Hudhuria “Hofu ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya!
Je! umefanya mipango ya kuhudhuria “Hofu ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1994 wa Mashahidi wa Yehova? Kwa hakika, wewe utanufaika kwa kuwapo siku zote tatu! Kukiwa na mikusanyiko 15 hivi ambayo imeratibiwa katika Afrika Mashariki pekee, yaelekea kwamba mkusanyiko utafanywa karibu na mahali unapoishi.
Hofu fulani yaweza kudhoofisha moyo mkuu na kuharibu tumaini; hata hivyo, hotuba ya msingi ya Ijumaa asubuhi itafasili hofu ya kimungu na kueleza manufaa zayo nyingi. Kwa kweli, programu yote ya mkusanyiko itakazia manufaa hizi.
Ijumaa alasiri utasikia jinsi hofu ya kimungu iwezavyo kuimarisha ndoa na maisha ya familia, na pia jinsi iwezavyo kuwasaidia wachanga wabaki wakiwa thabiti katika uaminifu-mshikamanifu wao kwa Mungu. Pindi ya alasiri itamalizia kwa hotuba yenye kuchangamsha moyo yenye kichwa “Faraja kwa Waliofiwa.” Utathamini ile habari yenye kutumika itakayoandaliwa wakati wa hotuba hiyo ili kuwasaidia wale ambao wamepoteza wapendwa katika kifo.
Programu ya Jumamosi itaonyesha jinsi hofu ya kimungu yaweza kutuimarisha tushikamane na mwelekezo wa Yehova kuhusiana na kutaniko na huduma yetu. Katika hotuba yenye kichwa “Soma Neno la Mungu, Biblia Takatifu, Kila Siku,” wajumbe watapokea madokezo yenye kutumika juu ya kusoma na kujifunza Biblia. Programu ya Jumamosi itamalizia kwa hotuba juu ya kile kichwa chenye kuamsha kupendezwa “Siku ya Yehova Yenye Kutia Hofu Imekaribia.”
Jambo kuu la programu ya Jumapili ni ile hotuba “Kutakuwa na Ufufuo wa Waadilifu.” Katika hotuba itakayofuata, “Waokolewa Wakiwa Hai Kupitia Dhiki Kubwa,” elezo litaandaliwa juu ya ile ahadi nzuri ajabu kuhusiana na wale ambao hawatakufa kamwe.—Yohana 11:26.
Pindi ya Jumapili asubuhi itamalizia kwa drama yenye kuchochea fikira ya muda wa dakika 40 yenye kichwa Machaguo Unayokabili. Wasikilizaji watakumbushwa siku za Yoshua na wataonyeshwa azimio lake imara la kumtumikia Yehova. Ule mtihani wa moto katika siku ya Eliya, utaonyeshwa pia, na masomo yatatolewa katika matukio hayo mawili yatakayowasaidia wajumbe waonyeshe hofu ya kimungu leo. Wakati wa alasiri, hotuba ya watu wote yenye kichwa, “Kwa nini Umhofu Mungu wa Kweli Sasa,” litakuwa jambo kuu la mkusanyiko.
Fanya mipango sasa ya kuhudhuria. Ili upate kujua mahali palipo karibu zaidi na nyumba yako, wasiliana na Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwenu au andikia watangazaji wa gazeti hili.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 32]
T. Rosenthal/SUPERSTOCK