Jitenge Mbali Hatari Itishapo
NI WATU wachache wanaoitikia hatari upesi zaidi ya mabaharia. Ni lazima wawe macho kuona mabadiliko yoyote katika halihewa, kiasi cha maji ya bahari, na umbali wa meli yao kutoka pwani. Maji mengi na pepo zinapoungana na kuisukuma meli kuelekea ufuoni, mabaharia hukabili kazi ngumu na hatari.
Chini ya hali hizo—ziitwazo lee shore (ufuo ulioko upande wa meli usioelekea upepo)—baharia hudumisha nafasi kubwa ya bahari ya kutosha kati ya mashua yake na pwani, hasa ikiwa chombo hicho kinaendeshwa kwa tanga pekee. Kitabu juu ya kuendesha meli chaeleza kwamba ‘kupatwa na upepo mkali karibu na ufuo ulioko upande wa meli usioelekea upepo labda ndiyo hali iliyo mbaya zaidi’ ambamo baharia aweza kujipata mwenyewe. Suluhisho lililopendekezwa? ‘Usiruhusu kamwe chombo chako kipatikane katika hatari hiyo.’ Njia salama ya kuepuka kuvunjikiwa meli kwenye fungu la mchanga au ufuo wenye miamba ni kujitenga mbali na hatari.
Ni lazima Wakristo wawe wepesi kuitikia hatari ambazo zingeweza kuharibu imani yao kama vile meli iliyovunjika. (1 Timotheo 1:19) Siku hizi, hali hazifai hata kidogo kuweza kudumisha mwendo ulio thabiti. Kama vile mashua iwezavyo kukengeushwa na pepo na maji mengi, ndivyo maisha zetu zilizowekwa wakfu zaweza kupotea njia kwa sababu ya kuvutwa daima na mwili wetu usio mkamilifu na kule kushindana daima na roho ya ulimwengu—ambayo sasa ina nguvu sawasawa na upepo wenye nguvu nyingi.
Mtu Fulani Aliyejihatarisha
Ni rahisi kama nini kujiingiza katika maji ya kiroho yaliyo hatari bila kukusudia!
Fikiria kielelezo kilichotokea karibu na Baharifu, ambayo ni bahari iliyozungukwa na bara. Twarejezea kielelezo cha Loti. Uamuzi wake wa kuishi katika Sodoma ulimletea matatizo mengi na huzuni nyingi. Baada ya mzozo kati ya wachungaji wao, Abrahamu na Loti walikuwa wamekubali kuishi katika sehemu tofauti-tofauti. Tunaambiwa kwamba Loti alichagua Wilaya ya Yordani akapiga hema miongoni mwa majiji ya Wilaya hiyo. Baadaye, aliamua kuishi katika Sodoma, hata ingawa mtindo-maisha wa Wasodoma ulimsononesha.—Mwanzo 13:5-13; 2 Petro 2:8.
Kwa nini Loti aliendelea kuishi katika jiji lenye sifa mbaya ya kiadili lililomwudhi Yehova sana na hata likasababisha kilio kutoka kwa watu walioishi karibu nalo? Sodoma lilikuwa lenye ufanisi, na bila shaka mke wa Loti alifurahia faida za kimwili za maisha ya jijini. (Ezekieli 16:49, 50) Labda hata Loti alivutiwa na hali nzuri sana ya kiuchumi ya Sodoma. Sababu yake ya kuishi huko hata iwe ilikuwa nini, yeye angalipaswa kuondoka mapema zaidi ya wakati alipotoka. Mwishowe familia ya Loti iliondoka eneo lile la hatari kwa sababu tu ya kusihiwa kwa uharaka na malaika wa Yehova.
Simulizi la Mwanzo lasema hivi: “Hata alfajiri ndipo malaika wakamhimiza Lutu, wakisema, Ondoka, mtwae mkeo na binti zako wawili waliopo hapa, usipotee katika maovu ya mji huu.” Lakini hata baada ya onyo hilo la haraka, Loti ‘alikawia-kawia.’ Mwishowe, malaika hao ‘wakamshika mkono, na mkono wa mkewe, na mkono wa binti zake wawili, wakamtoa wakamweka nje ya jiji.’—Mwanzo 19:15, 16.
Wakiwa nje ya jiji, malaika waliipa familia ya Loti maagizo fulani ya mwisho: “Jiponye nafsi yako; usitazame nyuma, wala usisimame katika hilo bonde po pote; ujiponye mlimani, usije ukapotea.” (Mwanzo 19:17) Hata hivyo, Loti aliomba ruhusa ya kwenda kwenye jiji la karibu la Soari badala ya kuondoka mkoa huo kabisa. (Mwanzo 19:18-22) Kwa wazi, Loti alisita kujitenga mbali awezavyo na hatari.
Njiani kwenda Soari, mke wa Loti alitazama nyuma kuelekea Sodoma, yaonekana akitamani vitu alivyokuwa ameacha nyuma. Kwa sababu ya kutotii maagizo ya malaika, alipoteza uhai wake. Loti—mtu mwadilifu—aliokoka uharibifu wa jiji hilo pamoja na binti zake wawili. Lakini alipatwa na hasara iliyoje kwa sababu ya kuchagua kuishi karibu na hatari!—Mwanzo 19:18-26; 2 Petro 2:7.
Kujitenga Mbali na Hatari
Ono chungu la Loti laonyesha ni nini laweza kutukia tukikaribia au kukaakaa katika mazingira ya hatari. Hekima ingeonyesha kwamba, kama vile mabaharia, hatujiruhusu kamwe kuingia katika hatari ya jinsi hiyo. Ni nini baadhi ya mambo ya hatari ambayo twapaswa kujitenga nayo? Wakristo wengine wamekengeushwa kwa kujiingiza mno katika shughuli za kibiashara, kwa kuwa na mahusiano ya karibu na washirika walimwengu, au kwa kushikamana kihisiamoyo na mtu wa jinsia tofauti wakati hali zao haziwaruhusu kufunga ndoa.
Katika kila hali, mwendo wenye hekima ni kujitenga mbali na hatari. Kwa kielelezo, je, tuko macho kuona hatari za kiroho ambazo zaweza kuletwa na ile iitwayo eti fursa nzuri ya biashara? Ndugu fulani wamejiingiza sana katika shughuli za kibiashara kwa hasara ya familia zao, afya yao, na madaraka yao ya kitheokrasi. Nyakati nyingine uvutano ni ule mtindo-maisha wenye ustarehe zaidi uwezao kupatikana kwa fedha. Nyakati nyingine ni ule mwito wa ushindani wa kutahini uwezo wao wa kufanikiwa katika biashara. Huenda wengine wakasababu kwamba kusudi lao ni kuwaandalia ndugu wengine kazi za kuajiriwa au kuweza kuchanga kwa ukarimu zaidi kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Labda wanafikiri kwamba biashara inapositawi, watakuwa na wakati mwingine zaidi wa kutolea masilahi ya Ufalme.
Ni nini baadhi ya mitego? Hali ya kiuchumi iwezayo kubadilika wakati wowote na “tukio lisilotazamiwa” zaweza kuharibu shughuli ya kibiashara iliyopangwa vizuri kabisa. (Mhubiri 9:11, NW) Kung’ang’ana na madeni mengi kwaweza kuleta uchungu na kuchukua mahali pa mambo ya kiroho. Na hata biashara inapositawi, yaelekea itatumia wakati na nishati nyingi ya kiakili, na huenda ikataka mtu ashirikiane sana na walimwengu.
Mzee mmoja wa Kikristo katika Uhispania alikuwa na magumu mengi ya kifedha wakati kampuni moja ya bima ilipomtolea fursa yenye kushawishi. Ingawa kulikuwa na mataraja ya kuchuma fedha nyingi sana akiwa muuzaji wa bima wa kujiandika, alikataa toleo hilo hatimaye. “Hilo halikuwa uamuzi rahisi kufanya, lakini nafurahi kwamba nilisema la,” yeye aeleza. “Kwanza, sikutaka kuchuma fedha—hata kwa njia isiyo ya moja kwa moja—kupitia wale niliowajua kitheokrasi. Na ingawa nilipenda kujifanyia kazi mwenyewe, ningalipaswa kusafiri sana na kutumia muda wa saa nyingi kazini. Hilo bila shaka lingalimaanisha kupuuza familia yangu na kutaniko. Zaidi ya yote, nasadiki kwamba ikiwa ningalikubali toleo hilo, ningalipoteza udhibiti wa maisha yangu.”
Hakuna Mkristo awezaye kukubali kupoteza udhibiti wa maisha yake. Yesu alionyesha matokeo yenye msiba ya mwendo wa jinsi hiyo kwa kusimulia kielezi cha mtu aliyelimbika mali zaidi na zaidi ili kustaafu na kufanya maisha yawe rahisi. Lakini ule usiku wenyewe alioamua kwamba hatimaye alikuwa amekusanya fedha za kutosha, alikufa. “Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu,” Yesu akaonya.—Luka 12:16-21; linganisha Yakobo 4:13-17.
Ni lazima pia tuwe macho dhidi ya kushirikiana kwa muda mrefu na walimwengu. Labda ni jirani, rafiki shuleni, mfanyakazi mwenzetu, au mshiriki wa biashara. Huenda tukasababu hivi, ‘Yeye hustahi Mashahidi, yeye ana adili nzuri, na sisi huongea juu ya kweli pindi kwa pindi.’ Lakini, ono la wengine lathibitisha kwamba baada ya wakati fulani huenda sisi tukajipata wenyewe tukipendelea ushirika huo wa kilimwengu kuliko ule wa ndugu au dada wa kiroho. Ni nini baadhi ya hatari za urafiki wa jinsi hiyo?
Huenda tukaanza kupuuza uharaka wa nyakati tunamoishi au kupendezwa zaidi na mambo ya kimwili badala ya mambo ya kiroho. Labda, kwa sababu ya kuwa na hofu ya kutompendeza rafiki mlimwengu, tungetamani hata kukubaliwa na ulimwengu. (Linganisha 1 Petro 4:3-7.) Kwa upande ule mwingine, mtunga-zaburi Daudi alipendelea kushirikiana na watu waliompenda Yehova. “Nitalihubiri jina lako kwa ndugu zangu, katikati ya kusanyiko nitakusifu,” yeye akaandika. (Zaburi 22:22) Tutalindwa tukiiga kielelezo cha Daudi, tukitafuta urafiki uwezao kutujenga kiroho.
Mwendo mwingine wa hatari ni mtu kuwa na uhusiano wa kihisiamoyo na mtu wa jinsia tofauti wakati hali yake haimruhusu kufunga ndoa. Hatari yaweza kutokea mtu anapovutiwa na mtu fulani mwenye sura ya kupendeza, ambaye mazungumzo yake yanasisimua, na ambaye hata ana mtazamo uleule na hufurahishwa na mambo yaleyale yanayotufurahisha. Mtu aweza kufurahishwa na ushirika wake, akisababu hivi, ‘Najua kiwango cha kufikia. Sisi ni marafiki tu.’ Hata hivyo, mara hisia zimeamshwa si rahisi kuzidhibiti.
Mary, dada mchanga aliyeolewa, alifurahia ushirika wa Michael.a Alikuwa ndugu mzuri lakini aliona ni vigumu kufanya marafiki. Walikuwa na mambo mengi yenye kufanana, na waliona kwamba waliweza kufanya utani pamoja. Mary alipendezwa kufikiri kwamba ndugu mseja alitaka kumwambia siri zake. Upesi, ule ulioonekana kuwa urafiki tu ulikuwa ushikamano wa kihisiamoyo wenye kina kirefu. Walitumia wakati mwingi zaidi na zaidi wakiwa pamoja na hatimaye wakafanya uasherati. “Ningalipaswa kung’amua hatari mwanzoni,” Mary apiga kite. “Mara urafiki huo ulipositawi, ilikuwa kama ule mchanga wa kudidimiza ukitufyonza ndani hata zaidi.”
Hatupaswi kusahau kamwe onyo hili la Biblia: “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua?” (Yeremia 17:9) Moyo wetu mdanganyifu, kama yale maji mengi yasukumayo mashua dhidi ya miamba, waweza kutusukuma tuingie katika uhusiano wa kihisiamoyo wenye kuleta msiba. Suluhisho ni nini? Ikiwa hali yako haikuruhusu kufunga ndoa, jitahidi kimakusudi kujitenga mbali kihisiamoyo na mtu unayemwona kuwa mwenye kuvutia.—Mithali 10:23.
Kujiweka Huru na Kuendelea Kuwa Huru Kutoka Katika Hatari
Namna gani ikiwa tayari twajipata wenyewe katika hatari ya kiroho? Wanaposukumwa na upepo na maji mengi kuelekea ufuo wenye miamba, mabaharia hujitahidi sana kuelekeza meli zao baharini, au kuwa na umbali wa kutosha kutoka ufuo, mpaka wafikie maji yaliyo salama zaidi. Vivyo hivyo, ni lazima tung’ang’ane ili kujiweka huru. Kwa kutii shauri la Kimaandiko, kuomba msaada wa Yehova kwa bidii, na kutafuta msaada wa ndugu Wakristo wakomavu, twaweza kurudi kwenye mwendo ulio salama. Tutabarikiwa tena kwa kupewa amani ya akili na ya moyo.—1 Wathesalonike 5:17.
Hata hali zetu ziwe ni nini, tunakuwa wenye hekima tukijitenga mbali na “mambo yaliyo ya ulimwengu.” (Wagalatia 4:3, NW) Tofauti na Loti, Abrahamu alichagua kuishi mbali na Wakaanani walimwengu, hata ingawa hilo lilimaanisha kuishi katika mahema kwa muda wa miaka mingi. Labda hakuwa na raha fulani za kimwili, lakini mtindo-maisha wake sahili ulimlinda kiroho. Badala ya imani yake kuharibiwa kama vile merikebu iliyovunjika, alikuwa “baba yao wote waaminio.”—Warumi 4:11.
Tukiwa tumezungukwa na ulimwengu wenye kula raha ambao “roho” yao ni yenye nguvu hata zaidi, twahitaji kufuata kielelezo cha Abrahamu. (Waefeso 2:2) Tukikubali mwongozo wa Yehova katika mambo yote, tutabarikiwa kwa kujionea wenyewe ulinzi wake wenye upendo. Tutahisi kama vile Daudi alivyohisi: “Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza katika njia za haki [uadilifu, NW] kwa ajili ya jina lake. Hakika wema na fadhili zitanifuata siku zote za maisha yangu; nami nitakaa nyumbani mwa BWANA [Yehova, NW] milele.” Hakuna shaka lolote, kwenda katika “njia za uadilifu,” badala ya kuelekea vijia vya hatari, kutaleta baraka za milele.—Zaburi 23:3, 6.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Ikiwa hali yako haikuruhusu kufunga ndoa, jitenge mbali kihisiamoyo na mtu unayemwona kuwa mwenye kuvutia