Karibuni—Ulimwengu Usio na Vita!
MNAMO Desemba 24, 1914, askari-jeshi mchanga Mwingereza aitwaye Jim Prince alivuka nchi ya ukiwa (kati ya mipaka miwili) ili kuongea na askari-jeshi mmoja wa miguu Mjerumani. “Mimi ni Msaksoni. Wewe ni Msaksoni-Mwingereza. Mbona sisi twapigana?” Mjerumani huyo akamuuliza. Miaka kadhaa baadaye, Prince alikiri hivi: “Bado sijui jibu la swali hilo.”
Kwa juma moja lisilo la kawaida katika 1914, askari-jeshi wa majeshi ya Uingereza na Ujerumani walifanya urafiki, wakacheza kandanda, na hata kubadilishana zawadi za Krismasi. Bila shaka, amani hiyo ya muda, haikuwa rasmi. Majemadari hawakutaka vikosi vyao vigundue kwamba yule “adui” hakuwa yule dubwana mkatili aliyeonyeshwa katika propaganda za vita. Askari-jeshi mmoja Mwingereza Albert Moren alikumbuka hivi baadaye: “Ikiwa huo muda wa kuacha kupigana ungaliendelea kwa juma jingine, ingalikuwa vigumu sana kuianzisha vita tena.”
Muda huo wa kuacha kupigana kwa hiari wadokeza kwamba hata askari-jeshi wengi ambao wamezoezwa hutamani amani kuliko vita. Askari-jeshi walio wengi ambao wamejua matisho ya mapigano wangekubaliana na mithali hii ya Kihispania: “Acha yule asiyejua jinsi vita ilivyo aende vitani.” Bila shaka, uchunguzi wa maoni wenye kufanywa ulimwenguni pote miongoni mwa watu kwa ujumla ungefunua kwamba watu walio wengi sana hupendelea amani kuliko vita. Lakini tamaa hiyo ya kupata amani ya watu wote ulimwenguni yaweza kugeuzwaje kuwa ulimwengu usio na vita?
Kabla ya vita kuweza kubatilishwa, ni lazima mitazamo ibadilike. Katiba ya Shirika la UM linaloshughulikia Elimu, Sayansi, na Utamaduni husema hivi: “Kwa kuwa vita huanza akilini mwa watu, ni lazima utetezi wa amani ufanyizwe akilini mwa watu.” Lakini jamii ya ki-siku-hizi, ambamo kutotumaini na chuki zimeenea sana, inakuwa yenye jeuri zaidi, si yenye amani zaidi.
Hata hivyo, Mungu mwenyewe aliahidi kwamba siku moja amani ingeandikwa juu ya akili za watu wenye mwelekeo mwadilifu. Kupitia nabii wake Isaya, alisema hivi: “Naye [Mungu] atafanya hukumu katika mataifa mengi, atawakemea watu wa kabila nyingi; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:4.
Kuendeleza Amani Akilini
Je! badiliko hilo la fikira lenye kutokeza laweza kutukia? Je! watu watajifunza wakati wowote kuilinda amani badala ya kutukuza vita? Fikiria kielelezo cha Wolfgang Kusserow. Katika 1942 Wanazi walikata kichwa cha Mjerumani huyo mwenye umri wa miaka 20 kwa sababu yeye ‘hangejifunza vita.’ Kwa nini alichagua kufa? Katika taarifa moja aliyoandika, yeye alinukuu kanuni za Kimaandiko kama vile, “Mpende jirani yako kama nafsi yako” na, “Wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 22:39; 26:52) Kisha akasema hivi kwa wazi: “Je! Muumba wetu aliamuru hayo yote yaandikiwe miti?”
Neno la Mungu, ambalo limerekodiwa katika Biblia, “lina nguvu” na lilimchochea Shahidi huyo mchanga wa Yehova afuatie amani, hata matokeo yawe ni nini. (Waebrania 4:12; 1 Petro 3:11) Lakini si Wolfgang Kusserow peke yake aliyefuatia amani hivyo. Katika kitabu The Nazi Persecution of the Churches 1933-45, J. S. Conway ataja hati rasmi za Nazi zinazoshuhudia kwamba Mashahidi wa Yehova wakiwa kikundi walikataa kutumia silaha. Kama vile Conway aonyeshavyo, msimamo huo wenye moyo mkuu ulimaanisha kwa kweli kutia sahihi hati ya kifo chao wenyewe.
Mashahidi wa Yehova leo huendelea kufuatia amani, wawe ni wa rangi au taifa jipi. Kwa nini? Kwa sababu wamejifunza kutoka katika Biblia kwamba watumishi wa kweli wa Mungu wapaswa kufua panga zao ziwe majembe. Alejandro, kijana mmoja Mwarjentina aliyehamia Israel katika 1987, aweza kushuhudia jambo hilo binafsi.
Kwa miaka mitatu Alejandro aliishi katika kibbutz (shamba) huku akijifunza kwenye chuo kikuu kimoja na kufanya kazi katika hoteli na mikahawa mbalimbali. Wakati huo, alianza kuisoma Biblia na alikuwa akitafuta-tafuta kusudi maishani. Zaidi ya yote, alitamani kuona ulimwengu ambamo watu wangeweza kufurahia amani na haki. Alejandro—ambaye ni Myahudi—alifanya kazi karibu na Wayahudi na Waarabu lakini alipendelea kutounga mkono upande wowote.
Katika 1990 rafiki mmoja aliyekuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova alimwalika Alejandro kwenye kusanyiko la siku moja katika Haifa. Akistaajabu kuona Wayahudi na Waarabu 600 wakichangamana kwa furaha kwenye kusanyiko, alijiambia, ‘Hii ndiyo njia ifaayo kwa watu kuishi.’ Katika muda wa miezi sita, yeye mwenyewe akawa Shahidi na sasa hutumia sehemu kubwa ya wakati wake akihubiri ujumbe wa Biblia wa amani.
Jinsi Mungu Atakavyoleta Amani
Ingawa vielelezo hivyo vyagusa moyo sana, hivyo si vya kawaida katika ulimwengu wa leo. Ingawa mfumo uliopo hutoa matangazo kuhusu amani, huo hutia maji mbegu za vita. Je! ungependa kuishi katika eneo ambalo wakazi hutumia kati ya asilimia 7 na 16 ya machumo yao kununua bunduki na vifaa vya kulinda nyumba zao? Kwa kweli, mataifa yamekuwa yakifanya hivyo katika miaka ya hivi karibuni kupitia gharama za kijeshi. Haishangazi kwamba, unabii wa Isaya hufunua kwamba ainabinadamu kwa ujumla haitafua kamwe panga zayo ziwe majembe mpaka Mungu ‘anyooshe mambo juu ya jamii za watu wengi.’ (New World Translation) Yeye atafanyaje hivyo?
Njia ya msingi ya kunyoosha mambo ni Ufalme wa Yehova Mungu. Nabii Danieli alitabiri kwamba ‘Mungu wa mbinguni angeusimamisha ufalme ambao haungeangamizwa milele.’ Ufalme huo, yeye aongeza, “utavunja falme hizi zote [serikali za kilimwengu] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” (Danieli 2:44) Maneno hayo yafunua kwamba Ufalme wa Mungu utasimamisha imara utawala wao juu ya dunia yote. Kwa kuondolea mbali mipaka yote ya kitaifa, Ufalme huo utabatilisha ushindani. Zaidi ya hayo, kwa kuwa raia wao watakuwa “watu waliofundishwa na Yehova,” amani yao “itakuwa nyingi.” (Isaya 54:13, NW) Si ajabu kwamba Yesu alituambia tusali kwa Mungu: “Ufalme wako uje”!—Mathayo 6:9. In Union Version Swahili
Kuondolea Mbali Vizuizi vya Kidini
Mungu ataondolea mbali pia vizuizi vya amani vinavyosababishwa na dini. Dini ndiyo iliyosababisha lile pigano lenye silaha la muda mrefu zaidi katika historia—zile Krusedi, au “Vita Vitakatifu,” vilivyoanzishwa na Papa Urban 2 katika 1095 W.K.a Katika karne yetu makasisi wamekuwa mashuhuri katika kuvutia wengi waunge mkono vita, hata vile vyenye asili ya kilimwengu kabisa.
Akirejezea fungu la makanisa ya Kikristo kwa jina wakati wa Vita ya Ulimwengu 1, mwanahistoria Paul Johnson aliandika hivi: “Makasisi hawakuweza, na kwa sehemu kubwa hawakutaka, kuweka imani ya Kikristo mbele ya taifa. Walio wengi walichagua njia iliyo rahisi zaidi na kuusawazisha Ukristo na uzalendo. Askari-jeshi Wakristo wa madhehebu yote walihimizwa wauane katika jina la Mwokozi wao.”
Dini imefanya mengi kuchochea vita kuliko kusitawisha amani. Kwa kweli, Biblia huonyesha dini bandia kuwa “kahaba” atoshelezaye watawala wa ulimwengu. (Ufunuo 17:1, 2) Mungu amjulisha kuwa msababishi mkuu wa umwagaji damu wa wale wote waliochinjwa duniani. (Ufunuo 18:24) Kwa hiyo, Yehova Mungu ataondolea mbali kizuizi hiki cha amani mara moja kwa wakati wote.—Ufunuo 18:4, 5, 8.
Hata mambo yenye kuleta migawanyiko kama vile siasa na dini bandia yakiwa yametoweka, amani haingekuwa salama kamwe bila kuondolewa kwa yule mchochezi wa vita mkuu zaidi ya wote—Shetani Ibilisi. Hilo ndilo jambo la mwisho ambalo Ufalme wa Mungu utafanya katika programu yao ya kuleta amani kamili duniani. Kitabu cha Biblia cha Ufunuo hueleza kwamba Shetani ‘atashikwa’ na ‘kufungwa’ na ‘kutupwa katika abiso’ ili “asipate kuongoza vibaya mataifa tena.” Baadaye ataangamizwa kabisa.—Ufunuo 20:2, 3, 10, NW.
Ahadi ya Biblia juu ya mwisho wa vita si ndoto tu. Mpango wa Yehova Mungu wa kuleta amani umeanzishwa tayari. Ufalme wake umesimamishwa mbinguni na uko tayari kutekeleza hatua zaidi za kuhakikisha amani ya duniani pote. Wakati uo huo, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova, ambao huunga mkono serikali hiyo ya kimbingu, wamejifunza kuishi katika amani.
Kwa wazi, basi, tuna sababu zifaazo za kuamini kwamba vita vyaweza kuepukwa. Jambo lililo bora zaidi ni kwamba, twaweza kutazamia ile siku iliyo karibu ambayo Yehova atakomesha vita milele. (Zaburi 46:9) Yeye atahakikisha kwamba karibuni kutakuwa na ulimwengu usio na vita.
[Maelezo ya Chini]
a Nyakati nyingine viongozi wa kidini wenyewe walikuwa wanavita. Katika Mapigano ya Hastings (1066), askofu Mkatoliki Odo alitetea kuhusika kwake sana katika vita kwa kutumia rungu lenye vyuma vinavyochomoza badala ya upanga. Alidai kwamba ikiwa damu haikumwagwa, mtu wa Mungu angeweza kuua kihalali. Karne tano baadaye, Kardinali Ximenes aliongoza binafsi shambulio la Kihispania dhidi ya Afrika Kaskazini.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Waweza kuishi katika ulimwengu mpya usio na vita