Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 8/15 kur. 17-22
  • “Utimamu wa Akili” Mwisho Ukaribiapo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Utimamu wa Akili” Mwisho Ukaribiapo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Utimamu wa Akili” Katika Mahusiano Yetu ya Kibinafsi
  • “Utimamu wa Akili” na Madaraka ya Familia
  • “Utimamu wa Akili” Katika Maoni Yetu Kuhusu Elimu
  • ‘Usitafute Mambo Makubwa’
  • Matumizi Mazuri ya Wakati Unaobaki
  • Endeleeni Kuishi kwa “Utimamu wa Akili”
  • Alijifunza Kuwa Mwenye Rehema
    Igeni Imani Yao
  • Alijifunza Kuwa Mwenye Rehema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Jitahidi Kuwaona Wengine Kama Yehova Anavyowaona
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Yona Ajifunza Juu ya Rehema ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 8/15 kur. 17-22

“Utimamu wa Akili” Mwisho Ukaribiapo

“Mwisho wa mambo yote umekaribia. Kwa hiyo, iweni timamu katika akili.” —1 PETRO 4:7.

1. Ni nini linalohusishwa na kuwa “timamu katika akili”?

MANENO yaliyo juu ya mtume Petro yapaswa kuwa na matokeo makubwa katika njia ambayo Wakristo huishi maisha yao. Hata hivyo, Petro hakuwaambia wasomaji wake waachane na madaraka ya kidunia na mahangaiko ya maisha; wala hakuwatia moyo wawe na hofu ya kuwazia kuhusu uharibifu unaokaribia. Badala ya hivyo, aliwasihi sana hivi: “Iweni timamu katika akili.” Kuwa “timamu katika akili” kwahusisha kuonyesha uamuzi mzuri, kuwa wenye akili, wenye busara, wenye kufikiri vizuri katika usemi na matendo yetu. Kwamaanisha kuacha Neno la Mungu litawale kufikiri kwetu na matendo yetu. (Waroma 12:2) Kwa kuwa twaishi “miongoni mwa kizazi kilicho kombo na kilichopotoka,” akili timamu yahitajiwa ili kuepuka matatizo na magumu.—Wafilipi 2:15.

2. Subira ya Yehova yanufaishaje Wakristo leo?

2 “Utimamu wa akili” pia hutusaidia tuwe na maoni yaliyo makini na yenye uhalisi juu yetu wenyewe. (Tito 2:12; Waroma 12:3) Hilo ni muhimu kwa kufikiria maneno yaliyorekodiwa kwenye 2 Petro 3:9: “Yehova si wa polepole kwa habari ya ahadi yake, kama watu fulani waonavyo kuwa ni upolepole, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” Ona kwamba Yehova ni mwenye subira, si kwa wasioamini tu, bali pia “kwenu” mlio washiriki wa kutaniko la Kikristo. Kwa nini? Kwa sababu “hataki yeyote aangamizwe.” Labda wengine wangali wanahitaji kufanya mabadiliko na marekebisho ili wastahili zawadi ya uhai udumuo milele. Kwa hiyo na tuangalie maeneo ambayo huenda yakahitaji marekebisho fulani.

“Utimamu wa Akili” Katika Mahusiano Yetu ya Kibinafsi

3. Ni maswali gani ambayo wazazi wanaweza kujiuliza kuhusu watoto wao?

3 Nyumbani papaswa kuwa mahali salama pa amani. Lakini kwa watu fulani ni “nyumba yenye . . . magomvi.” (Mithali 17:1) Vipi familia yako? Je, nyumba yako ni isiyo na “hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi”? (Waefeso 4:31) Vipi watoto wako? Je, wao huhisi wanapendwa na kuthaminiwa? (Linganisha Luka 3:22.) Je, wachukua wakati uwafundishe na kuwazoeza? Je, wewe ‘huwatia nidhamu katika uadilifu’ badala ya kuwatia nidhamu katika ghadhabu na hasira? (2 Timotheo 3:16) Kwa kuwa watoto ni “urithi wa BWANA,” yeye anapendezwa sana na jinsi wanavyotendewa.—Zaburi 127:3.

4. (a) Ni jambo gani laweza kutokea mume akimtenda mke wake kwa ukali? (b) Wake wanaweza kuendelezaje amani pamoja Mungu na furaha katika familia nzima?

4 Vipi mwenzi wetu wa ndoa? “Waume wapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Yeye apendaye mke wake ajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu aliyepata wakati wowote kuuchukia mwili wake mwenyewe; bali huulisha na kuutunza sana, kama vile Kristo pia alifanyiavyo kutaniko.” (Waefeso 5:28, 29) Mwanamume mwenye kutukana, mwenye uonevu, au asiyekubali sababu hahatarishi tu hali yenye utulivu ya nyumba yake bali pia huharibu uhusiano wake na Mungu. (1 Petro 3:7) Vipi wake? Hali kadhalika yawapasa “wawe katika ujitiisho kwa waume zao kama kwa Bwana.” (Waefeso 5:22) Kufikiria kumpendeza Mungu kwaweza kumsaidia mke asamehe kasoro za mume wake na kujitiisha kwake bila uchungu wa moyo. Nyakati nyingine, huenda mke akahisi anawajibika kutoa maoni yake. Andiko la Mithali 31:26 lasema hivi juu ya mke mwema: “Hufumbua kinywa chake kwa hekima, na sheria ya wema i katika ulimi wake.” Kwa kumtendea mume wake kwa njia ya fadhili na staha, yeye hudumisha amani pamoja na Mungu, naye huendeleza furaha ya familia nzima.—Mithali 14:1.

5. Kwa nini vijana wafuate shauri la Biblia kuhusu jinsi wanavyowatendea wazazi wao?

5 Vijana, mwawatendeaje wazazi wenu? Je, mwatumia usemi wa kejeli, usio na staha ambao mara nyingi huvumiliwa na ulimwengu? Au mnatii hii amri ya Biblia: “Watoto, iweni watiifu kwa wazazi wenu katika muungano na Bwana, kwa maana hili ni lenye uadilifu: ‘Heshimu baba yako na mama yako’; ambayo ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi: ‘Ili ipate kuwa vema kwako nawe upate kudumu muda mrefu juu ya dunia.’”—Waefeso 6:1-3.

6. Twaweza kutafutaje amani kwa waabudu wenzetu?

6 Pia twaonyesha “utimamu wa akili” ‘tunapotafuta sana amani na kuifuatia’ kwa waabudu wenzetu. (1 Petro 3:11) Mabishano na kutoelewana hutokea mara kwa mara. (Yakobo 3:2) Uhasama ukiruhusiwa uongezeke, amani ya kutaniko lote yaweza kuwa hatarini. (Wagalatia 5:15) Kwa hiyo tatueni mabishano upesi; tafuteni masuluhisho yenye amani.—Mathayo 5:23-25; Waefeso 4:26; Wakolosai 3:13, 14.

“Utimamu wa Akili” na Madaraka ya Familia

7. (a) Paulo alitiaje moyo kuonyesha “utimamu wa akili” katika mambo ya kidunia? (b) Waume na wake Wakristo wapaswa kuonyesha mtazamo gani kuelekea madaraka ya kinyumbani?

7 Mtume Paulo aliwashauri Wakristo ‘waishi kwa utimamu wa akili.’ (Tito 2:12) Inapendeza kwamba, katika huo muktadha, Paulo awahimiza sana wanawake ‘wawapende waume zao, wawapende watoto wao, wawe timamu katika akili, safi kiadili, wafanyakazi nyumbani.’ (Tito 2:4, 5) Paulo aliandika hivyo katika mwaka wa 61-64 W.K., miaka michache kabla ya mwisho wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi. Hata hivyo, mambo ya ulimwengu, kama vile kazi ya nyumbani, yalikuwa yangali mambo ya maana. Kwa hiyo waume na wake lazima wadumishe maoni yafaayo, yaliyo chanya kuhusu madaraka yao ya kinyumbani ili “neno la Mungu lisipate kusemewa kwa maneno yenye kuudhi.” Kichwa cha familia mmoja aliomba kuwiwa radhi na mgeni kwa sababu ya hali ya kuaibisha ya nyumba yake. Alieleza kwamba ilikuwa haijafanyiwa marekebisho “kwa sababu alikuwa akifanya upainia.” Ni jambo linalostahili pongezi tunapojidhabihu kwa ajili ya Ufalme, lakini lazima tuangalie tusihatarishe hali njema ya familia zetu.

8. Vichwa vya familia wanaweza kutunzaje mahitaji ya familia zao kwa njia ya usawaziko?

8 Biblia husihi sana akina baba watangulize familia zao, ikisema kwamba yule ashindwaye kuandalia kitu familia yake “ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Viwango vya kuishi vyatofautiana ulimwenguni pote, na ni vizuri kuweka matazamio ya kimwili yakiwa yenye kiasi. “Usinipe umaskini wala utajiri,” akasali mwandikaji wa Mithali 30:8. Hata hivyo, wazazi hawapaswi kupuuza mahitaji ya kimwili ya watoto wao. Kwa mfano, je, lingekuwa jambo la hekima kuacha kimakusudi familia yako bila mahitaji ya msingi ya maisha ili kufuatia mapendeleo ya kitheokrasi? Je, jambo hilo lisingewachukiza watoto wako? Kwa upande mwingine, andiko la Mithali 24:27 lasema hivi: “Tengeneza kazi yako huko nje, jifanyizie kazi yako tayari shambani, ukiisha, jenga nyumba yako.” Ndiyo, ingawa kuhangaikia mambo ya kimwili kuna mahali pake, ‘kujenga nyumba yako’—kiroho na kihisia-moyo—ni muhimu.

9. Kwa nini ni jambo la hekima kwa vichwa vya familia kufikiria kwa uangalifu uwezekano wa kifo chao na ugonjwa wao?

9 Je, umefanya maandalizi ya kutunza familia yako ukipatwa na kifo cha mapema? Andiko la Mithali 13:22 lasema hivi: “Mtu mwema huwaachia wana wa wanawe urithi.” Kuongezea urithi wa ujuzi kuhusu Yehova na uhusiano naye, wazazi watapendezwa na kuwaandalia kimwili watoto wao. Katika nchi nyingi vichwa vya familia wenye daraka hujaribu kuweka akiba fulani, wasia halali, na bima. Kwa vyovyote, watu wa Mungu si wasioweza kupatwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11, NW) Fedha ni “ulinzi,” na mpango wenye uangalifu mara nyingi waweza kuepusha shida. (Mhubiri 7:12) Katika nchi ambamo utunzi wa kitiba haulipwi na serikali, wengine huchagua kuweka kando fedha kwa ajili ya mahitaji ya afya au kupanga aina fulani ya bima ya afya.a

10. Wazazi Wakristo wanaweza ‘kuwekeaje akiba’ watoto wao?

10 Maandiko pia husema: “Watoto hawapaswi kuweka akiba kwa ajili ya wazazi wao, bali wazazi kwa ajili ya watoto wao.” (2 Wakorintho 12:14) Katika ulimwengu ni jambo la kawaida kwa wazazi kuwekea watoto wao fedha kwa ajili ya elimu na ndoa kwa wakati ujao ili wawape mwanzo mzuri maishani. Je, umefikiria kuwekea mtoto wako akiba kwa wakati ujao wa kiroho? Kwa mfano, tuseme kwamba mtoto ambaye amekua anafuatia utumishi wa wakati wote. Ijapokuwa haiwapasi watumishi wa wakati wote kudai wala kutazamia msaada kutoka kwa wengine, huenda wazazi wenye upendo wakachagua ‘kushiriki naye kulingana na mahitaji yake’ ili kumsaidia adumu katika utumishi wa wakati wote.—Waroma 12:13; 1 Samweli 2:18, 19; Wafilipi 4:14-18.

11. Je, kuwa na maoni yanayofaa kuhusu fedha kwaonyesha ukosefu wa imani? Eleza.

11 Kuwa na maoni ya kihalisi kuhusu fedha hakumaanishi ukosefu wa imani kwamba ulimwengu wa Shetani unakaribia mwisho wake. Ni kuonyesha tu ‘hekima itumikayo’ na uamuzi ufaao. (Mithali 2:7; 3:21) Wakati mmoja Yesu alisema kwamba “wana wa mfumo huu wa mambo ni wenye hekima zaidi kwa njia itumikayo . . . kuliko vile walivyo wana wa nuru” katika kutumia fedha zao. (Luka 16:8) Si ajabu basi, kwamba wengine wameona uhitaji wa kufanya marekebisho katika njia wanayotumia mali zao, ili waweze kuboresha utunzi wa mahitaji ya familia zao.

“Utimamu wa Akili” Katika Maoni Yetu Kuhusu Elimu

12. Yesu alifundishaje wanafunzi wake kujirekebisha wafaane na hali?

12 “Mandhari ya ulimwengu huu inabadilika,” na mabadiliko ya kiuchumi yenye kuenea sana na maendeleo ya kitekinolojia yanatokea kwa uharaka sana. (1 Wakorintho 7:31) Hata hivyo, Yesu alifundisha wanafunzi wake kuwa wenye kubadilikana. Alipowatuma kwenye kampeni yao ya kwanza ya kuhubiri aliwaambia hivi: “Msijipatie dhahabu wala fedha wala shaba kwa ajili ya vifuko vyenu vya mshipini, wala mfuko wa chakula kwa ajili ya safari, wala mavazi ya ndani mawili, wala makubazi wala fimbo; kwa maana mfanyakazi astahili chakula chake.” (Mathayo 10:9, 10) Ingawa hivyo, katika pindi ya baadaye, Yesu alisema: “Acheni yule ambaye ana kibeti akichukue, vivyo hivyo pia mfuko wa chakula.” (Luka 22:36) Ni nini kilichokuwa kimebadilika? Hali. Mazingira ya kidini yalikuwa yamekuwa yenye uhasama, na sasa iliwapasa kujifanyia maandalizi yao wenyewe.

13. Kusudi kuu la elimu ni nini, na wazazi wanaweza kuungaje mkono watoto kwa habari hiyo?

13 Vivyo hivyo leo, wazazi huenda wakahitaji kuweka akilini mambo halisi ya kiuchumi ya leo. Kwa kielelezo, je, unahakikisha kwamba watoto wako wanapokea masomo ya kutosha? Kusudi kubwa la elimu lapaswa kuwa kumtayarisha kijana kuwa mhudumu mwenye matokeo wa Yehova. Na elimu ya maana zaidi ya zote ni elimu ya kiroho. (Isaya 54:13) Wazazi pia wanahangaikia uwezo wa watoto wao wa kujitegemeza wenyewe kifedha. Kwa hiyo wape watoto wako mwongozo, wasaidie wachague masomo ya shule yafaayo, na uzungumze nao kama ni jambo la hekima kufuatia elimu yoyote ya ziada au la. Maamuzi hayo ni daraka la familia, na wengine hawapaswi kuchambua mwendo uliochukuliwa. (Mithali 22:6) Vipi wale ambao wamechagua kuelimisha watoto wao nyumbani?b Ingawa wengi wamefanya kazi inayostahili pongezi, watu fulani wameipata kuwa kazi ngumu kuliko walivyofikiria, na watoto wao wamepata hasara. Kwa hiyo ikiwa unafikiria kuelimisha nyumbani, hakikisha kuhesabu gharama, ukichanganua kwa uhalisi kama una stadi na nidhamu ya kibinafsi vihitajiwavyo ili kufaulu.—Luka 14:28.

‘Usitafute Mambo Makubwa’

14, 15. (a) Baruku alikosaje usawaziko wake wa kiroho? (b) Kwa nini ulikuwa upumbavu kwake ‘kutafuta mambo makuu’?

14 Kwa kuwa mwisho wa mfumo huu haujafika, wengine huenda wakaelekea kutafuta kile ambacho ulimwengu unatoa—kazi-maisha zenye sifa kubwa, kazi zenye faida, na utajiri. Fikiria kwa uangalifu Baruku, mwandishi wa Yeremia. Aliomboleza hivi: “Ole wangu! kwa maana BWANA ameongeza huzuni pamoja na maumivu yangu. Nimechoka kwa ajili ya kuugua kwangu, wala sioni raha.” (Yeremia 45:3) Baruku alikuwa amechoka. Kutumikia akiwa mwandishi wa Yeremia kulikuwa kazi ngumu, yenye mkazo mwingi. (Yeremia 36:14-26) Na hakukuonekana kama kulikuwa na mwisho wa mkazo huo. Ingepata miaka 18 kabla ya Yerusalemu kuharibiwa.

15 Yehova alimwambia Baruku hivi: “Tazama, niliyoyajenga nitayabomoa, na niliyoyapanda nitayang’oa; na haya yatakuwa katika nchi yote. Je! unajitafutia mambo makubwa? usiyatafute.” Baruku alikuwa ameacha usawaziko wake. Alikuwa ameanza ‘kujitafutia makubwa,’ labda utajiri, umaarufu, au usalama wa vitu vya kimwili. Kwa kuwa Yehova alikuwa ‘anang’oa nchi yote,’ kungekuwa na umaana gani kutafuta vitu vyote hivyo? Kwa hiyo Yehova alimpa Baruku kikumbusha hiki chenye kumfanya afikiri: “Kwa maana tazama, nitaleta mabaya juu ya wote wenye mwili . . . ; lakini roho [“nafsi,” NW] yako nitakupa iwe nyara, katika mahali pote utakapokwenda.” Mali za kimwili hazingeokoka uharibifu wa Yerusalemu! Yehova alihakikisha kuokoka tu kwa ‘nafsi yake iwe nyara.’—Yeremia 45:4, 5.

16. Ni somo gani ambalo watu wa Yehova leo wanaweza kujifunza kutokana na kielelezo cha Baruku?

16 Baruku alitii sahihisho la Yehova, na, kulingana na ahadi ya Yehova, Baruku aliokoka. (Yeremia 43:6, 7) Ni somo lenye nguvu kama nini kwa watu wa Yehova leo! Huu si wakati wa ‘kujitafutia mambo makuu.’ Kwa nini? Kwa sababu “ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao.”—1 Yohana 2:17.

Matumizi Mazuri ya Wakati Unaobaki

17, 18. (a) Yona aliitikiaje wakati watu wa Ninawi walipotubu? (b) Ni somo gani ambalo Yehova alimfundisha Yona?

17 Basi, twaweza kutumiaje vizuri zaidi wakati unaobaki? Jifunze kutokana na jambo lililoonwa la nabii Yona. “Akaenda Ninawi . . . , akapaza sauti yake, akasema, Baada ya siku arobaini Ninawi utaangamizwa.” Yona alishangaa kwamba, watu wa Ninawi waliitikia ujumbe wake nao wakatubu! Yehova alijiepusha na kuuharibu mji huo. Itikio la Yona lilikuwaje? “Basi, sasa, Ee BWANA, nakuomba, uniondolee uhai wangu; maana ni afadhali nife mimi kuliko kuishi.”—Yona 3:3, 4; 4:3.

18 Ndipo Yehova akamfundisha Yona somo la maana. Yeye “aliweka tayari mtango, akaufanya ukue juu ya Yona, ili uwe kivuli juu ya kichwa chake . . . Basi Yona akafurahi sana kwa sababu ya ule mtango.” Hata hivyo, kufurahi kwa Yona kulikuwa kwa muda mfupi, kwa kuwa mtango huo ulikauka haraka. Yona ‘akakasirika’ kwa kukosa faraja yake. Yehova akakazia hoja Yake, akisema: “Wewe umeuhurumia mtango . . . je! haikunipasa kuuhurumia Ninawi, mji ule mkubwa; ambao ndani yake wamo watu zaidi ya mia na ishirini elfu, wasioweza kupambanua katika mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto; tena wamo wanyama wa kufugwa wengi sana?”—Yona 4:6, 7, 9-11.

19. Ni njia ipi ya ubinafsi ambayo sisi tutataka kuiepuka?

19 Kusababu kwa Yona kulikuwa kwa ubinafsi kama nini! Yeye aliweza kuuhurumia mmea, lakini hakuwahurumia watu wa Ninawi hata kidogo—watu ambao, tukisema kuhusu hali ya kiroho, ‘hawakujua kutofautisha kati ya mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto.’ Huenda tukatamani hivyohivyo uharibifu wa ulimwengu huu mwovu uje na ndivyo ilivyo hasa! (2 Wathesalonike 1:8) Hata hivyo, tuungojeapo, tuna daraka la kusaidia watu wenye mioyo ya haki ambao, tukisema kuhusu hali ya kiroho, ‘hawajui kati ya mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto.’ (Mathayo 9:36; Waroma 10:13-15) Je, utatumia wakati mfupi unaobaki usaidie wengi iwezekanavyo wapate ujuzi wenye thamani kuhusu Yehova? Ni kazi ipi ambayo ingeweza kulingana na shangwe ya kusaidia mtu fulani kupata uhai?

Endeleeni Kuishi kwa “Utimamu wa Akili”

20, 21. (a) Ni katika baadhi ya njia zipi twaweza kuonyesha “utimamu wa akili” siku zijazo? (b) Ni baraka zipi zitakazotokana na kuishi kulingana na “utimamu wa akili”?

20 Kadiri mfumo wa Shetani uendeleavyo kuelekea uharibifu, magumu mapya kwa hakika yatatukabili. Andiko la 2 Timotheo 3:13 hutabiri: “Watu waovu na walaghai wataendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi.” Lakini “msipate kuchoka na kuzimia katika nafsi zenu.” (Waebrania 12:3) Tegemeeni Yehova mpate nguvu. (Wafilipi 4:13) Jifunzeni kuwa wenye kubadilikana, wenye kujirekebisha mfaane na hali hizi zenye kuharibika sana, badala ya kufikiria sana yaliyopita. (Mhubiri 7:10) Tumieni hekima yenye busara, mkifuata mwelekezo anaotoa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mathayo 24:45-47.

21 Hatujui ni kadiri gani ya wakati unaobaki. Hata hivyo, twaweza kusema kwa uhakika kwamba “mwisho wa mambo yote unakaribia.” Hadi mwisho huo utakapofika, na tuishi kwa “utimamu wa akili” katika shughuli zetu zote za mtu na mwenzake, katika njia tunayotunza familia zetu, na katika madaraka yetu ya kimwili. Kwa kufanya hivyo, sisi sote twaweza kuwa na uhakika kwamba tutapatwa hatimaye tukiwa “bila doa na bila waa na katika amani”!—2 Petro 3:14.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa mfano, katika Marekani, wengi huwa na bima ya afya, ingawa hiyo huelekea kuwa ghali sana. Baadhi ya familia za Mashahidi wameona kwamba madaktari huwa tayari sana kufikiria vibadala vya damu familia zinapokuwa na bima za afya. Matabibu wengi hukubali kiwango cha malipo kilichokubaliwa chini ya mipango ya bima au bima ya serikali ya afya isiyokuwa ya juu sana.

b Kama mtu anafuatia elimu ya nyumbani huo ni uamuzi wa kibinafsi. Ona makala “Kusomea Nyumbani—Je! Kunakufaa Wewe?” inayopatikana katika toleo la Amkeni! la Aprili 8, 1993.

Mambo ya Kupitia

◻ Twaweza kuonyeshaje “utimamu wa akili” katika mahusiano yetu ya kibinafsi?

◻ Twaweza kuonyeshaje usawaziko katika kutunza madaraka ya familia yetu?

◻ Kwa nini ni lazima wazazi wapendezwe na elimu ya kilimwengu ya watoto wao?

◻ Ni masomo gani tunayojifunza kutokana na Baruku na Yona?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mume na mke wanapotendana vibaya, wanaharibu uhusiano wao na Yehova

[Picha katika ukurasa wa 20]

Inawapasa wazazi kupendezwa na elimu ya watoto wao

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki