Kumpenda Jirani Kwawezekana
KIELEZI cha Yesu Kristo cha Msamaria kilionyesha kile kinachomaanishwa hasa na kumpenda jirani kikweli. (Luka 10:25-37) Yesu alifundisha hivi pia: “Mpende Bwana [Yehova, NW] Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako.”—Mathayo 22:37-39.
Kama ilivyo na watu wengi, je, unaona vigumu kumpenda jirani yako wa kabila lililo tofauti na lako mwenyewe? Labda ni hivyo kwa sababu umepata kujua juu ya ubaguzi na ukosefu wa haki au umepatwa na mambo hayo. Hata huenda ikawa wewe au wapendwa wako mmetendwa vibaya mikononi mwa watu wa kabila jingine.
Kwa kuwa Yesu alionyesha kwamba mojawapo ya amri za Mungu ni kwamba tumpende jirani yetu, ni lazima iwe inawezekana kushinda hisia hizo za chuki. Ufunguo wa kufanya hivyo ni kuwaona watu kama vile Mungu na Kristo wawaonavyo. Kwa habari hiyo acheni tuzungumzie kielelezo cha Yesu na cha Wakristo wa mapema.
Kielelezo Chema cha Yesu
Wayahudi wa karne ya kwanza walikuwa na hisia za chuki dhidi ya Wasamaria, watu walioishi katika eneo fulani kati ya Yudea na Galilaya. Katika pindi moja wapinzani wa Kiyahudi walimuuliza Yesu hivi kwa dharau: “Je! sisi hatusemi vema ya kwamba wewe u Msamaria, nawe una pepo? (Yohana 8:48) Mwelekeo wa kuwachukia Wasamaria ulikuwa wenye nguvu sana hivi kwamba Wayahudi fulani hata waliwalaani Wasamaria hadharani katika masinagogi na kusali kila siku kwamba Wasamaria wasipewe uhai wa milele.
Bila shaka kujua juu ya chuki hiyo yenye kina kirefu kulimchochea Yesu kutoa kile kielezi juu ya Msamaria aliyejithibitisha kuwa jirani wa kweli kwa kumtunza yule mwanamume wa Kiyahudi aliyepigwa na wanyang’anyi. Yesu angalijibuje wakati yule mwanamume wa Kiyahudi aliyezoeleana na Sheria ya Kimusa alipomuuliza: “Na jirani yangu ni nani?” (Luka 10:29) Yesu angaliweza kujibu moja kwa moja kwa kusema: ‘Jirani yako anatia ndani Myahudi mwenzako na pia watu wengine, hata Msamaria.’ Hata hivyo, Wayahudi wangaliona ni vigumu kukubali jambo hilo. Kwa hiyo alisimulia kile kielezi cha Myahudi aliyepokea rehema ya Msamaria. Hivyo Yesu aliwasaidia wasikilizaji wa Kiyahudi wafikie mkataa kwamba kupenda jirani kikweli kungeonyeshwa kwa wasio Wayahudi.
Yesu hakuwa na mwelekeo wa chuki dhidi ya Wasamaria. Pindi moja akisafiri kupitia Samaria, alipumzika kwenye kisima fulani wakati wanafunzi wake walipokwenda kwenye jiji la karibu ili kupata chakula. Wakati mwanamke mmoja Msamaria alipokuja kuteka maji, Yesu alisema hivi: “Nipe maji ninywe.” Kwa kuwa Wayahudi hawakushughulika na Wasamaria, aliuliza hivi: “Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria?” Kisha Yesu akamtolea ushahidi, hata akijulisha kwa wazi kwamba yeye alikuwa ndiye Mesiya. Aliitikia kwa kuingia jijini na kuwaita wengine waje na kumsikiliza. Tokeo lilikuwa nini? “Katika mji ule Wasamaria wengi walimwamini.” Hilo lilikuwa tokeo zuri kama nini kwa sababu Yesu hakuzuiwa na ule mtazamo ulioenea wa watu wa Kiyahudi wa wakati wake!—Yohana 4:4-42.
Mungu Si Mwenye Upendeleo
Kusudi la Mungu lilikuwa kwamba Yesu awahubiri Wayahudi hasa, “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mathayo 15:24) Kwa hiyo, wafuasi wake wa mapema walikuwa na malezi ya Kiyahudi. Lakini miaka mitatu tu baada ya kumwagwa kwa roho takatifu katika Pentekoste 33 W.K., Yehova alielewesha wazi kwamba alitaka waamini wa Kiyahudi waieneze ile kazi ya kufanya wanafunzi kwenye watu wa mataifa, Wasio Wayahudi.
Kwa akili ya Kiyahudi, mtu kumpenda Msamaria kama nafsi yake mwenyewe kungekuwa jambo gumu sana. Lingekuwa jambo gumu hata zaidi kuonyesha upendo wa jirani kwa Wasio Wayahudi wasiotahiriwa, watu waliokuwa tofauti sana na Wayahudi kuliko vile Wasamaria walivyokuwa. Ikieleza juu ya mtazamo wa Wayahudi kuelekea Wasio Wayahudi, The International Standard Bible Encyclopaedia yasema hivi: “Katika nyakati za A]gano] J[ipya], twaona karaha, dharau, na chuki yenye kupita kiasi zaidi. Wao [Wasio Wayahudi] walionwa kuwa wachafu, ambao kushughulika nao kirafiki, kulikuwa haramu. Walikuwa adui za Mungu na watu Wake, walionyimwa ujuzi juu ya Mungu isipokuwa kama wangegeuka kidini, na hata hivyo hawakuweza kuruhusiwa kuwa na ushirika wa kikamili, kama vile katika nyakati za zamani. Wayahudi walikatazwa kuwashauri, na ikiwa [Wasio Wayahudi] waliuliza swali juu ya mambo yaliyomhusu Mungu walipasa kulaaniwa.”
Ingawa wengi walikuwa na maoni hayo, Yehova alimsababisha mtume Petro aone njozi ambayo katika hiyo aliambiwa ‘asiviite najisi, vilivyotakaswa na Mungu.’ Kisha Mungu alimwelekeza kwenye nyumba ya Kornelio Asiye Myahudi. Petro alitoa ushahidi juu ya Kristo kwa Kornelio, familia yake, na Wasio Wayahudi wengine. “Hakika,” akasema Petro, “natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” Petro alipokuwa akihubiri, roho takatifu ilikuja juu ya waamini hao wapya, ambao walibatizwa wakati huo, wakawa wafuasi wa kwanza wa Kristo Wasio Wayahudi.—Matendo, Sura ya 10.
Wafuasi wa Kiyahudi walikubali jambo hilo, wakitambua kwamba amri ya Yesu ya ‘kufanya mataifa yote kuwa wanafunzi’ haikuwahusu Wayahudi tu katika mabara yote bali ilitia ndani Wasio Wayahudi. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 11:18) Wakishinda hisia zozote za kuwachukia Wasio Wayahudi ambazo huenda ikawa walikuwa nazo, walipanga kwa bidii kampeni ya kuhubiri ya kufanya wanafunzi miongoni mwa mataifa. Muda uliopungua miaka 30 baadaye, ingeweza kusemwa kwamba habari njema zilikuwa zimehubiriwa “katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu.”—Wakolosai 1:23.
Mtume Paulo alikuwa akiongoza katika kazi hiyo ya kuhubiri, yeye mwenyewe akiwa Mkristo mwenye malezi ya Kiyahudi. Kabla ya kuwa mfuasi wa Kristo, alikuwa amekuwa mshiriki mwenye bidii wa lile farakano la kidini la Mafarisayo. Waliwadharau Wasio Wayahudi na hata watu wa kawaida wa taifa lao wenyewe. (Luka 18:11, 12) Lakini Paulo hakuruhusu maoni hayo yamzuie asionyeshe upendo wa jirani kwa wengine. Badala ya hivyo, alikuja kuwa “mtume wa watu wa Mataifa [Wasio Wayahudi],” akitoa maisha yake kwa kazi ya kufanya wanafunzi kotekote katika mabara ya Mediterania.—Warumi 11:13.
Katika huduma yake, Paulo alipigwa kwa mawe, akachapwa, na kutiwa gerezani. (Matendo 14:19; 16:22, 23) Je! mambo hayo magumu yaliyompata yalimfanya awe mwenye uchungu na kukata maneno kwamba alikuwa akipoteza wakati wake miongoni mwa mataifa na makabila fulani? Hasha. Alijua kwamba kulikuwako watu mmoja-mmoja wenye mioyo ya kufuatia haki waliotawanyika kotekote miongoni mwa yale makabila mengi ya siku yake.
Paulo alipowapata Wasio Wayahudi waliokuwa na nia ya kujifunza njia za Mungu, alikuja kuwapenda. Kwa mfano, aliwaandikia Wathesalonike hivi: “Tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe. Vivyo hivyo nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na roho zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.” (1 Wathesalonike 2:7, 8) Maneno hayo ya kuhisiwa moyoni yanaonyesha kwamba Paulo aliwapenda kikweli wale Wathesalonike Wasio Wayahudi na hakuruhusu jambo lolote liharibu ile shangwe ya kuwa na uhusiano mzuri pamoja nao.
Kumpenda Jirani kwa Matendo
Leo, kama vile katika karne ya kwanza, wale wanaojiunga na kutaniko la Kikristo wanasitawisha upendo wa jirani kwa watu wa makabila yote. Kwa kusitawisha maoni ya kimungu kuelekea wengine na kwa kushiriki pamoja nao habari njema za Ufalme, Wakristo wa kweli wamepanua uelewevu wao juu ya watu ambao huenda ikawa wasingalipata kamwe kuwajua. Hata wanawaonyesha upendo wa kidugu. (Yohana 13:34, 35) Wewe pia waweza kujionea hayo.
Upendo huo umo miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, ingawa wanapatikana katika mabara 229 na kuwakilisha “watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” (Ufunuo 7:9) Wakiwa udugu wa duniani pote, wameungana katika ibada ya Yehova, katika kukataa kwao kushiriki katika mapigano ya kikabila na ugomvi mbalimbali, na katika kukatalia kwao mbali chuki zisizo na sababu zinazowanyang’anya watu mahusiano machangamfu pamoja na wanadamu wenzao.
Shirikiana na Mashahidi, na utaona jinsi watu wa malezi yote ya kikabila wanavyofanya mapenzi ya Mungu. Utaona upendo wa jirani kwa matendo wanapopiga mbiu ya habari njema za Ufalme wa Mungu. Naam, na katika makutaniko yao, utakutana na watu wenye fadhili, walio na mioyo myeupe wanaoonyesha kwa maisha zao kwamba kwa kweli wamejifunza kumpenda jirani yao.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]
Kuwasili kwa yule Msamaria Mwema Kwenye Nyumba ya Wageni/The Doré Bible Illustrations/Dover Publications, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, utaona watu wenye furaha wa rangi zote