Sura 73
Msamaria Mwenye Fadhili za Kijirani
LABDA Yesu yuko karibu na Bethania, kijiji ambacho kiko umbali wapata kilometa 3 kutoka Yerusalemu. Mwanamume mmoja stadi katika sheria ya Musa amwendea akiwa na swali, akiuliza hivi: “Mwalimu, ni kwa kufanya nini mimi nitarithi uhai wa milele?”
Yesu anatambua kwamba mwanamume huyo, mwanasheria, auliza si ili apate habari tu, bali, badala ya hivyo, anataka kumjaribu. Huenda kusudi la mwanasheria huyo likawa kwamba anataka Yesu atoe jibu katika njia ambayo itachukiza Wayahudi walio wepesi wa kuchukizwa. Kwa hiyo Yesu anamfanya mwanasheria huyo ajifunge mwenyewe, kwa kuuliza: “Imeandikwaje katika Sheria? Wewe unasomaje?”
Katika kujibu, mwanasheria huyo, akionyesha muono-ndani usio wa kawaida, ananukuu kutoka sheria za Mungu kwenye Kumbukumbu 6:5 na Walawi 19:18, NW, akisema: “‘Lazima wewe umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako mzima na kwa nafsi yako nzima na kwa nguvu zako nzima na kwa akili yako nzima,’ na, ‘jirani yako kama wewe mwenyewe.’”
“Umejibu kwa usahihi,” Yesu anaitikia. “Endelea kufanya hivyo nawe utapata uhai.”
Hata hivyo, mwanasheria huyo hatosheki. Jibu la Yesu si mahususi vya kutosha kwake. Anataka uthibitisho kutoka kwa Yesu kwamba maoni yake mwenyewe ni sahihi na kwa sababu hiyo yeye anawatendea wengine kwa uadilifu. Kwa hiyo anauliza: “Kwa kweli jirani yangu ni nani?”
Wayahudi wanaamini kwamba neno “jirani” linatumika kwa Wayahudi wenzao tu, kama vile mistari inayozunguka Walawi 19:18, NW, inavyoonekana ikionyesha. Kwa kweli, baadaye hata mtume Petro alisema: “Nyinyi mnajua jinsi lisivyo jambo la kisheria kwa Myahudi kujiunga mwenyewe na au kumwendea mwanamume wa kabila jingine.” Kwa hiyo yule mwanasheria, na labda wanafunzi wa Yesu pia, wanaamini kwamba wao ni waadilifu ikiwa wanawatendea Wayahudi wenzao tu kwa fadhili, kwa kuwa, kwa maoni yao, watu wasio Wayahudi si majirani wao kikweli.
Yesu anaweza kurekebishaje oni lao bila kuchukiza wasikilizaji wake? Yeye anasimulia hadithi, labda ikitegemea jambo ambalo lilitukia kikweli. “[Myahudi] fulani,” Yesu anaeleza, “alikuwa akiteremka kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko na akaanguka miongoni mwa wanyang’anyi, ambao walimvua mavazi na kumpiga pia, nao wakaondoka, wakimwacha akiwa karibu sana kufa.”
“Sasa, kwa sadfa,” Yesu anaendelea, “kuhani mmoja alikuwa akiteremka katika barabara hiyo, lakini, alipomwona, alimpita akaenda kwenye ule upande mwingine. Vivyo hivyo, Mlawi pia, alipoteremka akafika mahali hapo na kumwona, alipita akaenda kwenye ule upande mwingine. Lakini Msamaria mmoja akisafiri njia hiyo alimfikia na, alipomwona, alisukumwa na sikitiko.”
Makuhani wengi na Walawi wasaidizi wao wa hekaluni wanaishi Yeriko, umbali wa kilometa 23 katika barabara hatari ambayo inashuka meta 900 kutoka mahali ambapo wanatumikia kwenye hekalu katika Yerusalemu. Kuhani yule na Mlawi wangetazamiwa wasaidie Myahudi mwenzao akiwa katika taabu. Lakini wao hawafanyi hivyo. Badala ya hivyo, Msamaria anafanya hivyo. Wayahudi wanawachukia Wasamaria sana hivi kwamba hivi karibuni walimtukana Yesu kwa maneno yaliyo makali kupita yote kwa kumwita “Msamaria.”
Msamaria yule anafanya nini ili asaidie yule Myahudi? “Yeye alimwendea,” Yesu anasema, “na kuvifunga vidonda vyake, akimwaga mafuta na divai juu yavyo. Kisha akampandisha juu ya hayawani wake mwenyewe na kumleta katika mkahawa na kumtunza. Na siku ya pili alitoa dinari mbili [karibu mshahara wa siku mbili], na kumpa mtunza mkahawa, akisema, ‘Mtunze, na chochote utakachotumia zaidi ya hizi, mimi nitakulipa nitakaporudi hapa.’”
Baada ya kusimulia hadithi hiyo, Yesu auliza mwanasheria yule: “Ni nani kati ya hawa watatu anayeonekana kwako kuwa alijifanya mwenyewe kuwa jirani kwa mwanamume yule ambaye alianguka miongoni mwa wanyang’anyi?”
Akihisi kuwa ni jambo lisilofaa kumpa Msamaria sifa yoyote, mwanasheria yule anajibu hivi kwa urahisi: “Yule aliyetenda kwa rehema kumwelekea.”
“Enda zako na uwe ukifanya viyvo hivyo wewe mwenyewe,” Yesu anamalizia.
Kama Yesu alimwambia mwanasheria yule moja kwa moja kwamba watu wasio Wayahudi ni majirani wake pia, si kwamba tu mwanamume huyo hangekubali hilo, bali yaelekea walio wengi kati ya wasikilizaji wangekubaliana naye katika mazungumzo yake pamoja na Yesu. Hata hivyo, hadithi hii inayoeleza matukio ya kweli maishani inaonyesha waziwazi katika njia isiyoweza kukanushika kwamba majirani wetu wanatia ndani watu zaidi ya wale wa kabila na taifa letu tu. Lo! Yesu ana njia nzuri ajabu kama nini ya kufundisha! Luka 10:25-37; Matendo 10:28; Yohana 4:9; 8:48, NW.
▪ Mwanasheria anauliza Yesu maswali gani, na kwa wazi kusudi lake la kuuliza ni nini?
▪ Wayahudi wanaamini ni nani walio majirani wao, na kuna sababu gani ya kuamini kwamba hata wanafunzi wanashiriki oni hilo?
▪ Yesu anaonyeshaje oni lililo sahihi hivi kwamba mwanasheria huyo hangeweza kulikanusha?