Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 7/15 kur. 5-8
  • Yehova—Mungu wa Kweli na Aliye Hai

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova—Mungu wa Kweli na Aliye Hai
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jina Lake na Umaarufu Wake
  • Yehova na Sifa Zake
  • Mfalme wa Kimbingu Asiye na Kifani
  • Yehova Ndiye Mungu wa Kweli na Aliye Hai
  • Mungu wa Kweli Ni Nani?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Mungu Ana Jina
    Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
  • Mungu Ana Jina
    Kumsikiliza Mwalimu Mkuu
  • Mungu Anataka Jina Lake Lijulikane
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 7/15 kur. 5-8

Yehova—Mungu wa Kweli na Aliye Hai

FARAO wa Misri alisema kwa ukaidi na kwa madharau alipouliza hivi: “BWANA [Yehova, NW] ni nani?” (Kutoka 5:2) Kama ilivyoonyeshwa katika makala inayotangulia, mtazamo huo ulileta mapigo na kifo juu ya Wamisri, kutia ndani kaburi la maji kwa Farao na majeshi yake.

Katika Misri ya kale, Yehova Mungu alithibitisha ukuu wake juu ya vijimungu bandia. Lakini kuna mengi zaidi ya kujifunza juu yake. Ni zipi baadhi ya sehemu za utu wake? Naye anataka nini kwetu?

Jina Lake na Umaarufu Wake

Alipomwomba Farao wa Misri, Musa hakusema: ‘Bwana asema hivi na hivi.’ Farao na wale Wamisri wengine waliwaona vijimungu bandia vyao vingi kuwa mabwana. La, Musa alitumia jina la mungu, Yehova. Yeye mwenyewe alikuwa amelisikia likinenwa kutoka juu alipokuwa kwenye kichaka chenye kuwaka moto katika nchi ya Midiani. Rekodi iliyopuliziwa yasema hivi:

“Kisha Mungu akasema na Musa, akamwambia, Mimi ni YEHOVA. . . . Nimesikia kuugua kwao wana wa Israeli, ambao Wamisri wanawatumikisha, nami nimelikumbuka agano langu. Basi waambie wana wa Israeli, Mimi ni YEHOVA, nami nitawatoa ninyi mtoke chini ya mizigo ya Wamisri, nami nitawaokoa na utumwa wao, nami nitawakomboa kwa mkono ulionyoshwa, na kwa hukumu kubwa, nami nitawatwaeni kuwa watu wangu, nitakuwa Mungu kwenu; nanyi mtajua ya kuwa mimi ni YEHOVA, Mungu wenu, niwatoaye mtoke chini ya mizigo ya Wamisri. Nami nitawaleta hata nchi ile [ya Kanaani] ambayo naliinua mkono wangu, niwape [babu zenu] Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo; nitawapa iwe urithi wenu; Mimi ni YEHOVA.”—Kutoka 6:1-8.

Hilo ndilo Yehova alilofanya hasa. Aliwaweka huru Waisraeli kutoka katika utumwa wa Kimisri akawawezesha waingie nchi ya Kanaani. Kama alivyoahidi, Mungu alisababisha hayo yote yatukie. Yafaa kama nini! Jina lake, Yehova, lamaanisha “Yeye Husababisha Iwe.” Biblia humrejezea Yehova kwa majina ya cheo kama vile “Mungu,” “Bwana Mwenye Enzi Kuu,” “Muumba,” “Baba,” “Mweza Yote,” na “Aliye Juu Zaidi.” Lakini jina lake Yehova humtambulisha kuwa Mungu wa kweli anayetimiza makusudi yake matukufu hatua kwa hatua.—Isaya 42:8.

Ikiwa tungesoma Biblia katika lugha zayo za awali, tungepata jina la Mungu mara nyingi sana. Katika Kiebrania linawakilishwa kwa zile konsonanti (herufi zisizo vokali) nne Yod He Waw He (יהוה), zinazoitwa Tetragramatoni, zinazosomwa kutoka kulia hadi kushoto. Wale waliosema Kiebrania waliandaa sauti za vokali, lakini leo watu hawajui kwa hakika vokali hizo zilikuwa gani. Ingawa wengine hupendelea mwendelezo Yahweh, namna Yehova ni ya kawaida na humtambulisha Muumba wetu ifaavyo.

Matumizi ya jina Yehova humtofautisha Mungu pia na yule aitwaye “Bwana wangu” kwenye Zaburi 110:1, ambapo fasiri moja ni: “Neno la BWANA [Kiebrania, יהוה] kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako.” Ikifahamu kuwapo kwa jina la Mungu hapa katika maandishi ya Kiebrania, New World Translation yasomwa hivi: “Tamko la Yehova kwa Bwana wangu ni: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kulia mpaka niwaweke maadui wako kuwa mahali pa kuweka miguu yako.’” Maneno hayo ya Yehova Mungu yanarejeza kiunabii kwa Yesu Kristo, ambaye mwandishi huyo alimwita “Bwana wangu.”

Yehova alifanya jina kwa ajili yake mwenyewe katika siku ya Farao. Kupitia Musa, Mungu alimwambia mtawala huyo mwenye moyo mgumu hivi: “Wakati huu nitaleta mapigo yangu yote juu ya moyo wako, na juu ya watumishi wako, na juu ya watu wako; ili upate kujua ya kuwa hapana mmoja mfano wa mimi ulimwenguni mwote. Kwa kuwa wakati huu ningekwisha kuunyosha mkono wangu, na kukupiga wewe na watu wako, kwa tauni, nawe ungekatiliwa mbali na kuondolewa katika nchi; lakini, nilikusimamisha wewe kwa sababu ii hii, ili nikuonyeshe uweza wangu, tena kwamba jina langu litangazwe katika dunia yote.”—Kutoka 9:14-16.

Kwa habari ya kutoka kwa Israeli katika Misri na kupinduliwa kwa wafalme fulani Wakanaani, yule mwanamke Rahabu wa Yeriko aliwaambia wapelelezi Waebrania wawili hivi: “Mimi najua ya kuwa BWANA [Yehova, NW] amewapa ninyi [Waisraeli] nchi hii, na ya kuwa hofu imetuangukia mbele yenu, na ya kuwa wenyeji wote wa nchi wanayeyuka mbele yenu. Maana tumesikia jinsi BWANA [Yehova, NW] alivyoyakausha maji ya bahari ya Shamu mbele yenu, hapo mlipotoka Misri, tena mambo hayo mliyowatendea wafalme wawili wa Waamori waliokuwa huko ng’ambo ya Yordani, yaani, Sihoni na Ogu, mliowaangamiza kabisa. Na mara tuliposikia hayo mioyo yetu iliyeyuka, wala haukusalia ujasiri wo wote katika mtu awaye yote, kwa sababu yenu; kwa kuwa BWANA [Yehova, NW], Mungu wenu, yeye ndiye Mungu, katika mbingu juu na katika nchi chini.” (Yoshua 2:9-11) Naam, umaarufu wa Yehova ulikuwa umeenea.

Yehova na Sifa Zake

Mtunga zaburi alionyesha tamaa yake ya kuhisiwa moyoni: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” (Zaburi 83:18) Kwa kuwa enzi kuu ya Yehova ni ya ulimwengu wote mzima, wafuasi wa Yesu walionyanyaswa wangeweza kusali hivi: “Mola [Bwana Mwenye Enzi Kuu, NW] wewe ndiwe Mungu, ndiwe uliyefanya mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo.” (Matendo 4:24) Na inafariji kama nini kujua kwamba Yehova ndiye “Msikiaji wa sala”!—Zaburi 65:2, NW.

Sifa kuu ya Yehova ni upendo. Kwa kweli, “Mungu ni upendo”—kielelezo bora kabisa cha sifa hiyo. (1 Yohana 4:8) Zaidi ya hayo, “hekima na amri zina yeye.” Yehova ni mwenye hekima yote na mwenye nguvu zote, lakini yeye hazitumii nguvu zake vibaya kamwe. (Ayubu 12:13; 37:23) Twaweza pia kuwa na uhakika kwamba Yehova atatutendea kwa haki sikuzote, kwani “haki na hukumu ndio msingi wa kiti chake.” (Zaburi 97:2) Tukikosea lakini tuwe wenye kutubu, twaweza kupata faraja kujua kwamba Yehova ni “mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.” (Kutoka 34:6) Haishangazi kwamba twaweza kuwa na shangwe katika kumtumikia Yehova!—Zaburi 100:1-5.

Mfalme wa Kimbingu Asiye na Kifani

Mwana wa Yehova, Yesu Kristo, alisema: “Mungu ni Roho.” (Yohana 4:24) Kwa hiyo, Yehova hawezi kuonwa kwa macho ya kibinadamu. Kwa kweli, Yehova alimwambia Musa hivi: “Huwezi kuniona uso wangu, maana mwanadamu hataniona akaishi.” (Kutoka 33:20) Mfalme huyu wa kimbingu ni mtukufu sana hivi kwamba wanadamu hawangeweza kuokoka ono la kumwona.

Ingawa Yehova hawezi kuonwa kwa macho yetu, kuna ushuhuda mwingi wa kuwako kwake akiwa Mungu Mweza Yote. Kwa kweli, “mambo yake yasiyoonekana [sifa zake zisizoonekana, NW] tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake.” (Warumi 1:20) Dunia—pamoja na nyasi, miti, matunda, mboga, na maua yayo—hushuhudia Uungu wa Yehova. Tofauti na vijimungu-sanamu visivyofaa kitu, Yehova hutoa mvua na majira yenye mavuno. (Matendo 14:16, 17) Ebu ziangalie nyota katika anga la usiku. Huo ni ushuhuda mtukufu kama nini wa Uungu wa Yehova na uwezo wake wa kitengenezo!

Yehova pia amewapanga kitengenezo viumbe wake wa roho, wenye akili mbinguni. Wakiwa tengenezo lenye upatano, wanatimiza mapenzi ya Mungu, kama vile mtunga zaburi anavyosema: “Mhimidini BWANA [Yehova, NW], enyi malaika zake, ninyi mlio hodari, mtendao neno lake, mkiisikiliza sauti ya neno lake. Mhimidini BWANA [Yehova, NW], enyi majeshi yake yote, ninyi watumishi wake mfanyao mapenzi yake.” (Zaburi 103:20, 21) Yehova pia amewapanga kitengenezo watu wake duniani. Taifa la Israeli lilipangwa vema kitengenezo, na pia wafuasi wa mapema wa Mwana wa Mungu. Vivyo hivyo leo, Yehova ana tengenezo la ulimwenguni pote la Mashahidi wenye bidii, wanaopiga mbiu habari njema kwamba Ufalme wake u karibu.—Mathayo 24:14.

Yehova Ndiye Mungu wa Kweli na Aliye Hai

Uungu wa Yehova umeonyeshwa katika njia nyingi sana! Alitweza vijimungu bandia vya Misri na kuwaleta Waisraeli kwa usalama ndani ya Bara Lililoahidiwa. Muumbo hutoa uthibitisho mwingi wa Uungu wa Yehova. Na hakuna ulinganifu hata kidogo kati ya yeye na vile vijimungu-sanamu visivyofaa kitu vya dini bandia.

Nabii Yeremia alionyesha ile tofauti kubwa kati ya Yehova, yule Mungu aliye hai, na sanamu zilizofanywa na mwanadamu zisizo na uhai. Tofauti hiyo inaelezwa vizuri katika Yeremia sura ya 10. Miongoni mwa mambo mengine, Yeremia aliandika hivi: “BWANA [Yehova, NW] ndiye Mungu wa kweli; ndiye Mungu aliye hai, Mfalme wa milele.” (Yeremia 10:10) Mungu aliye hai na wa kweli, Yehova, aliviumba vitu vyote. Aliwakomboa Waisraeli waliokuwa wakinyong’ony’ea katika utumwa wa Kimisri. Hakuna kitu kisichowezekana kwake.

Yehova, “Mfalme wa milele,” atajibu sala hii: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni.” (1 Timotheo 1:17; Mathayo 6:9, 10) Ufalme wa Kimesiya wa kimbingu, ulio mikononi mwa Yesu Kristo tayari, utachukua hatua hivi karibuni dhidi ya waovu na kuwaharibu maadui wote wa Yehova. (Danieli 7:13, 14) Ufalme huo pia utaleta ulimwengu mpya wenye baraka za milele kwa ainabinadamu tiifu.—2 Petro 3:13.

Kuna mengi zaidi ya kujifunza juu ya Yehova na makusudi yake. Kwa nini usiazimie kutwaa ndani ujuzi huo na kutenda kulingana nao? Ukifanya hivyo, utakuwa na pendeleo la kufurahia uhai wa milele katika paradiso ya kidunia chini ya utawala wa Ufalme. Utaishi wakati ambapo huzuni, maumivu, na hata kifo vitakuwa vimepitilia mbali na ujuzi wa Yehova kuijaza dunia. (Isaya 11:9; Ufunuo 21:1-4) Hilo laweza kuwa tokeo la wakati wako ujao ukitafuta, upate, na kutenda kupatana na majibu yenye msingi wa Biblia ya lile swali, “Yehova ni nani?”

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki