Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Kijana Mwenye Kupenda Gari-Moshi Sana Ajifunza Kweli
IKIWA moyo wa mtu una mbetuko kuelekea uadilifu, basi Yehova Mungu, akitumia Kristo Yesu na malaika wa kimbingu, atahakikisha kwamba mtu huyo mwenye mfano wa kondoo anapata habari njema za Ufalme hatimaye. Mwishoni huenda mtu huyo akaja kwenye mkono wa kulia wa Yesu wa upendeleo. (Mathayo 25:31-33) Ndivyo ilivyokuwa kwa kijana mmoja katika Austria aliyependa gari-moshi sana ambaye alipata kufahamu kweli kwa njia ya pekee.
Sehemu yenye kusisimua zaidi ya utendaji uliomfurahisha kijana huyo ilikuwa kwenda kwa gari-moshi akiwa katika behewa la dereva, kwa ruhusa ya wasimamizi wa reli. Alirekodi kila safari kwenye kamera yake ya vidio ili aweze kuiona tena akiwa nyumbani. Kwenye safari moja kutoka Vienna hadi Salzburg, dereva wa hilo gari-moshi alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alitumia fursa hiyo ili kuongea juu ya Ufalme na kijana huyo aliyependa sana magari-moshi. Mwanzoni kijana huyo alishangaa kusikia dereva huyo akiongea juu ya Mungu na Biblia, lakini katika safari hiyo, alikaza fikira zaidi juu ya mandhari kuliko juu ya yale ambayo dereva huyo alikuwa akimwambia.
Aliporudi nyumbani, kijana huyo alipenda magari-moshi sana alitazama vidio yake si mara moja bali mara kumi, kwa kuwa alipendezwa sana na safari hiyo. Kwa kuwa alikuwa amerekodi sauti pia, alisikia kwa kurudia-rudia yale ambayo Shahidi huyo alikuwa amemwambia. Kadiri alivyozidi kuitazama vidio hiyo, ndivyo alivyozidi kufahamu yale aliyokuwa ameambiwa. Sasa alianza kuyafikiria mambo hayo, na mwishoni akawa na idili juu ya ile habari nzuri ajabu iliyotolewa kutoka katika Biblia. Alitaka kujua zaidi.
Alikumbuka jina la huyo dereva na alijua kwamba aliishi mahali fulani katika Vienna. Kwa hiyo alikwenda posta akaanza kupiga nambari moja ya simu baada ya nyingine zilizoorodheshwa chini ya jina hilo katika kitabu cha nambari za simu. Swali lake kwa wale walioijibu simu lilikuwa: “Je! wewe ni dereva wa gari-moshi?” Ikiwa jibu lilikuwa la, yeye angepiga nambari nyingine ya simu. Mwishoni, alimpata huyo dereva. Alimsimulia yale yaliyompata na kwamba alipendezwa na ujumbe wa Biblia aliokuwa ameusikia kwenye vidio.
Shahidi huyo alifanya mipango kupitia ofisi ya tawi ili mtu fulani aliyeishi karibu ya kijana huyo aweze kumtembelea. Ilitukia kwamba katika kutaniko la mahali hapo, kulikuwa Shahidi mwingine aliyekuwa dereva wa gari-moshi pia. Dereva huyo wa pili alimtembelea kijana huyo aliyependa magari-moshi sana, na funzo la Biblia likaanzishwa. Katika kiangazi cha 1991, kijana huyo alibatizwa.
Yehova, anayechunguza mioyo yote, ni lazima iwe aliona kwamba mtu huyo alikuwa na upendo wenye moyo mweupe kwa ajili ya uadilifu. Kwa hiyo, alimwezesha apate kujua kweli ya Biblia—ingawa ilikuwa kwa njia ya pekee.—1 Mambo ya Nyakati 28:9; Yohana 10:27.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 9]
Hisani ya Austrian Railways