikuja akaniuliza ikiwa nilikuwa nimeandika barua kwa ubalozi wa Naijeria. “Naam,” nikajibu.
“Kwa nini ulifanya hivyo? Kwa nini hukunijulisha?” akauliza.
Nilimwambia kwamba jambo hilo halikumhusu. Lakini nilimhakikishia kwamba sikuwa nimeandika jambo lolote dhidi yake, kwa kuwa hakuwa amehusika hata kidogo na kutumwa kwangu gerezani. “Hata mama yangu hajui niliko,” nikasema. Halafu akataka kujua namna ambayo nilikuwa nimeipeleka barua hiyo, lakini nilikataa kumwambia.
Siku ifuatayo walinzi walitayarisha Land-Rover wakaniambia kwamba Djagli na mimi tulikuwa tunahamishwa. Tuliletwa nje, tukavuliwa nguo, na kupekuliwa-pekuliwa. Mapema zaidi nilikuwa nimempa Biblia yule mfungwa niliyekuwa nikijifunza naye kwa sababu nilijua kwamba walinzi wangeichukua ikiwa wangenipata nayo. Mtu huyo alituambia kwamba wakati ambapo angeachiliwa, angekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Twaomba kwamba atafanya hivyo.
Muda mfupi baadaye, niliondoshwa nchini kwenda Naijeria, na katika Februari 1985, nilianza huduma yangu tena nikiwa mwangalizi asafiriye katika Naijeria. Tangu 1990, nimekuwa nikitumikia nikiwa mwangalizi wa wilaya katika Naijeria. Djagli sasa anatumikia akiwa Shahidi mwaminifu katika Côte d’Ivoire.
Kutokana na ono hilo, nimejifunza kwa kujionea mwenyewe kwamba Yehova Mungu aweza kututegemeza hata chini ya mbano mkali zaidi. Tena na tena tuliona mkono wake ukitulinda gerezani. Kuachiliwa kwetu kulinikazia kwamba Yehova hajui tu mahali ambapo watumishi wake wapo na yale yanayowapata bali pia ajua jinsi ya kuwakomboa kutoka katika jaribu.—2 Petro 2:9.