Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 3/15 kur. 21-23
  • “Lisha Kinywa, Si Miguu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Lisha Kinywa, Si Miguu”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Desturi za Mazishi za Kimapokeo
  • Itikadi za Kimapokeo za Afrika
  • Yale Ambayo Biblia Husema
  • Kwa Nini Wawe Tofauti?
  • Je, Wafu Wapasa Kuheshimiwa?
    Amkeni!—1999
  • Maoni ya Mkristo Kuhusu Desturi za Mazishi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Wazazi Wetu wa Kale Wako Wapi?
    Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
  • Jihadhari na Desturi Zisizompendeza Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 3/15 kur. 21-23

“Lisha Kinywa, Si Miguu”

Kutazama Desturi za Mazishi za Kimapokeo za Afrika

“HAWAZIKI wafu wao!” Hayo ni maneno yanayosemwa kwa kawaida juu ya Mashahidi wa Yehova katika Afrika Magharibi. Lakini, yajulikana vema kwamba kwa kweli, Mashahidi huwazika wafu wao.

Kwa nini watu husema kwamba Mashahidi wa Yehova hawaziki wafu wao? Wao husema hivyo kwa sababu Mashahidi hawashikilii desturi nyingi za mazishi zinazopendwa na wengi mahali wanapoishi.

Desturi za Mazishi za Kimapokeo

Aliu huishi katika kijiji kidogo katika Naijeria ya Kati. Mama yake alipokufa, yeye alijulisha watu wake wa ukoo juu ya kifo chake, kisha akapanga ili hotuba ya Kimaandiko itolewe nyumbani mwao. Hotuba hiyo iliyotolewa na mzee katika kutaniko la mahali hapo la Mashahidi wa Yehova ilikazia hali ya wafu na tumaini la ufufuo lenye kutia moyo linalorejezewa katika Biblia. Baada ya hotuba hiyo, mama ya Aliu alizikwa.

Watu wa ukoo walikasirika sana. Kwao, mazishi hayajakamilika bila makesha kufanywa, kwa kawaida yakifanywa usiku unaofuatia kifo cha mtu huyo. Katika jumuiya ya Aliu, makesha ni wakati wa sherehe, si wa kuomboleza. Maiti huoshwa, huvalishwa sanda, na kulazwa kitandani. Yule aliyefiwa huwaita wanamuziki, hununua masanduku ya pombe na vibuyu vya tembo ya mnazi, na kupanga dhabihu ya fahali au mbuzi itolewe. Halafu watu wa ukoo na marafiki hufika na kuimba, kucheza dansi, kula, na kunywa hadi asubuhi siku inayofuata.

Wakati wa sherehe hizo, chakula huwekwa miguuni pa maiti. Sehemu fulani za nywele, kucha za mikono, na kucha za miguu za mtu huyo aliyekufa hukatwa na kuwekwa kando kwa ajili ya “maziko ya pili.” Hiyo hutukia masiku, majuma, au hata miaka baadaye.

Maiti huzikwa siku inayofuatia makesha, ingawa sherehe za mazishi huendelea kwa juma moja au zaidi. Baadaye, maziko ya pili hutukia. Zile sehemu za nywele, kucha za mikono na kucha za miguu hufungwa kwa nguo nyeupe, ambayo hufungwa kwenye ubao wenye urefu wa futi tano hadi sita. Katika mwandamano wa kuimba na kucheza dansi, ubao huo huchukuliwa hadi kwenye kaburi na kuzikwa karibu na yule mtu ambaye huo wawakilisha. Kwa mara nyingine tena, kuna muziki, unywaji, na ulaji mwingi. Ili kutamatisha sherehe za maziko, bunduki hufyatuliwa mara moja angani.

Kwa kuwa Aliu hakuruhusu yoyote ya mambo hayo, yeye alishtakiwa kukosa staha ama kwa wafu ama kwa mapokeo yanayowaheshimu. Lakini kwa nini Aliu, aliye Shahidi wa Yehova, alikataa kushikilia mapokeo? Ni kwa sababu yeye hangeweza kukubali kwa kudhamiria yale mawazo ya kidini ambayo mapokeo hayo yanategemea.

Itikadi za Kimapokeo za Afrika

Kotekote katika Afrika, watu huamini kwamba wanadamu wote walikuja kutoka kwa ulimwengu wa kiroho na watarudi huko. Wayoruba wa Naijeria husema hivi: “Dunia ni soko, na mbinguni ni nyumbani.” Na msemo wa Waigbo ni: “Kila mtu azaliwaye ni lazima atarudi nyumbani, haidhuru ni muda gani anaokaa duniani.”

Fikiria zile desturi zilizotajwa mapema. Kusudi la makesha ni kuipa roho ile kwaheri istahiliyo. Sanda nyeupe huonwa kuwa yafaa kwa ulimwengu wa kiroho. Kuweka chakula miguuni hushirikishwa na wazo la kwamba yule maiti hula kupitia miguu na lazima alishwe ili asione njaa akiwa kwenye safari ya kwenda kwenye bara la mababa zake.

Zaidi ya hiyo, watu kwa ujumla huamini kwamba wakati roho iachapo mwili, hiyo hukaa-kaa karibu na wale walio hai na hairudi kwa mababa hadi inaporuhusiwa hatimaye kwa maziko ya pili. Isipokuwa maziko ya pili yafanywe, watu huogopa kwamba roho huyo atakasirika na kuwapiga walio hai kwa ugonjwa au kifo. Kufyatuliwa kwa bunduki ni “kupeleka roho hiyo” mbinguni.

Ingawa desturi za mazishi hutofautiana mahali-mahali katika Afrika, mara nyingi wazo kuu ni kwamba roho hiyo huokoka kifo cha mwili. Kusudi kuu la sherehe hizo ni kusaidia roho hiyo iitikie “mwito wa mbinguni.”

Itikadi na mazoea hayo yameendelezwa na fundisho la Jumuiya ya Wakristo la kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu na ibada yayo ya “watakatifu.” Maelezo yaliyo ya kawaida ni yale ya kasisi wa jeshi katika Swaziland aliyesema kwamba Yesu alikuja, si ili aharibu itikadi za kimapokeo, bali ili azitimize au kuzithibitisha. Kwa kuwa mara nyingi makasisi husimamia shughuli za mazishi, watu wengi huhisi kwamba Biblia huunga mkono itikadi za kimapokeo na pia desturi zinazotokana nazo.

Yale Ambayo Biblia Husema

Je! Biblia huunga mkono itikadi hizo? Kuhusu hali ya wafu, Mhubiri 3:20 husema: “Wote [wanadamu na pia wanyama] huenda mahali pamoja; wote hutoka katika mavumbi; na hata mavumbini hurudi tena.” Maandiko husema hivi zaidi: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote . . . Mapenzi yao na machukio yao, na husuda yao, imepotea yote pamoja . . . Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [kaburi] uendako wewe.”—Mhubiri 9:5, 6, 10.

Andiko hilo na mengineyo huonyesha waziwazi kwamba wafu hawawezi kutuona wala kutusikia wala kutusaidia wala kutuumiza. Je! hilo halipatani na yale ambayo umeona? Huenda ukajua juu ya mtu tajiri mwenye uwezo ambaye amekufa na ambaye familia yake imeteseka baadaye, ingawa wao walifanya kikamili sherehe zote za mazishi za kidesturi. Ikiwa mtu huyo yuko hai katika ulimwengu wa roho, kwa nini yeye hasaidii familia yake? Yeye hawezi kufanya hivyo kwa sababu yale ambayo Biblia husema ni kweli—kwa kweli wafu hawako hai, ‘wamekwisha kufa,’ na hivyo hawawezi kusaidia yeyote.—Isaya 26:14.

Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alijua hilo ni kweli. Fikiria yale yaliyotokea baada ya kifo cha Lazaro. Biblia husema hivi: “[Yesu] akawaambia [wanafunzi wake], Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha. Basi wale wanafunzi wakamwambia, Bwana, ikiwa amelala, atapona. Lakini Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake.”—Yohana 11:11-13.

Angalia kwamba Yesu alifananisha kifo na kulala, kupumzika. Alipowasili Bethania, yeye alimfariji dada za Lazaro Mariamu na Martha. Akisukumwa na huruma, Yesu alilia machozi. Lakini, yeye hakusema au kufanya lolote lililodokeza kwamba Lazaro alikuwa na roho iliyokuwa bado hai na iliyotamani msaada ili ifikie bara la mababa zayo. Badala ya hivyo, Yesu alifanya yale aliyosema angefanya. Alimwamsha Lazaro kutoka kwa usingizi wa kifo kwa njia ya ufufuo. Hilo lilitoa ithibati kwamba Mungu angemtumia Yesu hatimaye kufufua wote waliomo katika makaburi ya ukumbusho.—Yohana 11:17-44; 5:28, 29.

Kwa Nini Wawe Tofauti?

Je! kuna kosa lolote kushikilia desturi za mazishi zinazotegemea itikadi zisizo za kimaandiko? Aliu na mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wengine waamini kwamba kuna kosa. Wao wanajua kwamba haingefaa—na ni unafiki—kwao kuunga mkono zoea lolote ambalo limetegemezwa waziwazi juu ya mafundisho ya uwongo yenye kupotosha. Wao hawataki wawe kama waandishi na Mafarisayo, ambao Yesu alishutumu kwa ajili ya unafiki wa kidini.—Mathayo 23:1-36.

Mtume Paulo alimwonya mfanyakazi mwenzake Timotheo hivi: “Roho anena waziwazi ya kwamba nyakati za mwisho wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani; kwa unafiki wa watu wasemao uongo.” (1 Timotheo 4:1, 2) Je! wazo kwamba wafu wa ainabinadamu wako hai katika ulimwengu wa kiroho ni fundisho la kishetani?

Naam, ni la kishetani. Shetani Ibilisi, ‘baba wa uwongo,’ alimwambia Hawa kwamba hangekufa, akionyesha kwamba yeye angeendelea kuishi katika mwili. (Yohana 8:44; Mwanzo 3:3, 4) Hiyo haikuwa sawa na kusema kwamba nafsi isiyokufa huendelea kuishi baada ya kifo cha mwili. Hata hivyo, Shetani na mashetani wake hujaribu kuwakengeusha watu kutoka katika kweli ya Neno la Mungu kwa kuendeleza wazo kwamba uhai huendelea baada ya kifo. Kwa sababu wanaamini yale ambayo Mungu husema katika Biblia, Mashahidi wa Yehova hawaungi mkono maoni na mazoea yanayounga mkono uwongo wa Shetani.—2 Wakorintho 6:14-18.

Kwa kuepuka mazoea ya mazishi yasiyo ya kimaandiko, watumishi wa Yehova wamechukiwa na baadhi ya wale wasiounga mkono maoni yao. Mashahidi fulani wamenyimwa urithi. Wengine wametengwa na familia zao. Hata hivyo, wakiwa Wakristo wa kweli, wao hung’amua kwamba utii mwaminifu kwa Mungu huleta chuki kutoka kwa ulimwengu. Kama vile mitume waaminifu-washikamanifu wa Yesu Kristo, wanaazimia “kumtii Mungu kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29; Yohana 17:14.

Huku wakikumbuka kwa uthamini wapendwa wao waliolala usingizi katika kifo, Wakristo wa kweli hujitahidi kudhihirisha upendo kwa walio hai. Kwa kielelezo, Aliu alikuwa amemchukua mamaye nyumbani mwake baada ya baba yake kufa na alikuwa amemlisha na kumtunza katika maisha yake yote. Wengine wanaposema kwamba Aliu hakumpenda mama yake kwa sababu hakumzika kulingana na desturi zinazopendwa na wengi, yeye hurejezea msemo huu unaojulikana na wengi wa watu wake: “Lisha kinywa changu kabla ya kulisha miguu yangu.” Kulisha kinywa, au kutunza mtu wakati yeye yu hai, ni jambo la maana zaidi ya kulisha miguu, lile zoea lililoelezwa mapema na linaloshirikishwa na makesha baada ya mtu huyo kufa. Kwa kweli, kulisha miguu hakumnufaishi hata kidogo mtu aliyekufa.

Aliu huuliza wachambuzi wake hivi, ‘Wewe ungependelea nini—kwamba familia yako ikutunze wakati wa uzee wako au kwamba wafanye sherehe kubwa baada ya wewe kufa?’ Wengi wao huchagua kutunzwa wanapokuwa wangali hai. Wao pia huthamini kujua kwamba iwapo watakufa, watapata hotuba yenye staha inayotegemea Biblia na wapate maziko yafaayo.

Hilo ndilo Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufanyia wapendwa wao. Wao hulisha kinywa, si miguu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki