‘Waite Wazee wa Kundi’
“Je! yuko mgonjwa kati yenu? Anapaswa kuwaita wazee wa kanisa [kundi, NW].”—YAKOBO 5:14, Habari Njema kwa Watu Wote.
1, 2. (a) Watumishi wa Yehova hujipata wenyewe katika hali gani ya hatari, na huenda wakahisije? (b) Ni maswali gani yanayohitaji majibu sasa?
HIZI ndizo siku “zilizo ngumu kushughulika nazo.” Watu wanatenda kwa ubinafsi, kwa njia ya kuonyesha upendo wa vitu vya kimwili, kwa majivuno, mara nyingi wakichochea ghasia katika “siku [hizi] za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5, NW) Tukiwa Wakristo wanaoishi katika mfumo wa mambo wa sasa ulio mbovu, tunajipata wenyewe tukitishwa na hatari kubwa tatu: Shetani Ibilisi, ulimwengu wa ainabinadamu isiyomhofu Mungu, na mielekeo yetu wenyewe yenye dhambi iliyoridhiwa.—Warumi 5:12; 1 Petro 5:8; 1 Yohana 5:19.
2 Tukiwa twatishwa na hatari hizo, huenda nyakati nyingine tukahisi tumeshindwa. Basi, tunaweza kupata wapi utegemezo wa kutusaidia kuvumilia kwa uaminifu? Tunaweza kumgeukia nani ili kupata mwongozo tunapokabiliwa na maamuzi kuhusu utendaji wetu wa Kikristo na ibada yetu?
Msaada Wapatikana
3. Tunaweza kupata uhakikishio wenye kufariji kutoka kwa nani, na kwa jinsi gani?
3 Kujua kwamba Yehova ndiye Chanzo cha nguvu zetu hutupa sisi uhakikishio wenye faraja. (2 Wakorintho 1:3, 4; Wafilipi 4:13) Mtunga zaburi Daudi, aliyepata msaada wa kimungu, alijulisha hivi: “Umkabidhi BWANA [Yehova, NW] njia yako, pia umtumaini, naye atafanya.” “Umtwike BWANA [Yehova, NW] mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 37:5; 55:22) Tunaweza kushukuru kama nini kwa ajili ya utegemezo huo!
4. Petro na Paulo pia wanatoaje faraja?
4 Tunaweza pia kupata faraja kutokana na kujua kwamba hatuko peke yetu tunapokabili majaribu na hatari. Mtume Petro aliwahimiza Wakristo wenzake hivi: “Mpingeni huyo [Shetani Ibilisi], mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani.” (1 Petro 5:9) Kwa hakika, Wakristo wote hutamani kusimama thabiti katika imani. Ni kweli, huenda mara nyingi tukahisi tukiwa ‘tumebanwa pande zote,’ (NW) kama vile mtume Paulo alivyohisi. Hata hivyo, yeye ‘hakusongwa.’ Kama vile yeye, huenda sisi tukaona shaka “bali hatukati tamaa.” Hata tukinyanyaswa, “hatuachwi.” Ikiwa “twatupwa chini,” “hatuangamizwi.” Kwa hiyo, “hatulegei.” Tunajitahidi “tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana.” (2 Wakorintho 4:8, 9, 16, 18) Tunaweza kufanyaje hivyo?
5. Yehova huandaa msaada gani wenye sehemu tatu?
5 Yehova, “Msikiaji wa sala,” huandaa msaada wenye sehemu tatu. (Zaburi 65:2, NW; 1 Yohana 5:14) Kwanza, yeye huandaa mwelekezo kupitia Neno lake, Biblia, lililopuliziwa. (Zaburi 119:105; 2 Timotheo 3:16) Pili, roho takatifu yake hutupa sisi nguvu za kufanya mapenzi yake. (Linganisha Matendo 4:29-31.) Na tatu, tengenezo la Yehova la kidunia huwa tayari kutusaidia. Ni lazima tufanye nini ili kupokea msaada?
“Zawadi Katika Wanaume”
6. Yehova aliandaa msaada gani huko Tabera, na kwa jinsi gani?
6 Tukio moja katika siku ya nabii Musa hutusaidia tuthamini hangaiko la Yehova lenye upendo katika kuwaandalia watumishi Wake msaada. Hilo lilitukia Tabera, linalomaanisha “kuchoma; uteketezo; mwako wa moto.” Kwenye mahali hapo pa jangwa la Sinai, Mungu alisababisha moto uwake dhidi ya Waisraeli waliokuwa wakilalamika. “Mkutano wa wafuasi” uliokuwa umeandamana na watu wa Israeli kutoka Misri ulikuwa umejiunga nao katika kuonyesha kutokuridhika na ugavi wa chakula uliokuwa umeandaliwa kimungu. Akiona hasira ya Mungu na kuhisi kuwa ameshindwa na lile daraka juu ya watu na mahitaji yao, Musa alipaza sauti hivi: “Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda. Na kama ukinitenda hivi, nakuomba uniulie mbali, kwamba nimepata fadhili mbele ya macho yako; nami nisiyaone haya mashaka yangu.” (Hesabu 11:1-15) Yehova aliitikiaje? Aliweka “watu sabini, miongoni mwa wazee wa Israeli” akaweka roho yake juu yao ili waweze kushiriki ifaavyo ile kazi ya usimamizi pamoja na Musa. (Hesabu 11:16, 17, 24, 25) Kukiwa na wanaume hao waliostahili, msaada ulipatikana kwa urahisi zaidi kwa Waisraeli na lile “kundi kubwa la watu waliochangamana nao.”—Kutoka 12:38.
7, 8. (a) Yehova aliandaaje “zawadi katika namna ya wanaume” katika Israeli wa kale? (b) Paulo alifanya matumizi gani ya karne ya kwanza ya Zaburi 68:18?
7 Baada ya Waisraeli kuwa katika lile Bara Lililoahidiwa kwa miaka mingi, Yehova alipaa Mlima Sayuni kitamathali akafanya Yerusalemu jiji kuu la ufalme halisi ambao mfalme wao alikuwa Daudi. Akimsifu Mungu, “Mweza Yote,” (NW) Daudi aliinua sauti yake kuimba: “Wewe umepaa juu, umeteka mateka, umepewa vipawa katikati ya wanadamu [zawadi katika namna ya wanaume, NW].” (Zaburi 68:14, 18) Kwa kweli, wanaume waliotekwa nyara wakati wa ushindi wa Bara Lililoahidiwa waliweza kutumiwa kuwasaidia Walawi na wajibu wao mbalimbali.—Ezra 8:20.
8 Katika karne ya kwanza W.K., mtume Mkristo Paulo alielekeza fikira kwenye utimizo wa kiunabii wa maneno ya mtunga zaburi. Paulo aliandika hivi: “Kila mmoja wetu alipewa neema kwa kadiri ya kipimo cha kipawa chake Kristo. Hivyo husema, Alipopaa juu aliteka mateka, akawapa wanadamu vipawa [akatoa zawadi katika wanaume, NW]. Basi neno hilo, Alipaa, maana yake nini kama siyo kusema kwamba yeye naye alishuka mpaka pande zilizo chini za nchi? Naye aliyeshuka ndiye yeye aliyepaa juu sana kupita mbingu zote, ili avijaze vitu vyote.” (Waefeso 4:7-10) Nani huyo “aliyeshuka”? Si mwingine ila mwakilishi wa Yehova, Daudi Mkuu Zaidi na Mfalme wa Kimesiya, Yesu Kristo. Yeye ndiye aliyefufuliwa na Mungu akakwezwa kwenye “cheo kikubwa.”—Wafilipi 2:5-11, NW.
9. (a) Ni nani waliokuwa zawadi katika wanaume wa karne ya kwanza? (b) Ni nani walio zawadi katika wanaume wa ki-siku-hizi?
9 Basi, “zawadi katika wanaume” (au, “zinazotia ndani wanaume”) ni nani? Paulo aeleza kwamba Mwakilishi Mkuu wa Mungu “[alitoa] wengine kuwa mitume; na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti; na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe.” (Waefeso 4:11, 12) Wafuasi wote wa Kristo waliotumikia wakiwa mitume, manabii, wainjilisti, wachungaji, na waalimu walifanya hivyo chini ya mwelekezo wa kitheokrasi. (Luka 6:12-16; Matendo 8:12; 11:27, 28; 15:22; 1 Petro 5:1-3) Katika siku yetu, wazee wastahilio kiroho wanaowekwa na roho takatifu hutumikia wakiwa waangalizi katika makundi yapata 70,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Wao ndio zawadi zetu katika wanaume. (Matendo 20:28) Upanuzi wa ulimwenguni pote wa kazi ya kuhubiri Ufalme ukiendelea kasi, ndugu wengi zaidi ‘wanajitahidi kufikia’ na kuchukua madaraka yanayohusiana na “cheo cha mwangalizi.” (1 Timotheo 3:1, NW) Wanapowekwa, wao pia huwa zawadi katika wanaume.
10. Usimulizi wa Isaya wa “wakuu” hufaanaje na daraka la wazee Wakristo leo?
10 Wazee hao Wakristo, au zawadi katika wanaume, hufaana na ule usimulizi ambao nabii Isaya alitoa alipokuwa akitabiri juu ya daraka la “wakuu,” wale wasimamizi chini ya utawala wa Ufalme. Ni lazima kila mmoja awe “kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” (Isaya 32:1, 2) Hilo lafunua jinsi usimamizi wenye upendo wa watu hao waliowekwa upasavyo kuwa wenye kuunga mkono. Unaweza kunufaikaje kutokana nao kwa kadiri kubwa zaidi?
Kuchukua Hatua ya Kwanza
11. Tunaposhuka kiroho, tunaweza kupokeaje msaada?
11 Mtu anayezama majini hutoa vilio vya kuomba msaada kisilika. Hakuna kusita-sita. Uhai unapokuwa hatarini, hakuna anayehitaji kuchochewa kuomba msaada. Je! Mfalme Daudi hakumwomba Yehova msaada kwa kurudia-rudia? (Zaburi 3:4; 4:1; 5:1-3; 17:1, 6; 34:6, 17-19; 39:12) Tunaposhuka kiroho, labda tukizama katika hali ya kukata tamaa, sisi vilevile humgeukia Yehova katika sala na kumwomba atuongoze kwa roho yake takatifu. (Zaburi 55:22; Wafilipi 4:6, 7) Tunatafuta faraja kutoka katika Maandiko. (Warumi 15:4) Tunaendea vichapo vya Kikristo vya Watch Tower Society ili kupata shauri lenye mafaa. Mara nyingi hilo hutusaidia kusuluhisha matatizo yetu wenyewe. Lakini ikionekana kana kwamba twashindwa na magumu, tunaweza pia kutafuta shauri kutoka kwa wazee wa kundi waliowekwa. Kwa kweli, kuna nyakati nyingi tunapohitaji kwelikweli ‘kuwaita wazee.’ Kwa nini tuwaite wazee Wakristo? Wanaweza kuwasaidiaje wale wenye uhitaji wa msaada wa kiroho?
12-14. (a) Ni nini mwendo wenye hekima wa kufuata mtu anapokuwa mgonjwa? (b) Kulingana na Yakobo 5:14, Wakristo “wagonjwa” wanashauriwa kufanya nini? (c) Yakobo 5:14 linarejeza kwenye ugonjwa wa aina gani, na kwa nini wajibu hivyo?
12 Tunapokuwa wagonjwa, sisi hupumzika ili kuzipa nguvu za mwili za kuponya fursa ya kutenda. Lakini ugonjwa wetu ukiendelea, sisi hutafuta kwa hekima msaada ustahilio wa kitiba. Je! tusifanye vivyo hivyo tukiwa dhaifu kiroho?
13 Ona lile mwanafunzi Yakobo analotushauri kuhusu hilo. Yeye asema hivi: “Je, yuko mgonjwa kati yenu? Anapaswa kuwaita wazee wa kanisa [kundi, NW], nao watamwombea na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana [Yehova, NW].” (Yakobo 5:14, HNWW) Yakobo arejezea ugonjwa wa aina gani? Wafafanuzi wengine wa Biblia hukata maneno kwamba huo ni ugonjwa wa kimwili, wakitoa sababu kwamba kupaka mafuta kulikuwa zoea la kawaida la kitiba katika siku hiyo. (Luka 10:34) Wao huamini pia kwamba Yakobo alikuwa akifikiria uponyaji wa kimuujiza kupitia zawadi ya kuponya. Lakini muktadha huonyesha nini?
14 ‘Kujisikia vema’ kunatofautishwa na ‘kuteseka vibaya.’ Hilo ladokeza kwamba Yakobo alikuwa akizungumzia ugonjwa wa kiroho. (Yakobo 5:13, NW) “Wazee wa kanisa [kundi, NW],” si madaktari au hata wale waliokuwa na zawadi ya kuponya ya kimuujiza, walipaswa kuitwa. Nao walipaswa kufanya nini? Yakobo alisema hivi: “Nao wamwombee. . . . Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule.” (Yakobo 5:14, 15; linganisha Zaburi 119:9-16.) Jambo linalothibitisha kabisa kwamba Yakobo anarejezea ugonjwa wa kiroho ni kwamba yeye atia moyo ungamo la dhambi kuhusiana na kule kuponywa kunakotazamiwa. Yeye aandika hivi: “Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana, mpate kuponywa.” Ikiwa dhambi nzito ndiyo kisababishi cha ugonjwa wa kiroho, yule aliye mgonjwa aweza kutazamiwa kuponywa ikiwa tu aitikia ifaavyo himizo lenye msingi wa Neno la Mungu, kutubu, na kugeuka kutoka kwenye mwendo wake wenye dhambi.—Yakobo 5:16; Matendo 3:19.
15. Ni hatua ya aina gani inayopendekezwa kwenye Yakobo 5:13, 14?
15 Kuna jambo jingine la kuonwa kutokana na shauri ambalo Yakobo atoa. Anapoteseka vibaya, Mkristo anapaswa “aombe.” Ikiwa anajisikia vema, “na aimbe zaburi.” Kila hali—iwe mtu anateseka vibaya iwe anajisikia vema—inahitaji hatua ichukuliwe. Sala inahitajiwa kwenye upande mmoja, semi za furaha kwenye upande ule mwingine. Kwa hiyo, basi, tunapaswa kutazamia nini wakati Yakobo anapouliza hivi: “Je, yuko mgonjwa kati yenu?” Tena yeye apendekeza hatua ifaayo ichukuliwe, naam, kuchukua hatua ya kwanza. “Anapaswa kuwaita wazee wa kanisa [kundi, NW].”—Zaburi 50:15; Waefeso 5:19; Wakolosai 3:16.
Namna “Wazee” Husaidia
16, 17. Wazee hutusaidiaje kutumia kanuni za Biblia?
16 Nyakati nyingine ni vigumu kwetu kujua namna ya kutumia kanuni za Biblia kuhusu hali zetu za kibinafsi. Wazee Wakristo wanaweza kuthibitika kuwa chanzo cha msaada chenye thamani kubwa sana katika jambo hilo. Kwa mfano, wao wanamwombea yule aliye mgonjwa kiroho na ‘kumpaka mafuta katika jina la Yehova’ kwa kutumia kwa ustadi maagizo yenye kufariji kutoka katika Neno la Mungu. Hivyo wazee wanaweza kuchangia sana kuponywa kwetu kiroho. (Zaburi 141:5) Mara nyingi, jambo tunalohitaji tu ni uhakikisho kwamba tunasababu kwa njia ifaayo. Kuzungumzia mambo pamoja na mzee Mkristo mwenye ujuzi kutaimarisha azimio letu kufanya lililo sawa.—Mithali 27:17.
17 Wanapoitwa kufanya ziara, wazee Wakristo wanahitaji ‘kusema kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo.’ (NW) Pia ‘watawatia moyo walio dhaifu, na kuwavumilia watu wote.’ (1 Wathesalonike 5:14) Uhusiano huo, wa karibu sana, wenye uelewevu kati ya “wazee” na “walio dhaifu” huongeza uwezekano wa kurudishiwa kabisa afya ya kiroho.
Daraka la Kibinafsi na Sala
18, 19. Wazee Wakristo wana daraka gani kuhusiana na Wagalatia 6:2, 5?
18 Ni lazima wazee Wakristo wachukue daraka lao kuelekea kundi la Mungu. Ni lazima wawe wenye kuunga mkono. Kwa mfano, Paulo alisema hivi: “Ndugu zangu, mtu akighafilika katika kosa lo lote, ninyi mlio wa Roho mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho ya upole, ukijiangalia nafsi yako usije ukajaribiwa wewe mwenyewe. Mchukuliane mizigo [yenye kulemea, NW] na kuitimiza hivyo sheria ya Kristo.” Mtume aliandika hivi pia: “Kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe.”—Wagalatia 6:1, 2, 5.
19 Tunaweza kuchukulianaje mizigo yenye kulemea na hata hivyo kulichukua furushi letu wenyewe? Tofauti katika maana ya yale maneno ya Kigiriki ambayo yametafsiriwa “mizigo yenye kulemea” na “furushi” ndiyo hutoa jibu. Mkristo akipatwa na ugumu wa kiroho unaomlemea sana, wazee na waamini wenzake wengine wangemsaidia, hivyo wakimsaidia kuchukua “mizigo” yake yenye kulemea. Hata hivyo, mtu huyo mwenyewe anatazamiwa kuchukua “furushi” lake mwenyewe la daraka kwa Mungu.a Wazee huchukua kwa furaha “mizigo yenye kulemea” ya ndugu zao kupitia kitia-moyo, shauri la Kimaandiko, na sala. Hata hivyo, wazee hawaondoi “furushi” letu la kibinafsi la daraka la kiroho.—Warumi 15:1.
20. Kwa nini sala isipuuzwe?
20 Sala ni muhimu na haipasi ipuuzwe. Lakini Wakristo wengi walio wagonjwa kiroho huona kusali kuwa kugumu. Wazee wanapotoa sala za imani kwa ajili ya mtu aliye mgonjwa kiroho, kusudi ni nini? “Bwana [Yehova, NW] atamwinua,” kama vile kutoka katika hali ya kukata tamaa, na atamwimarisha kufuatia mwendo wa kweli na uadilifu. Mkristo aliye mgonjwa kiroho huenda akawa na mtazamo usiofaa lakini si lazima iwe ametenda dhambi nzito, kwani Yakobo asema hivi: “Hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.” Shauri la Kimaandiko la wazee pamoja na sala yenye bidii nyakati nyingine humchochea yule mtu aliye dhaifu kiroho aungame dhambi nzito ambazo huenda ikawa alifanya na kudhihirisha roho ya kutubu. Kisha hilo, hutokeza msamaha kwa upande wa Mungu.—Yakobo 5:15, 16.
21. (a) Kwa nini Wakristo wengine husita kuwaita wazee? (b) Ni jambo gani litakalochunguzwa katika makala ifuatayo?
21 Wakikabili ugumu wa kuyatunza misongamano ya wapya wanaoingia kundi la Kikristo, wazee wenye kudhamiria wana mengi ya kufanya katika kuandaa uangalizi wa kutosha. Kwa kweli, zawadi hizo katika wanaume ni uandalizi mzuri kutoka kwa Yehova wa kutusaidia kuvumilia katika nyakati hizi za hatari. Hata hivyo, Wakristo wengine husita kuomba msaada wao, wakifikiri kwamba ndugu hawa ni wenye shughuli mno au wanalemewa kupita kiasi na matatizo. Makala ifuatayo itatusaidia tuthamini kwamba wanaume hao wanafurahia kutoa msaada, kwani wao hutumikia kwa hiari wakiwa waangalizi wa chini katika kundi la Kikristo.
[Maelezo ya Chini]
a A Linguistic Key to the Greek New Testament, cha Fritz Rienecker, chafasili phor·tiʹon kuwa “mzigo ambao mtu hutazamiwa kuchukua” na chaongeza hivi: “Lilitumiwa likiwa neno la kijeshi la kifurushi cha mtu au vifaa vya askari-jeshi.”
Ungejibuje?
◻ Tunapohitaji kusaidiwa, Yehova huandaa msaada gani wenye sehemu tatu?
◻ Ni nani walio zawadi katika wanaume wa ki-siku-hizi?
◻ Tunapaswa kuwaita wazee wakati gani?
◻ Tunaweza kutazamia msaada gani kutoka kwa wazee Wakristo?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Je! wewe hufurahia manufaa za kiroho za sala, funzo la Biblia, na msaada kutoka kwa wazee Wakristo?