Iweni Timamu Katika Akili—Mwisho U Karibu
“Mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili [timamu katika akili, NW], mkeshe katika sala.”—1 PETRO 4:7.
1. (a) Kiongozi mmoja wa kidini pamoja na wafuasi wake walikatishwa tamaa namna gani? (b) Kwa sababu matazamio fulani hayajatimizwa, ni maswali gani yanayoweza kuulizwa?
NILIPOKEA mwito kutoka kwa Mungu katika sala ya mwisho ya usiku huu. Alisema watu 116,000 wangepaa kwenda mbinguni na makaburi ya waamini million 3.7 ambao wamekufa yatafunguka kuelekea mbingu.” Ndivyo alivyosema kiongozi mmoja wa Mission for the Coming Days (Utume wa Siku Zijazo) jioni ya Oktoba 28, 1992, siku yao ya kutozwa hesabu iliyotolewa unabii. Hata hivyo, Oktoba 29 ilipofika, hakuna hata mtu mmoja aliyekuwa ameenda mbinguni, na hakuna makaburi ya wafu yaliyokuwa yamefunguka. Badala ya kunyakuliwa upesi kwenda mbinguni kimwili, wale waamini wa siku ya uharibifu katika Korea waliona tu siku nyingine ikipambazuka. Wakati uliowekwa wa siku za uharibifu umekuja na kwenda, lakini wenye kuutangaza wakati huo wa uharibifu wanaendelea bila hofu. Wakristo wanapaswa kufanya nini? Je! waache kuamini kwamba mwisho unakaribia kwa kasi?
2. Ni nani aliyewaambia mitume juu ya siku ya hukumu ya wakati ujao, nao walipata kujifunza hilo chini ya hali zipi?
2 Ili kujibu hilo, acheni tukumbuke ile pindi ambayo Yesu alikuwa na mazungumzo ya faragha pamoja na wanafunzi wake. Huko, katika wilaya ya Kaisaria-Filipi, kaskazini-mashariki mwa Bahari ya Galilaya, kukiwa na mandhari yenye kutokeza ya Mlima Hermoni wenye fahari, walimsikia akisema waziwazi kwamba angeuawa. (Mathayo 16:21) Maneno mengine yenye uzito yangefuata. Baada ya kuwaeleza kwamba uanafunzi unamaanisha kuishi maisha ya kujidhabihu daima, Yesu alionya hivi: “Mwana wa Adamu atakuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika zake; ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake [mwenendo wake, NW].” (Mathayo 16:27) Yesu alisema juu ya kuja kwa wakati ujao. Hata hivyo, kwenye pindi hiyo, angekuwa Hakimu. Wakati huo kila jambo lingetegemea juu ya kama angempata mtu akimfuata kwa uaminifu au sivyo. Hukumu ya Yesu ingetegemea mwenendo, haidhuru ni kiasi gani cha mali za kilimwengu mtu huyo huenda akawa nacho au asiwe nacho. Wanafunzi wake walihitaji kukumbuka jambo hilo kwa uthabiti. (Mathayo 16:25, 26) Kwa hiyo, ni Yesu Kristo mwenyewe anayewaambia wafuasi wake watazamie kuja kwake kwenye utukufu, pamoja na hukumu ya kuja huko.
3. Yesu alitoaje kielezi cha uhakika wa kuja kwake kwa wakati ujao?
3 Yale ambayo Yesu asema baadaye yaonyesha uhakika wa kuja kwake wakati ujao. Kwa mamlaka asema hivi: “Amin, nawaambieni, Pana watu katika hawa wasimamao hapa, ambao hawataonja mauti kabisa, hata watakapomwona Mwana wa Adamu akija katika ufalme wake.” (Mathayo 16:28) Maneno hayo yanatimizwa siku sita baadaye. Njozi nyangavu ya Yesu akiwa amegeuka sura inawastaajabisha wanafunzi wake wa karibu sana. Kwa kweli waona uso wa Yesu uking’aa kama jua na mavazi yake yakiwa meupe kwa kumeta-meta. Kugeuka sura huko kulikuwa mwono wa kimbele wa utukufu na Ufalme wa Kristo. Huo ni uhakikisho wenye kutia nguvu kama nini wa ule unabii mwingi wa Ufalme! Hicho ni kichocheo chenye nguvu kama nini kwa wanafunzi kuwa timamu katika akili!—2 Petro 1:16-19.
Sababu kwa Nini Ni Muhimu Kuwa Timamu Katika Akili
4. Kwa nini ni lazima Wakristo wawe macho kiroho kuhusiana na kuja kwake?
4 Muda unaopungua mwaka mmoja baadaye, twamwona Yesu akiwa ameketi juu ya Mlima wa Mizeituni, akishiriki tena mazungumzo ya faragha pamoja na wanafunzi wake. Wanapokazia macho jiji la Yerusalemu, yeye aeleza ishara ya kuwapo kwake katika wakati ujao utakuwa nini na kisha aonya hivi: “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu.” Ni lazima wafuasi wake wawe macho daima kwa sababu wakati wa kuja kwake haujulikani. Ni lazima wawe tayari wakati wote kwa ajili ya kuja huko. —Mathayo 24:42.
5. Uhitaji wa kukesha unaweza kutolewaje kielezi?
5 Kwa namna ya kuja kwake, Bwana afanana na mwivi. Aendelea kusema hivi: “Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa.” (Mathayo 24:43) Mvunjaji nyumba hatoi tangazo la kumwarifu mwenye nyumba wakati atakapokuja; silaha yake kuu ni kushtua. Kwa hiyo, ni lazima mwenye nyumba awe macho daima. Hata hivyo, kwa Mkristo mwaminifu, kukesha bila kulegea si kwa sababu ya wasiwasi wowote wenye hofu. Bali, kunachochewa na matazamio yenye hamu ya kuja kwa Kristo katika utukufu ili kuleta Mileani (Miaka Elfu) ya amani.
6. Kwa nini ni lazima tuwe timamu katika akili?
6 Kujapokuwa kulinda huko kote, hakuna atakayehesabu kimbele siku barabara ambayo anakuja. Yesu asema hivi: “Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.” (Mathayo 24:44) Kwa hiyo kuna uhitaji wa kuwa timamu katika akili. Ikiwa Mkristo angefikiri kwamba Kristo asingekuja katika siku fulani, labda hiyo ingekuwa ndiyo siku hasa ambayo yeye angekuja! Bila shaka, Wakristo waaminifu wenye nia njema katika wakati uliopita wamejaribu kwa moyo mweupe kutabiri wakati mwisho ungekuja. Hata hivyo, onyo la Yesu limethibitishwa kuwa kweli tena na tena: “Habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake.”—Mathayo 24:36.
7. Ili tuwe wafuasi wa Kristo, ni lazima tuishi maisha zetu jinsi gani?
7 Kwa hiyo, tufikie mkataa gani? Kwamba ili tuwe wafuasi wa Kristo, ni lazima tuishi tukiamini sikuzote kwamba mwisho wa mfumo huu mbovu unakaribia sana.
8. Alama ya Wakristo imekuwa nini tangu siku za mapema zaidi za Ukristo?
8 Mtazamo huo umekuwa alama ya Wakristo sikuzote, kama vile wanahistoria walimwengu na wasomi wa Biblia wanavyotambua. Kwa kielelezo, wahariri wa The Translator’s New Testament, wanasema hivi, chini ya neno “Siku” katika maelezo yao ya maneno: “Wakristo wa nyakati za A[gano] J[ipya] waliishi wakitazamia ile Siku (yaani wakati ule) ambapo ulimwengu uliopo pamoja na ubaya na uovu wao wote ungekomeshwa na Yesu angerudi duniani kuihukumu ainabinadamu yote, kusimamisha enzi mpya ya amani na kuanza Ubwana wake juu ya ulimwengu wote.” Encyclopædia Britannica yasema hivi: “Ule upanuzi wa Ukristo wa duniani pote ulio wa pekee unahusika moja kwa moja na matazamio ya Kikristo ya wakati wa mwisho, katika namna ya matazamio ya kukaribia sana kwa kuja kwa Kristo. Matazamio ya Kikristo ya wakati wa mwisho hayakutia ndani kutamani tu bila kutenda kuja kwa Ufalme wa Mungu.”
Kinachomaanishwa na Kuwa Timamu Katika Akili
9. Hata ingawa baadhi ya matazamio ya Petro kuhusu Mesiya hayakuwa sahihi, kwa nini angeweza kuendelea akiwa na uhakika?
9 Miaka 30 hivi baada ya mazungumzo hayo ya kindani sana ambayo Yesu alikuwa nayo pamoja na wanafunzi wake wa karibu zaidi, mtume Petro hakuwa amechoka kungojea mwisho uje. Hata ingawa matazamio yake ya kwanza na yale ya wanafunzi wenzake juu ya Mesiya hayakuwa sahihi, aliendelea akiwa na uhakika kwamba upendo na nguvu za Yehova zilihakikisha utimizo wa tumaini lao. (Luka 19:11; 24:21; Matendo 1:6; 2 Petro 3:9, 10) Yeye asema jambo linalosikiwa kwa upatano kotekote katika Maandiko ya Kigiriki anaposema hivi: “Mwisho wa mambo yote umekaribia.” Kisha awahimiza Wakristo wenzake hivi: “Iweni na akili [timamu katika akili, NW], mkeshe katika sala.”—1 Petro 4:7.
10. (a) Ni nini maana ya kuwa timamu katika akili? (b) Ni nini linalohusika katika kuona mambo ifaavyo kuhusiana na mapenzi ya Mungu?
10 Kuwa “timamu katika akili” hakumaanishi kuwa mwerevu kutokana na maoni ya kilimwengu. Yehova asema hivi: “Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, na akili zao wenye akili nitazikataa.” (1 Wakorintho 1:19) Neno ambalo Petro atumia linaweza kumaanisha “kuwa na akili yenye uzito.” Uzito huo wa kiroho unahusiana na ibada yetu. Kwa hiyo, tukiwa thabiti katika akili, tunaona mambo ifaavyo kuhusiana na mapenzi ya Yehova; tunaelewa ni mambo gani yaliyo ya maana na yale yasiyo ya maana. (Mathayo 6:33, 34) Ingawa mwisho unakaribia sana, hatukumbwi na mtindo-maisha wenye wasiwasi; wala hatuonyeshi hali ya kutojali pindi ya wakati tunamoishi. (Linganisha Mathayo 24:37-39.) Bali, tunaongozwa na kiasi na usawaziko wa mawazo, mtazamo, na mwenendo, unaoonyeshwa kwanza kumwelekea Mungu (‘kukesha katika sala’) na kisha kumwelekea jirani yetu (‘kuwa na juhudi nyingi katika kupendana’).—1 Petro 4:7, 8.
11. (a) Ni nini maana ya kufanywa “wapya katika kani itendeshayo akili [yetu]”? (b) Kani mpya ya akilini hutusaidiaje kufanya maamuzi mazuri?
11 Kuwa timamu katika akili kunahusisha ndani kufanywa kwetu “wapya katika kani itendeshayo akili [yetu].” (Waefeso 4:23, NW) Kwa nini tufanywe wapya? Kwa kuwa tumerithi kutokamilika na tunaishi katika mazingira yenye dhambi, akili yetu inaongozwa na mwelekeo unaopinga hali ya kiroho. Kani hiyo sikuzote husukuma mawazo na mitazamo kuelekea mambo ya kimwili, na yenye ubinafsi. Kwa hiyo, mtu anapokuwa Mkristo, anahitaji kani, au mtazamo mkuu mpya wa akili, utakaosukuma mawazo yake kwa njia ifaayo, njia ya kiroho, kuelekea utayari wa kuwa mwenye kujidhabihu. Hivyo, kwa kielelezo, uchaguzi unapotokezwa katika elimu, kazi-maisha, kazi ya kuajiriwa, vitumbuizo, tafrija, mtindo wa mavazi, au iwe ni nini, mwelekeo wake wa kwanza utakuwa ni kuchunguza jambo hilo kutokana na maoni ya kiroho badala ya maoni ya kimwili, yenye ubinafsi. Mtazamo huo mpya hufanya iwe rahisi zaidi kuamua mambo kwa utimamu wa akili na kwa kutambua kwamba mwisho u karibu.
12. Tunaweza kuendeleaje “wazima katika imani”?
12 Kuwa timamu katika akili kunadokeza kwamba tumo katika afya njema ya kiroho. Tunaweza kuendeleaje kuwa “wazima katika imani”? (Tito 2:2) Ni lazima tuilishe akili yetu aina ifaayo ya chakula. (Yeremia 3:15) Mlo wa kawaida wa Neno la Mungu la kweli unaotegemezwa na utendaji wa roho takatifu yake utatusaidia tudumishe usawaziko wetu wa kiroho. Kwa hiyo, ukawaida katika funzo la kibinafsi, pamoja na utumishi wa shambani, sala, na ushirika wa Kikristo, ni muhimu.
Jinsi Utimamu wa Akili Unavyotulinda
13. Utimamu wa akili hutulindaje tusifanye makosa ya kipumbavu?
13 Utimamu wa akili unaweza kutulinda tusifanye kosa la kipumbavu ambalo lingeweza kutugharimu uhai wetu wa milele. Hilo linawezekanaje? Mtume Paulo asema juu ya “sheria ya akili.” Kwa mtu mwenye afya katika imani, sheria hiyo ya akili inaongozwa na jambo fulani analofurahia, yaani, “sheria ya Mungu.” Ni kweli, “sheria ya dhambi” hupiga vita dhidi ya sheria ya akili. Hata hivyo, Mkristo aweza kuwa mshindi kwa msaada wa Yehova.—Warumi 7:21-25.
14, 15. (a) Ni mavutano gani mawili yanayon’gang’ania kuidhibiti akili? (b) Tunaweza kushindaje pigano la akili?
14 Paulo aendelea kwa kuonyesha tofauti kubwa kati ya akili inayoongozwa na mwili wenye dhambi, ambayo hukazia maisha ya kula raha, na akili inayoongozwa na roho ya Mungu, ambayo hukazia maisha ya kujidhabihu katika utumishi wa Yehova. Paulo aandika hivi kwenye Warumi 8:5-7: “Wale waufuatao mwili huyafikiri mambo ya mwili; bali wale waifuatao roho huyafikiri mambo ya roho. Kwa kuwa nia ya mwili ni mauti; bali nia ya roho ni uzima na amani. Kwa kuwa ile nia ya mwili ni uadui juu ya Mungu, kwa maana haitii sheria ya Mungu, wala haiwezi kuitii.”
15 Katika mstari 11, ndipo Paulo aeleza jinsi akili inayoshirikiana na roho takatifu hushinda pigano: ‘Lakini, ikiwa roho yake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu yakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa roho yake inayokaa ndani yenu.’
16. Utimamu wa akili hutulinda dhidi ya vishawishi vipi?
16 Kwa hiyo, tukiwa timamu katika akili, hatutashawishwa na vishawishi vya ulimwengu huu vilivyopo kila mahali, vyenye mwelekeo wa kutaka kula raha kupita kiasi katika namna zote za anasa, vitu vya kimwili, na mwenendo mbaya katika ngono. Akili yetu timamu itatuambia ‘tukimbie zinaa’ na kuepuka matokeo yayo yenye msiba. (1 Wakorintho 6:18) Mtazamo wetu timamu wa akili utatuchochea tuweke masilahi ya Ufalme kwanza nao utalinda mawazo yetu tunaposhawishwa kwa kutolewa kazi-maisha ya kilimwengu iwezayo kudhoofisha uhusiano wetu na Yehova.
17. Dada mmoja painia alionyeshaje utimamu wa akili alipokabiliwa na wajibu mbalimbali wa kifedha?
17 Kwa kielelezo, katika nchi moja ya kitropiki katika Esia Kusini-mashariki, kulikuwa dada mmoja kijana aliyeweka masilahi ya Ufalme kwanza akilini. Alikuwa amesitawisha upendo wa utumishi wa wakati wote. Katika nchi hiyo kazi nyingi zinahitaji siku sita au saba za kazi ya wakati wote. Baada ya yeye kuhitimu chuo kikuu, baba yake, ambaye hakuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alimtazamia kuchuma fedha nyingi kwa ajili ya familia. Lakini kwa kuwa alikuwa na tamaa yenye nguvu ya kufanya upainia, yeye alipata kazi ya muda-muda akaanza utumishi wa painia. Hilo lilimkasirisha baba yake, aliyetisha kutupa mali za dada huyo barabarani. Kwa sababu ya kucheza kamari, baba yake alikuwa na madeni mengi, na alimtazamia binti yake ayalipe madeni yake. Ndugu mdogo wa dada huyo alikuwa akisoma kwenye chuo kikuu kimoja, na kwa sababu ya madeni hayo, hakukuwa fedha za kulipia masomo yake. Ndugu huyo mdogo aliahidi kwamba ikiwa dada yake angemsaidia, angeitunza familia wakati ambapo angepata kazi. Moyo wa dada uligawanyika kati ya upendo wake kwa ndugu yake na upendo wake wa utumishi wa painia. Baada ya kufikiria jambo hilo kwa uangalifu, aliazimia kuendelea kufanya upainia na kutafuta kazi tofauti. Kwa jibu la sala yake, alipata kazi ambayo ilimwezesha kusaidia familia yake na ndugu yake mdogo kifedha na pia kuendelea na upendo wake wa kwanza, utumishi wa painia.
Tafuta Msaada wa Yehova Katika Kudumisha Utimamu wa Akili
18. (a) Kwa nini huenda watu wengine wakahisi kuvunjika moyo? (b) Ni maandiko gani ambayo huenda yakawafariji wale waliovunjika moyo?
18 Huenda ikawa wafuasi wengine wa Kristo wanaliona kuwa jambo gumu kudumisha utimamu wao wa akili. Huenda ikawa subira yao inapungua kwa sababu mfumo huu mbovu wa mambo unaendelea kwa muda mrefu zaidi ya vile walivyotazamia. Huenda wakahisi kuvunjika moyo juu ya hilo. Hata hivyo, mwisho utakuja. Yehova aahidi hilo. (Tito 1:2) Paradiso yake ya kidunia iliyoahidiwa itakuja pia. Yehova ahakikisha hilo. (Ufunuo 21:1-5) Ulimwengu mpya unapokuja, kutakuwako “mti wa uzima” kwa ajili ya wale wote waliodumisha utimamu wao wa akili.—Mithali 13:12.
19. Utimamu wa akili unaweza kudumishwaje?
19 Tunaweza kudumishaje utimamu wa akili? Tafuta msaada wa Yehova. (Zaburi 54:4) Kaa karibu naye. Tunashangilia kama nini kwamba Yehova atamani kuwa karibu sana nasi! “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi,” aandika mwanafunzi Yakobo. (Yakobo 4:8) Paulo asema hivi: “Furahini katika Bwana sikuzote; tena nasema Furahini. Upole wenu na ujulikane na watu wote. Bwana yu karibu. Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zote na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:4-7) Na wakati mizigo yenye kulemea ya mfumo huu wa mambo unaopotelea mbali inapoonekana kuwa mikubwa mno kuendelea kuchukua, mtwike Yehova mizigo hiyo, naye mwenyewe atakutegemeza.—Zaburi 55:22.
20. Tunapaswa kuendelea katika mwendo gani, kulingana na 1 Timotheo 4:10?
20 Naam, mwisho u karibu, kwa hiyo iweni timamu katika akili! Hilo lilikuwa shauri zuri miaka 1,900 iliyopita; ni shauri muhimu leo. Acheni tuendelee kutumia uwezo wetu wa akili timamu kumsifu Yehova anapoendelea kutuongoza kwa usalama kuingia ulimwengu wake mpya.—1 Timotheo 4:10.
Ungejibuje?
◻ Utimamu wa akili ni nini?
◻ Kwa nini ni muhimu sana kuwa timamu katika akili?
◻ Tunaweza kufanywaje wapya katika kani itendeshayo akili yetu?
◻ Ni lazima tuwe na pigano jipi la daima akilini mwetu?
◻ Tunadumishaje utimamu wa akili?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kumkaribia Mungu katika sala kunatusaidia tudumishe utimamu wa akili
[Picha katika ukurasa wa 17]
Tukiwa timamu katika akili, hatutashawishwa na vishawishi vya ulimwengu huu