Wewe Waweza Kuishi Muda Gani?
WENGI wetu tutakubali kwa utayari kwamba kuna matatizo katika kijia cha maisha. Lakini, tunafurahi kuwa hai. Haturidhiki na utoto wetu tu wala na muda mfupi wa maisha; tungependa kuishi kwa miaka mingi. Hata hivyo, kifo chaonekana kuwa kisichoepukika. Je! ni kweli?
Je! kifo chaweza kukawizwa? Je! muda wa maisha yetu waweza kurefushwa?
Muda wa Maisha Uliorefushwa?
Katika 1990 ripoti fulani ya habari ilitangaza uwezekano wa kurefusha muda wa maisha wa kibinadamu hadi “miaka mia na kumi.” Bila shaka hilo lilikuwa rejezeo lisilo la moja kwa moja kwenye maneno haya ya mtunga-zaburi wa Biblia, Musa: “Siku za miaka yetu ni miaka sabini, na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; na kiburi chake ni taabu na ubatili, maana chapita upesi tukatokomea mara.” (Zaburi 90:10) Kwa hiyo Biblia hutoa miaka 70 au 80 kuwa wastani wa muda wa maisha wa kibinadamu. Lakini ni nini kinachoelekea kuwa idadi ya miaka ambayo mtu aweza kutazamia kuishi leo?
Ripoti moja iliyochapwa na WHO (Shirika la Afya Ulimwenguni) katika 1992 iliweka wastani wa muda wa maisha ulimwenguni pote kuwa miaka 65. Kulingana na WHO, huo “ulitazamiwa kuongezeka kwa karibu miezi minne kwa mwaka kwa muda wa miaka mitano ifuatayo, hasa kwa sababu ya kupungua kwa vifo vya watoto wachanga.” Hata hivyo, hata ikiwa muujiza wa kitiba ungezuia kifo cha mtu yeyote kabla ya umri wa miaka 50, gazeti Time lasema kwamba katika United States, “ongezeko katika wastani wa muda wa kuishi ungekuwa miaka 3 1/2 tu.”
Kwa Nini Maisha Ni Mafupi Hivyo?
Dakt. Jan Vijg wa Taasisi ya Kuchunguza ya Uzee ya Uholanzi atoa hoja kwamba kama vile tu magonjwa fulani yanavyohusianishwa na kasoro katika muundo wa chembe za mwili wa kibinadamu, ndivyo utaratibu wa kuzeeka waonekana huathiriwa na mambo ya kijeni [urithi]. Watafiti fulani huamini kwamba tungeweza kuishi muda mrefu zaidi ikiwa mahali pa “jeni kuu chache” pangeweza kuchukuliwa na jeni mpya tunapozeeka. Wengine huita dokezo hilo “sahili mambo kupita kiasi.”
Hata hivyo, wanasayansi hukubali kwamba “yaonekana kuna aina fulani ya mpaka wa kibiolojia uliojengwa ndani ya chembe za mwili wa kibinadamu,” laripoti gazeti Time. Hata wale wabishao kwamba “tumebuniwa kuendelea kuwa hai” hukiri kwamba “jambo fulani huharibika.” Kwa kweli, tukiwa wenye miaka 65, 70, au 80 au miaka zaidi kidogo, uhai wetu ‘unatokomea mara’ katika kifo, kama vile Biblia isemavyo.
Lakini, yule mtume Mkristo Paulo wa karne ya kwanza W.K. alitabiri hivi kwa uhakika: “Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti [kifo, New World Translation].” (1 Wakorintho 15:26) Kifo chaweza kumalizwaje? Hata kikimalizwa, wewe waweza kukabilianaje na kifo cha wapendwa leo?