Ufundishaji Wenye Kusaidia kwa Ajili ya Nyakati Zetu Zenye Hatari
“Ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. . . . Watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika.”—2 TIMOTHEO 3:1, 13.
1, 2. Kwa nini tupendezwe na mafundisho tunayofuata?
JE! UNASAIDIWA, au unaumizwa? Je! matatizo yako yanatatuliwa, au yanafanywa kuwa mabaya zaidi? Na nini? Na mafundisho. Naam, mafundisho yaweza kuathiri sana maisha yako kwa uzuri au kwa ubaya.
2 Maprofesa washirika watatu walichunguza jambo hili hivi karibuni wakatoa magunduzi yao katika jarida liitwalo Journal for the Scientific Study of Religion. Ni kweli, huenda ikawa hawakukuchunguza wewe au familia yako. Hata hivyo, yale waliyopata yaonyesha uhusiano kati ya mafundisho na kule kufanikiwa au kushindwa kwa mtu, katika kushughulika na nyakati zetu zenye hatari. Katika makala inayofuata, tutachunguza yale waliyogundua. Katika makala ifuatayo, tutaona yale waliyopata.
3, 4. Ni nini baadhi ya mathibitisho yanayoonyesha kwamba twaishi katika nyakati za hatari?
3 Lakini, kwanza fikiria swali hili: Je! wewe wakubali kwamba tunaishi katika nyakati zilizo ngumu kushughulika nazo? Ikiwa ndivyo, basi kwa hakika ungeona kuwa uthibitisho waonyesha kwamba hizi ndizo “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5, NW) Watu huathiriwa katika njia tofauti-tofauti. Kwa kielelezo, labda wewe wajua juu ya mabara ambayo sasa hivi yanagawanyika kwa sababu vikundi mbalimbali vinapigania uongozi wa kisiasa. Kwingineko, mauaji husababishwa na tofauti za kidini na za kikabila. Si askari-jeshi pekee wanaoumizwa. Fikiria wanawake na wasichana wasiohesabika ambao wametendwa kikatili, watu wazee-wazee ambao wamenyimwa chakula, joto, na makao. Idadi za watu wasiohesabika wanateseka vibaya, hilo likifanya kuwe na idadi kubwa mno ya wakimbizi, na misiba mingi ihusianayo.
4 Nyakati zetu zimekumbwa pia na matatizo ya kiuchumi, yakitokeza viwanda vilivyofungwa, ukosefu wa kazi ya kuajiriwa, kupotezwa kwa manufaa za kifedha na malipo ya uzeeni, kupungua kwa thamani ya pesa na milo midogo zaidi au michache zaidi. Je! wewe waweza kuongezea orodha hiyo ya matatizo? Labda. Mamilioni mengine tufeni pote huteseka kwa sababu ya upungufu wa chakula na magonjwa. Labda umeona zile picha zenye kuhuzunisha kutoka Afrika Mashariki zikionyesha wanaume, wanawake, na watoto waliokonda. Mamilioni ya watu katika Asia huteseka vivyo hivyo.
5, 6. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba ugonjwa pia ni jambo kubwa sana katika nyakati zetu ngumu?
5 Sisi sote tumesikia juu ya magonjwa yenye kuhofisha yanayoongezeka. Katika Januari 25, 1993, The New York Times lilisema hivi: “Mweneo wa UKIMWI katika Amerika ya Latini unaendelea kupita ule wa United States, ukisitawi kwa sababu ya ngono za ovyo-ovyo, unafiki na njia zisizofaa za kuuzuia . . . Mwingi wa ukuzi huo unasababishwa na viwango vya ambukizo vinavyozidi miongoni mwa . . . wanawake.” Katika Oktoba 1992, U.S.News & World Report lilisema hivi: “Ilikuwa miongo miwili tu iliyopita kwamba daktari mkuu wa U.S., akishangilia mojawapo ushindi mkubwa zaidi wa afya ya umma, alitangaza kwamba wakati ulikuwa umetimia wa ‘kutohangaikia tena magonjwa ya kuambukiza.’” Lakini namna gani sasa? “Kwa mara nyingine tena, hospitali zinajaa wagonjwa wa tauni zilizodhaniwa kuwa zimeshindwa. . . . Vijiumbe-maradhi vinabuni njia za urithi-tabia zilizo za akili zaidi kila mara, zikivifanya viongezeke haraka zaidi ya uvumbuzi wa viuavijasumu vipya. . . . ‘Tunaingia katika muhula mpya wa magonjwa ya kuambukiza.’”
6 Kikiwa kielelezo kimoja, Newsweek la Januari 11, 1993, liliripoti hivi: “Vimelea vya malaria sasa huambukiza watu wanaokadiriwa kuwa milioni 270 kila mwaka, vikiua kufikia watu milioni 2 . . . na kusababisha angalau visa milioni 100 vya ugonjwa mbaya . . . Wakati uo huo, ugonjwa huo unazidi kukinza dawa zilizouponya hapo mbele. . . . Huenda hivi karibuni vimelea fulani visiweze kutibika.” Hilo lafanya mtu ateteme kwa hofu.
7. Wengi leo wanaitikiaje nyakati hizi ngumu?
7 Huenda ukawa umeona kwamba katika nyakati hizi zenye hatari zilizo ngumu kushughulika nazo, wengi wanatafuta msaada ili kutatua matatizo yao. Wafikirie wale wanaochunguza vitabu vinavyozungumzia kushughulika na mikazo au ugonjwa fulani mpya. Wengine wanatamani sana kupata shauri juu ya ndoa inayovunjika, juu ya kutunza watoto, juu ya matatizo ya kileo au ya madawa ya kulevya, au juu ya kusawazisha matakwa ya kazi yao na misongo wanayohisi nyumbani. Ndiyo, wao wanahitaji msaada kwelikweil! Je! wewe unang’ang’ana na tatizo la kibinafsi au unapatwa na baadhi ya matatizo yanayoletwa na vita, njaa, au msiba? Hata ikiwa tatizo kubwa linaonekana kuwa haliwezi kutatulika, una sababu ya kuuliza hivi, ‘Kwa nini tumefikia hali ya hatari hivyo?’
8. Kwa nini tuiendee Biblia ili kupata mwono-ndani na mwongozo?
8 Kabla ya sisi kuweza kushughulika ifaavyo na kupata uradhi maishani sasa na katika wakati ujao, tunahitaji kujua kwa nini twakabili nyakati hizi zenye hatari. Kwa kweli, hilo laandaa sababu kwa kila mmoja wetu kufikiria Biblia. Kwa nini twaelekeza kwenye Biblia? Kwa sababu ni hiyo pekee iliyo na unabii sahihi, historia iliyoandikwa kimbele, ionyeshayo sababu za taabu yetu, mahali tulipo, na mahali tunakoelekea.
Somo Kutokana na Historia
9, 10. Unabii wa Yesu katika Mathayo sura ya 24 ulitimizwaje katika karne ya kwanza?
9 Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 1994, liliandaa pitio listahililo kukumbukwa la unabii wa Yesu ulio wazi katika Mathayo sura ya 24. Ukifungua Biblia yako kwenye sura hiyo waweza kuona katika mstari wa 3 kwamba mitume wa Yesu walimuuliza awape ishara juu ya kuwapo kwake wakati ujao na umalizio wa mfumo wa mambo. Kisha, katika mstari wa 5 hadi 14, Yesu alitabiri juu ya Makristo bandia, vita, upungufu wa chakula, kunyanyaswa kwa Wakristo, uasi-sheria, na kuhubiriwa kwa Ufalme wa Mungu kotekote.
10 Historia huthibitisha kwamba mambo ayo hayo yalitukia hasa wakati wa umalizio wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi. Kama ungaliishi wakati huo, je! hizo zisingalikuwa nyakati ngumu? Hata hivyo, mambo yalikuwa yakielekea kwenye upeo, dhiki isiyopata kutokea namna yayo juu ya Yerusalemu na mfumo wa Kiyahudi. Katika mstari wa 15 twaanza kusoma juu ya yale yaliyotukia baada ya Waroma kushambulia Yerusalemu katika 66 W.K. Matukio hayo yalifikia upeo katika ile dhiki ambayo Yesu alitaja katika mstari wa 21—kuharibiwa kwa Yerusalemu katika 70 W.K., dhiki mbaya zaidi iliyopata kukumba jiji hilo. Hata hivyo, wajua kwamba historia haikukomea hapo, wala Yesu hakusema kwamba ingekomea hapo. Katika mstari wa 23 hadi 28 yeye alionyesha kwamba baada ya ile dhiki ya 70 W.K., mambo mengine yangetukia.
11. Utimizo wa karne ya kwanza wa Mathayo sura 24 wahusiana kwa njia gani na siku zetu?
11 Wengine leo huenda wakawa na mwelekeo wa kutupilia mambo hayo ya zamani mbali kwa kuuliza ‘Kwa hiyo nini?’ Hilo lingekuwa kosa. Utimizo wa unabii huko nyuma ni wa maana sana. Kwa nini? Naam, vita, njaa, matetemeko ya dunia, tauni, na mnyanyaso wakati wa umalizio wa mfumo wa Kiyahudi yangetukia katika utimizo mkubwa zaidi baada ya “nyakati zilizowekwa za mataifa” kwisha katika 1914. (Luka 21:24, NW) Wengi wanaoishi sasa walijionea kwa macho Vita ya Ulimwengu 1 wakati utimizo huu wa kisasa ulipoanza. Lakini hata ikiwa ulizaliwa baada ya 1914, umejionea unabii wa Yesu ukitimizwa. Matukio ya karne hii ya 20 yanathibitisha kabisa kwamba sasa tunaishi katika umalizio wa mfumo huu mwovu uliopo.
12. Kulingana na Yesu, twaweza kutazamia kuona nini bado?
12 Hilo lamaanisha kwamba ile “dhiki” ya Mathayo 24:29 iko mbele yetu. Hiyo itatia ndani matukio ya kiajabu-ajabu ya kimbingu ambayo huenda yasiweze kuwazika. Mstari wa 30 waonyesha kwamba ndipo watu watakapoona ishara tofauti—ile inayothibitisha kwamba uharibifu umekaribia. Kulingana na masimulizi yanayofanana na hayo kwenye Luka 21:25-28, wakati huo ujao ‘watu watavunjika mioyo kwa hofu, na kwa kutazamia mambo yatakayoupata ulimwengu.’ Masimulizi ya Luka yasema pia kwamba ndipo Wakristo watakapoinua vichwa vyao kwa sababu ukombozi wao utakuwa karibu sana.
13. Ni mambo gani makuu mawili yanayostahili uangalifu wetu?
13 ‘Ni sawa kabisa, ninakubaliana na hayo,’ huenda wewe ukasema, ‘lakini nilifikiri swali lilikuwa naweza kuelewaje na kushughulikaje na nyakati zetu ngumu?’ Wewe hukosei. Jambo letu la kwanza ni kutambua matatizo makubwa na kuona jinsi tuwezavyo kuyaepuka. Linalohusiana na hilo ni jambo la pili, jinsi mafundisho ya Kimaandiko yawezavyo kutusaidia tufurahie maisha bora zaidi sasa. Kuhusiana na hili, fungua Biblia yako kwenye 2 Timotheo sura ya 3, uone jinsi maneno ya mtume Paulo yawezavyo kukusaidia kushughulika na nyakati ngumu.
Unabii Kuhusu Nyakati Zetu
14. Kwa nini kuna sababu ya kuamini kwamba ufikirio wa 2 Timotheo 3:1-5 waweza kutunufaisha?
14 Mungu alimpulizia mtume Paulo amwandikie Mkristo mwaminifu-mshikamanifu Timotheo mashauri mengi mazuri yaliyomsaidia awe na maisha yenye ufanisi na yenye furaha zaidi. Baadhi ya yale aliyoandika Paulo yangekuwa na utimizo mkuu katika siku zetu. Hata ukihisi kwamba unayajua vizuri, fuata kwa ukaribu sasa maneno ya unabii kwenye 2 Timotheo 3:1-5. Paulo aliandika hivi: “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa [ujitoaji kimungu, NW], lakini wakikana nguvu zake.”
15. Kwa nini 2 Timotheo 3:1 liwe na upendezi wa pekee kwetu sasa?
15 Tafadhali ona kwamba kulikuwa na mambo 19 yaliyoorodheshwa. Kabla ya sisi kuchunguza mambo hayo na hivyo tuweze kunufaika, ufikirie unabii wote. Tazama mstari wa 1. Paulo alitabiri hivi: “Siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.” “Siku za mwisho” gani? Kumekuwako siku za mwisho nyingi, kama vile siku za mwisho za Pompeii ya kale au siku za mwisho za mfalme au familia inayotawala. Biblia hata hutaja siku za mwisho kadhaa, kama vile zile siku za mwisho za mfumo wa Kiyahudi. (Matendo 2:16, 17) Hata hivyo, Yesu alituwekea msingi ili tuweze kuelewa kwamba “siku za mwisho” ambazo Paulo alitaja zarejezea wakati wetu.
16. Mfano wa ngano na magugu ulitabiri hali gani kwa wakati wetu?
16 Yesu alifanya hivyo kwa mfano wa ngano na magugu. Hivi vilipandwa katika shamba na kuachwa vikue. Yeye alisema kwamba ngano na magugu vinafananisha watu—Wakristo wa kweli na bandia. Tunautaja mfano huo kwa sababu wathibitisha kwamba kipindi kirefu cha wakati kingepita kabla ya umalizio wa mfumo wote mwovu. Wakati umalizio huo ungefika, jambo fulani lingesitawi sana. Jambo gani? Uasi-imani, au kugeukia mbali kutoka Ukristo wa kweli, kukitokeza uovu mwingi sana. Unabii mwingine wa Biblia wathibitisha kwamba hili lingetukia wakati wa siku za mwisho za mfumo mwovu. Humo ndimo tulimo leo, katika umalizio wa mfumo wa mambo.—Mathayo 13:24-30, 36-43.
17. Ni habari gani ifananayo na hiyo inayoandaliwa na 2 Timotheo 3:1-5 kuhusu umalizio wa mfumo wa mambo?
17 Je! wewe waiona maana? Timotheo wa Pili 3:1-5 latupatia dokezo lenye kufanana kwamba wakati wa umalizio wa mfumo, au siku za mwisho, matunda yote yanayozunguka Wakristo yangekuwa mabovu. Paulo hakuwa akisema kwamba yale mambo 19 yaliyoorodheshwa yangekuwa ndiyo njia kuu ya kuthibitisha kwamba siku za mwisho zingekuwa zimewasili. Badala ya hivyo, yeye alikuwa akionya juu ya yale ambayo tungelazimika kushughulika nayo wakati wa siku za mwisho. Mstari wa 1 wasema juu ya “nyakati za hatari [zilizo ngumu kushughulika nazo, NW].” Maneno hayo yanatokana na Kigiriki, na yanamaanisha kihalisi “nyakati zilizowekwa kali.” (Kingdom Interlinear) Je! wewe hukubali kwamba neno “kali” laeleza kwa usahihi yale tunayokabili leo? Fungu hilo la maneno yaliyopuliziwa laendelea kutoa mwono-ndani wa kimungu katika wakati wetu.
18. Twapaswa kukazia fikira nini tunapochunguza maneno ya Paulo ya kiunabii?
18 Kupendezwa kwetu na unabii huu kwapaswa kuturuhusu tutambulishe vielelezo vyenye msiba vinavyoonyesha jinsi kipindi chetu kilivyo hatari, au kikali. Kumbuka mambo yetu makuu mawili: (1) kutambulisha matatizo yanayofanya nyakati zetu ziwe ngumu na kuona jinsi ya kuyaepuka; (2) kufuata mafundisho yanayoweza kufanya kazi kikweli na yanayoweza kutusaidia tufurahie maisha yaliyo bora zaidi. Basi badala ya kukazia mambo yasiyofaa, tutakazia mafundisho yanayoweza kutusaidia sisi na familia zetu katika nyakati hizi zilizo ngumu kushughulika nazo.
Vuna Manufaa Tele
19. Tumeona uthibitisho upi kwamba watu wanajipenda wenyewe?
19 Paulo aanza orodha yake kwa kutabiri kwamba katika siku za mwisho, “watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe.” (2 Timotheo 3:2) Yeye alimaanisha nini? Wewe ungekuwa hukosei kwa kusema kwamba katika historia yote kumekuwa wanaume na wanawake wenye majivuno, wenye kushughulikia mambo yao wenyewe. Lakini, hakuna shaka kwamba tatizo hili limeenea sana leo kwa njia isiyo ya kawaida. Kwa wengi linapita kiasi. Karibu ni la kawaida katika ulimwengu wa kisiasa na wa kibiashara. Wanaume na wanawake hufuatilia kujipatia mamlaka na umashuhuri hata iweje. Mara nyingi hiyo ni kwa gharama yoyote ya wengine, kwani hao wenye kujipenda hawajali jinsi wanavyowaumiza watu wengine. Wao ni wepesi kushtaki wengine mahakamani au kuwapunja. Waweza kuelewa ni kwa nini wengi hukiita hiki “kizazi cha umimi.” Watu wenye kupiga ubwana na wale wenye kufikiria mambo yao wenyewe ni wengi.
20. Shauri la Kibiblia linatofautianaje na mtazamo unaoenea wa kujipenda mwenyewe?
20 Hatuhitaji kukumbushwa juu ya mambo machungu tuliyopatwa nayo katika kushughulika na watu ambao ni “wenye kujipenda wenyewe.” Hata hivyo ni kweli kwamba kwa kutambulisha tatizo hilo waziwazi, Biblia inatusaidia, kwani inatufundisha jinsi ya kuepuka mtego huo. Hivi ndivyo husema: “Msitende neno lolote kwa kujitakia makuu kwa uchoyo au kwa tamaa isiyofaa ya kujisifu, bali mnyenyekeane, mkiwaona wengine kuwa bora kuliko nyinyi. Na mwangalie mapendezi ya mmoja na mwenzake, si yenu wenyewe tu.” “Usijione mwenyewe kuwa mkuu zaidi ya vile upaswavyo. Badala ya hivyo, uwe na kiasi katika kufikiri kwako.” Mashauri hayo bora yanapatikana kwenye Wafilipi 2:3, 4 na Warumi 12:3, kama yalivyotafsiriwa katika Today’s English Version.
21, 22. (a) Kuna uthibitisho upi mwingi kwamba shauri hilo laweza kuwa lenye kusaidia leo? (b) Shauri la Mungu limeathirije watu mmoja-mmoja wenye akili timamu?
21 Huenda mtu fulani akateta akisema, ‘Hayo yasikika kuwa mazuri, lakini hayawezi kufanya kazi.’ Oh, ndiyo, yanaweza. Yanaweza kufanya kazi, na hayo hufanya kazi kwa wanadamu wenye akili timamu leo. Katika 1990, mtangazaji wa Chuo Kikuu cha Oxford alichapa kichapo The Social Dimensions of Sectarianism. Sura ya 8 ilikuwa na kichwa “Mashahidi wa Yehova Katika Nchi ya Kikatoliki,” na kilieleza juu ya uchunguzi katika Ubelgiji. Twasoma hivi: “Tukigeukia ule uvutio chanya wa kuwa Shahidi, zaidi ya ule uvutio wa ‘ile Kweli’ yenyewe, kwa mara nyingine tena wale waliohojiwa walitaja zaidi ya sifa moja. . . . Uchangamfu, urafiki, upendo, na muungano ndizo sifa zilizotajwa mara nyingi zaidi, lakini ufuataji haki, na mwenendo wa kibinafsi katika ‘kufuatia kanuni za kibiblia’ zilikuwa pia sifa ambazo Mashahidi walithamini sana.”
22 Twaweza kufananisha yote hayo tuliyozungumzia na picha inayopigwa kwa lenzi pembepana; ikiwa badala ya hiyo, ungetumia lenzi zumu (inayokuza au kupunguza ukubwa wa picha), au lenzi darubini, ungeona picha za karibu, maono mengi ya maisha halisi. Hayo yangetia ndani wanaume waliokuwa wenye kiburi, wenye kupiga ubwana, au wenye ubinafsi sana lakini ambao sasa ni wapole zaidi, wakiwa waume na baba waonyeshao shauku nyororo na fadhili zaidi kwa wenzi wao, watoto wao, na wengineo. Hayo pia yangetia ndani wanawake waliokuwa wenye kunyakua ukichwa au wasio na huruma na ambao sasa huwasaidia wengine kujifunza njia ya Ukristo halisi. Kuna mamia ya maelfu ya vielelezo kama hivyo. Sasa, tafadhali sema wazi. Je! usingeliona kuwa jambo bora zaidi kuwa miongoni mwa watu wa aina hiyo kuliko kushughulika na nyakati zote na wanaume na wanawake wanaojipenda kwanza na kujitanguliza wenyewe? Je! isingefanya iwe rahisi zaidi kushughulika na nyakati zetu zenye hatari? Kwa hiyo je! kufuata mafundisho hayo ya Kibiblia kusingekufanya uwe mwenye furaha zaidi?
23. Kwa nini itafaa kuelekeza uangalifu zaidi kwenye 2 Timotheo 3:2-5?
23 Lakini, tumezungumzia jambo la kwanza tu katika orodha ya Paulo iliyorekodiwa kwenye 2 Timotheo 3:2-5. Namna gani yale mengine? Je! kuyachunguza kwako kutakusaidia pia kutambulisha matatizo makuu ya wakati wetu ili uyaepuke na kukuwezesha uelewe ni mwendo gani utakaokuletea wewe na wapendwa wako furaha nyingi zaidi? Makala ifuatayo itakusaidia ujibu maswali hayo na kupokea baraka tele.
Mambo ya Kukumbuka
◻ Ni nini baadhi ya mathibitisho kwamba twaishi katika nyakati ngumu?
◻ Kwa nini twaweza kuwa na hakika kwamba twaishi katika siku za mwisho?
◻ Ni mambo gani makuu mawili tuwezayo kupata kutokana na uchunguzi wa 2 Timotheo 3:1-5?
◻ Katika wakati huu ambapo wengi ni wenye kujipenda wenyewe, mafundisho ya Biblia yamesaidiaje watu wa Yehova?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]
Picha iliyo juu kushoto: Andy Hernandez/Sipa Press; picha iliyo chini kulia: Jose Nicolas/Sipa Press