Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 5/1 kur. 4-7
  • Biblia—Mwongozo Ufaao kwa Mwanadamu wa Kisasa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Biblia—Mwongozo Ufaao kwa Mwanadamu wa Kisasa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Weka Akiba ya Hekima Lenye Mafaa
  • Kitabu Chenye Kutumika Kwa Maisha Ya Kisasa
    Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
  • Unaweza Kushindana na Matatizo ya Maisha
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Jinsi ya Kudhibiti Mfadhaiko
    Amkeni!—2010
  • Kujenga Maisha ya Furaha ya Jamaa
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 5/1 kur. 4-7

Biblia—Mwongozo Ufaao kwa Mwanadamu wa Kisasa

“Andiko lote limepuliziwa na Mungu na linaweza kutumiwa kwa faida . . . kwa kuongoza maisha za watu.”—2 Timotheo 3:16, “The Jerusalem Bible.”

ANDIKO hilo hueleza sababu ya msingi kwa nini Biblia lafaa katika siku yetu. Imepuliziwa na Mungu. Kwa kuwa Mungu ndiye aliyetuumba, hakuna ajuaye zaidi juu ya miili, akili, hisia, na mahitaji yetu kuliko yeye. Mfalme Mwisraeli Daudi alisema hivi wakati mmoja juu ya Yehova Mungu: “Macho yako yaliniona kabla sijakamilika; chuoni mwako ziliandikwa zote pia.” (Zaburi 139:16) Ikiwa Muumba wetu ajua mengi hivyo juu yetu, basi kwa kufuatana vizuri ni lazima kwa hakika shauri na mawaidha yake juu ya jinsi tunavyoweza kuwa na furaha na mafanikio maishani yastahili kuchunguzwa.

Ujuzi umeonyesha kwamba kanuni za Biblia zafaa na ni za kihalisi kwa siku yetu. Pia zataja mambo kimahususi. Vifuatavyo ni vielelezi vinne vinavyoonyesha faida za Biblia za kila siku.

Mahusiano ya Kibinadamu na Mwenendo wa Kibinafsi: Biblia huendeleza mpangilio mzuri wa adili za kibinafsi unaoweza kuongoza kwenye mahusiano yafaayo, na yenye mafanikio pamoja na wengine. Kwa kielelezo, taifa la Israeli liliamriwa hivi: “Usifanye kisasi, wala kuwa na kinyongo . . . bali umpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mambo ya Walawi 19:18) Ingawa hatumo chini ya sheria ya Kiisraeli, kufuata kanuni zayo za Kibiblia kwaweza kutusaidia kuwa na amani pamoja na wanadamu wenzetu. Kwa kielelezo, ebu wazia ni matatizo mengi kadiri gani ambayo ingeweza kusuluhishwa ikiwa kila mtu angejaribu kusitawisha zile sifa za kiroho zinazopatikana kwenye Wagalatia 5:22, 23: “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo hayo hakuna sheria.”—Linganisha Warumi 8:5, 6.

Kwa kusikitisha, mibano ya maisha inapoongezeka, mara nyingi mkazo na mabishano hutokea. Katika hali hizo, kutumia maneno ya onyo yanayopatikana kwenye Mithali 29:11 kungeweza kutuzuia tusipatwe na matatizo mengi. “Mpumbavu hudhihirisha hasira yake yote; bali mwenye hekima huizuia na kuituliza.”—Linganisha Mithali 15:1; Mathayo 7:12; Wakolosai 3:12-14.

Hilo ni shauri zuri—lakini je, lafanya kazi katika maisha halisi? Chukua kisa cha mwanamume mmoja katika Ufaransa aliyekuwa na tatizo zito la hasira yake. Mara nyingi sana alikuwa akijipata matatani, hata gerezani, kwa ajili ya kuhusika katika kupigana. Hali ilikuwa mbaya zaidi kwa sababu alikuwa bondia stadi. Katika pindi moja ugomvi ulitokea kati ya mwanamume huyo na baba yake. Kabla ya yeye kung’amua chochote, alikuwa amemwangusha baba yake kwa ngumi moja. Hilo lilifuatwa na mtengano wenye uchungu katika uhusiano wao.

Kwa wakati huo, mwanamume huyo alikutana na Mashahidi wa Yehova akaanza kujifunza kanuni za Biblia. Hilo lilimsukuma achunguze kwa uzito njia aliyokuwa akijiendesha kuelekea wengine. Kwa jitihada nyingi mwenendo wake wa kibinafsi ulianza kubadilika, naye akawa mwenye amani zaidi. Halafu siku moja mwanamume huyo alirudi kwa baba yake ili kupatanisha mambo. Baba yake alivutiwa sana na mabadiliko ambayo mwana wake alikuwa amefanya hivi kwamba uhusiano wao ulirudishwa.

Hicho ni kimoja kati ya vielelezo vingi vinavyoshuhudiza ukweli wa maneno haya ya mtume Paulo: “Maana Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili . . . tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.”—Waebrania 4:12.

Maisha ya Familia: Je! familia yako ina furaha? Familia nyingi hazina furaha. “Jambo la kwamba maisha ya familia ukiwa mpango umo katika hali ya kutishwa ni la hakika sasa,” laeleza The Natal Witness, gazeti la habari la Afrika Kusini, likiongeza kwamba “watoto wa leo wanazaliwa ndani ya mapinduzi makubwa ya kijamii.”

Hata hivyo, Biblia imejaa pomoni shauri lifaalo ambalo limekusudiwa kusaidia familia zifanikiwe hata wakati matatizo yanapotokea. Kwa kielelezo, kuhusu daraka la waume, Biblia husema hivi: “Imewapasa waume kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” Mume anapotimiza takwa hilo, ni jambo la kupendeza kwa mke wake kumtendea vilevile kwa kuwa na ‘staha kwa mumewe.’ (Waefeso 5:25-29, 33) Uhusiano kati ya wazazi na watoto umeelezwa katika Waefeso 6:4: “Nanyi, akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana [Yehova, NW].” Hilo, kisha, latokeza hali ya familia inayoifanya iwe rahisi zaidi kwa watoto kuifuata amri ya Biblia na kuwa watiifu kwa wazazi wao.—Waefeso 6:1.

Habari inayotangulia ni kisehemu tu cha maelezo ya Biblia juu ya maisha ya familia. Kwa kuitikia mwongozo wa Mungu, wengi wamepata mafanikio na huona furaha nyumbani. Edward, baba wa watoto wawili, aeleza manufaa alizofurahia kwa kutumia kanuni za Biblia. “Ndoa yangu ilikuwa ikivunjika,” yeye akumbuka. “Sikuwa na wakati wa kuwa na uhusiano wa maana pamoja na watoto wangu. Jambo pekee lililotuleta pamoja ni kule kutumia kwetu yale ambayo Biblia husema juu ya maisha ya familia.”—Mithali 13:24; 24:3; Wakolosai 3:18-21; 1 Petro 3:1-7.

Afya ya Kiakili, Kimwili, na Kihisiamoyo: Utafiti umeonyesha kwamba afya ya mtu ya kimwili huhusika, kwa kadiri fulani, na hali ya afya yake ya kiakili na ya kihisiamoyo. “Ishara za kawaida za mkazo,” yasema The World Book Encyclopedia, “zinatia ndani ongezeko la pigo la moyo, msukumo wa damu wa juu zaidi, mkazo wa misuli, mshuko wa kiakili, na kutoweza kukazia fikira jambo lolote.” Hata hivyo, wengine huamini kwamba kuchochea matendo ya jeuri ni njia ya kutuliza mkazo. “Kupigana ngumi kwaweza kuwa njia nzuri sana ya kupunguza mkazo,” ladai gazeti la habari la Afrika Kusini, The Star. Linanukuu maneno haya ya mshauri mmoja wa afya ya kimwili Jannie Claasens: “Ikiwa mwanamke amekuwa na siku yenye kufadhaisha sana, yeye aweza kuondosha mkazo wake kwa kupigapiga fuko [lile la kufanyia mazoezi ya kupiga ngumi].”

Lakini, je, kusingefaa zaidi kujifunza namna ya kukabiliana na kisababishi cha msingi kinacholeta hali ya kufadhaika? Katika jarida Stress—The Modern Scourge, Dakt. Michael Slutzkin asema kwamba “kutambua mkazo . . . ni jambo la maana, kwa sababu visababishi vingi vyaweza kusuluhishwa.” Yeye aongeza kwamba “kudhibiti mkazo . . . kwaweza hata kuchochea utaratibu wa uponyaji katika hali mbalimbali.”

Biblia hueleza njia yenye matokeo sana ambayo kwayo mkazo waweza kudhibitiwa: “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno . . . haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Kudhibiti mkazo katika njia hiyo kuna faida nyingi—hasa za kimwili. Mithali moja ya Biblia husema hivi: “Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili.” (Mithali 14:30) Mithali nyingine hutaarifu hivi: “Moyo uliochangamka ni dawa nzuri; bali roho iliyopondeka huikausha mifupa.”—Mithali 17:22.

Wakijaribu kuponyoka mkazo na mbano, wengi hutegemea tumbaku, kileo, dawa za kulevya. Uharibifu unaosababishwa na uzoevu huo umethibitishwa vizuri. Hata hivyo, sikuzote Biblia imependekeza kujiweka safi kutoka kwa “uchafu wote wa mwili.” (2 Wakorintho 7:1; linganisha Mithali 23:29-35.) Kwa hakika, kuepuka mazoea hayo mabaya ni ulinzi ufaao katika ulimwengu wa leo.

Kazi, Fedha, na Kufuata Yaliyo ya Haki: Uvivu haunufaishi kamwe. “Mtu mvivu hataki kulima wakati wa baridi; hivyo wakati wa mavuno ataomba, hana kitu,” yasema Mithali 20:4. Kwa upande ule mwingine, kazi ngumu hunufaisha. “Mwibaji asiibe tena,” lataarifu Waefeso 4:28. Andiko hilo laongeza kwamba ni afadhali mtu afanye “juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe, apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji.”—Linganisha Mithali 13:4.

Je! ulijua kwamba kanuni za Biblia zaweza kutumiwa hata kuhusu mahusiano kazini? Wafanyakazi, kama vile “watumwa” wa nyakati za Biblia, hufanya vema “[kuwatii] hao ambao kwa mwili ni bwana [zao], katika mambo yote.” Kwa upande ule mwingine, waajiri, au ‘mabwana,’ wanapaswa ‘kuwapa waajiriwa wao yaliyo haki na ya adili.’—Wakolosai 3:22-24; 4:1; linganisha 1 Petro 2:18-20.

Mengi husemwa katika Biblia juu ya shughuli za kibiashara zenye kufuata yaliyo ya haki. Ingawa kwa kusikitisha, kufuata yaliyo ya haki kunakosekana leo, mara nyingi kufuata yaliyo ya haki hutambuliwa na kuthaminiwa kuwa sifa yenye kutamanika. Biblia hukazia hiyo. Yesu alisema hivi wakati mmoja: “Aliye mwaminifu katika lililo dogo sana, huwa mwaminifu katika lililo kubwa pia; na aliye dhalimu katika lililo dogo, huwa dhalimu katika lililo kubwa pia.”—Luka 16:10; linganisha Mithali 20:10; 22:22, 23; Luka 6:31.

Katika nchi moja ya Afrika, wizi na shughuli nyingi za magendo zilikuwa zikitendeka katika kiwanda kimoja cha almasi. Iliamuliwa kwamba mtu tofauti awekwe ili kusimamia kiwanda hicho. Mawaziri wa serikali waliombwa watoe majina ya wale ambao walifikiri wangeweza kufaa cheo hicho. Wakati baraza la mawaziri lilipokutana kufanya uamuzi, majina hayo yalifutwa moja baada ya jingine, kwa sababu hasa ya kufanya magendo. Mwishoni, walifikia jina la mwisho kwenye orodha hiyo—yule aliyekuwa amechaguliwa na rais.

“Lakini yeye si mshiriki wa chama!” akapinga waziri mmoja.

Rais alijibu kwamba hicho hakikuwa cheo cha kisiasa.

“Yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova,” akasema mwingine.

“Na hiyo ndiyo sababu anapata kazi hiyo,” akasema rais. Kisha akaongeza hivi: “Tunajua wao ni wenye kufuata yaliyo ya haki, na huyo ndiye mtu tunayehitaji. Tunajua twaweza kumtumaini.”

Ndiyo, mara nyingi wale wanaotumia kanuni za Biblia hupata kwamba hiyo ni kwa faida yao hata katika ulimwengu wa leo.

Weka Akiba ya Hekima Lenye Mafaa

Tumeona kisehemu kidogo tu cha maana ya “kupata kumjua Mungu.” (Mithali 2:1-9) Wingi wa shauri lifaalo, na lenye mafaa sana unapatikana katika Biblia. Kanuni zinazohusu usafi, bidii ya kazi, mawasiliano, ngono, talaka, kulipa kodi, kushughulika na tofauti za kiutu, na kukabiliana na umaskini ni baadhi tu ya sehemu za maisha zinazozungumziwa na Biblia. Mamilioni watashuhudia kwamba tofauti kati ya kufaulu na kutofaulu maishani mwao imetegemea kadiri ambayo wametumia kanuni za Biblia.

Ingawa faida za Biblia za wakati uu huu zinahakikishiwa, Biblia hutoa pia tumaini la manufaa nyingi za muda mrefu. Kwa kielelezo, Biblia huahidi kwamba visababishi vya msingi vya maumivu na kuteseka katika ulimwengu wa leo vitarekebishwa hivi karibuni kupitia kujiingiza kwa Mungu.—Danieli 2:44; 2 Petro 3:11-13; Ufunuo 21:1-5.

Kwa hiyo, tunakutia moyo ujifunze mengi kadiri uwezavyo juu ya Biblia. Ikiwa huna nakala, hakikisha unapata moja. Watangazaji wa gazeti hili watafurahi kukusaidia. Kama vile wengine wengi wamenufaika kwa kutumia yale madokezo yafaayo kutoka kwa Biblia, wewe pia waweza kusaidiwa kuthamini thamani ya Neno la Mungu, sasa na katika wakati ujao pia.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Biblia ni mwongozo ufaao kwa ajili ya kufanya maisha ya familia yawe yenye furaha

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki