Sababu kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hufuliza Kulinda
“Fulizeni kulinda kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu anakuja.”—MATHAYO 24:42, NW.
1. Lile himizo la ‘kufuliza kulinda’ lahusu nani?
KWA kila mtumishi wa Mungu—awe ni mchanga au mwenye umri mkubwa, awe amejiweka wakfu hivi karibuni au ametumikia kwa muda mrefu—himizo hili la Biblia lamhusu: “Fulizeni kulinda”! (Mathayo 24:42, NW) Kwa nini hilo ni jambo la maana?
2, 3. (a) Yesu alifafanua wazi ishara gani, na utimizo wa unabii umeonyesha nini? (b) Ni hali zipi zinazorejezewa katika Mathayo 24:42 zinazotahini ukweli wa imani yetu, na kwa jinsi gani?
2 Kuelekea mwisho wa huduma yake duniani, Yesu alitabiri ishara ya kuwapo kwake kusikoonekana katika mamlaka ya Ufalme. (Mathayo, sura za 24 na 25) Alifafanua wazi wakati wa kuwapo kwake kwa kifalme—na matukio yanayotimiza unabii unaoonyesha kwamba alitawazwa kuwa Mfalme mbinguni katika 1914. Pia alitaja jambo fulani ambalo lingejaribu ukweli wa imani yetu. Hilo lilirejezea wakati ambapo angechukua hatua akiwa Mfishaji ili kuangamiza mfumo wa sasa ulio mwovu wakati wa dhiki kubwa Yesu aliposema hivi: “Kuhusu siku hiyo na saa hiyo hakuna mtu ajuaye, wala hao malaika wa mbingu, wala Mwana, ila Baba tu.” Alikuwa akifikiria hilo aliposema hivi: “Kwa hiyo, fulizeni kulinda kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu anakuja.”—Mathayo 24:36, 42, NW.
3 Kutojua kwetu siku ile wala saa ile ambapo dhiki kubwa itaanza kwamaanisha kwamba ikiwa twadai kuwa Wakristo, twapaswa kuishi kila siku jinsi iwapasavyo Wakristo wa kweli. Je! jinsi unavyotumia maisha yako itafanya ukubaliwe na Bwana dhiki kubwa ifikapo? Ama ukifa kwanza, je, atakukumbuka kuwa ulimtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu kufikia mwisho wa maisha yako ya sasa?—Mathayo 24:13; Ufunuo 2:10.
Wafuasi wa Mapema Walijitahidi Kulinda
4. Twaweza kujifunza nini kutokana na kielelezo cha Yesu cha kulinda kiroho?
4 Yesu Kristo mwenyewe aliweka kielelezo chema zaidi cha kulinda kiroho. Alisali mara nyingi na kwa bidii kwa Baba yake. (Luka 6:12; 22:42-44) Alipokabili majaribu, yeye alitegemea sana mwelekezo uliomo katika Maandiko. (Mathayo 4:3-10; 26: 52-54) Hakukengeushwa kutoka kwenye kazi ambayo Yehova alimpa. (Luka 4:40-44; Yohana 6:15) Je! wale ambao wangejiona kuwa wafuasi wa Yesu wangekuwa wenye kulinda vivyo hivyo?
5. (a) Kwa nini mitume wa Yesu walikuwa na matatizo ya kudumisha usawaziko wa kiroho? (b) Yesu aliwapa mitume wake msaada gani baada ya ufufuo wake?
5 Nyakati nyingine, hata mitume wa Yesu walikosea. Kwa sababu ya kuwa wenye shauku kupita kiasi na kuwa na maoni yenye kosa, iliwabidi wakabiliane na hali ya kuvunjika moyo. (Luka 19:11; Matendo 1:6) Kabla hawajajifunze kumtegemea Yehova sana, majaribu ya ghafula yaliwavuruga. Hivyo, Yesu alipokamatwa, mitume wake walitoroka. Baadaye usiku huo, kwa sababu ya hofu, Petro alikana kwa kurudia-rudia kwamba hata hamjui Kristo. Mitume hawakuwa wamezingatia moyoni shauri hili la Yesu: “Fulizeni kulinda na kusali kwa uendelevu.” (Mathayo 26:41, 55, 56, 69-75, NW) Baada ya kufufuliwa Yesu alitumia Maandiko ili kuimarisha imani yao. (Luka 24:44-48) Na wakati ulipoonekana kwamba huenda baadhi yao wasitangulize huduma waliyopewa, Yesu aliimarisha azimio lao la kukazia akili ile kazi muhimu zaidi.—Yohana 21:15-17.
6. Hapo awali Yesu alikuwa ameonya wafuasi wake dhidi ya mitego gani miwili?
6 Hapo awali, Yesu alikuwa amewaonya wanafunzi wake kwamba wao hawakupaswa kuwa sehemu ya ulimwengu. (Yohana 15:19) Yeye alikuwa amewashauri pia wasipige ubwana mmoja na mwenzake bali watumikie pamoja wakiwa ndugu. (Mathayo 20:25-27; 23:8-12) Je! walitii shauri lake? Je! walitanguliza kazi waliyopewa naye?
7, 8. (a) Rekodi ya Wakristo wa karne ya kwanza inaonyeshaje kwamba walizingatia moyoni himizo la Yesu? (b) Ni kwa nini lilikuwa jambo la maana kuendelea kulinda kiroho?
7 Maadamu mitume walikuwa wangali hai, walilinda kutaniko. Historia yashuhudia kwamba Wakristo wa mapema hawakujihusisha na mambo ya kisiasa ya Milki ya Roma na kwamba hawakuwa na jamii ya makasisi iliyotukuka. Kwa upande mwingine, wao walikuwa wapiga-mbiu ya Ufalme wa Mungu wenye bidii. Kufikia mwisho wa karne ya kwanza, walikuwa wametoa ushahidi kotekote katika Milki ya Roma, wakifanya wanafunzi katika Asia, Ulaya, na Afrika Kaskazini.—Wakolosai 1:23.
8 Hata hivyo, mambo hayo yaliyotimizwa katika kuhubiri hayakumaanisha kwamba hakukuwa tena na uhitaji wa kufuliza kulinda kiroho. Kuja kwa Yesu kulikotabiriwa kulikuwa kungali ni kwa wakati ujao ulio mbali. Na kutaniko lilipoingia katika karne ya pili W.K., hali zilitokea ambazo zilihatarisha hali ya kiroho ya Wakristo. Kwa njia gani?
Wale Walioacha Kulinda
9, 10. (a) Baada ya kifo cha mitume, ni matukio gani yaliyoonyesha kwamba wengi waliodai kuwa Wakristo hawakuwa wakilinda? (b) Ni maandiko yapi yaliyotajwa katika fungu hili ambayo yangesaidia wale waliodai kuwa Wakristo kubaki imara kiroho?
9 Baadhi ya wale walioingia kutanikoni walianza kueleza itikadi zao kwa kutumia falsafa ya Kigiriki, ili kufanya yale waliyohubiri yakubalike zaidi kwa watu wa ulimwengu. Hatua kwa hatua, mafundisho ya kipagani, kama vile Utatu na kutokufa kiasili kwa nafsi, yakawa sehemu ya aina ya Ukristo wenye waa. Hilo lilifanya lile tumaini la mileani liachwe. Kwa nini? Wale walioitikadi katika kutokufa kwa nafsi walifikia mkataa kwamba baraka za utawala wa Kristo zingepatikana katika ulimwengu wa roho na nafsi ambayo ingeendelea kuishi baada ya kifo cha mwili wa kibinadamu. Kwa hiyo hawakuona uhitaji wa kulinda kwa ajili ya kuwapo kwa Kristo katika mamlaka ya Ufalme.—Linganisha Wagalatia 5:7-9; Wakolosai 2:8; 1 Wathesalonike 5:21.
10 Hali hiyo ilichochewa na matukio mengine. Baadhi ya wale waliodai kuwa waangalizi Wakristo walianza kutumia makutaniko yao kuwa njia ya kujipatia umashuhuri. Kwa hila, waliona maoni yao na mafundisho yao wenyewe kuwa na thamani kama Maandiko au hata kuzidi Maandiko. Fursa ilipojitokeza, kanisa hilo lililoasi imani hata lilijitokeza lenyewe liweze kutumikia masilahi ya taifa la kisiasa.—Matendo 20:30; 2 Petro 2:1, 3.
Matokeo ya Kulinda Zaidi
11, 12. Ni kwa nini Mapinduzi ya Kiprotestanti hayakurudisha ibada ya kweli?
11 Baada ya Kanisa Katoliki la Roma kutenda vibaya kwa karne nyingi, baadhi ya Wapinduzi walitoa upinzani katika karne ya 16. Lakini hilo halikumaanisha kurudia ibada ya kweli. Kwa nini?
12 Ingawa vikundi mbalimbali vya Kiprotestanti vilijiweka huru na utawala wa Roma, viliendeleza mengi kati ya mafundisho ya msingi na mazoea ya uasi-imani.—wazo la mgawanyiko kati ya makasisi na watu wa kawaida, pia imani katika Utatu, kutokufa kwa nafsi, na mateso ya milele baada ya kifo. Na, kama ilivyo na Kanisa Katoliki la Roma, vikundi hivyo viliendelea kuwa sehemu ya ulimwengu, vikishirikiana kwa ukaribu na sehemu za kisiasa. Kwa hiyo vilielekea kukataa matarajio yoyote ya kuja kwa Kristo akiwa Mfalme.
13. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba watu fulani walithamini kikweli Neno la Mungu? (b) Katika karne ya 19, ni tukio gani lililokuja kupendeza baadhi ya wale waliodai kuwa Wakristo? (c) Ni kwa nini wengi walivunjika moyo?
13 Lakini, Yesu alikuwa ametabiri kwamba baada ya kifo cha mitume wake, wale warithi wa kweli wa Ufalme (ambao aliwafananisha na ngano) wangeendelea kukua kando ya Wakristo bandia (au, magugu) hadi wakati wa mavuno. (Mathayo 13:29, 30) Leo hatuwezi kuorodhesha kwa uhakika wale wote ambao Bwana-Mkubwa aliwaona kuwa ngano. Lakini ni jambo linalostahili kuangaliwa kwamba katika kipindi cha karne ya 14, 15, na 16, kulikuwa na watu waliohatarisha uhai na uhuru wao wenyewe ili kufanya Biblia ipatikane katika lugha ya watu wa kawaida. Wengine walikataa Utatu kuwa si la kimaandiko na kuikubali Biblia kuwa Neno la Mungu. Baadhi yao walikataa itikadi ya kutokufa kwa nafsi na mateso katika moto wa helo kuwa haipatikani kabisa na Neno la Mungu. Pia katika karne ya 19, kwa sababu ya kujifunza Biblia zaidi, vikundi katika United States, Ujerumani, Uingereza, na Urusi vilianza kuonyesha usadikisho wavyo kwamba wakati wa kurudi kwa Kristo ulikuwa karibu. Lakini mengi ya matarajio yao hayakutimizwa. Kwa nini? Sababu kubwa ilikuwa kwamba wao walitegemea sana wanadamu bila kutegemea sana Maandiko.
Jinsi Hao Walivyolinda
14. Eleza njia ambayo C. T. Russell na washiriki wake walitumia kujifunza Biblia.
14 Ndipo, katika 1870, Charles Taze Russell na baadhi ya washirika wake walifanyiza kikundi cha funzo la Biblia katika Allegheny, Pennsylvania. Wao hawakuwa wa kwanza kufahamu kweli nyingi za Biblia walizokubali, lakini wakati walipokuwa wakijifunza, walikuwa na zoea la kuchunguza maandiko yote kwa uangalifu juu ya swali fulani.a Kusudi lao lilikuwa kuhakikisha kwamba walifikia mikataa iliyopatana na yote yale ambayo Biblia ilisema juu ya jambo hilo bali si kutafuta maandiko yaliyothibitisha wazo lililoshikiliwa kimbele.
15. (a) Mbali na Ndugu Russell, wengine walikuwa wameng’amua jambo gani? (b) Ni nini kilichofanya Wanafunzi wa Biblia wawe tofauti na hao?
15 Wengine wachache kabla yao walikuwa wameng’amua kwamba Kristo angerudi bila kuonekana akiwa roho. Wengine walikuwa wameona kwamba kusudi la kurudi kwa Kristo halikuwa kuchoma dunia na kuondolea mbali uhai wote wa kibinadamu, bali, badala ya hivyo, lilikuwa ni kubariki familia zote za dunia. Kulikuwako hata wachache waliokuwa wameng’amua kwamba mwaka 1914 ungetia alama mwisho wa Nyakati za Wasio Wayahudi. Lakini kwa Wanafunzi wa Biblia walioshirikiana na Ndugu Russell, hayo yalikuwa mambo ya maana kuliko kuwa tu mambo ya kitheolojia ya kuzungumzwa tu. Wao walizingatia kweli hizo maishani mwao nao wakazitangaza kwa mataifa yote kwa kiwango kisichopata kufikiwa katika kipindi hicho.
16. Kwa nini Ndugu Russell aliandika hivi katika 1914: “Sisi tumo katika majira ya kutahini”?
16 Bado, wao walihitaji kufuliza kulinda. Kwa nini? Kwa kielelezo, ingawa wao walijua kwamba mwaka 1914 ulitiwa alama na unabii wa Biblia, wao hawakujua kwa hakika ni nini hasa kingetukia katika mwaka huo. Hilo liliwatahini. Katika Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1914, Ndugu Russell aliandika hivi: “Na tukumbuke kwamba sisi tumo katika majira ya kutahini. . . . Ikiwa kuna sababu yoyote ambayo ingemwongoza yeyote kuacha Bwana na Kweli Yake na kuacha kutoa dhabihu kwa ajili ya Kusudi la Bwana, basi si kumpenda Mungu tu moyoni ambako kumemsukuma apendezwe na Bwana, bali ni jambo jingine; labda kutumaini kwamba wakati ulikuwa mfupi; kujitoa kulikuwa kwa wakati fulani tu.”
17. A. H. Macmillan, na wengine kama yeye, walidumishaje usawaziko wa kiroho?
17 Wengine huko nyuma waliacha utumishi wa Yehova. Lakini A. H. Macmillan hakuacha. Miaka mingi baadaye, yeye alikiri hivi kwa moyo mweupe: “Nyakati nyingine matarajio yetu ya tarehe fulani yalikuwa zaidi ya yale ambayo Maandiko yaliruhusu.” Ni nini kilichomsaidia kudumisha usawaziko wa kiroho? Kama alivyosema, yeye aling’amua kwamba “wakati matarajio hayo yalipokosa kutimizwa, hilo halikubadili makusudi ya Mungu.” Yeye aliongeza hivi: “Nilijifunza kwamba tunapaswa kukubali makosa yetu na kuendelea kutafuta katika Neno la Mungu ili kupata kuelimishwa zaidi.”b Kwa unyenyekevu, hao Wanafunzi wa Biblia wa mapema waliacha Neno la Mungu lirekebishe mtazamo wao.—2 Timotheo 3:16, 17.
18. Kulinda kwa Wakristo kulitokeza mafaa gani hatua kwa hatua juu ya habari ya kutokuwa sehemu ya ulimwengu?
18 Katika miaka iliyofuata, uhitaji wao wa kufuliza kulinda haukupungua. Bila shaka, wao walijua kwamba Wakristo hawakupaswa kuwa sehemu ya ulimwengu. (Yohana 17:14; Yakobo 4:4) Kwa kupatana na hayo, wao hawakujiunga na Jumuiya ya Wakristo katika kuunga mkono Ushirika wa Mataifa kuwa wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu. Lakini haikuwa hadi 1939 kwamba waliona waziwazi suala la kutokuwamo kwa Kikristo.—Ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 1939, Kiingereza.[16a]
19. Kumetokea mafaa gani katika uangalizi wa kutaniko kwa sababu tengenezo limefuliza kulinda?
19 Wao hawakuwa kamwe na jamii ya makasisi, ingawa wazee wengine waliochaguliwa walihisi kwamba yote waliyotakiwa kufanya ni kuhubiri kutanikoni tu. Hata hivyo, likiwa na tamaa kubwa ya kushikamana na Maandiko, tengenezo lilipitia daraka la wazee kwa kutumia Maandiko, likifanya hivyo tena na tena kupitia Mnara wa Mlinzi. Mabadiliko ya kitengenezo yalifanywa kwa kupatana na mambo yaliyoonyeshwa na Maandiko.
20-22. Tengenezo zima limekuwa likijitayarishaje hatua kwa hatua ili kutimiza kazi iliyotabiriwa ya kupiga mbiu ya Ufalme duniani kote?
20 Tengenezo zima lilikuwa likijitayarisha kutimiza kikamili kazi ambayo Neno la Mungu lilikuwa limeonyesha kuwa ya siku zetu. (Isaya 61:1, 2) Ni kwa kadiri gani habari njema ingepigwa mbiu katika siku zetu? Yesu alisema hivi: “Na sharti Injili ihubiriwe kwanza katika mataifa yote.” (Marko 13:10) Kwa maoni ya binadamu, mara nyingi kazi hiyo imeonekana kuwa haiwezekani.
21 Na wakiwa na uhakika katika Kristo akiwa Kichwa cha kutaniko, jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili imesonga mbele. (Mathayo 24:45) Kwa uaminifu na uthabiti wao wamewaonyesha watu wa Yehova kazi ambayo yahitaji kufanywa. Kuanzia 1919 na kuendelea, mkazo wenye kuongezeka uliwekwa juu ya huduma ya shambani. Kwa wengi, haikuwa rahisi kwenda nyumba kwa nyumba na kuzungumza na watu wasiowajua. (Matendo 20:20) Lakini makala za funzo kama “Wabarikiwa Ni Wasioogopa” (katika 1919) na “Iweni Wenye Moyo Mkuu” (katika 1921) zilisaidia wengine waanze kazi hiyo, wakitumaini Yehova.
22 Ule mwito, katika 1922, uliosema “mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake” uliandaa kichocheo kilichohitajiwa ili kuipa kazi hiyo umaana uliostahili.[19a] Kuanzia 1927 na kuendelea, wazee ambao hawakukubali daraka hilo la Kimaandiko waliondolewa. Karibu na wakati huo, wawakilishi wa Sosaiti wenye kusafiri, wale mapilgrimu, walipewa mgawo wa kuwa waelekezi wa utumishi wa kimkoa, wakitoa maagizo ya kibinafsi kwa wahubiri katika utumishi wa shambani. Si kila mtu angeweza kupainia, lakini kwenye miisho-juma wengi walikuwa wakitumia siku nzima katika utumishi, wakianza mapema asubuhi, wakipumzika kidogo tu ili kula kipande cha mkate, na kisha kuendelea katika utumishi hadi jioni. Hizo zilikuwa nyakati za maana katika ukuzi wa kitheokrasi, na tunanufaika sana kwa kujikumbusha njia ambazo Yehova alikuwa akiongoza watu wake. Yeye aendelea kufanya hivyo. Kwa baraka zake, kazi ya kuhubiri habari njema za Ufalme uliosimamishwa italetwa kwenye tamati yenye ufanisi.
Je! Wewe Unafuliza Kulinda?
23. Kwa habari ya upendo wa Kikristo na kutokuwa sehemu ya ulimwengu, sisi mmoja-mmoja twaweza kuonyeshaje kwamba tunafuliza kulinda?
23 Kwa kuitikia mwelekezo wa Yehova, tengenezo lake huendelea kutuonya dhidi ya mazoea na mitazamo ambayo inaweza kututambulisha kuwa sehemu ya ulimwengu, na hivyo kuwa katika hatari ya kupitilia mbali nao. (1 Yohana 2:17) Nasi pia tukiwa mtu mmoja-mmoja tunahitaji kufuliza kulinda kwa kuitikia mwelekezo wa Yehova. Yehova pia hutufundisha juu ya kuishi na kufanya kazi pamoja. Tengenezo lake limetusaidia kukuza uthamini kwa yale yanayomaanishwa kikweli na upendo wa Kikristo. (1 Petro 4:7, 8) Kufuliza kwetu kulinda kwamaanisha kwamba tujitahidi sana kutumia shauri hilo tujapokamilika tukiwa binadamu.
24, 25. Twapaswa kufuliza kulinda kwa mambo yapi muhimu, tukiwa na matazamio gani?
24 Mtumwa mwaminifu mwenye akili ametukumbusha hivi kila mara: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe.” (Mithali 3:5) “Ombeni bila kukoma.” (1 Wathesalonike 5:17) Tumeshauriwa tujifunze kutegemeza maamuzi yetu juu ya Neno la Mungu, kuacha neno hilo liwe ‘taa ya miguu yetu, na mwanga wa njia yetu.’ (Zaburi 119:105) Kwa upendo, tumetiwa moyo kutanguliza maishani mwetu kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu, kazi ambayo Yesu alitabiri kwa siku zetu.—Mathayo 24:14.
25 Naam, kwa hakika mtumwa mwaminifu mwenye akili analinda. Sisi watu mmoja-mmoja twahitaji pia kufuliza kulinda. Na kwa kufanya hivyo, na tuwe miongoni mwa wale wanaopata kibali mbele za Mwana wa Adamu anapokuja kutekeleza hukumu.—Mathayo 24:30; Luka 21:34-36.
[Maelezo ya Chini]
a Faith on the March, cha A. H. Macmillan, Prentice-Hall, Inc., 1957, kurasa 19-22.
b Ona Mnara wa Mlinzi, Agosti 15, 1966, kurasa 504-10, Kiingereza.
Kwa Kupitia
◻ Kama ilivyoonyeshwa katika Mathayo 24:42, kwa nini twahitaji kufuliza kulinda?
◻ Yesu pamoja na wafuasi wake wa karne ya kwanza waliendeleaje kulinda kiroho?
◻ Tangu 1870, ni maendeleo yapi yametokea kwa sababu ya watumishi wa Yehova kufuliza kulinda?
◻ Ni nini kitakachoonyesha kwamba sisi mmoja-mmoja tunafuliza kulinda?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Yesu alijishughulisha na kazi aliyopewa na Baba yake. Pia alisali kwa bidii
[Picha katika ukurasa wa 24]
Charles Taze Russell akiwa katika miaka yake ya baadaye
[Picha katika ukurasa wa 25]
Zaidi ya wapiga-mbiu 4,700,000 ya Ufalme ni watendaji duniani kote