Karibuni Kwenye “Hofu ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya!
NAAM, wakati umekaribia wa mikusanyiko ya wilaya ya 1994 ya Mashahidi wa Yehova. Tokea Juni 1994 mpaka Januari 1995, programu hiyo ya siku tatu ya mkusanyiko itasikizwa katika mamia ya majiji ulimwenguni kote—kwanza katika Amerika Kaskazini, kisha katika Ulaya ya Mashariki na ya Magharibi, Asia, Amerika ya Kati na ya Kusini, Afrika, Australia, na visiwa vya bahari.
Hicho ni kichwa chenye kuchochea fikira kama nini—“Hofu ya Kimungu”! Hiyo si hofu mbaya kama ya mtu ambaye uhai wake umo hatarini bali ni hofu ya Mungu, hofu inayoleta amani ya akili na shangwe. Mithali moja ya Biblia yasema hivi: “Matokeo ya unyenyekevu na hofu ya Yehova ni utajiri na utukufu na uhai.” (Mithali 22:4, NW) Kumhofu Mungu kwaweza kutokezaje “utajiri na utukufu na uhai”? Jambo hilo litadhihirishwa wazi wakati kichwa cha mkusanyiko kitakapokuzwa katika siku tatu zitakazojawa na hotuba, mazungumzo, maonyesho, na drama moja.
Mtume Paulo aliandika kwamba “tusiache kukusanyika pamoja.” (Waebrania 10:25) Mashahidi wa Yehova huchukua jambo hilo kwa uzito, wakikutana mara tatu kwa juma kwa ajili ya funzo la kutaniko na ibada. Lakini, mkusanyiko wa wilaya wa kila mwaka ni tukio la kipekee. Wao huutazamia kwa hamu na kuuzungumzia miezi kadhaa baadaye. Twakukaribisha kwa uchangamfu, hata uwe wa dini gani, ujiunge nao kwenye mkusanyiko wao na kufurahia ushirika mchangamfu wa Kikristo na habari zilizo muhimu za kiroho. Mshiriki wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova la mahali penu atafurahi kukueleza mahali na siku ambapo mkusanyiko ulioko karibu zaidi nawe utafanywa.