Walifanya Mapenzi ya Yehova
Msamaria Athibitika Kuwa Jirani Mwema
KATIKA siku ya Yesu, uhasama wenye kuonekana wazi ulikuwako kati ya Wayahudi na wasio Wayahudi. Baada ya muda, Mishnah ya Kiyahudi hata ilitia ndani sheria iliyowakataza wanawake Waisraeli kuwasaidia wasio Wayahudi wakati wa kuzaa, kwa kuwa jambo hilo lingesaidia tu kuleta mtu mwingine asiye Myahudi duniani.—Abodah Zarah 2:1.
Wasamaria walikuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Wayahudi kidini na pia kijamii, kuliko wale wasio Wayahudi. Hata hivyo, wao pia walionwa kuwa watu waliotengwa na jamii. “Kwa maana Wayahudi hawana shughuli pamoja na Wasamaria,” akaandika mtume Yohana. (Yohana 4:9) Kwa kweli Talmud ilifundisha kwamba “kipande cha mkate ambacho Myahudi alipewa na Msamaria kilikuwa kichafu zaidi kuliko nyama ya nguruwe.” Wayahudi wengine hata walitumia neno “Msamaria” kama usemi wa kudharau na kuaibisha.—Yohana 8:48.
Kwa sababu ya hali hiyo, maneno ya Yesu kwa mtu mwenye ujuzi mwingi katika sheria ya Kiyahudi ni yenye kuelimisha sana. Huyo mwanamume alimfikia Yesu na kumwuliza hivi: “Mwalimu, ni kwa kufanya nini mimi nitarithi uhai udumuo milele?” Kwa kujibu, Yesu alimwelekeza kwenye Sheria ya Kimusa, ambayo hutoa agizo la ‘kumpenda Yehova kwa moyo wako wote, nafsi, nguvu, na akili,’ na ‘kupenda jirani yako kama wewe mwenyewe.’ Ndipo huyo mwanasheria akamwuliza Yesu: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” (Luka 10:25-29; Mambo ya Walawi 19:18; Kumbukumbu la Torati 6:5) Kulingana na Mafarisayo, neno “jirani” lilitumiwa kuwahusu wale tu walioshika mapokeo ya Kiyahudi—kwa hakika si kuwahusu wasio Wayahudi au Wasamaria. Kama mwanasheria huyo mwenye udadisi alifikiri kwamba Yesu angeunga mkono maoni yake, jambo la kushangaza lilimngoja.
Msamaria Mwenye Huruma
Yesu alijibu swali la mwanamume huyo kwa kusimulia mfano wenye somo.a “Mtu fulani,” akasema, “alikuwa akiteremka kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko.” Umbali kati ya Yerusalemu na Yeriko ulikuwa kilometa 23 hivi. Barabara iliyounganisha majiji hayo mawili ilikuwa na kona kali na miamba iliyojitokeza, ikifanya iwe rahisi kwa wezi kujificha, kushambulia, na kuponyoka. Kama ilivyotokea, msafiri katika mfano wenye somo wa Yesu “a[li]anguka miongoni mwa wapokonyaji, ambao walimvua nguo na pia kumpiga, wakaenda zao, wakimwacha yeye nusura kufa.”—Luka 10:30.
“Kwa sadfa,” Yesu aendelea, “kuhani fulani alikuwa akiteremka katika barabara hiyo, lakini, alipomwona, akaenda kupita kando upande wa pili. Hivyohivyo, Mlawi pia, alipofika chini kwenye mahali hapo na kumwona, akaenda kupita kando upande wa pili.” (Luka 10:31, 32) Makuhani na Walawi walikuwa walimu wa Sheria—kutia na sheria ya upendo kwa jirani. (Mambo ya Walawi 10:8-11; Kumbukumbu la Torati 33:1, 10) Bila shaka, wao hasa, walipaswa kuhisi kuwa wamelazimika kumsaidia huyo msafiri mwenye majeraha.
Yesu aliendelea kusema hivi: “Msamaria fulani mwenye kusafiri katika ile barabara alikuja akamkuta.” Bila shaka kutajwa kwa Msamaria kuliongeza udadisi wa huyo mwanasheria. Je, Yesu angekubali maoni yasiyofaa ya jamii hiyo? Kinyume cha hilo, huyo Msamaria alipomwona msafiri aliyepatwa na msiba “akasukumwa na sikitiko.” Yesu akasema hivi: “Kwa hiyo akamkaribia akafunga majeraha yake, akimwaga mafuta na divai juu yayo. Kisha akampandisha juu ya hayawani wake mwenyewe akamleta kwenye hoteli ndogo na kumtunza.b Na siku iliyofuata akatoa dinari mbili, akampa hizo mtunza-hoteli, na kusema, ‘Mtunze, na chochote kile utumiacho mbali na hiki, mimi nitakulipa nirudipo hapa.’”—Luka 10:33-35.
Yesu sasa alimwuliza mdadisi wake hivi: “Ni nani kati ya watatu hawa aonekana kwako kuwa alijifanya mwenyewe jirani kwa mtu aliyeanguka miongoni mwa wapokonyaji?” Huyo mwanasheria alijua jibu, hata hivyo alionekana kuwa mwenye kusitasita kusema “yule Msamaria.” Badala yake, alijibu tu: “Yeye aliyetenda kwa rehema kumwelekea.” Ndipo Yesu akamwambia: “Shika njia yako uende na uwe ukifanya hilohilo wewe mwenyewe.”—Luka 10:36, 37.
Somo Kwetu
Mwanamume aliyemwuliza Yesu maswali alifanya hivyo katika jitahada ya kutaka “kujithibitisha mwenyewe kuwa mwadilifu.” (Luka 10:29) Labda alifikiri kwamba Yesu angesifu kufuata kwake kwa uangalifu sana Sheria ya Kimusa. Lakini mtu huyu mwenye kujitanguliza alihitaji kujua ukweli wa mithali hii ya Biblia: “Kila njia ya mtu ni sawa machoni pake mwenyewe; bali BWANA huipima mioyo.”—Mithali 21:2.
Mfano wenye somo wa Yesu waonyesha kwamba, mtu aliye mnyoofu kwa kweli ni yule ambaye hutii si sheria za Mungu tu, bali pia huiga sifa zake. (Waefeso 5:1) Kwa mfano, Biblia hutuambia kwamba “Mungu si mwenye ubaguzi.” (Matendo 10:34) Je, sisi humwiga Mungu kuhusiana na jambo hilo? Mfano wenye somo wa Yesu ambao ni wenye kusisimua waonyesha kwamba ujirani wetu mwema wapaswa kushinda vizuizi vya kitaifa, kitamaduni, na kidini. Kwa kweli, Wakristo wanaagizwa ‘kufanya lililo jema kuelekea wote’—si kuelekea tu watu wa tabaka lilelile la kijamii, mbari, au taifa na si kuelekea tu waamini wenzao.—Wagalatia 6:10.
Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufuata onyo la upole la Kimaandiko. Kwa mfano, misiba ya kiasili itokeapo, wao hutoa msaada wa kibinadamu kwa waamini wenzao na vilevile wasio Mashahidi.c Kwa kuongeza, wote kwa ujumla hutumia muda wa saa zaidi ya bilioni moja kila mwaka wakiwasaidia watu wapate kujua Biblia vizuri zaidi. Wao hujitahidi kufikisha ujumbe wa Ufalme kwa kila mtu, kwa maana mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:4; Matendo 10:35.
[Maelezo ya Chini]
a Mfano wenye somo kwa kawaida ni simulizi fupi la kubuniwa, ambalo hutokeza kweli ya kiadili au ya kiroho.
b Ni wazi kwamba hoteli fulani katika siku ya Yesu ziliandaa si mahali pa kujisetiri tu, bali pia chakula na huduma nyingine. Hiyo yaweza kuwa aina ya makao ambayo Yesu alikuwa akifikiria, kwa maana neno la Kigiriki lililotumiwa hapa ni tofauti na lile litafsiriwalo “chumba cha makao” kwenye Luka 2:7.
c Kwa ajili ya mifano, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi, Desemba 1, 1996, ukurasa wa 3-8, na la Januari 15, 1998, ukurasa wa 3-7.