Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 2/15 kur. 5-7
  • Je! Mashahidi wa Yehova Ni Kidhehebu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Mashahidi wa Yehova Ni Kidhehebu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kile Ambacho Ithibati Yaonyesha
  • Dini Ijulikanayo Vema
  • “Wenye Kujishughulisha Sana na Wanadamu”
  • Kushikamana Sana na Biblia
  • Kiongozi Wao Ni Nani?
  • Mashahidi wa Yehova
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Je, Mashahidi wa Yehova Ni Dhehebu?
    Maswali Yanayoulizwa Mara Nyingi Kuhusu Mashahidi wa Yehova
  • Vidhehebu—Hivyo Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Wakristo na Jamii ya Kibinadamu Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 2/15 kur. 5-7

Je! Mashahidi wa Yehova Ni Kidhehebu?

YESU KRISTO alishtakiwa kuwa mlevi, mlafi, mvunja-Sabato, shahidi bandia, mkufuru Mungu, na mjumbe wa Shetani. Pia alishtakiwa kuwa mwenye kufitini serikali.—Mathayo 9:34; 11:19; 12:24; 26:65; Yohana 8:13; 9:16; 19:12.

Baada ya kifo na ufufuo wa Yesu, wanafunzi wake vilevile walikuwa shabaha ya mashtaka mabaya. Kikundi kimoja cha Wakristo wa karne ya kwanza walikokotwa hadi kwa watawala wa jiji na watu waliokuwa wakipaaza sauti: ‘Watu hawa wameupindua ulimwengu.’ (Matendo 17:6) Kwenye pindi nyingine mtume Paulo na mwandamani wake Sila walipelekwa kwa wenye mamlaka na kushtakiwa kuvuruga sana jiji la Filipi.—Matendo 16:20.

Baadaye Paulo alishtakiwa kuwa “mkorofi, mwanzilizi wa fitina katika Wayahudi wote duniani” na kujaribu “kulitia hekalu unajisi.” (Matendo 24:5, 6) Wakuu wa Wayahudi katika Roma walieleza kwa usahihi hali ya wafuasi wa Yesu walipokiri hivi: “Kwa maana katika habari za madhehebu hiyo imejulikana kwetu kwamba inanenwa vibaya kila mahali.”—Matendo 28:22.

Kwa wazi, kikundi hicho kipya kilichoanzishwa na Yesu Kristo kilionwa na wengine kuwa kikundi cha kidini chenye maoni na mazoea tofauti yaliyopingana na mwenendo wa kijamii uliokubaliwa kuwa wa kawaida katika siku hizo. Bila shaka, wengi leo wangaliwaona Wakristo kuwa kidhehebu chenye uharibifu. Mara nyingi wenye kushtaki walikuwa washiriki mashuhuri wa jumuiya waliostahiwa, na laonekana hilo liliongeza uzito wa mashtaka hayo. Wengi waliamini yale mashtaka dhidi ya Yesu na wanafunzi wake. Lakini, kama vile huenda ukajua, kila moja la mashtaka hayo lilikuwa bandia! Uhakika wa kwamba watu walisema mambo hayo haukuyafanya yawe kweli.

Namna gani leo? Je! ingekuwa sahihi kuwarejezea Mashahidi wa Yehova kuwa kikundi cha kidini chenye maoni na mazoea tofauti yanayopingana na mwenendo wa kijamii unaokubaliwa kuwa wa kawaida? Je! Mashahidi wa Yehova ni kidhehebu?

Kile Ambacho Ithibati Yaonyesha

Ofisa mmoja wa serikali wa jiji la St. Petersburg, Urusi, alieleza hivi: “Tulijulishwa kwamba Mashahidi wa Yehova ni aina fulani ya kidhehebu cha kichini-chini kinachofanya mambo gizani na kuchinja watoto na kujiua.” Hata hivyo, hivi karibuni watu wa Urusi wamekuja kufahamu vema zaidi jinsi Mashahidi walivyo. Baada ya kufanya kazi pamoja na Mashahidi wa Yehova kuhusiana na mkusanyiko wa kimataifa, ofisa uyo huyo alionelea hivi: “Sasa naona watu wa kawaida, wenye kutabasamu, hata walio bora zaidi ya watu wengi niwajuao. Wao ni wenye amani na watulivu, nao hupendana sana.” Aliongeza hivi: “Kwa kweli sielewi kwa nini watu husema uwongo mwingi jinsi hiyo juu yao.”

Mashahidi wa Yehova hawafanyi mikutano ya kisherehe, wala ibada yao si ya kisiri. Mtunga-vitabu mmoja asiye Shahidi, Julia Mitchell Corbett, aonyesha hivi: “Wakutanapo, kwa kawaida zaidi ya mara moja kwa juma, katika Majumba ya Ufalme (mahali pao pa kukutania hapaitwi makanisa), wakati wao mwingi hutumiwa katika kujifunza na kuzungumzia Biblia.” Mahali pao pa kukutania huonyeshwa waziwazi kwa ubao (wenye maneno “Jumba la Ufalme”). Mikutano ni ya peupe, na watu wote wanaalikwa kuhudhuria. Wageni wasiotazamiwa wanakaribishwa sana.

“Mashahidi wamejipatia sifa ya kuwa wenye kufuatia haki, wenye adabu nzuri, na wenye bidii ya kazi,” aongeza Corbett katika kitabu chake Religion in America. Wengi wasio Mashahidi hukiri kwa utayari kwamba hakuna jambo lolote la kiajabu au la kigeni kuhusu Mashahidi wa Yehova. Mwenendo wao haupingani na mwenendo wa kijamii unaokubaliwa kuwa wa kawaida. The New Encyclopædia Britannica yasema kwa usahihi kwamba Mashahidi “husisitiza juu ya kiwango cha juu cha kiadili katika mwenendo wa kibinafsi.”

Mkurugenzi mmoja wa habari na miradi ya pekee wa kituo kimoja cha televisheni katika United States aliwaandikia Mashahidi wa Yehova hivi kwa kuitikia ripoti yenye ubaguzi dhidi ya Mashahidi katika programu ya habari za televisheni iitwayo 60 Minutes. Alisema hivi: “Ikiwa watu wengi zaidi wangeishi jinsi imani yenu iishivyo, taifa hili lisingekuwa katika hali lililomo. Mimi ni mwandishi mmoja wa habari ajuaye kwamba tengenezo lenu lina msingi wa upendo na imani yenye nguvu katika Muumba. Nataka mjue kwamba si waandishi wa Habari wote walio na ubaguzi [dhidi yenu].”

Dini Ijulikanayo Vema

Je! yafaa kusema kwamba Mashahidi wa Yehova ni kikundi kidogo cha kidini chenye maoni ya kupita kiasi? Katika maana fulani, Mashahidi wa Yehova ni wachache zaidi wakilinganishwa na dini fulani. Hata hivyo, kumbuka yale ambayo Yesu alisema: “Mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache.”—Mathayo 7:13, 14.

Hata hivyo, Mashahidi si kidhehebu kidogo chenye maoni yenye kupita kiasi hata kidogo. Katika masika ya 1993, watu zaidi ya milioni 11 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo uliofanywa na Mashahidi. Lakini la maana zaidi ya idadi yao ni sifa yao ya kiadili na mwenendo wao wenye kielelezo chema, ambao umewaletea pongezi ulimwenguni pote. Bila shaka hilo limekuwa jambo la kuchangia katika nchi ambazo zimewapa utambuzi wa kisheria ikiwa dini ya kweli inayojulikana.

Wenye kutokeza ni uamuzi uliofikiwa hivi karibuni na Mahakama ya Haki za Kibinadamu ya Ulaya. Ulijulisha kwamba Mashahidi wapaswa kufurahia uhuru wa wazo, dhamiri, na dini na kwamba wana haki ya kusema juu ya imani yao na kuifundisha kwa wengine. Isingekuwa hivyo hata kidogo ikiwa Mashahidi wa Yehova walijulikana kutumia ufundi mbalimbali wenye udanganyifu na usio wa kiadili ili kupata washiriki au ikiwa walitumia njia za kuvuta kwa hila ili kudhibiti akili za wafuasi wao.

Watu wengi mno kotekote ulimwenguni wanawafahamu vema Mashahidi wa Yehova. Kati ya wale mamilioni wasio Mashahidi wanaojifunza Biblia pamoja na Mashahidi au ambao wamejifunza nao wakati mmoja au mwingine, twauliza, Je! kulikuwa na majaribio ya kukudanganya? Je! Mashahidi walitumia ufundi mbalimbali wa kuidhibiti akili yako? Bila shaka jibu lako la wazi lingekuwa “la.” Kwa wazi, ikiwa njia hizo zingalitumiwa, kungalikuwa watu wengi sana waliojionea hayo ambao wangepinga hoja yoyote ya kuwapendelea Mashahidi wa Yehova.

“Wenye Kujishughulisha Sana na Wanadamu”

Mara nyingi washiriki wa kidhehebu hujitenga na familia, marafiki, na hata na jamii kwa ujumla. Je! ndivyo ilivyo na Mashahidi wa Yehova? “Mimi si mmoja wa Mashahidi wa Yehova,” akaandika mwandishi mmoja wa habari katika Jamhuri ya Cheki. Lakini aliongeza hivi: “Ni wazi kwamba [Mashahidi wa Yehova] wana nguvu nyingi sana za kiadili. . . . Wao hutambua wenye mamlaka wa kiserikali lakini huamini kwamba ni Ufalme wa Mungu pekee ulio na uwezo wa kusuluhisha matatizo yote ya kibinadamu. Lakini ona kwamba—wao si washupavu. Wao ni watu wenye kujishughulisha sana na wanadamu.”

Nao hawaishi katika jumuiya ndogo-ndogo, wakijitenga wenyewe na watu wa ukoo na wengine. Mashahidi wa Yehova hutambua kwamba ni daraka lao la Kimaandiko kupenda na kutunza familia zao. Wao huishi na kufanya kazi pamoja na watu wa rangi na dini zote. Misiba itokeapo, wao wanaitikia upesi kwa kupeleka vifaa vya kusaidia na msaada mwingine wa fadhili.

La maana zaidi, wanashiriki katika programu ya kielimu ambayo haina kifani. Ni dini ngapi zilizo na mpango mzuri wa kufanya ziara za binafsi kwa kila mtu mmoja-mmoja katika jumuiya zazo? Mashahidi wa Yehova hufanya hivyo katika mabara zaidi ya 200 na katika lugha zaidi ya 200! Kwa wazi, Mashahidi wa Yehova ni “wenye kujishughulisha sana na wanadamu.”

Kushikamana Sana na Biblia

Kwa kweli, mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni tofauti na yale yanayoandaliwa na makanisa. Mashahidi wa Yehova huamini kwamba Yehova ndiye Mungu mweza yote na kwamba Yesu ndiye Mwanae, si sehemu ya kiabudiwa cha utatu. Imani yao inategemea itikadi kwamba Ufalme wa Mungu pekee ndio waweza kuleta kitulizo kwa wanadamu wanaoteseka. Wao huonya watu juu ya uharibifu unaokaribia wa mfumo huu wa mambo wenye ufisadi. Wao huhubiri juu ya ahadi ya Mungu kuhusu paradiso ya kidunia kwa ajili ya ainabinadamu tiifu. Hawatolei msalaba heshima ya kiibada. Hawaadhimishi Krismasi. Wao huamini kwamba nafsi inaweza kufa na kwamba hakuna moto wa helo. Hawatakula damu, wala kukubali kutiwa damu mishipani. Wao huepuka kujiingiza katika siasa wala hawashiriki katika vita. Je! umepata kujiuliza kwa nini mafundisho ya Mashahidi wa Yehova ni tofauti jinsi hiyo?

Gazeti la habari la Massachusetts, Daily Hampshire Gazette, laeleza kwamba “ufasiri wa kihalisi sana wa Biblia wa [Mashahidi wa Yehova] hukataza utendaji mwingi ambao wengine huona kuwa wenye kufaa . . . , yote hayo ni kwa kujitahidi tu kufuata kielelezo cha Wakristo wa karne ya kwanza na neno la Biblia.” The Encyclopedia of Religion yakubali kwamba “yote ambayo wao huamini yanategemea Biblia. Wao ‘huthibitisha kimaandiko’ (yaani, kuandaa mtajo wa kibiblia ili kutegemeza) karibu kila taarifa ya imani, wakikubali bila shaka yoyote mamlaka ya Biblia, ishindayo mapokeo kabisa.” Kitabu Religion in America chasema hivi: “Kikundi hicho hakijapata kamwe kuacha kukazia funzo la Biblia, na mafundisho yacho yanategemezwa na marejezo mengi kwenye andiko.”

Kiongozi Wao Ni Nani?

Ni kwa sababu hasa ya kushikamana sana na mafundisho ya Biblia kwamba kule kutolea watu heshima ya kiibada na kuwafanya sanamu kunakoonekana sana katika vidhehebu leo hakupatikani miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Wao hukatalia mbali wazo la kuwagawanya viongozi wa kidini na watu wa kawaida. The Encyclopedia of Religion yasema hivi kwa kufaa juu ya Mashahidi wa Yehova: “Jamii ya viongozi wa kidini na vyeo mbalimbali vinakatazwa.”

Wao humfuata Yesu Kristo akiwa kiongozi wao na Kichwa cha kutaniko la Kikristo. Ni Yesu aliyesema hivi: “Ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni. Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo.”—Mathayo 23:8-12.

Ni wazi kwamba Mashahidi wa Yehova si kidhehebu hata kidogo kama vile Yesu hakuwa mlafi wala mlevi hata kidogo. Kwa kweli, si kila mtu aliyevutwa na ripoti bandia juu ya Yesu na wanafunzi wake aliyeangukia katika mtego wa kumchongeza. Huenda ikawa wengine waliarifiwa vibaya tu. Ikiwa una maswali juu ya Mashahidi wa Yehova na imani zao, kwa nini usipate kuwajua vema zaidi? Milango ya Majumba ya Ufalme yao iko wazi kabisa kwa wote watafutao kweli.

Wewe pia waweza kunufaika na kutafuta kwao kwa uangalifu ujuzi sahihi wa Biblia na kujifunza jinsi ya kumwabudu Mungu kulingana na maneno ya Yesu: “Saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.”—Yohana 4:23.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki